Search This Blog

Saturday, June 8, 2013

LIVE SCORE: MOROCCO VS TANZANIA


Unaweza kuangalia mpira huu live kupitia hiyo link hapa chini.
Morocco XI v Taifa Stars: Lamyaghri, Jebbour, El Adoua, Kantari, Bergdich, Hermach, Obbadi, Chafni, Barrada, El Arabi, Hamdallah

TaifaStars XI v Morocco: @JumaKaseja (c); Kapombe, Nyoni, Yondan, Morris; Domayo, Sureboy, Kiemba; Ngassa, Samatta & Ulimwengu.

BAYERN MUNICH WATANGAZA KUUZA TIKETI ZOTE ZA MECHI ZA NYUMBANI MSIMU UJAO - ANGALIA NAMNA EPL INAVYOUZA



Mabingwa wa Bundesliga Bayern Munich wametangaza kwamba wameshauza tiketi zote za mechi zao nyumbani za msimu ujao kasoro mechi moja tu kati ya 17.

Uwanja wa Allianz Arena unaoingiza watu 71,000 tayari umeshapokea oda ya watu 140,000 kwa ajili ya kuangalia michezo mbalimbali ya msimu ujao wa Bundesliga, huku klabu hiyo ikitangaza jambo hilo siku tano baada ya kuisha kwa msimu na wiki tisa kabla ya kuanza kwa msimu mpya.

'Tayari tuna oda kuanzia watu 80,000 mpaka 140,000 kwa kila mchezo,' alisema mkurugenzi wa bodi, Jan-Christian Dreesen.
'Ni mchezo mmoja tu dhidi ya Hoffenheim ambapo tuna oda 68,000 hivyo kuna tiketi kadhaa zimebaki.'
Lakini sio jambo la kushangaza sana kuona Bayern wamemaliza tiketi zote za msimu ujao kwasababu mabavarian wapo katika listi ya timu zinazouza kwa bei chee tiketi zao za msimu.


BEI YA TIKETI: NAMNA PREMIER  LEAGUE NA BUNDESLIGA ZINAVYOTOFAUTIANA

PREMIER LEAGUE
BUNDESLIGA

Arsenal £985-£1,955
Augsburg £274-£469

Aston Villa £295-£580 (Earlybird), £325-£595 afterwards
Bayer Leverkusen £133-£450

Chelsea £595-£1,250
Bayern Munich £104-£540

Everton £399-£597.60 (Earlybird), £443-£672
Borussia Dortmund £303-£823

Fulham £399-£597.60 (Earlybird), £499-£959
Borussia Monchengladbach £274-£511

Liverpool £725-£780
Eintracht Frankfurt £267-£635

Manchester City £275-£745
Fortuna Dusseldorf £212-£574

Manchester United £532-£950
Freiburg £307-£590

Newcastle United £373-£717
Greuther Furth £258-£407

Norwich City £547-£608
Hamburg £230-£603

Queens Park Rangers £499-£949
Hannover £75-£278

Reading £375-425 (Earlybird), £525-£595
Hoffenheim £212-£475

Stoke City £399-£599
Mainz £155-£516

Sunderland £425-£525
Nuremburg £200-£729

Swansea City £449-£499
Schalke 04 £303-£735

Tottenham Hotspur £730-£1,845
Stuttgart £145-£607

West Bromwich Albion £349-£449
Werder Bremen £141-£498

West Ham United £600-£850
Wolfsburg £174-£450

Wigan Athletic £255-£350
All prices for the 2012-13 season

EXCLUSIVE: JUMA NYOSSO ASAINI RASMI COASTAL UNION

Aliyekuwa mchezaji wa klabu ya Simba Juma Nyosso akisaini mkataba wa kujiunga na klabu ya Coastal Union ya Tanga. 
Nyosso jana alivunja mkataba na klabu ya Simba na leo hii amekuwa mchezaji wa pili kutoka Simba kujiunga na Coastal, Haruna Moshi Boban alikuwa wa kwanza.
Boban na Nyosso wote wamesaini mikataba ya muda wa mwaka mmoja mmoja.

Friday, June 7, 2013

TIGER WOODS KINARA KWA KUINGIZA FEDHA NYINGI - BECKHAM AENDELEA KUWAKIMBIZA MESSI NA RONALDO PAMOJA NA KUTOCHUKUA SENTI TANO YA MSHAHARA WA PSG

Tiger Woods amerudi kwenye uongozi wa wanamichezo wanaongoza kutengeneza fedha nyingi kwa mwaka kwa mujibu wa jarida la Forbes la Marekani.

Mcheza gofu huyo namba namba moja duniani mwenye miaka 37, alikuwa akishika nafasi ya tatu katika listi iliyopita, lakini safari hii mmarekani huyo ameingiza kiasi cha  $78.1m (£50.7m) ikatika kipindi cha miezi 12 kutoka 1 June 2013 baada ya kuingia kwenye mikataba kadhaa ya matangazo na hivyo kuongeza mapato yake.

Mcheza Tennis Roger Federer ameibuka na kushika nafasi ya pili rose kwa kuingiza $71.5m (£46.4m) wakati mwanasoka aliyestaafu David Beckham, amebaki nafasi ya nane.

Taarifa hiyo ya Forbes inaonyesha kwamba Beckham, wakati akiwa mmoja ya wanamichezo maarufu zaidi duniani kote, alishika nafasi ya nne katika wale waliotengeneza fedha nyingi kupitia mikataba ya matangazo.

Nahodha huyo wa zamani wa England alitangaza kustaafu kucheza soka baada ya kushinda ubingwa wa ligue 1 na Paris Saint Germain, aliongeza mapato yake mpaka kufikia $47.2m (£30.6m), lakini fedha hizo alizotengeneza kupitia mikataba ya biashara ilimfanya awe nyuma ya Woods, Federer na mwanagofu Phil Mickelson, na mcheza basketball LeBron James.

Beckham bado anabakia mwanasoka anayetengeneza fedha nyingi zaidi, akifuatiwa na winga wa Real Madrid Cristiano Ronaldo ($44m/£28.6m) na mpinzani wake mshambuliaji wa Barcelona Lionel Messi ($41.3m/£26.8m), ambao wanaitimiza top 10.

