Search This Blog

Saturday, October 26, 2013

PICHA ZA NANI MATANI JEMBE JIJINI MBEYA

 Wasani wa kundi la chacharito group wakiwaburudisha wateja katika kampeni ya nani matani jembe kupitia bia yake ya kilimanjaro premiu lager inayo washindanisha mashabiki wa yanga na simba promosheni hiyo ilifanyika katika bar ya New SITY PUB iliyopo mwanjerwa jijini la Mbeya
 Wasani wa kundi la chacharito group wakiwaburudisha wateja katika kampeni ya nani matani jembe kupitia bia yake ya kilimanjaro premiu lager inayo washindanisha mashabiki wa yanga na simba promosheni hiyo ilifanyika katika bar ya New SITY PUB iliyopo mwanjerwa jijini la Mbeya
 Shabiki wa simba akifurahia jezi ya timu yake baada ya kuzawadiwa na timu ya promosheni kupitia bia yake ya kilimanjaro premium lage katika kampeni ya nani matani jembe.
 Mteja wa bia ya Kilimanjaro kupitia kampeni ya nani mtani jembe akipuliza vuvuzela baada ya kuzawadiwa na mhudumu wa timu ya uhamasihaji wa kampeni hiyo .
Shabiki wa timu ya yanga Louis Smai toka South Africa akifurahia kuzawadiwa jezi akiwa kama mteja wa bia ya kilimanjaro premiu lager kupitia kampeni ya nani mtani jembe
Baada ya kupiga penati na kutumbukiza golini.

Friday, October 25, 2013

TENGA: TUNAFURAHI KUSIKIA AJENDA KATIKA KAMPENI ZA UCHAGUZI


Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) anayemaliza muda wake, Leodegar Tenga amesema amefurahishwa na jinsi kampeni za uchaguzi zinazokwenda kutoka na ukweli kuwa wagombea wamekuwa wakielezea kile wanachotaka kuufanyia mpira wa miguu.

Akizungumza na waandishi wa habari kwenye ofisi za TFF leo mchana, Rais Tenga ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) amesema Watanzania wanataka kusikia ajenda za wagombea.

“Ombi langu ni kwamba kampeni zimeanza vizuri, watu wanazungumza hoja zaidi. Ni jukumu la wajumbe kupima na kufanya uamuzi. Kwangu mimi nimejitayarisha kumkabidhi Katiba, Rais mpya wa TFF,” amesema.

Tenga ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) amesema kazi kubwa iliyofanywa na uongozi wake ni kujenga taasisi (TFF) pamoja na kuweka mifumo (structure) inayoainisha majukumu ya kila mmoja.

“Ajenda yetu wakati tunaingia madarakani mwaka 2005 ilikuwa ni kujenga taasisi. Tayari taasisi ipo, sasa mtazamo uwe kuushughulia mpira wa miguu wenyewe,” amesema.

Mkutano Mkuu wa TFF unafanyika kesho kwenye ukumbi wa mikutano wa NSSF Waterfront, na tayari wajumbe wa mkutano huo ambao pia utakuwa na ajenda ya uchaguzi siku inayofuata wameshawasili jijini Dar es Salaam.

Wawakilishi kutoka Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Ashford Mamelodi ambaye ni Ofisa Maendeleo wa kanda hii, Magdi Shams El Din ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya CAF na Rais wa Chama cha Mpira wa Miguu Zanzibar (ZFA) ni miongoni mwa wageni watakaohudhuria mkutano huo.

HAMAD YAHYA ASHINDA UCHAGUZI BODI YA LIGI


HAMAD Yahya ameibuka mshindi wa uchaguzi wa Bodi ya Ligi Tanzania (Tanzania Professional League- TPL Board) uliofanyika leo Oktoba 25 kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Golden Jubilee Tower kuanzia saa 3 asubuh. 

Kwa mujibu wa habari zilizotufikia hivi punde, Yahya anayetokea Mtibwa Sugar ameshinda kwa asilimia 100. 


UCHAGUZI BODI YA LIGI KUFANYIKA LEO KWA KURA YA NDIYO AU HAPANA.



