Search This Blog

Saturday, February 23, 2013

YANGA WALIVYOKATA NGEBE ZA AZAM FC LEO JIONI

 Mshambuliaji wa Yanga, Jerry Tegete, akijilaumu baada ya kukosa bao la wazi.
 Mshambuliaji wa Yanga Jerry Tegete (kuli) akijaribu kumchambua kipa wa Azam Fc, Mwadin Ally, wakati wa mchezo huo, ambapo Tegete alikosa baada ya kipa huyo kuudaka mpira huo.
 WATANI WA JADI BWANA!!!!, Mashabiki wa Yanga, wakiwakebehi watani wao Mashabiki wa Simba waliokuwa wakiishangilia Azam Fc, kwa Bango lenye Ujumbe huu. ''Msomaji soma mwenyewe''.
 Kikosi cha kwanza cha Yanga kilichoanza.
 Sehemu ya mashabiki wa Yanga, waliojitokeza kuishangilia timu yao leo, ambao wanakadiliwa kuwa kama 25,0000 hivi.
Kikosi cha Azam Fc kilichoanza. 
 
 Beki wa Yanga, Nadir Haroub 'Canavaro', akimkabili mshambuliaji wa Azam, Kipre Tchetche, wakati wa mchezo wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara
 
Wachezaji wa Yanga wakimpongeza Niyonzima baada ya kutupia bao.(PICHA KWA HISANI YA SUFIANI MAFOTO)

HIVI NDIVYO CLOUDS THE DREAM TEAM ILIVYOPOKEA KIPIGO CHA 4-1















LIVE MATCH CENTRE: AZAM FC 0 - 1 YANGA FULL TIME

Dk 90+5 FULL TIME! YANGA 1-0 AZAM.

Dk 90+4 Kavumbagu anaangushwa ndani ya eneo la hatari lakini mwamuzi anapeta. Kavumbagu na Mwantika wanaumia baada ya tukio hilo.

Dk 87 Cannavaro wa Yanga anaonyeshwa kadi ya njano.

Dk 87 Azam imefanya mabadiliko, ametoka Bolou ameingia Jabir Azizi. Yanga 1-0 Azam.

Dk 86, Seif Abdallah wa Azam anaonyeshwa kadi ya njano baada ya kumchezea vibaya Niyonzima.

Dk 85 Beki wa Yanga, Kelvin Yondan anaumia na kutibiwa kwa muda baada ya kuchezewa vibaya na viungo wa Azam.

Dk 82 Yanga inafanya mabadiliko, ametoka Kiiza ameingia Said Bahanunzi. Yanga 1-0 Azam.

Dk 80 Mustapha anaonyeshwa kadi ya njano baada ya kutibiwa. Anaonekana alikuwa anapoteza muda.

Dk 77 Kipa wa Yanga, Ali Mustapha anaumia baada ya kukanyagwa na Seif Abdallah. Mpira umesimama na Mustapha anatibiwa. Yanga 1-0 Azam.

Dk 72 Azam imefanya mabadiliko, ametoka Mcha ameingia Seif Abdallah.

Dk 71 Tchetche anakosa bao la wazi kwa shuti lake kupanguliwa na kipa wa Yanga.

Dk 65 Kavumbagu anakosa bao baada ya kugongana na kipa wa Azam.

Dk 64 Yanga inafanya mabadiliko anatoka Tegete anaingia Didier Kavumbagu.

Dk 62 Tcheche anapiga shuti kali langoni kwa Yanga lakini mpira unagonga mwamba wa juu na kutoka nje.

Dk 57 Tegete anafunga bao lakini mwamuzi anakataa na kusema mfungaji aliotea.

Dk 55 Azam wamebadilika na sasa wanacheza soka la kasi na kufika langoni kwa Yanga mara kadhaa.

Dk 50 Mcha wa Azam anaichambua ngome ya Yanga lakini anapiga shuti linalopaa juu ya lango.

Dk 45 Azam imefanya mabadiliko, ametoka Ibrahim Mwaipopo ameingia Himid Mao. Yanga 1-0 Azam.

Dk 45 HALF TIME! YANGA 1-0 AZAM.

Dk 44 Tegete anakosa tena bao la wazi akiwa amebaki na kipa wa Azam. Alikuwa amepewa pasi safi na Hamis Kiiza. Yanga 1-0 Azam.

Dk 41 Tegete anakosa bao la wazi baada ya mpira wa kichwa alioupiga kutoka nje ya lango.

Dk 33 Bocco anaifungia Azam, lakini mwamuzi anakataa bao kwa kuwa kipa wa Yanga Ali Mustapha alichezewa faulo. Bocco analalamikia hali hiyo na mwamuzi anamuonyesha kadi ya njano. Yanga 1-0 Azam.

Dk 31 GOOO....! Niyonzima anaipatia Yanga bao la kwanza kwa shuti kali baada ya kupokea pasi ya Tegete. Yanga 1-0 Azam.

Dk 26 Beki wa Azam, David Mwantika anaonyeshwa kadi ya njano baada ya kumchezea vibaya Tegete. Yanga 0-0 Azam.

Dk 24 Beki ya Azam inaonekana haijatulia na inajichanganya katika kuokoa.

Dk 20 Atudo wa Azam anaushika mpira na kuutoa nje, mwamuzi Hashim Abdallah anapeta kwa kuwa hajaona.

Dk 19 Timu zinashambuliana kwa zamu.

Dk 16 Jerry Tegete wa Yanga anakosa bao la wazi akiwa amebaki na kipa wa Azam, Mwadini. Anapiga mpira hafifu unaodakwa. Yanga 0-0 Azam.

Dk 12 Beki Jockins Atudo wa Azam anamchezea vibaya Haruna Niyonzima wa Yanga nje kidogo ya eneo la hatari la Azam. Faulo isiyo na madhara inapigwa.

Dk 9 Kipre Tchetche wa Azam anapiga shuti kali langoni kwa Yanga lakini mpira unatoka nje kidogo ya lango.

Dk 4 Hamis Kiiza wa Yanga anakosa bao la wazi baada ya shuti lake kudakwa na kipa wa Azam, Mwadin Ali. Awali mabeki wa Azam walijichanganya katika kuokoa.

Mpira umeanza hapa uwanja wa taifa timu zote zikicheza soka la kasi sana.


KIKOSI CHA YANGA DHIDI YA AZAM
1.Ally Mustafa 'Barthez'
2.Mbuyu Twite
3.Oscar Joshua
4.Nadir Haroub 'Cannavaro'
5.Kelvin Yondani
6.Athumani Idd 'Chuji'
7.Saimon Msuva
8.Frank Domayo
9.Jerson Tegete
10.Hamis Kiiza
11.Haruna Niyonzima

Subs:
1.Said Mohamed
2.Juma Abdul
3.David Luhende
4.Nurdin Bakari
5.Nizar Khalfani
6.Didier Kavumbagu
7.Said Bahanuzi


KIKOSI CHA AZAM FC

1: Mwadini Ally, Balou Kipre, Kipre Tchetche, Waziri Salum, Jockins Atudo, David Mwantika, Ibrahim Mwaipopo, Salaum Aboubakar, John Bocco, Humphrey Mieno, Mcha Khamis
 

UHAMISHO WA STOPPILA SUNZU READING WAKWAMA - SUNDERLAND WAMTAMANI

Itabidi Sunderland wavunje benki ili kuweza kushinda vita ya kugombea saini ya Stoppila Sunzu kutoka klabu ya Congo TP Mazembe. 

Sunderland wamekuwa wakihusishwa na suala la kumsajili beki huyo wa kati, ingawa mdogo huyo wa mshambuliaji wa Simba Felix Sunzu ameshafanya mazoezi na Reading mwezi uliopita.


Lakini uhamisho wa mchezaji huyo kujiunga na Reading ukaingia na mtafaruku kutokana na mkanganyiko wa mkataba wake, wakati wawakilishi wa mchezaji na mchezaji mwenyewe wakisema hawana mkataba na TP Mazembe lakini kumbe ilikuwa tofauti.

Mmiliki wa TP Mazembe Moise Katumbi: "Suala la mkataba wa Sunzu lilishawekwa sawa baada ya kuupitia vizuri mkataba na mchezaji na wawakilishi wake wakakubali kwamba mkataba bado ulikuwa hai baina yetu. 