Mcheza gofu wa Ireland  Rory Mcllroy alitengeneza $29.6m (£19.2m) na kushika nafasi ya 21, wakati dereva wa Formula 1 Lewis Hamilton alifuatia kwenye nafasi ya 26 akiwa na $27.5m (£17.6m).
Mshambuliaji wa Manchester United na England Wayne Rooney alishika nafasi ya 24 akiingiza $21.1m (£13.7m), huku nahodha wa England na Liverpool Steven Gerrard akimfuatia $17.2m (£11.2m).
Boxer Floyd Mayweather aliyeshika nafasi ya kwanza mwaka uliopita ameshuka mpaka nafasi ya 14 kwa mapato ya $34m (£22.1m) kupitia mapambano yake. 


MOROCCO VS TAIFA STARS: POULSEN AHAIDI SOKA LA KASI - KASEJA ASEMA WANAIHESHIMU MOROCCO ILA HAWAIOGOPI

Marrkech, Morocco
Huku Timu ya Taifa Taifa Stars ikikabiliwa na mechi muhimu kesho (Jumamosi) dhidi ya Morocco kusaka tiketi ya kucheza fainali za Kombe la Dunia, Kocha Kim Poulsen amesema amejiandaa kucheza mpira wa kasi na wenye pasi za uhakika ili kuivuruga beki ya Morocco.
Kocha huyo ameyasema hayo katika mkutano na waandishi wa habari na kusisitiza kuwa ni muhimu kuhakikisha Morocco hawaupati mpira kwa urahisi.
“Wachezaji wako katika hali nzuri kabisa na wana ari ya kushinda mechi hii…tuna nguvu na tunajua namna ya kuwapiga Morocco,” alisema kocha huyo.
Alisema suala si mchezaji gani anaanza au washambulizi ni wangapi, bali ni kazi itakayofanyika uwanjani na ubora wa wachezaji wa Taifa Stars, inayofurahia udhamnini mnono wa Bia ya Kilimanjaro Premium Lager.
Alisema Morocco ni timu kubwa na ina wachezaji wengi wa kulipwa lakini inafungika na Taifa Stars itaweka nguvu kuanzia mwanzo wa mechi.
“Unapocheza mechi kama hii inabidi uweke nguvu dakika za kwanza za mechi ili umpe mpinzani wakati mgumu kwa hivyo dakika za mwanzo zitakuwa muhimu sana katika mechi hii,” alisema.
Poulsen alisema baadhi ya watu nchini Morocco bado wanaamini kuwa ushindi wa mechi ya awali Jijini Dar es Salaam wa 3-1 dhidi ya Morocco ulikuwa wa kibahati tu. “Tunataka kuwadhihirishia kuwa tunaweza na Taifa Stars sio timu ndogo kama wanayodhani.”
Alisema mazingira ya kambi ni mazuri kabisa na wachezaji wote wako katika hali nzuri na tayari kwa mchezo huu.
“Katika hali ya kawaida ungetegemea hujuma nyingi ikiwemo hoteli mbovu, viwanja vibovu vya mazoezi na kadhalika lakini hapa ni tofauti kabisa…kwani mazingira ni mazuri,” alisema Poulsen.
Taifa Stars imeweka kambi katika Hoteli ya Pullman iliyoko nje kidogo ya Mji wa Marrakech.
Naye nahodha wa Taifa Stars, Juma Kaseja alisema wamefanya mazoezi ya kutosha hasa ikizingatiwa kambi ilianzia Addis Ababa, Ethiopia ambako walicheza mechi ya kirafiki na Sudan na kutoa sare ya 0-0 kabla ya kuelekea Marrakech.
“Morocco ni timu kubwa, tunapaswa kuiheshimu lakini sio kuiogopa…tutapambana ili timu ipate matokeo,” alisema Kaseja.
Naye Meneja wa Bia ya Kilimanajro Premium Lager, George Kavishe, akizungumza kutoka Dar es Salaam alisema wao kama wadhamini wa Taifa Stars wana imani kubwa sana na Stars na wanaitaka iwape Watanzania raha kwa mara nyingine kwa kushinda mechi hiyo.
“Tumewaona wakifanya vizuri nyumbani kwa kushinda mechi tano mfululizo na sasa ni muda wa kupata ushindi nje,” alisema.
Stars iko katika kundi C pamoja na Ivory Coast, Morocco na Gambia. Kundi hilo linaongozwa na Ivory Coast yenye pointi 7, Tanzania 6, Morocco 2 na Gambia 1.
Mechi ya kesho itapigwa katika Uwanja wa Marrakech saa tatu usiku kwa saa za Morocco ambayo itakuwa saa tano kamili Tanzania.
Baada ya Morocco Stars itacheza na Ivory Coast nyumbani Jumapili ijayo na mechi ya mwisho itakuwa dhidi ya Gambia Septemba mwaka huu.

JAPHET KASEBA KUPAMBANA NA MMALAWI KESHO DDC MAGOMENI KONDOA - WAPIMA UZITO LEO



Bondia Japhet Kaseba leo amepima tayari kumkabili mpinzani wake Rasco Chimwanza wa Malawi katika pambano la ubingwa wa kimataifa.
Zoezi zima la upimaji lilisimamiwa na Anthony Ruta, Ibrahim Kamwe, Pendo Njau na Dr. John Lugambila wa Muhimbili na kueleza kuwa mabondia wote wapo katika hali nzuri ya ushindani.
 
Kaseba amejinadi kumsambaratisha mpinzani wake katika raundi za mapema za mchezo huo. Pia kutakuwepo na mapambano ya utangulizi kama Juma Fundi atazipiga na Hasan Kiwale (moro best), Joseph Onyango toka Kenya atazipiga na Seba Temba wa Morogoro, huku Issa Omar Peche boy atakapomvaa bondia mkongwe Juma Seleman na mapambano mengineyo mengi yatapigwa katika ukumbi huo wa DDC Magomeni Kondoa 



TENGA: SERIKALI NDIO INA MAAMUZI YA MWISHO KUHUSU USHIRIKI WA SIMBA NA YANGA KAGAME CUP HUKO DARFUR


Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amesema kuwa ushiriki wa klabu za Tanzania kwenye mashindano ya Kombe la Kagame yaliyopangwa kufanyika kwenye miji ya Darfur Kaskazini na Gordofan Kusini nchini Sudan unategemea tamko la Serikali ambayo kwa sasa inafanya tathmini ya hali ya usalama.

Tenga, ambaye alikuwa akizungumza na waandishi wa habari kwenye ofisi za TFF, alisema tayari TFF na Serikali zimeshafanya mazungumzo, na Serikali imepewa taarifa zote muhimu kuhusu mashindano kwa ujumla, malazi ya klabu za Tanzania, uhakika wa usalama, usafiri wa ndani na mambo mengine muhimu hivyo kwa sasa Serikali inatathmini taarifa hizo kabla ya kutoa tamko.