"Tatizo ni kwamba wawakilishi wake wamekuwa wakimdanganya ili aende kinyume dhidi yetu. Tunahisi wanataka kuchukua ada yote ya uhamisho kwa kusema kwamba ni mchezaji huru. 

"TP Mazembe ni professional club na hatutojaribu kuzuia haki za mchezaji yoyote ili mradi tu afuate sheria na kanuni zote. 

"Kama kuna klabu inamtaka mchezaji huyu, wawasiliane na sisi na hakika hatutomzuia kuondoka lakini hizo au hizo klabu inabidi ziongee kwanza na sisi kama sheria isemavyo."

Friday, February 22, 2013

AZAM FC VS YANGA: UMONY NA KIPRE BALOU WARUDI DIMBANI - KOCHA WA YANGA ASEMA ANATEGEMEA UPINZANI MKALI

YANGA inashuka leo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kumenyana na Azam FC katika mchezo wa kuwania taji la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Kocha wa Azam, Stewart Hall amesema kurejea kwa majeruhi Brain Omony na Kipre Balou kumempa faraja kubwa na kutamba kushinda mchezo huo na kukalia kiti cha usukani wa ligi.
"Nafikiri Omony na Balou wana mchango mkubwa kwenye timu. Uwepo wao unaongeza chachu ya timu kufanya vizuri." anasema kocha huyo.
Kwa upande wake kocha wa Yanga, Ernest Brandts amesema Azam ni moja kati ya timu bora kabisa kwenye ligi hivyo anatarajia kupata upinzani mkali.
"Azam ni timu nzuri. Ina wachezaji wenye vipaji na uwezo wakucheza kwa maelewano makubwa." anasema kocha huyo.
"Nilikuwa shuhuda wakicheza na JKT Ruvu nakushinda mabao 4-0. Nafikiri ni timu nzuri. Mchezo utakuwa mgumu. Siwezi kutabiri lolote."
Timu hizo mbili zina pointi 36 isipokuwa Yanga inaongoza ligi kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa.
Azam inashika nafasi ya pili, lakini yenyewe imecheza mechi 17 wakati vinara Yanga ikicheza 16.
Endapo Yanga itapoteza mchezo huo itakuwa imejiweka kwenye nafasi ngumu ya kutwaa taji hilo kwa msimu huu.
Yanga na Azam zimekutana mara tano tangu msimu wa 2011/12 katika mashindano tofauti.
Katika mechi hizo Yanga imeshinda mara mbili kama ilivyo kwa Azam FC.
Yanga iliifunga Azam FC mabao 2-0 katika mchezo wa fainali Kombe la Kagame na mechi ya ligi mzunguko wa kwanza kwa mabao 2-0.
Azam yenyewe iliifunga Yanga mechi mbili za ligi msimu uliopita kwa mabao 1-0 mchezo wa kwanza na ule wa marudiano ikiilaza 3-1 na kutokea vurugu kubwa baada ya Haruna Niyonzima kupewa kadi nyekundu na mwamuzi Israel Nkongo ikiwa ni kadi yake ya pili ya njano kwa kosa la kumchezea rafu beki Aggrey Morris wa Azam ambaye amesimamishwa pamoja na Said Morad, Erasto Nyoni na Deogratius Minishi kwa tuhuma za kuchukua rushwa kwenye mchezo wa Simba.

Vita nyingine itakuwa kati ya washambuliaji Kipre Tchetche wa Azam na Didier Kavumbagu kama atanzishwa kikosi cha kwanza.
Jamaa hawa ndio vinara wa kufunga mabao kwenye ligi. Tchetche amefunga mabao 10 huku Kavumbagu akizamisha tisa na kuziweka timu zao katika nafasi mbili za juu.

FIFA KUTUA TANZANIA KUKAGUA MIRADI YA MAENDELEO

OFISA Maendeleo wa Kusini mwa Afrika wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Ashford Mamelodi amewasili leo kwa ajili ya kufuatilia shughuli za maendeleo ya mpira wa miguu nchini.

Mamelodi, ambaye amekuwa msaada mkubwa kwa shughuli za maendeleo nchini Tanzania tangu alipoteuliwa kushika nafasi hiyo, pia amekuja kumtambulisha msaidizi wake, Patrick Onyango aliyeteuliwa kushika nafasi hiyo hivi karibuni.

Wakiwa nchini, wawili hao wanatarajiwa kupata taarifa ya maendeleo ya mradi wa kuweka nyasi bandia kwenye Uwanja wa Nyamagana jijini Mwanza, baada ya FIFA kuipa Tanzania mradi wa nne (GOAL Project 4) wa kuweka miundombinu kusaidia maendeleo ya mpira wa miguu.

Mwanza ilipata mradi huo baada ya Halmashauri ya Jiji hilo kukubali masharti ya mradi huo ya kulipia nakisi ya fedha zinazolipwa na FIFA, ambazo ni sh. milioni 700. Mradi huo wa kuweka nyasi bandia Nyamagana utagharimu sh. milioni 900, hivyo nakisi y ash. milioni 200 italipiwa na Jiji la Mwanza.

Pia Mamelodi na Onyango watapata taarifa ya maendeleo ya Uwanja wa Gombani uliowekwa nyasi za bandia kwa msaada wa FIFA katika mradi wa GOAL Project 3; na pia kupata mikakati ya maendeleo ya TFF kwa mwaka 2013, ikiwa ni pamoja na kozi na semina mbalimbali zitakazofanyika nchini mwaka huu.

Mamelodi na Onyango pia watapata taarifa ya maendeleo ya uboreshaji wa mashindano ya Copa Coca-Cola baada ya FIFA kuingia rasmi kwenye mashindano hayo mwaka jana kwa kuendesha kozi kwa walimu wa timu za kombaini ya mikoa na waamuzi.

Kwa sasa mashindano hayo yanashirikisha vijana wenye umri chini ya miaka 17, lakini FIFA inataka yahusishe umri mdogo zaidi ili kuendeleza soka ya vijana na kushirikisha kikamilifu shule. Maofisa hao wataondoka nchini Jumatatu asubuhi. 

USHAHIDI HUU HAPA MALKIA WA NYUKI AMLIPA MILOVAN CIRKOVIC


Ushahidi wa cheki aliyopewa Milovan Cirkovic na Malkia wa Nyuki kulipa deni alilokuwa akiidai Simba

YANGA VS AZAM FC - NANI KUKAA KILELENI - VITA YA KAVUMBAGU DHIDI YA KIPRE TCHETCHE

LIGI Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Februari 23 mwaka huu) kwa mechi tatu, lakini macho na masikio ya washabiki wa mpira wa miguu yatakuwa Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Uwanja huo wa kisasa utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Yanga na makamu bingwa Azam. Ingawa Azam imecheza mechi moja zaidi, lakini timu hizo zinatofautishwa kwa uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa kwenye msimamo wa ligi huku kila moja ikiwa na pointi 36.

Pia vinara wa ufungaji kwenye ligi kwa sasa wanatoka katika timu hizo mbili. Kipre Tchetche aliyepachika mabao tisa hadi sasa ndiye anayeongoza akifuatiwa na Didier Kavumbagu wa Yanga mwenye mabao manane.

Iwapo timu yoyote itafanikiwa kuondoka na pointi tatu katika mechi hiyo itakayochezeshwa na mwamuzi Hashim Abdallah wa Dar es Salaam, kasi ya mbio za kuwania ubingwa itaongezeka. Waamuzi wasaidizi watakuwa Hamis Chang’walu wa Dar es Salaam na John Kanyenye kutoka Mbeya wakati mezani atakuwepo Oden Mbaga.

Mechi nyingine za kesho ni Mgambo Shooting dhidi ya JKT Ruvu itakayochezwa Uwanja wa Mkwakwani, Tanga wakati Tanzania Prisons watakuwa wenyeji wa Polisi Dodoma kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Jumapili (Februari 24 mwaka huu), Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam utakuwa katika hekaheka nyingine kwa Simba chini ya Mfaransa Patrick Liewig kuikabili Mtibwa Sugar inayonolewa na nahodha wa zamani wa Taifa Stars, Mecky Maxime.

DOLA 5000 ZA ASAMOAH KUWAPELEKA YANGA FIFA

Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limesema linapeleka rasmi madai ya mchezaji wa zamani wa Yanga, Kenneth Asamoah kwenye chombo chake cha utatuzi wa migogoro (Dispute Resolution Chamber) baada ya klabu hiyo kutojibu chochote.

Awali FIFA ilipokea malalamiko ya Asamoah kuwa anaidai Yanga dola 5,000 za Marekani ambapo ilikuwa ni sehemu ya malipo yake (signing fee) baada ya kujiunga na klabu hiyo.

Desemba mwaka jana FIFA iliiandikia barua Yanga kupitia Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ikitaka maelezo yake kuhusu madai hayo ya Asamoah, lakini hadi sasa haijajibu madai hayo.

Kwa mujibu wa FIFA, hatua ya uchunguzi wa suala hilo umekamilika, na sasa linapelekwa rasmi katika chombo chake cha utatuzi wa migogoro (Dispute Resolution Chamber) kwa ajili ya kufanya uamuzi.

SIMBA VS LIBOLO: SIFA ZA MCHEZAJI BORA NA LIBOLO ILIVYOIKAMATA SIMBA


WIKIENDI iliyopita katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Simba ilicheza na CRD Libolo ya Angola katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika.

Katika mchezo huo, Simba ilifungwa bao 1-0, bao lililofungwa dakika ya 24 kwa kichwa na Joao Martins akiunganisha krosi ya Carlos Almeida.

Libolo ilionekana kuwa timu iliyosheheni wachezaji wenye miili mikubwa ambao walionekana kuwa na nguvu, uwezo wa kumiliki mpira na akili ya mchezo.

Ungeweza kuona katika mchezo huo kwamba kuna muda Simba ilionekana kucheza soka safi lakini mipango yake mingi ilionekana kufa haraka tofauti na Libolo waliokuwa anaweza kumiliki mpira kwa muda mrefu.

Hapa chini ni sifa zinazomfanya mchezaji aonekane bora wakati wote; Katika zama hizi ambazo soka linahitaji uwezo wa hali ya juu ili mafanikio yapatikane, ni muhimu kufahamu mambo yanayofanya mchezaji awe tofauti na wenzie, zifuatazo ni sifa zinazomtambulisha mchezaji bora.

Nguvu
Kwanza kabla ya kitu kingine chochote, uwezo wa mchezaji kwenye upande wa fizikia lazima ufanyiwe uchambuzi . Hiki siyo kitendo cha haraka wala cha kufanyia wepesi na hii ndiyo hatua ya mwanzo ya kumtofautisha mchezaji wa ukweli au ambaye kwa lugha ya kigeni anaitwa A GREAT PLAYER  na mchezaji wa kawaida anayefahamika kama MEDIOCRE / AVERAGE PLAYER .
Tofauti au kinyume na mawazo na imani za wengi kutambua sifa mbalimbali za mchezaji kwa upande wa nguvu au fizikia ndiyo hatua ngumu kuliko zote kwenye mchakato wa kumtambua mchezaji.
Unapotazama sifa za wachezaji kwenye upande wa nguvu lazima uwe na uhakika wa kuwaweka kwa utofauti na sifa zao nyingine za kimchezo  na usiwafananishe na wachezaji wengine. Ni muhimu sana kugawanya sifa tofauti za mchezaji.
Unaweza kuona wachezaji wengi wa Simba wana uwezo mkubwa wa kumiliki mpira, kuuchezea, kupiga chenga kama ilivyo kwa wale wa Libolo, lakini tatizo lilikuwepo katika nguvu, Libolo walikuwa na nguvu zaidi ya Simba. Hilo halina ubishi.
Viungo kama Manuel Lopez na Sidnei Mariano waliweza kuwazidi nguvu viungo wa Simba, Amri Kiemba na Mwinyi Kazimoto na kutawala sehemu kubwa ya mchezo.
Lopez na Mariano waliweza kukimbia haraka pindi Kiemba au Kazimoto walipopata mpira na kuwazuia kisha kuwapokonya mipira kadiri walivyotaka. Wakati mwingine wachezaji wa Libolo hasa beki Gamaliel Musumari alikuwa akitumia nguvu tu na akili kidogo kuzima mashambulizi ya Simba yaliyokuwa yakitokea pembeni kwa Mrisho Ngassa.  


Kasi
Baada ya hapa kuona nguvu, sasa tunaanza kutazama sifa mbalimbali zinazomtengeneza mchezaji wa ukweli au mchezaji mwenye uwezo mkubwa. Tunaanza na sifa zile ambazo ni za wazi kwa kila mmoja. Kasi au Spidi.
Chini ya mwavuli wa kasi kuna maelezo mengine madogo madogo. Kwa makocha na wachezaji, spidi yenyewe kama yenyewe haitoshi. Hata hivyo, wachezaji wakubwa wanaonyesha uwezo mkubwa wa kubadilisha kasi yao wakati wa mchezo.
Zaidi ya hapo haya mabadiliko ya kasi nayo yako kwenye migawanyiko mingi midogo midogo. Kuzielewa sifa hizi ndogo ndogo kwa sifa ya mchezaji kiujumla kama kasi ni muhimu sana na si katika kujua kuwa kasi ni muhimu tu, bali kumfanya mchezaji ajue jinsi ya kuifanya kasi yake imsaidie kuwa mchezaji bora.
Katika mchezo dhidi ya Libolo, Ngassa wa Simba amezoeleka kuwa na kasi mchezoni hata chipukizi Haruna Chanongo anaweza kuwa hivyo pia. Kasi inaweza kutumiwa na mchezaji kutengeneza nafasi kwa ajili yao na hata wenzao, Je, Ngassa alikuwa na uwezo wa kutumia kasi yake kujitengenezea nafasi akiwa amebanwa?
Unaweza kuona jibu likikuwa hapana, kwani Ngassa mara nyingi alikuwa akirudisha nyuma mipira alipoona amebanwa na hata wachezaji wenzake hawakuwa wakienda sawa na kasi yake anapokuwa na mpira.
Pia kuna wakati Ngassa hakuweza kuendana na wenzake katika matumizi ya kasi, anawajua vyema wenzake kuhusu uwezo wao wa kasi, hivyo hakupaswa kuwa na haraka ya kukimbia na mpira huku akiwaacha wenzake nyuma.
Katika kiungo, mwanzo Mussa Mudde alikuwa anacheza kwa kasi lakini mpira ukifika kwa wenzake ulikuwa ukipozwa na kucheza kwa kasi ndogo, hilo lilikuwa tatizo. Rhythm ya kasi haikuwa sawa kwa Simba
Ukiwa unatazama kasi ya mchezaji, unapaswa kuweza kutambua kuwa mchezaji anatumia kasi kwa wakati gani na anaitumiaje kasi yake na zaidi ya hapo lazima uwe una uwezo wa kutambua kuwa kasi ya mchezaji ina sababisha hatari kwa timu pinzani wakiwa nao mpira na wakiwa hawana mpira.

Kuhusu hilo, Libolo walikuwa na kasi ya mpira mara zote, wakiwa na mpira na wasipokuwa nao. Tazama Almeida alivyopiga krosi ya bao, hakuna aliyedhani kama angeweza kufanya hivyo na ndiyo maana mfungaji aliruka kichwa peke yake na kufunga kirahisi.

Wachezaji wa Simba hawakudhani kama krosi itapigwa, tena mbele ya beki Shomari Kapombe aliyedhani labda Almeida angemgongesha mpira ili uwe wa kurushwa ama kona.

Libolo waliweza kuwa na kasi ile ile wanapokuwa na mpira hata wasipokuwa nao, waliweza kutengeneza mipira mingi kuelekea lango la Simba na mara nyingi mipira yao ilipotea nje ya kidogo ya eneo la hatari la Simba.

Kutokana na kucheza bila kasi, wachezaji wa Simba mara nyingi walikuwa wakipokonywa mipira miguuni na wenzao wa Libolo waliokuwa na kasi muda wote. 

Uwezo wa kimwili
Kipengelea kingine cha kasi ni uwezo wa kimwili wa kimichezo yaani ATHLETICISM.  Hii ni jinsi ya mchezaji anavyotumia wepesi wa mwili pamoja na mienendo yake akiwa kwenye mapambano ya uwanjani.