“Masuala ya usalama yako nje ya uwezo wa CECAFA. Kwa hiyo, kama Serikali itabaini kuwa hali usalama ya huko si nzuri, hatutaziruhusu na kama ikiona hali ni nzuri, itaruhusu,” alisema Tenga.

“Jukumu la CECAFA (Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu vya Nchi za Afrika Mashariki na Kati) ni kuandaa mashindano na kupata uhakika wa usalama kutoka nchi mwenyeji.
“Kama tukipata uhakika huo wa usalama, mashindano yanafanyika. Lakini nchi moja moja zinayo haki ya kuhoji usalama kwa kuwa ni wajibu wa Serikali hizo kujali maisha ya wananchi wake.”

Tenga alisema kuwa mashindano hayo yalikuwa yafanyike Ethiopia, lakini katika dakika za mwisho nchi hiyo iliomba isiandae mashindano hayo hadi mwakani na ndipo Sudan ilipojitokeza kuokoa mashindano hayo.

Alisema wakati wa Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Mpira wa Miguu (FIFA) uliofanyika Mauritius, CECAFA iliitisha mkutano mkuu wa dharura na kupewa taarifa ya maandalizi ya mashindano hayo kutoka uongozi wa Chama cha Mpira wa Miguu cha Sudan na wanachama wakaridhia baada ya kuhakikishiwa usalama.

“Hivyo nchi wanachama wa CECAFA zimeridhia kushiriki baada ya kuhakikishiwa usalama, lakini kwa kuwa Waziri wetu ameonyesha wasiwasi kuhusu usalama wa Darfur, hatuna la kufanya zaidi ya kumsikiliza. Ni kauli ya kiongozi anayeonekana kuwajibika na ni lazima tusubiri tamko la Serikali,” alisema Tenga.

“Lakini napenda kuishukuru Serikali ya Sudan kwa uamuzi huo kwa sababu kuandaa mashindano hayo si kitu kidogo. Tayari Katibu Mkuu wa CECAFA (Nicholas Musonye) ameshakwenda kwenye maeneo hayo na kukaa wiki nzima akikagua viwanja na hoteli zitakazotumika na kuridhika nazo,” alisema.

Alisema watu wasipotoshe tamko la Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe alilolitoa Bungeni kuhusu ushiriki wa timu zetu Darfur.

“Mhe. Membe alisema Serikali itafanya uchunguzi ijihakikishie kuwa hali ya usalama ni nzuri… alisema Serikali haitakubali kuruhusu raia wake kwenda Darfur wakati hali ya usalama si nzuri,” alisema Tenga.

“Kwa maana hiyo, na baada ya TFF kuipa Serikali taarifa zote muhimu kuhusu hali itakavyokuwa wakati wa mashindano, sasa tunasubiri tamko la Serikali. Na hii ni kawaida kabisa kwa kuwa hata hapa tunapoaandaa mashindano, ni lazima kwanza tupata uhakika wa usalama kutoka serikalini ndipo tuziite timu.”

Alifafanua kuwa si jukumu la CECAFA kuamua mashindano yafanyike mji gani na kwamba chama cha nchi mwenyeji ndicho kinachoamua mashindano yafanyike mji gani.

“Sasa kwa suala la Sudan, magavana wa majimbo hayo mawili ya Darfur Kaskazini na Gordofan Kusini waliomba kwa chama chao mashindano hayo yafanyike kwenye miji hiyo na Serikali ya Sudan ikaihakikishia CECAFA usalama,” alisema.


“Sasa ikitokea Serikali yetu ikasema hali si nzuri, hatutaziruhusu timu zetu ziende kwa sababu masuala ya usalama yako nje ya CECAFA.”

TAIFA STARS VS MOROCCO: TENGA ASEMA TAIFA STARS SASA INAJITOSHELEZA


TAIFA STARS SASA INAJITOSHELEZA- TENGA
 Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limeishukuru Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kwa kuiwezesha timu ya taifa, Taifa Stars kuondokana na matatizo na kuwaomba Watanzania kuiombea timu ili ifanye vizuri katika mechi yake ya kesho (Juni 8 mwaka huu) dhidi ya Morocco mjini Marrakech.

Stars, ambayo inashika nafasi ya pili kwenye kundi lake la mashindano ya awali ya Kombe la Dunia ikiwa nyuma ya Ivory Coast kwa tofauti ya pointi moja, inacheza na Morocco katika mechi ya nne itakayofanyika Marrakech baada ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 katika mechi ya kwanza iliyofanyika Dar es Salaam mwezi Machi.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Rais wa TFF, Leodegar Tenga alisema kuwa tangu kuanza kwa udhamini, TFF haijawahi kupata udhamini mkubwa kama wa Kilimanjaro Premium Lager ambayo imeingia mkataba wa miaka mitano wa kuidhamini Stars wenye thamani ya dola milioni 10 za Marekani.

“Katika kipindi chote hiki hatujawahi kupata udhamini ambao umekidhi mahitaji yote ya timu kama huu wa TBL,” alisema Tenga kwenye mkutano na waandishi uliofanyika kwenye ofisi za TFF.

“Lakini katika mwaka mmoja uliopita (tangu TBL ianze kudhamini) hatujawahi kushindwa kuisafirisha timu; kushindwa kulipa posho za wachezaji; kutanguliza watu wetu kwenda nje kuiandalia timu sehemu nzuri; kuzilipia tiketi za ndege timu tunazocheza nazo mechi za kirafiki na hata kuzilipia ada ya kucheza mechi (appearance fee).

“Posho za wachezaji zimepanda kwa karibu mara mbili na ndio maana leo wachezaji wanaijali timu yao. Yote haya ni kutokana na udhamini huu. Watu wanasema usione vinaelea….”

Tenga alisema kuwa udhamini huo ndio sasa umeanza kuzaa matunda na timu inafanya vizuri ikiwa ni pamoja na kuwa na maandalizi ya muda mrefu.

“Sasa tunawaomba Watanzania waiombee timu na tunawashukuru wale waliokwenda Morocco kuishangilia kwa kuwa vijana wetu wanapata nguvu pale wanapoona kuna watu wako nyuma yao,” alisema Tenga.

Rais huyo wa TFF pia alisifu kitendo cha Rais Jakaya Kikwete kuiita timu Ikulu na kuongea na kula na wachezaji, akisema kitendo hicho kitasaidia kuongeza hamasa kwenye timu.