Hapa kama ilivyokuwa  kwenye nguvu na kasi unapaswa kufahamu kama mchezaji anatumia wepesi wake wa kimichezo au hiyo ATHLETICIMS yake kufanya mambo fulani yatokee uwanjani.

Je, ndiyo kitu pekee anachokitegemea mchezaji awapo uwanjani au anatumia uwezo wa mwili wake kimichezo kama kitu cha kawaida?

Mtazame beki wa kulia wa Simba, Nassoro Masoud ‘Chollo’, huyu ni mwepesi wa kuanzisha mashambulizi, kupandisha timu na hata kupiga mashuti langoni. Simba haikutumia vyema uwezo wa Chollo ili kuikabiri vyema Libolo.

Mchezaji anayetumia uwezo wa mwili wake kimichezo ni aina ya mchezaji ambaye ana uwezo mkubwa wa kujiendeleza kimichezo kuliko mchezaji anayetegemea uwezo wake wa kimichezo.

Kumbuka siku zote kuna mchezaji ambaye ana kasi, nguvu ana akili na siku zote anafanya vizuri uwanjani lakini haimaanishi kuwa mchezaji amejiandaa kwa ubora.

Ukubwa au udogo wa kimo cha mchezaji
Ukubwa au udogo wa kimo cha mchezaji umeonekana kuwa jambo muhimu sana kwenye mchezo wa soka kwa sasa na dhana hii inazidi kupata nguvu kadri siku zinavyozidi kwenda mbele.
Libolo ilikuwa na wachezaji wengi warefu na wenye nguvu kuliko Simba. Mabeki wa kati Pedro Ribeiro na Musumari ni warefu na wanaotumia nguvu kupita kiasi katika kuzuia. Sasa beki wa namna hiyo anapokutana namchezaji kma Ngassa au Chanongo hali haiwezi kuwa ya kawaida.
Kuna njia nyingi ambazo mchezaji anaweza kuonyesha au kudhihirishwa uwezo wake huku akiwadhuru wapinzani, kwa mahusiano na nguvu ya mchezaji.
Ni muhimu kutazama kuwa mchezaji ana uwezo wa kutimiza malengo yake kwa wenzie na kwa wapinzani. Hiki ni kitu ambacho timu ingependa mchezaji binafsi akifanye kama timu inataka kutafuta ushindi.

FITNESS
Sehemu nyingine ya nguvu za mchezaji ni kuwa kwenye hali nzuri ya kimchezo kimwili yaani FITNESS na pamoja na uwezo wa kuvumilia na kubakia na nguvu pale ambapo mapambano yanazidi kuwa magumu uwanjani.
Hii inaweza kuwa sehemu muhimu kuliko zote kwenye maendeleo ya mchezaji kwani angalau kila mchezaji ana uwezo wa kucheza ila performance inaathiriwa na FITNESS.
Katika mchezo dhidi ya Libolo, Simba haikucheza katika kiwango chake kwa muda mrefu na kutoa mwanya kwa Libolo kucheza wanavyotaka. Kuna muda Simba walionekana kupungua nguvu na hata kasi yao.
Tazama dakika ya 90, Libolo waliweza kugongeana pasi kama 25 hivi bila Simba kugusa mpira. Wachezaji wa Simba walionekana kukata tamaa, na kushindwa kuwakaba Libolo wasiweze kucheza pasi hizo hadi mpira unaisha. 
Kama mchezaji akiwa katika hali nzuri basi ataonyesha kiwango cha hali ya juu na kinyume na hapo haijalishi kipaji alichonacho, kama FITNESS inakosekana uwezo wa mchezaji lazima utashuka.
Zaidi ya hapo bila kuwa na FITNESS mchezaji hawezi kuwa na bidii mchezoni na hapo ndiyo umuhimu wa PHYSIQUE ya mchezaji unapokuja, bila nguvu WORK RATE ya mchezaji itakuwa chini.
Katika soka la leo mchezaji anahitajika kuonyesha WORK RATE ya kiwango cha juu maradufu.
USIKOSE SEHEMU YA PILI….

Thursday, February 21, 2013

AZAM FC YATUMA MASHUSHU SUDAN KWA AL NASR

WAKATI klabu ya Azam ikituma 'mashushu' nchini Sudan Kusini, Serikali imewahakikishia wawakilishi hao wa Tanzania kwenye michuano ya kombe la Shirikisho, usalama wao kwa kipindi chote watakachokuwa Sudan Kusini.

Azam itacheza mechi ya marudiano na timu ya Al Nasri ya nchi hiyo kati ya Machi 2 na 3, mchezo utakaopigwa mjini Juba nchini humo.

Waziri wa Mambo ya nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe alikiri kuwepo kwa vita baina ya Sudan na Sudan Kusini licha ya kuwahakikishia Azam usalama wao.

" Azam iwe na amani kwani mapigano hayo yanafanyika mbali na mahali itakapochezwa mechi hiyo," alisema Waziri Membe katika mahojiano na Mwananchi.

Kwa mujibu wa Membe mapigano hayo yanafanyika mpakani mwa Sudan na Sudan Kusini ambako ni mbali na Juba itakapochezwa mechi hiyo ya kimataifa.

"Juba ni mbali na yanapofanyika mapigano na shughuli zinaendelea kama kawaida hakuna tofauti na Dar es Salaam kuna amani ya kutosha," alisema Waziri Membe.

Akifafanua umbali wa kutoka Juba hadi yanapofanyika mapigano hayo Waziri Membe alisema ni sawa na Dar es Salaam na Songea.

"Cha msingi Azam ijiandae kikamilifu kwa ajili ya kupeperusha vema bendera ya Tanzania bila kuwa na uoga wowote zaidi wazingatie nidhamu ya ndani na nje ya uwanja kwenye mechi yao.

Azam inahitaji sare ya aina yoyote ili iweze kusonga mbele baada ya kuibuka na ushindi wa magoli 3-1 kwenye mechi yao ya kwanza iliyochezwa jijini Dar es Salaam.

Wakati huo huo klabu ya Azam itaweka kambi nchini Uganda kabla ya kuondoka kwenda Sudan Kusini kwenye mechi yao ya marudiano.

Kocha mkuu wa timu hiyo, Stewart Hall alisema timu hiyo itaondoka kati ya Jumatatu na Jumanne kwenda jijini Kampala itakapoweka kambi hiyo ikiwa ni baada ya mechi yao ya kesho dhidi ya Yanga kwenye uwanja wa taifa jijini Dar es Salaam.

"Mechi yetu na Yanga itakuwa kipimo cha mwisho kabla ya kwenda Uganda," alisema kocha huyo raia wa Uingereza.

Kwa mujibu wa Hall, klabu yake imetuma wapelelezi nchini humo kwa ajili ya kuweka sawa mazingira watakayofikia ikiwa ni sambamba na kuangalia hali ya hewa ya mji wq Juba ambayo wameambiwa haina tofauti na ile Kampala.

Akizungumzia muonekano wa vijana wake kabla ya mechi hiyo Hall alisema wako katika hali nzuri na kusisitiza Azam inanafasi ya kusonga mbele kwenye michuano hiyo na hatimaye kutwaa ubingwa.

HATIMAYE TAIFA STARS WAKABIDHIWA BASI LAO LA MIL.200 NA KILIMANJARO

HATIMAYE  Kampuni ya Bia Tanzania(TBL) kupitia bia ya Kilimanjaro imeikabidhi Timu ya Taifa(Taifa Stars)basi jipya la kisasa lenye thamani ya Sh 200 litakalotumika kwa safari za timu hiyo.

Hafla ya makabidhiano hayo ilifanyika makao makuu wa TBL jijini Dar es Salaam jana na kuhudhuriwa na maofisa wa ngazi za juu wa TFFna baadhi ya wadau wa soka.


TBL ilikabidhi basi hilo kama sehemu ya utekelezaji wa udhamini wake kwa timu hiyo ulioingiwa Mei mwaka jana kati yake ya Shirikisho la Soka Tanzani(TFF).

Akizungumza wakati wa hafla hiyo,Meneja  wa Bia Kilimanjaro,George Kavishe alisema kuwa basi hilo kutoka kampuni ya Yutong limezingatia vigezo kwa matumizi ya timu ya taifa.

"Wachezaji wetu lazima wawe na nafasi nzuri ya kupumzika wakati wa safari ,na hiyo ndiyo sababu iliyotufanya tununue basi hili la kisasa,tunaomba mlitunze,".alisema Kavishe.