Naye Meneja wa Bia ya Kilimanjaro, George Kavishe alisema kampuni yake itaendelea kuwa bega kwa bega na TFF na kwamba uhusiano baina ya pande hizo mbili umeimarika na utaendelea kuimarika.

Katika mkutano huo, Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) lilikabidhi fulana maalum kwa ajili ya mashabiki ambao wamekwenda Morocco kuishangilia timu.

Ofisa Uhusiano Mwandamizi wa NSSF, Juma Kintu alisema tayari fulana 250 zimegawiwa kwa mashabiki walioko Morocco na nyingine zilitarajiwa kusafirishwa jana.

BAADA YA KUMNYAKUA BOBAN - COASTAL UNION YAMSAJILI JUMA NYOSSO, KENNETH MASUMBUKO NA MARCUS NDAHELI KUTOKA OLJORO

Juma Nyosso leo amevunja mkataba na klabu ya Simba - na taarifa zisizo rasmi zinasema anaenda kujiunga na Coastal Union ya Tanga, ambayo hivi karibuni imekuwa katika harakati za kuunda vyema kikosi chake baada ya wiki iliyopita kumsaini Haruna Moshi Boban, na jana kutangaza usajili wa wachezaji Marcus Ndaheli kutoka JKT Oljoro na Kenneth Masumbuko

Mlinzi wa kati wa JKT Oljoro, Marcus Ndeheli akisaini mkataba wa miaka miwili wa kuichezea Coastal Union

Kiungo mshambuliaji, Kenneth Masumbuko akisaini mkataba wa miaka miwili kuichezea Coastal Union

BREAKING NEWS: YANGA NAYO KUTOENDA DARFUR KUTETEA KOMBE LAKE

Habari za kuaminika kutoka kwa chanzo cha karibu na uongozi wa klabu wa Yanga ni kwamba mabingwa hao watetezi wa kombe la Kagame hawatoenda kushiriki michuano hiyo mwaka huu iliyopangwa kuanza hivi karibuni huko Darfur Sudan.

Hatua hiyo inakuja siku chache baada ya serikali kupitia wizara ya mambo ya nje ya Tanzania kusema kwamba haioni busara kwa vilabu kwenda Darfur kwa sababu eneo hilo bado halina usalama wa kutosha - kauli iliyopelekea mwenyekiti wa klabu ya Simba Ismail Aden Rage kusema kwamba timu yake haitokwenda Darfur kushiriki michuano hiyo mwaka huu.

Kwa mujibu wa CECAFA na chama cha soka cha Sudan ni kwamba michuano hiyo itachezwa kwenye lililo salama na lenye ulinzi mkubwa hivyo timu hazihitaji kuwa na wasiwasi juu ya usalama wao pindi watakapoenda kushiriki michuano hiyo mapema mwezi ujao.

Hatua ya Yanga kujitoa inazidi kuongeza idadi ya vilabu ambavyo vimesema ikiwa michuano hiyo itafanyika Darfur basi havitashiriki Kagame Cup mwaka huu, vilabu vikubwa vya Sudan AL Hila na El Merreikh, Tusker ya Kenya na Simba SC vyenyewe vilishatangaza uamuzi wa kutokwenda Darfur kwa ajili ya michuano hiyo.

BAADA YA SIMBA, AL HILAL, NA EL MERREIKH SASA TUSKER YA KENYA NAYO YAJIONDOA KAGAME CUP

Siku chache baada ya vilabu vya Simba, El Merreikh na Al Hilal kusema havipo tayari kushiriki michuano ya Kagame Cup iliyopangwa kupigwa nchini Sudan kwenye eneo la Darfur kwa kuhofia usalama wao, leo hii Tusker F.C ya Kenya wamesema rasmi kuwa wamejiondoa kwenye michuano hiyo inayotarajiwa kuanza mwezi ujao.

Kwenye taarifa iliyotolewa na mkuu wa klabu hiyo, Charles Obiny, klabu hiyo imejiondoa kwa sababu ya kiusalama zinazotokana na mgogoro katika jimbo la Dafur, ambako walitarajiwa kuchezea mechi zao.

Wanasema eneo hilo sio salama.
Hatua ya kilabu ya Tusker, inakuja licha ya hakikisho kutoka kwa Bwana Magdi Shams Eldin katibu mkuu wa wa ligi ya soka ya Sudan katika barua iliyoandikwa kwa vilabu vyote tarehe 23 Mei mwaka huu.
Mwenyekiti wa shirikisho la kandanda la Kenya, Sam Nyamweya amethibitisha kuwa, amepokea ombi kutoka kwa klabu ya Tusker ikielezea wasiwasi wa usalama wakisema kuwa hawawezi kuruhusu wachezaji wao kucheza katika eneo lisilokuwa na usalama na ni juu ya CECAFA kutafuta sehemu nyingine iliyo salama kwa wachezaji kutoka vilabu vyote kuweza kushiriki michuano hiyo

Thursday, June 6, 2013

VILABU VYA PREMIER LEAGUE VYAVUJA REKODI YA MAPATO - VYAINGIZA PAUNDI BILLIONI 2.36 KWA MWAKA

Vilabu vya Premier League ya England vimeweka rekodi ya kukusanya mapato yanayofikia kiasi cha £2,360m katika msimu wa 2011/12, kwa mujibu wa ripoti ya 22 ya masuala ya fedha kwenye soka kutoka Sports Business Group ya Deloitte.
kwa jumla, mapato ya vilabu 92 vya juu vya England yanazidi £3 billion kwa mara ya kwanza.
Dan Jones, Partner in the Sports Business Group kwenye kampuni ya Deloitte, alisema: "Pamoja na kuendesha shughuli zao kwenye mazingira magumu ya kiuchumi, vilabu vya Uingereza vinazidi kupata majina, kutambulika na kuzidi kuvutiwa watu wengi duniani mambo yanayopelekea mkusanyo mkubwa wa mapato yao.
"Mapato yote ya vilabu vya Premier League yameongezeka kwa asilimia  4% karibia kufikia £2.4 billion"

Karibia 75% ya mapato ya vilabu vya Premier League yaliongeka msimu wa 2011/12 yalitumika kwenye mishahara, ambayo ni ongezeko la £64m (4%) ya £1.7 billion ya mishahara ya yote vilabu vya Premier League.

Mapato kwenye  Football League Championship yameongezeka kwa zaidi ya £53m (13%) ya £476m msimu wa 2011/12.

BIFU LAIBUKA KATI YA MARIO BALOTELLI DHIDI YA USAIN BOLT

Mshambuliaji wa Italia Mario Balotelli amejibu maneno ya mwanariadha Usain Bolt kwa kumwambia asipende kuwahukumu watu asiowajua kiundani. 

Bolt, ambaye ana medali 3 za dhahabu alizoshinda kwenye michuano ya Olympic ya 2008 na 2012, yupo jijini Roma kwa ajili ya Diamond League usiku wa kesho, na alimzungumzia mshambuliaji huyo wa AC Milan na TGI mapema wiki hii.

"Balotelli ni mchezaji mkubwa, ingawa ni mtu wa vurugu," alisema Bolt. "Hajawahi kukosa penati. Nimekutana nae mara kadhaa na kiukweli sina mapenzi nae sana." 

Balotelli akajibu kupitia akaunti yake rasmi ya "@usainbolt get to no people before to judge them! Isnt very kind what u said about me..." aliandika muitaliano huyo kwenye tweet yake kabla ya kuifuta. 

Balotelli amecheza misimu miwili na nusu kwenye klabu ya Manchester City na kuhamia Milan mwezi January mwaka huu - Bolt ni mshabiki mkubwa wa mahasimu wa City klabu ya Manchester United.s

MAONI YA MDAU: WORLD CUP BRAZIL 2014 TANZANIA ISAHAU – PART 4


Watanzania wenzangu, hii ni part 4 ya maoni yangu niliyoanza tangia mwaka Jana November kabla Tanzania haijagusa mpira kwenye huu mzunguko wa pili wa Kombe la Dunia mtoano. Naandika leo ili isiwe kwamba namimi nilikumbwa na kile kihoma cha kuona mwanga mzima palipo giza katika soka letu la Tanzania. Nilianza kuandika part 4 siku chache baada ya Waziri wetu kuteua kamati ya kuipeleka Tanzania Brazil. Kabla ya hapo ni mara nyingi nimekuwa nikitaka kuandika kwenye kile tukio muhimu ambalo limepita tangia mwaka jana. Kwa kila tukio lipitalo naona sisi kama watanzania tunapoteza ile nafasi nyingine ya kweli na ya kwanza ya kujenga kitu cha muda mrefu.

Ukianza na programmu mpya ya miaka 3 ambayo TFF ya sasa iliona ni busara kuileta mbeleni kwetu wakati bado wanajua mabadiliko ya uongozi yalikuwa yanakuja sio chini ya miezi 2. Hii ilikuwa kabla ya FIFA kutuongezea muda. Tukatoka hapo tukasikia yale ya Copa CocaCola ambayo umri wa ushindani ulishushwa chini. Tukumbuke ingawa maamuzi yalikuwa ni mazuri sio TFF walioyoyaamua ni Copa CocaCola wenyewe. Tukapita tena kwenye maamuzi ya kumwongezea mkataba mpya Kocha wetu wa sasa ambaye kwa ukweli amefanya kazi nzuri na timu yake mpya. 

 Swali la kwanza niliuliza bila kupata jibu, vigezo alivyopewa kwa mkataba huu ni vipi maana hivi ndio vinamuamulia yeye maamuzi yake. Na hii ndio ishara nzuri kwetu sisi kujua TFF wana mpango gani na mpira wetu wa hapa nyumbani. Ukimsikia Kocha na la zaidi sana ukaangalia maamuzi yake ambayo amekuwa akiyafanya ya wachezaji ni dhariri kutambua kwamba ajira yake inategemea mafanikio ya karibuni na sio ya mbali. Inakuwa rahisi kujua anatagemewa alete raha kwa watanzania leo na sio kesho. Kwa swala la mpira (leo ni miaka 1-2 ijayo, wakati kesho ni miaka 3-6 years later).

Lakini nilianza kuandika hata kabla ya uteuzi huo, niliandika pale TBL walipotangaza udhamini mpya wa Taifa Stars ambao ni mnono. Nikawapongeza TFF kwa kupata mkataba mnono lakini hapo hapo ikaonekana TFF wakapoteza nafasi murua ya kujenga programmu ya muda mrefu kutumia hilo fungu. Mwenyekiti  alizungumzia zaidi uwezo wa timu yetu kucheza mechi za kirafiki nyingi zaidi na kuwa kambini zaidi na kulipa wachezaji zaidi. Yote hayo ni mazuri sana kwa yule ambaye analenga leo na sio kesho na hiyo ndio TFF yetu. Mmeonyesha mnaangalia umbali gani katika swala la maendeleo ya mpira wetu.

Watanzania tunaupenda mpira na tunahamu sana na mafanikio na kwa ukweli vijana waliopo sasa hivi wanatia moyo. Sema tusidanganywe na TFF kwamba wingi wa vijana ni kutokana na falsafa fulani ya vijana iliyowekwa na TFF au Kocha. Generation X ya vikongwe imeisha, wamecheza mpaka miguu yao imeshindwa kucheza zaidi na ndio maana hawaonekani tena, sio tu kwenye Taifa Stars lakini hata kwenye ligi yetu. Vijana waliopo wako sio kwa sababu ni vijana, lakini kwa sababu mpira wao wa sasa (ambao bado mapungufu ni mengi sana) unasaidia timu yetu kuliko mpira wa wale Generation X. Hio sio falsafa ya vijana. Tuelewe hilo kwanza. Kwahiyo tuwashukuru Generation X, maana hao walikaa sana tangia ujana wao alipokuja Maximo. Nae harufu ya mafanikio ya haraka ilimponza maana alianza vizuri sana kwa kumjenga mtanzania kwamba mafanikio sio leo au kesho. Ile kosa kosa na mafanikio madogo ikambidi abadili agenda. Mengieno tunayajua. Kinachosikitisha ni kushindwa kwetu kuliona hilo.

Nirudi kwenye Mada, nayo ni Brazil 2014 tusahau. TBL wadhamini wetu wametoa hela nyingi na kibiashara ni lazima wapate chao na kwa sasa wanapata sana chao kutokana na mafanikio ya vijana wetu. Lakini TBL hawawezi kuipangia TFF na serikali mpango wa maendeleo ya mpira wetu. Hawawezi kuwasukuma TAIFA zima tukaingia kwenye programmu ambayo kiukweli hatuna nyenzo ya kuiendeleza kwa spidi hiyo hiyo pale tushindwapo kuingia Brazil na nafasi ya kushindwa kwenda bado ni kubwa mno. Tusidanganyane na mafanikio yetu ya karibuni.