Kwa upande wake Rais wa TFF,Leodegar Tenga aliishukuru TBL kwa kukabidhi basi hilo na kusema shirikisho lake litaendeleza kutekeleza yale yote yaliyomo katika mkataba baina ya pande hizo mbili.

"Ahadi yangu ni kwamba  TFF itaendelea kushirikiano nanyi sambamba na kutekeleza yake yote yaliyomo katika mkataba baina yetu,".alisema Tenga.

HALI MBAYA YA KIUCHUMI NCHINI ITALIA - YATISHIA UMILIKI WA AC MILAN KWA BERLUSCONI

Mmiliki wa AC Milan Silvio Berlusconi amesema matamanio yake ni kuifanya klabu hiyo iendelee kuwa chini ya familia yake, lakini amekiri hali inaweza kubadilika kutokana na hali ya mbaya kiuchumi ya Italia. 

Waziri Mkuu huyo wa zamani wa Italia amkeuwa akiiongoza klabu hiyo ya Serie A tangu 1986 na uongozi wake umeifanya Milan kuwa moja ya vilabu tajiri barani ulaya. Japokuwa, hali imebadilika miaka ya hivi karibuni huku maofisa wa juu wa klabu wakisema kwamba msimu huu ni muhimu na lazima kuwa na mipango sahihi ya kiuchumi. 

“Ningependa kuendelea kuifanya Milan kitu cha familia yangu."  Berlusconi aliliambia shirika la habari la Italia ANSA.Bado nakumbuka wakati baba yangu aliponichukua kwenda uwanjani na sikulipia tiketi kwa sababu nilikuwa mdogo sana. Klabu hii ni sehemu ya familia. Mtoto wangu Barbara sasa hivi ni sehemu ya kampuni, na ningependa kuendeleza jambo hilo. Kwangu mimi, Milan ipo moyoni mwangu. Kwa miaka mingi tumetumia fedha nyingi nyingi sana, inawezekana nyingi mno."

Milan imekuwa ikihusishwa na kununuliwa katika kipindi cha miezi kadhaa na Berlusconi amekubali kwamba wanaweza kufungua uwezekano wa kuingiza mwekezaji. "Japokuwa kupenda kwangu hii timu iendelee kuwa chini ya familia, haimanishi kamba nafunga uwezekano wa kuingiza mwekezaji. Ikiwa hali ya uchumi itaendelea kuwa hivi ilivyo sasa, mabo yanaweza yakabadilika. Kuingiza fedha kutoka nje ndani ya Milan? Labda ikinibidi kufanya hivyo."

KIFAA CHA UMEME KUFUNGWA KWENYE JEZI KUZUIA MATATIZO YALIYOCHUKUA UHAI WA MARC-VIVIEN FOE NA KUTISHIA MAISHA YA FABRICE MUAMBA DIMBANI

Bodi ya soka la kimataifa (IFAB) na FIFA wanajiandaa kuanza mchakato wa majaribio ya kuweka kifaa cha umeme kwenye jezi za wachezaji ili kupunguza matatizo ya kiafya kwa wachezaji yanayotokea uwanjani.
 Hatua hiyo itafanya vifaa hivyo kuwekwa kwenye pindo la shingo la jezi, ili kuweza kukusanya taarifa kuhusu mapigo ya moyo, joto la mwili na umbali ambao mchezaji anakuwa amekimbia uwanjani. Sheria za soka za sasa zinakataza mawasiliano yoyote ya kieletroniki kati ya wachezaji na makocha na watu wa wanaohusika na mambo ya afya, lakini kumekuwepo na wito kuibadili sheria hiyo ili kuleta utaratibu wa kuweka vifa vitakvyokuwa vinafuatilia maendeleo ya afya za wachezaji uwanjani, hasa kufuatiwa kutokea kwa matukio hivi karibuni ya wachezaji kama akina Fabrice Muamba, aliyendondoka uwanjani kufuatiwa kupata mshtuko wa moyo na hatimaye ikabidi aastafu soka.

Suala hili litapelekwa kwenye mkutano wa IFAB - ambayo inahusisha vyama vya soka vya England, Scotland, Wales na Northern Ireland – na FIFA katika mkutano wake wa mwaka March 3. IFAB, ambayo wanaamua sheria za mchezo, watakuwa na kura nne - moja kwa kila chama cha soka - wakati FIFA pia itakuwa itakuwa na kura nne kuamua kupitisha suala hilo. 

PELE: "NEYMAR NI MCHEZAJI WA KAWAIDA ANAPOKUWA NDANI YA JEZI ZA BRAZIL"

Pele
 
 
Brazil imeweka majukumu mazito kwenye mabega ya kinda la nchi hiyo Neymar na mchezaji huyo anakuwa wa kawaida anapoiwakilisha nchi yake, amesema mfalme wa soka duniani Pele. 

Neymar, ambaye anaichezea Santos timu ambayo Pele aliichezea kwa zaidi ya nusu ya maisha yake ya soka, amekuwa akitajwa mchezaji bora kuwahi kutokea nchini Brazil katika miaka ya hivi karibuni na anategemewa kuiongoza Brazil kwenye kombe la dunia 2014.

Lakini wachambuzi wanasema anakosa uzoefu dhidi ya mabeki wa daraja la dunia na anahitaji kujikaza na kupambana vizuri na sio kujiangusha angusha kutafuta free kicks.
 
"Kuna kumtegemea sana Neymar lakini anakuwa mchezaji wa kawaida anapoichezea Brazil," Pele aliiambia gazeti la Estado de Sao Paulo kwenye mahojiano. 

"Kila kitu kinamzunguka Neymar, lakini ni mchezaji ambaye hana uzoefu wa kwenye ngazi ya kimataifa." 

"Ni mchezaji mzuri lakini hana uzoefu wa kucheza nje ya mipaka ya Brazil. Kila mtu anafikiria ataweza kutoa suluhisho la matatizo ya timu ya Brazil lakini hajajiandaa kuubeba mzigo huo," aliongeza mshindi huyo wa kombe la dunia kwa mara ya tatu. 

Huku akiwa na mikataba 11 ya udhamini kuiangalia, kumekuwepo na hali ya kutokueleweka kuhusu maisha ya nje ya uwanja ya Neymar. 

"Hachezi nje ya nchi na soka la ulaya. Pale Santos, wanasema ni mchezaji bora duniani lakini ananipa wasiwasi kuhusu tabia yake ya kuwa hodari kwenye kutokea kwenye vyombo vya habari kuliko alivyo uwanjani," alisema Pele.

"Anapenda kupata free kicks nyepesi .... michezo ni migumu nchini England, Italy, Germany. Marefa huwa hawana tabia ya kupiga filimbi ovyo ovyo. 

Mshambuliaji huyo mwenye miaka 21 alipata kadi yake nyekundu ya tano kwenye maisha yake ya soka kwenye mechi waliyofungwa na Ponte Preta wikiendi iliyopita. 

Pele alisema Neymar huwa anajaribu kufanya vitu vingi sana anapoichezea klabu yake.

"Free kicks zote, penati, na kona zinapigwa na Neymar. Kila mara anapopiga free kick, ina maana anakuwa nje ya mchezo kwa karibia dakika moja.

"Anatumia muda mwingi nje ya mchezo.....inabidi awe nje ya box la penati, akusanye mipira na kutumia ujuzi wake wa kuuchezea kusababisha madhara kwa wapinzani."

GALATASARY KUTOKA KWENYE DIMBWI LA MADENI MPAKA KUWA KLABU TAJIRI - FUNZO KWA VILABU VYA SIMBA NA YANGA



Mnamo mwaka 2011, Unal Aysal alichaguliwa kuwa Raisi mpya wa Galatasaray, klabu ambayo wakati huo ilikua na deni linalozidi euro milioni 240.
Kwa kifupi klabu ilikuwa ni kama mufilisi.
Tangu Unal Aysal alipoichukua timu takribani miaka miwili iliyopita Galataray mambo yake kiuchumi yanakwenda vizuri, kwasasa wanashika nafasi ya 30 kwenye msimamo wa vilabu tajiri ulimwenguni.