Ni kweli mpira ni duara na hali ya timu yetu tunaweza kuwa surprise na tukaenda. Lakini kwa vijihela tudogo tulivyonavyo kwanini tusivitumie zaidi kujenga timu hii ili kweli 2018 tuwe na timu ambayo nafasi ya kwenda Kombe la Dunia itakuwepo kutokana na uwezo wa timu yenyewe?

TFF kama mnauelewa mpira hamuwezi kuweka kigezo cha renewal ya mkataba kwa kocha kuwa kushiriki 2014. Kuna timu zisizofika 10 Africa hii ambazo zinaweza kufanya hivyo maana kweli zinategemea hilo, kama nchi na timu kwenda 2014 kuko mikononi mwao. Tegemeo la dua sio kubwa sana kama kina sisi.

Kwa nini tunawapa vijana wetu pressure yote hii? Mheshimiwa Waziri, kamati ya mechi tatu ijayo ni kamati gani maana nao mnawaweka kwenye pressure ya bure ya kuleta mafanikio wakati ni ngumu sana. Tunakuwa kama tunarudi kwenye kamati zinaozoundwa kabla watani hawajacheza tu. Tunatambua vyema kabisa tukitumia historia yetu kwamba baada ya kushindwa hizi kamati zinakufa maana msukumo unaisha. Zinarudi tena pale tunaponusa kanafasi ka miujiza tena kama hii sasa ya 2014 ambayo mimi naiita nafasi ya miujiza. Huwezi kuwalaumu maana msukumo unaendana na muda. Ukiwapa target ya 2018 basi watajipanga ipasavyo. Haimaanishi hawatajaribu kuweka nguvu kwa 2014 lakini hiyo nguvu itatumika kwa busara maana watakuwa wanatambua mipango/fungu watakalotengeneza ni la kutimiza project ya miaka 5 ijayo sio miezi mitatu ijayo.

TFF kwa bahati mbaya hamna cha kupoteza na mwenendo huu, maana mnachoangalia ni kuonyesha tu kwamba mlitusogeza mpaka tukaanza kufikiria kwamba kweli tunaweza kwa 2014. Lakini mnachokosea ni kwamba mnafanya hivyo kwa kutowajali wale wanaokuja maana mnawaweka kwenye mazingira ya kuanza upya kwa kiasi fulani, kama mngekuwa mmeweka system yetu ambayo mnajua ikiendeshwa vizuri 2018 tutaweza kushindana kabisa kuchukua moja ya hizo nafasi.

Hamna nafasi nzuri kama hii ya kuweka mipango mizuri ya timu zetu za Taifa. Tusiende kwa pupa ambayo kushindwa kwetu 2014, kutaathiri nafasi yetu ya kushindana mbeleni. Tumeshapitia situation hizi tayari ingawa mtanzania mwenye hamu ya kufarijika anaweza kusema amesahau. Lakini nyie TFF hamuwezi kusema mmesahau kwahiyo inasikitisha sana kuona mnaelekea barabara hiyo hiyo bila tahadhari yoyote.


TFF mmefanya maamuzi mengi magumu hizi sekunde chache za mwisho bila kutuelimisha hizo programmes tofauti zilizopo zinakutania wapi? Kuna Umisseta, Umitashumta, Copa Coca Cola, Airtel Rising na wengineo. Tunajua macho na masikio kwenu ni kwenye hizi zenye mvuto wa fungu. Tunachoomba ni mtuelimishe baada ya yote mnakutania wapi na lini?

Ukiangalia magazeti, na sehemu nyingi zote, imani ya vijana wetu kufanikiwa iko vizuri. Tumetokea mbali sana na hii imani sio imani hewa tu, tumeona maendeleo ya mpira ya timu yetu na inatia moyo. Siandiki haya kuwavunja moyo watanzania wenzangu, natoa tahadhari kwamba na nyie mnachangia sana sana sana kwa hali yetu duni ya mpira hapa. Bila nyie kwanza kuwa na subiria, viongozi wetu mtawayumbisha maana wengi wanafanya maamuzi kwa kusikilizia maswala ya leo na sio kwa lile wanaloliona la msingi kufanywa kesho na keshokutwa.

Media, tunawahitaji sana sana kwenye swala la kuwahamasisha vijana wetu lakini lazima liwe na uwiano. TBL wasiwaburuze na nyie mkaanza kuimba wimbo huo huo bila tahadhari yoyote. Huu ni muda mzuri kwa wadau wa mpira kushirikiana na kuweka mikakati ya mpira wetu kwa siku za mbeleni. Msibakie kusukumia 2014.

Tuwaombee Taifa Stars mafanikio mema kwenye mechi zijazo.


KAMA HATUA HAZITACHUKULIWA MAPEMA, DAWA ZA KULEVYA ZITAMALIZA KIZAZI CHA MICHEZO NA MUZIKI NCHINI



DAWA za kulevya ni hatari, ni hatari sana. Maisha ya baadhi ya wasanii na wachezaji yamepotea kutokana na matumizi ya dawa hizo.
Aidha, dawa za kulevya husababisha baadhi ya wasanii na wachezaji kushindwa kuendelea na fani zao.
Orodha ya wasanii waliopoteza maisha kutokana na matumizi ya dawa za kulevya ni ndefu lakini baadhi yao ni Elvis Presley, Whitney Houston, Brenda Fassie wa Afrika Kusini.
Tanzania imepata mshtuko kwamba kimeripotiwa kifo cha msanii kutokana na matumizi ya dawa za kulevya. Tukiwa tunangoja ripoti kamili ya daktari juu ya kifo chake, msanii mahiri wa muziki wa kizazi kipya ‘Bongo Fleva’, Albert Mangwea ‘Mangwair au Ngwea’ anadaiwa kufariki kutokana na dawa za kulevya nchini Afrika Kusini mapema wiki iliyopita.
Habari hizo ziwe kweli au la, Mangwair amefariki na mwili wake ulirejeshwa nchini juzi kwa mazishi yatakayofanyika leo hii huko Morogoro. Hata hivyo kifo chake, kitoe changamoto kwa wasanii wengine akiwemo Ray C aliyeko kwenye kituo cha kujirekebisha kutokana na matumizi ya dawa za kulevya.

DAWA ZA KULEVYA
Hizi ni dawa ambazo zimepigwa marufuku kutumiwa na jamii kutokana na kiwango chake cha athari kwa binadamu. Dawa hizi ambazo miongoni mwake ni bangi, heroin na cocaine, zina athari zaidi katika mwili wa binadamu kuliko faida.
Wasanii wanaotumia dawa za kulevya husukumwa zaidi na tabia ya kuiga ili waweze kufanya maonyesho jukwaani kwa ukakamavu mkubwa.
Wasanii hawa wanaamini wanapotumia dawa hizo zinawasisimua mwili ili wapate uwezo wa kutumbuiza jukwaani kwa muda mrefu bila kuchoka tena bila aibu.
Upande wa wanamichezo hasa soka na riadha, msukumo mkubwa upo katika kuwa na pumzi ya kuweza kucheza soka kwa dakika 90 bila kuchoka na moyo wa ujasiri hata kwenye riadha hali ni hivyo hivyo.

ATHARI ZA DAWA ZA KULEVYA MICHEZONI
Serikali duniani kote zinapiga marufuku matumizi ya dawa za kulevya. Kwa bahati mbaya, dawa hizi hutengenezwa, husafirishwa na hutumiwa kwa kificho japokuwa madhara hujionyesha wazi.
Kwa mujibu wa wataalam, mtu anapotumia dawa za kulevya, moja kwa moja huathiri baadhi ya viungo vya mwili kinyume cha imani ya watumiaji.
Mtumiaji hupata ganzi na kutoka katika hali ya kawaida. Kutokana na ganzi hiyo taarifa hutumwa katika ubongo na ubongo nao hutuma vichocheo katika kiungo hicho na hufanya kazi maradufu.
Jinsi dawa inavyotumiwa kwa wingi ili kurekebisha hali ya ganzi ndivyo nguvu inavyozidi kutengenezwa na hivyo ndivyo vinavyowamaliza wasanii na wanamichezo.
Wataalam wanasema matumizi haya ya dawa za kulevya huufanya mwili wa mtumiaji kuchoka na kukosa hamu ya kula kutokana na seli nyingi mwilini kushindwa kufanya kazi.
Matokeo yake, mwili wa mtu huyo hudhoofu kwa kukosa chakula na hata uwezo wa kutengeneza chembechembe hai za kuulinda mwili na kujikinga dhidi ya magonjwa hupungua, hivyo mwili huruhusu magonjwa ya mara kwa mara.
Hali hii inapotokea uwezo wa msanii au mwanamichezo huonekana umepungua na muda wowote mahala popote anaweza kuchukua maamuzi anayoyajua yeye.

KITU CHA KUFANYA
Masomo ya dini za Kikristo na Kiislamu na elimu maalum ya dawa za kulevya yatumike ili kuwaweka vijana katika misingi mizuri ya maadili na athari za dawa za kulevya.
Hii itasaidia vijana kufahamu kwa undani faida za dawa zilizoidhinishwa na Serikali na athari za dawa zilizopigwa marufuku zikiwemo za kulevya ili kupunguza kwa wimbi la vijana kutumbukia katika matumizi ya dawa za kulevya.
MAKALA HII IMETOLEWA KATIKA GAZETI LA MAWIO NA IMEANDIKWA NA ELIUS KAMBILI

MALIPO YA DA YA UHAMISHO YA NEYMAR: SANTOS WADAIWA KUWADANGANYA WAWEKEZAJI KIASI HALISI WALICHOLIPWA NA BARCA

Mmoja wa wawekezaji wa Neymar amewaambia FIFA wahunguze uhamisho wa wa mshambuliaji wa huyo wa Brazil aliyehamia Barcelona, akidai kwamba hajapata mgao wake kwenye ada ya uhamisho ya kiasi cha €57 million waliyolipwa Santos na Barcelona. 

Wakati wa utambulisho wa Neymar kule Camp Nou siku ya Jumatatu, makamu wa Raisi wa Barca Jose Maria Bartomeu alisema kwamba klabu yake imelipa jumla ya €57 million iliyogawanywa kwa Santos na na wawekezaji wengine wa Neymar.

Bartomeu pia alithibitisha kwa waandishi kwamba Barca walishatoa 'kishika uchumba' cha €10 million huko nyuma, fedha ambazo zimejumlisha kwenye €57 million.
Mmoja wa wawekezaji waliohusika na Neymar ilikuwa kampuni ya uwekezaji ya DIS, ambayo mkurugenzi wake ni Roberto Moreno ameiambia radio ya Catalan iitwayo RAC1 kwamba Barca wamevunja sheria za FIFA kwa kulipa €10 million kabla, wakati mchezaji huyo akiwa bado na mkataba na Santos.

"Barca wanatambua kwamba walilipa malipo ya €10 million wakati Neymar akiwa bado ni mchezaji wa Santos," Moreno alisema. "Huu ni uvunjaji mkubwa wa Kanuni za FIFA kwa sababu mchezaji huyo alikuwa bado kwenye mkataba na Santos." 

Kampuni ya DIS iliripotiwa kuwa na umiliki wa 40% ya haki za usajili wa Neymar mpaka wiki hii, hivyo walitegemewa kupokea kiasi cha €22.8 million kama mgao kwenye ya uhamisho. Japokuwa, Moreno amesema DIS wameambiwa watapokea kiasi cha €9.6 million kutoka Santos [40% ya €17 million].
"Tumeona kwenye TV kwamba Barca wamesema uhamisho ulikamilika kwa €57 million," Moreno alisema. "Lakini hapa Santos wanaongelea kiasi cha €17 million. Tunahisi tunachezewa mchezo mchafu. Santos wanauficha ukweli ili wawekezaji wapokee fedha kidogo."
Akiongea siku ya Jumatatu, Bartomeu alisema kwamba majadiliano yalichukua muda mrefu lakini hakuweza kusema maelezo zaidi kuhusu mgawanyo wa fedha kwa wawekezaji wote wa Neymar.

EXCLUSIVE INTERVIEW NA STEVE OWEN: ROONEY ATABAKI - KATI YA RONALDO AU BALE MMOJAWAPO ATATUA OLD TRAFFORD MSIMU UJAO


Tetesi za mchezaji Cristiano Ronaldo kurejea Old Trafford zinazidi kupamba moto kila kukicha, jana zilitoka taarifa kwamba United wanajpanga kutuma ofa ya paundi millioni 65 kwa Real Madrid kwa ajili ya kumrudisha mreno huyo Theatre of Dreams. Huku pia kukiwepo na taarifa kwamba Ronaldo amekataa kuongeza mkataba na Madrid pia tayari ameiweka sokoni nyumba yake anayoishi kule Madrid sokoni.
Siku chache zilizopita mie nilipata nafasi ya kutembelea Old Trafford, wakati nikiwa OT nilipata nafasi ya kufanya mahojiano na mmoja ya wafanyakazi wa United Bwana Steve Owen kuhusiana na mambo mbalimbali yakiwemo masuala ya usajili ya wachezaji kama Rooney, Ronaldo na Bale na namna wachezaji wanavyokuwa vivutio vya biashara za klabu hiyo.