Baadhi ya wanasoka mahiri ulimwenguni kama vile Didier Drogba na Wesley Sneijder wamevutiwa na Gala inayoutumia uwanja mpya wa kisasa wa Turk Telekom pamoja na wachezaji wengine wenye majina kama Fernando Muslera, Emmanuel Eboue, Johan Elmander na Burak Yilmaz.

Namna gani mambo yamebadilika ghafla bin vuu?

Jibu jepesi la mafanikio ya Galatasary ni jina la mmiliki wa timu hiyo ndugu Aysal, tajiri anayeshika nafasi ya 45 kwenye orodha ya matajiri nchini Uturuki, aliutumia utajiri wake kutatua matatizo lukuki yaliyokuwa yanaikabili Gala kama ambavyo Abramovich alifanya kuinusuru chelsea. 

Aysal aliwekeza kwa wachezaji wapya mara tu baada ya kuwasili pamoja na kumuuza aliyekuwa nahodha  Arda Turan kwenda Atletico Madrid, aliwasajili wachezaji kama golikipa wa timu ya taifa ya Uruguay  Muslera, Eboue, Elmander na Felipe Melo.

Uwekezaji huo ulilipa mara moja kwani Galatasaray walishinda ubingwa wa Uturuki, ubingwa uliowaingizia kitita cha euro milioni 30m, kwa kufuzu tu kwenye michuano ya Uefa champions league pia waliweka kibindoni kiasi cha euro milioni 27. Kufunguliwa kwa uwanja mpya wa Turk Telekom Arena wenye uwezo wa kuingiza mashabiki 52,000 wakiwa wameketi vitini walifanikiwa kuingiza kiasi kingine cha Euro milioni 30 kutokana na VIP lounges pamoja na ununuzi wa tiketi za msimu.

Sehemu ya utata kwenye deals za biashara za Galatasaray ilionekana kwenye soko la hisa . Kati ya mwezi agosti na mwezi desemba mwaka 2011, waliuza asilimia 28.35 ya hisa za klabu toka kwenye kampuni mama ya Galatasaray AS deal ambayo iliingizia klabu euro milioni 70 .

Hii ilifuatiwa na tangazo kuwa mapato yote ya mlangoni kwenye uwanja wa Turk Telkom Arena yataenda moja kwa moja kwenye tawi la soka la timu hiyo  kinyume na ilivyokuwa awali chini ya kampuni mama ambayo iliingiza sehemu ndogo ya mapato kwneye maendeleo ya timu.
Kisha likaja ongezeko la asilimi 400% la hisa za kampuni ongezeko ambalo lilishusha thamani ya wana hisa binafsiambao walilazimika kulipa euro 11 kwa kila hisa jambo ambalo liliongeza mapato na kufikia idadi ya euro milioni 117. Kinyume na ilivyo kawaida, klabu haikulipa faida kwa wanahisa kama inavyohitajika faida ya euro 65 bali iliandika toka kwenye makato ya mlangoni ya mechi za usoni .

Miezi mitano baadaye kampuni iliripoti ongezeko la asilimia 300% kwenye hisa za msingi, jambo ambalo bodi maalum ya uangalizi wa masuala ya biashara ilizuia .

Kubalance mahesabu ilikuwa sehemu ya mpango mkubwa wa kuifanya Gala kuwa kampuni inayofanya vizuri kibiashara . Mfano mzuri ni usajili wa Drogba na Sneijder ambao wamesajiliwa kwa malengo ya kuleta ushindi uwanjani na upande wa biashara huku kodi zao zikilipwa na watu wengine.
CEO wa kampuni inayomiliki Galatasaray amesema kuwa lengo ni kutwaa ubingwa wa ligi ya Uturuki na kufanya vizuri Ulaya na kuifanya Gala kuwa klabu bora ulimwenguni. Hilo linaendana na kauli ya mkurugenzi huyo ambaye amesema kuwa klabu hiyo inahitaji wachezaji wakubwa ili kutimiza malengo makubwa.
Wakati Gala walipotwaa kombe la UEFA mwaka 2000 , mishahara ya Gheorge Hagi, Gheorge Popescu, Claudio Tafarrel na wengine ilileta balaa katika miaka iliyofuatia hali iliyosababisha kikosi kupunguzwa na hili liko hatarini kutokea kwa sasa.
Jinsi ya kutatua tatizo hili Aysal anasema kuwa falsafa yake kama mfanyabiashara anaamini kuwa mfanyabiashara anapaswa kuwa mtu mwenye uthubutu, na mbishi. Kwake kuwa mbahili hakukufanyi uwafurahishe mashabiki na kuuza tiketi.
Mashabiki kwa sasa wana furaha, na Aysal anaamini kuwa Gala itakuwa klabu kubwa duniani siku si nyingi na hili ni jambo ambalo mashabiki wa Fernabace na Besiktas wanacheka wakilisikia. Ila hawacheki wakiona Gala inawapanga Drogba na Sneijder kwenye mechi zao huku wakijiandaa kucheza 16 ya Ligi ya mabingwa.
Kamari aliyocheza Aysal inaonekana kulipa ila lazima klabu ishinde nyumbani na ulaya ili kuepuka historia ya kina Hagi na Tafarel kujirudia .

MILOVAN KULIPWA FEDHA ZAKE ANAZOIDAI SIMBA NA MALKIA WA NYUKI NDANI YA KIPINDI CHA WIKI

MWENYEKITI wa Kamati ya Utendaji ya Simba, Rahma Al Kharusi ameahidi kumlipa aliyekuwa kocha wa timu hiyo Milovan Cirkovic dola 32,000 ambazo anaidai klabu hiyo.

Milovan anaidai Simba fedha hizo kutokana na kuvunjwa kwa mkataba, malimbikizo ya mshahara miezi mitatu iliyobaki pamoja na mshahara wa mwezi mmoja.

Al Kharusi alimwalika Milovan raia huyo wa nchini Serbia na kuzungumza naye kwa kirefu juu ya madai yake kwa Simba katika hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Kharusi ambaye ameondoka jana kurejea Oman alisema:

"Nitamlipa Milovan (Cirkovic) fedha zake zote ambazo anaidai Simba kabla ya Jumatano ijayo.

Alisema yeye haogopi chochote na anasema kitu ambacho anakiona hakifai ndani ya uongozi wa timu hiyo.

"Kwa sababu sitaki kuona ubabaishaji nitasema jambo lolote ambalo naliona halina mashiko na timu."

"Unajua ni kitu cha ajabu, kocha huyu tunaweza kumwitaji baadaye, kwa hiyo si vizuri kumchosha,"alisema Al Kharusi.

Akizungumzia pambano la Simba na Libolo Ligi ya Mabingwa alisema; "Timu haikucheza vizuri kabisa naona kama walikuwa wanafanya mazoezi."

KOCHA WA STARS ASEMA ATAENDELEA KUKITUMIA KIKOSI CHAKE KILE KILE MECHI YA MOROCCO


KOCHA wa Taifa Stars, Kim Poulsen amesema hakuna uwezekano wa yeye kuita wachezaji mpya katika kikosi chake kitakachokabiliana na Morocco.

Stars itacheza na Morocco Machi 22 Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam kusaka tiketi yakushiriki fainali za Kombe la dunia zitakazofanyika Brazil mwakani.

Akizungumza jijini Dar es Salaam Kim  alisema sababu kubwa yakutofikiria kongeza mchezaji mpya kwenye kikosi hicho ni muda mchache wa timu hiyo kujiandaa na kabla ya mchezo huo.

"Sifikiri kuongeza mchezaji mpya kwakua muda wa kujiandaa ni mchache mno."

Alisema; "Ligi inaendelea na wachezaji wanatumikia klabu zao, hii ina maana pengine nitatumia siku nne au tano kukaa kambini na wachezaji."

"Sina maana mbaya isipokuwa muda wa kujiandaa ni mdogo mno. Nilipenda sana kuongeza mchezaji mpya katika safu ya ulinzi na kiungo, lakini siwezi kufanya hivyo tena."

Stars imeshinda mechi mbili za kirafiki dhidi ya Zambia na Cameroon kwa idadi ya bao 1-0 kila mechi.

Wednesday, February 20, 2013

LIVE MATCH CENTRE: AZAM 4 - 0 JKT RUVU - SIMBA 1 - 0 PRISONS FULL TIME


 DK 45 za kipindi cha pili zinaisha hapa uwanja wa Sokoine na Simba inaondoka na ushindi umuhimu kujaribu kukimbizana na wapinzani wao walioko juu yao Azam na Yanga.

 DK 40: Kipindi cha pili kinaelekea mwishoni na Simba inaendelea kuongoza 1-0 dhidi ya Prisons.

 Kutoka Sokoine Mbeya - DK 70 - Simba wanaendelea kuongoza lakini wanashambuliwa sana na Prisons.

Chamazi: AZAM FC 4 - 0 JKT RUVU

 Dk 90 Mwamuzi anaongeza dakika nne za nyongeza. JKT wanachangamka kidogo na kuliandama lango la Azam. JKT  0-4 AZAM.

Dk 86 Azam inaendelea kutawala mchezo hasa kiungo na kufanya mashambulizi kadhaa langoni kwa JKT. JKT 0-4 AZAM.

Kutoka Mkwakwani: Coastal 2 - 0 JKT Oljoro

 Dk 81 Azam inafanya mabadiliko, ametoka Ibrahim Mwaipopo ameingia Gaudence Mwaikimba. JKT 0-4 AZAM.

Dk 76 Kocha wa Yanga, Ernie Brandts na msaidizi wake Fred Minziro wanaondoka uwanjani baada ya kuitazama Azam ambaya watacheza nayo Jumamosi hii katika muendelezo wa Ligi Kuu ya Bara. JKT 0-4 AZAM.

Dk 72 Gooo....! Abdi Kasim 'Babi' anaipatia Azam bao la nne kwa shuti kali baada ya kupokea pasi ya Seif Abdallah. Babi anafunga bao hilo akiwa anagusa mpira wa kwanza tangu aingie dakika moja iliyopita. JKT 0-4.

Dk 71 Azam inafanya mabadiliko, ametoka Bocco ameingia Abdi Kasim. JKT 0-3 AZAM.

Dk 70 JKT inafanya mabadiliko, ametoka Amos Mgisa ameingia Emmanuel Pius.

Kutoka Mbeya - Sokoine - Kipindi kinaanza na Simba wanaendelea kuongoza 1 - 0 

 Dk 67 Azam inafanya mabadiliko, ametoka Kipre Tchetche ameingia Seif Abdallah. JKT 0-3 AZAM.

Dk 60 JKT inafanya mabadiliko, wametoka Kisimba Luambano na Mussa Mgosi, wameingia Hussein Dumba na William Sylevester.

 Dk 54 Kipa wa JKT, Shaaban Dihile anaumia baada ya kuokoa mpira wa shuti kali lililopigwa na Mcha. Mpira unasimama kwa muda ili Dihile atibiwe.

Dk 51 JKT wanacharuka na kupanga mashambulizi lakini safu ya ulinzi ya Azam inaonekana kuwa makini na kuokoa hatari zote.

Kutoka Mbeya Soine Stadium - Simba inaongoza kwa bao moja lilofungwa na Amri Kiemba kwenye dakika ya 26 kipindi cha kwanza. Sasa hivi ni kipindi cha kwanza kinaendelea.

 Dk 46 Gooo...! Mcha anaipatia Azam bao la pili kwa shuti kali baada ya kupokea pasi ya Bocco. JKT 0-3 AZAM.

Dk 45 KIPINDI CHA PILI KIMEANZA. JKT 0-2 AZAM.

Dk 45 HALF TIME! JKT 0-2 AZAM.

Dk 45 Gooo....! John Bocco anaipatia Azam bao la pili akiunganisha pasi ya Humphrey Mieno. JKT 0-2 AZAM.

Dk 42 Samwel Kamuta wa JKT anapiga shuti kali langoni kwa Azam, lakini mpira unagonga mwamba na kurudi uwanjani. JKT 0-1 AZAM

Dk 38 Damas Makwaya wa JKT anaonyeshwa kadi ya njano baada ya kumchezea vibaya Kipre Tchetche.

Dk 34  JKT wanafika mara kadhaa langoni kwa Azam lakini Mussa Mgosi anapoteza nafasi  kadhaa za kufunga. JKT 0-1 AZAM.

Kutoka Mkwakwani Tanga - COASTAL UNION 1 - 0 JKT OLJORO


 Dk 25 Mpira haujatulia sana kila timu inacheza kwa kukamia zaidi bila ufundi.

Dk 11 Kisimba Luambano wa JKT anapiga penalti, lakini kipa Mwadini anapangua mpira. JKT 0-1 AZAM

Dk 10 Penalti...! Kipa wa Azam, Mwadini Ally anamchezea vibaya Samuel Kamuta na mwamuzi anaamuru penalti.

Dk 2 Gooo...! Khamis Mcha anaipatia Azam bao la kwanza kwa shuti hafifu akiunga krosi ya Himid Mao. JKT 0-1 AZAM

JKT RUVU V AZAM. MPIRA UMEANZA

AZAM LINE UP: Mwadini Ali, Himid Mao, Wazir Salum, David Mwantika, Jockins Atudo, Jabir Aziz, Kipre Tchetche, Ibrahim Mwaipopo, John Bocco, Humphrey Mieno, Mcha Khamis.

JKT RUVU LINE UP: Shaaban Dihile, Musa Zubeir, Kessy Mapande, Kisimba Luambano, Damas Makwaya, Jimmy Shoji, Amos Mgisa, Nashon Matal, Samwel Kamuta, Mussa Mgosi na Hussein Bunu

ANGALIA VIDEO HIGHLIGHTS - ARSENAL 1 - 3 BAYERN MUNICH

YANGA YAENDELEA KUIANDALIA MAUAJI AZAM FC HUKO MBEGANI BAGAMOYO


              Wachezaji wa Young Africans wakiwa mazoezini (picha na maktaba)
Kikosi cha Young Africans leo asubuhi kimeendelea na mazoezi katika uwanja wa Mbegani nje kidogo ya mji wa Bagamoyo ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya mchezo wake dhidi ya timu ya Azam Fc siku ya jumamosi katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
 
Young Africans ambayo imeweka kambi katika hoteli ya Kiromo - Bagamoyo tangu jana mchana kujiandaa na mchezo huo, leo asubuhi imefanya mazoezi chini ya kocha mkuu Brandts, kocha msaidizi Fred Felix 'Minziro' na kocha wa makipa Razaki Siwa huku wachezaji wote wakiwa katika hali nzuri kiafya na kiakili kuelekea katika mchezo wa jumamosi.
 
Kikosi cha mholanzi Ernest Brandts kinaonekana kuwa kwenye hali nzuri na wachezaji wote wanaoekana kuwa kwenye ari ya mchezo huo wa jumamosi kwani mechi hiyo ndio itakayotoa taswira ya msimamo wa Ligi Kuu kuelekea katika mbio za kutwaa Ubingwa.
 
Young Africans ambayo katika mchezo wake wa mwisho iliibuka na ushindi wa jumla ya mabao 4-0 dhidi ya timu ya African Lyon huku safu ya ushambuliaji wa timu ya Yanga ikionekana kuwa na uchu wa kucheka na nyavu katika kila mchezo.
 
Akiongea na www.youngafricans.co.tz Brandts amesema kikosi chake kipo katika hali nzuri, mazingira ya kambi ni mazuri, wachezaji wanapata fursa ya kukaa pamoja na kushiriki mazoezi kwa pamoja katika hali ya utulivu hali inayongeza umakini katika kuelewa maelekezo yake.
 
Najua macho na masikio ya wapenzi wa soka nchini yansubiri kuona nini kitatokea siku ya jumamosi, ukweli ni kwamba huo ni mchezo muhimu sana kwetu ili kujijweka katika hali nzuri ya kuendelea kuongoza ligi , hivyo nachoweza kusema ni kwamba nimekiandaa kikosi changu ili kiweze kuibuka na ushindi katika mcheo huo siku ya jumamosi 'alisema Brandst'
 
Aidha Brandts alisema anafarijika kuwa na wachezaji wake wote 26 kambini kujiandaa na mchezo huo wa jumamosi, wachezaji wote wapo safi kiafya, kiakili na morali ya kuhakikisha tunapata ushindi katika mchezo huo, hivyo nashukuru kuwa fit kwa kikosi changu chote nitapata fursa ya kumtumia yoyote kati yao.
 