Swali: Mnapata wageni wangapi kwa siku moja?

Jibu: Inategemea tunaweza kupata wageni elfu moja kwenye siku ya kawaida na kwa siku ambayo kunakuwa na watu wengi wanaweza kufika hata elfu tatu.


Swali: Wanatokea nje au ndani ya nchi?


Jibu: Asilimia 20 wanatokea hapa England na asilimia 80 wanatoka nje .


Swali: Wageni ni moja ya njia za United kujiingizia hela ?


Jibu: Kuna njia nyingi,duka letu kubwa la vifaa vya United linangiza fedha nyingi, jumba la makumbusho, wadhamini haya yote yanaleta fedha nyingi, kila mtu anajua United ni timu kubwa na tuna mashabiki kila kona ya dunia .


Swali: Unadhani nini kimeleta mafanikio haya kwa United .

 


Jibu: Wadhamini na wachezaji, unapokuwa na wachezaji unatengeneza fedha, ni muhimu kuwa na wachezaji bora duniani na ndio maana tunamhitaji Ronaldo kwa sasa.


Swali: Unadhani ni mchezaji gani ambaye mnaweza kumsajili .


Jibu: Yaweza kuwa Ronaldo,yaweza kuwa Bale,natumai mmojawapo atasajiliwa sina hakika kama uongozi umeanza nao mazungumzo lakini ningeoenda kuona mmoja wao


Swali: Vipi kuhusu Rooney, atabaki msimu ujao?


 
 Jibu- Nadhani Rooney atabaki, uliona lile bango kubwa ambalo liliwekwa nje ya Old Trafford, wasingeweka lile bango kama Rooney anaondoka, kwenye lile jukwaa la Streford End waliweka bango kubwa na Rooney ndio alionekana mbele pale sasa sidhani kama ataondoka kwa kuwa wasingeweka bango lile nadhani amebadili mawazo yake.

Wednesday, June 5, 2013

EXCLUSIVE INTERVIEW NA ADAM NDITI PART 1: KUTOKA KUWA MSHAMBULIAJI MPAKA BEKI WA KUSHOTO NDANI YA KIKOSI CHA CHELSEA

Kuanzia leo nitakuwa nakuletea mfululizo wa mahojiano yangu na mchezaji mtanzania anayekipiga kwenye klabu ya Chelsea- Adam Nditi niliyofanya nae wakati nikiwa jijini London hivi karibuni.

Shafih: Ulianza kucheza soka nyumbani Tanzania na baadae ukahamia huku, je umeona tofauti gani kwa soka la hapa na la nyumbani?

Adam Nditi: Kiukweli kabisa utofauti upo, na sisemi kwamba mpira wa nyumbani ni mrahisi au mgumu kiunshindani kwa sababu niliondoka nikiwa bado sijacheza soka la ushindani wa ukweli. Nilikuwa nacheza soka na marafiki zangu katika kujifurahisha tu. Lakini nilipokuja huku nikiwa kwenye timu tu za mtaani mpira ulikuwa na ushindani mkubwa - nyumbani nilikuwa nacheza kujifurahisha huku nilianza kucheza mpira kwa maana ya kutaka kufanikiwa mchezaji mkubwa baadae.

Shaffih: Ni kitu kinachohitajika ili mchezaji awe proffessional?
Adam Nditi: Juhudi ni lazima sana, heshima kwa sababu kama huna heshima basi huwezi kufanikiwa pia la umuhimu kabisa ni talent, kama huna talent hata uwe unafanya kazi vipi itakuwa kazi bure.

Shaffih: Mwanzoni ulikuwa ukicheza nafasi ya ushambuliaji baadae ukarudishwa kucheza beki wa kushoto. Ni wapi zaidi ulikuwa comfortable kucheza zaidi, kwenye nafasi ya ulinzi au kwenye nafasi ya ushambuliaji?

Adam Nditi: Nilipoanza kucheza soka nilikuwa nacheze mbele tu na sikuwahi kucheza sehemu nyingine yoyote. Lakini waliniponileta upande wa beki ya kushoto sikuona tofauti yoyote kwa sababu kote nilitimiza majukumu yangu ya kuzuia na nilikuwa nakwenda mbele na kufunga magoli pia. Kwahiyo nafasi zote mbili zilikuwa sawa kwangu.

Shaffih: Baada ya miaka mitano inayokuja tumtarajie Adam Nditi yupi?
Adam Nditi: Baada ya miaka mitano ninataka kuwa mchezaji mkubwa duniani. Niongeze idadi ya wachezaji wa East Africa tunaocheza barani ulaya ili niweze hata kusaidia vijana wengine kufikia mahala pazuri.

Shaffih: Wakati unaanza kucheza soka ni mchezaji gani aliyekuwa akikuvutia sana?
Adam Nditi: Kwa nafasi niliyokuwa nacheza - ushambuliaji, nilikuwa namuangalia sana Ronaldinho. Kwa sasa hivi kwa nafasi ninayocheza namuangalia sana Ashley Cole, hata kabla ya mechi huwa najaribu sana kuangalia video za mechi zake ili niweze kujifunza vitu kutoka kwake. Wakati naanza kucheza nafasi ya beki wa kushoto kocha wangu aliniagiza niende kwa Ashley Cole ili niweze kupata mafunzo mawili matatu ili kunijenga zaidi.
    

MAN CITY WAANZA BALAA LA USAJILI - MBRAZIL FERNANDINHO YUPO MANCHESTER KWA VIPIMO



Fernandinho amewasili jijini Manchester kwa ajili ya kukamilisha vipimo vya afya ili aweze kukamilisha usajili wake wa kujiunga na klabu ya Manchester City akitokea Shakhtar Donetsk.

Kiungo huyo mwenye miaka 28 anaweza kuwa mchezaji wa kwanza kusajiliwa chini ya utawala mpya wa kocha Manuel Pellegrini.

Mbrazil huyo aliisadia Shakhtar kubeba ubingwa wa Ukraine msimu uliopita na sasa anahamia Manchester City ili kuweka hai ndoto yake ya kuiwakilisha Brazil kwenye michuano ya Kombe la Dunia mwaka ujao. 

Mapema leo mchana Mbrazil huyo alionekana akiingia kwenye hosptali a Bridgewater tayari kukamilisha usajili wake.