Young Africans inaongoza  msimamo wa VPL kwa kuwa na pointi 36 huku ikiwa imecheza michezo 16, imeshinda jumla ya michezo 11, imetoka sare michezo mitatu (3) na kupoteza michezo miwili (2) huku ikiwa imefunga jumla ya mabao 33 na kufungwa mabao 12 tu.

Nafasi ya pili inashikiliwa na timu ya Azam FC yenye pointi 33 ikiwa na mabao 27 ya kufunga na ikiwa imefungwa mabao 14 ambayo leo inashuka dimba la chamanzi kucheza na timu ya JKT Ruvu katika muendelezo wa michezo ya Ligi Kuu ya Vodacom.

Tuesday, February 19, 2013

LIBOLO YATUMIA ZAIDI YA TSH. MILIONI 180 KUIFUNGA SIMBA KWENYE MCHEZO MMOJA TU.

KLABU ya soka ya CRD Libolo ya Angola imetumia zaidi ya Sh. 180 milioni katika maandalizi yake ya mechi ya awali ya Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi Simba na kuweza kuibuka na ushindi wa bao 1-0.
Katika kiasi hicho cha fedha za maandalizi, Libolo ikiwa chini ya afisa mipango wake, Edson Naval iliweza kujilipia yenyewe kila kitu ilipokuwa nchini.


Mtandao wa shaffihdauda.com ulizungumza na Kasim Malinda aliyekuwa sambamba na maafisa wa Libolo waliotangulia nchini mwezi mmoja kabla ya kuivaa Simba, ambaye anasema timu hiyo ilikuwa imejiandaa ipasavyo kuhakikisha inashinda.
Katika mchezo wake wa Jumapili iliyopita kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Libolo ilishinda bao 1-0 lililofungwa na Joao Martins kwa kichwa dakika ya 24 akiunganisha krosi ya Carlos Almeida kutoka wingi ya kulia.
“Jamaa walikuwa wamejipanga katika vitu vingi. Walikuwa wakilipa wenyewe vitu vingi kuanzia uwanja hadi mabwawa ya kuogelea. Hawakuwa na mambo ya kulalamika kuonewa wala nini, kila kitu chao kilikuwa kimepangwa na watu waliotangulia kuja,” anasema Malinda ambaye alikaa na maafisa hao wa Libolo kwa muda wa zaidi ya siku 27. 
Katika mchanganuo wa matumizi ya Sh. 180 milioni, Malinda alisema, watu wasiopungua 40 walikuwepo katika msafara wa Libolo na walikaa katika hoteli ya Double Tree kwa siku 10 huku gharama ya chumba kwa siku moja ikiwa si chini ya dola 200, hivyo malazi tu walitumia Sh. 120 milioni.
Kwa chakula, watu 40 walitumia gharama ya dola 80 kwa siku 10 ambapo jumla yake ni Sh. 48 milioni. Usafiri, walikodi basi kubwa aina ya YUTON kwa gharama ya dola 350 kwa siku, hivyo kwa siku 10 walitumia Sh. 5,250,000.
Libolo ilikuwa ikifanyia mazoezi yake kwenye viwanja vya Gymkhana ambapo kwa siku walikuwa wakilipa Sh. 500,000 ambapo kwa siku 10 walitumia Sh. 5,000,000.
Ukijumlisha gharama za malazi, chakula, usafiri na uwanja, jumla Libolo ilikuwa imetumia kiasi cha Sh. 178 milioni. Fedha hizo ni nje ya matumizi mengine ambayo hayakuweza kuhainishwa mara moja kama ukodishaji wa mabwawa ya kuogelea baada ya kushindwa kulitumia lile la hoteli waliyofikia lililokuwa katika matengenezo.
Katika hayo matumizi mengine ndipo unapopata zaidi ya Sh. 2 milioni ambazo zinafikisha gharama za Sh. 180 milioni na zaidi.
“Libolo walikuwa wakikodi hadi mapipa maalum ambayo mchezaji alikuwa akiingia ndani yake yakiwa na maji baridi kila baada ya mazoezi,” anasema Malinda.


WALIIPIGA PICHA SIMBA WAKIHOFU USALAMA;
Malinda anakiri kufanya kazi na Libolo katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kurekodi mechi za Simba dhidi ya African Lyon na nyingine dhidi ya JKT Ruvu. Baadhi ya magazeti yaliwaona, lakini walipoulizwa walidai wao ni watalii.
“Wale jamaa ni waoga mno na kila kitu wanakifanya kwa tahadhari kubwa. Walikuwa wakiogopa usalama wao kwani waliwahi kuvunjiwa kamera zao Afrika Kusini na Nigeria walipokwenda kurekodi mechi za wapinzani wao, ndiyo maana walijibu wao ni watalii,” anasema Malinda.


UGUMU WA MECHI YA MARUDIANO;
Baada ya wiki mbili zijazo Simba inatarajiwa kwenda Angola kurudiana na Libolo lakini Malinda anaipa tahadhari klabu hiyo kwani inaweza kukumbana na soka tofauti kutoka kwa wapinzani wao.
Malinda anasema, kwa alivyoiona Libolo katika mazoezi na kwenye mechi ni vitu viwili tofauti. “Walikuwa wakicheza mazoezi aina nyingine ya soka na kwenye mechi wamecheza tofauti, labda zile dakika tano za mwisho ndiyo wamecheza soka lao la kasi na pasi nyingi,” alisema Malinda.


SIMBA HAIKUWA MAKINI
Malinda anasema kwa muda wote ambao Libolo ilikuwa ikifanya mazoezi kwenye viwanja vya Gymkhana, viongozi wa Simba hawakuweza kutuma mtu kwenda kuwatazama Libolo.
“Kwa muda wote tuliokuwa Gymkhana sikuwahi kuona watu wa Simba wanakuja labda kuiba mbinu za Libolo na jamaa walicheza mazoezi bila kificho na hata wao walishangaa hali hiyo, yaani hawajafuatiliwa kabisa,” anasema Malinda.

SIMBA KUVUNJA UTEJA KWA PRISONS KESHO SOKOINE?

BAADA ya sare mbili mfululizo, mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL), Simba kesho (Februari 20 mwaka huu) wanashuka Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya wakiwa wageni wa Tanzania Prisons.

Katika mechi zake mbili zilizopita, Simba iliondoka pointi mbili tu kati ya sita ilizokuwa ikizipigania. Ilitoka sare na timu za JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam na baadaye sare ya 1-1 ugenini dhidi ya Oljoro JKT.

Hiyo itakuwa mechi ya nne kwa Mfaransa Patrick Liewig tangu aanze kuinoa Simba huku akifanikiwa kuondoka na ushindi katika mechi moja dhidi ya African Lyon inayokamata mkia kwenye ligi hiyo. Simba iliilaza Lyon mabao 3-1.

Kwa upande wa kocha Jumanne Chale anashusha kikosi chake uwanjani kesho akiwa na kumbukumbu nzuri ya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya African Lyon katika mechi iliyochezwa kwenye uwanja huo huo Februari 9 mwaka huu.

Hekaheka nyingine itakuwa Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza wenye uwezo wa kuchukua watazamaji 25,000 utakapokuwa mwenyeji wa mechi kati ya Toto Africans na African Lyon. Wakati Lyon ikikamata mkia, Toto Africans yenye pointi 14 inashika nafasi ya 12 katika ligi hiyo inayoshirikisha timu 14.

Mwamuzi Simon Mberwa wa Pwani atakuwa shuhuda wa mechi kati ya Coastal Union ya Tanga na Oljoro JKT ya Arusha itakayofanyika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga. Mechi hiyo inatarajiwa kuwa na upinzani mkubwa kutokana na uimara wa timu zote mbili.

Nayo JKT Ruvu ambayo haijafanya vizuri msimu huu kulinganisha na minne iliyopita itacheza Azam kwenye Uwanja wa Azam ulioko Chamazi, Dar es Salaam. JKT Ruvu chini ya kocha Charles Kilinda inakamata nafasi ya nne kutoka chini ikiwa na pointi 16 baada ya kucheza mechi 15.

Iwapo itafanikiwa kushinda mechi hiyo, Azam itaendelea kujiimarisha katika nafasi ya pili nyuma ya vinara Yanga. Azam ambayo ni moja ya timu zenye safu kali ya ushambuliaji katika ligi hiyo ikiwa imefunga mabao 27 ina pointi 33.