UCHAGUZI wa Bodi ya Ligi Tanzania (Tanzania Professional League- TPL Board) unafanyika leo Oktoba 25 kwenye ukumbi wa mikutano uliopo Golden Jubilee Tower kuanzia saa 3 asubuhi.
Mgeni rasmi katika uchaguzi huo wa Bodi ya TPL ambao unafanyika kwa mara ya kwanza atakuwa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Leodegar Tenga.
Kwa mujibu wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, wajumbe wanaounda Mkutano wa Uchaguzi ni wenyeviti kutoka klabu 24 za Ligi Daraja la Kwanza (FDL), na 14 wa klabu za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL).
Viongozi wa klabu za FDL wamefikia hoteli ya Royal Valentino iliyoko Barabara ya Uhuru wakati wale wa VPL ambao pia watashiriki Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) wamefikia hoteli ya Landmark iliyopo Ubungo.
Kitu cha kushangaza na kufurahisha katika uchaguzi huo ni kwamba nafasi nyingi zinawania na mtu mmoja mmoja tu, hivyo mpiga kura atakuwa na kazi ya kupiga kura ya NDIYO au HAPANA.
Wagombea kwenye uchaguzi huo ni Hamad Yahya Juma (Mwenyekiti), Said Muhammad Said Abeid (Makamu Mwenyekiti) wakati wanaoumba ujumbe wa Kamati ya Uendeshaji ni Khatib Omari Mwindadi na Kazimoto Muzo.
Hii ina maana kwamba, kuna uwezekano mdogo wa wagombea hao kushindwa na hata kama ikitokea mmoja ameshindwa, waliochaguliwa wataendelea na uongozi huku nafasi hiyo ikizibwa baadaye.
  

NYAMLANI AANZA KAMPENI KWA AHADI TISA ZA KUMMALIZA MALINZI



MGOMBEA nafasi ya U-Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Athuman Jumanne Nyamlani amezindua kampeni zake za kuwania ukuu wa shirikisho hilo akipambana na Jamal Malinzi.
Akizindua kampeni zake jana jijini Dar es Salaam, Nyamlani aliweka wazi jinsi atakavyoendeleza mipango ya sasa ya TFF kwa kuwa alishiriki katika kuiandaa na kuipanga chini ya uongozi wa sasa wa Leodegar Tenga.
Nyamlani anaenda mbali zaidi kwa kuweka pia ahadi zake tisa za kutekeleza endapo atapewa ridhaa ya kuliongoza shirikisho hilo. Miongoni mwa ahadi hizo za Nyamlani ni pamoja na;
Moja: 
KUIMARISHA USIMAMIZI NA MENEJIMENTI YA SOKA KATIKA NGAZI ZOTE.
Nyamlani anasema akiwa rais wa TFF, kwa kushirikiana na viongozi wa klabu na vyama vya soka vya wilaya na mikoa pamoja na serikali ataimarisha usimamiaji na menejimenti ya soka katika ngazi zote kwa kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa viongozi pamoja na kusimamia sheria na taratibu za uendeshaji wa soka Tanzania.
Mbili: RUSHWA KATIKA SOKA NCHINI.
Nyamlani anakiri kwamba kumekuwa na malalamiko na vitendo vya rushwa ambavyo vinawahusisha viongozi wa soka. Anasema kwa kushirikiana na serikali na viongozi wa soka katika ngazi zote atahakikisha anaendeleza mapambano dhidi ya rushwa katika soka nchini.
Tatu: KUKUZA SOKA LA WATOTO, VIJANA NA WATOTO.
Endapo Nyamlani atachaguliwa kuwa rais mpya wa TFF amesema atalipa uzito wa kipekee soka la watoto wenye umri chini ya miaka 16 na soka la vijana na kukuza vipaji (miaka 9-12, miaka, miaka 13-14, miaka 15-17 na miaka 18-21) pamoja na soka la wanawake. Kazi hii Nyamlani ataitekeleza kwa kuanzisha program mbalimbali za mashindano za kukuza vipaji kwa makundi haya ya vijana kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa soka.
Nne: KUIMARISHA UWEZO WA RASILIMALI FEDHA WA TFF.
Nyamlani anasema akishinda nafasi ya U-Rais wa TFF atahakikisha shirikisho hilo linapata vyanzo endelevu na vya kuaminika vya fedha ili kujenga uwezo wa TFF katika kutekeleza mipango yake na kufikia malengo kikamilifu. Vilevile ataimarisha idara ya masoko ili kuweza kupata wadhamini zaidi na kuweza kuuza nembo za shirikisho hilo.
Tano: KUONGEZA IDADI NA UBORA WA WAAMUZI, MAKOCHA NA WATAALAM WA AFYA YA MICHEZO.
Nyamlani anasema atahakikisha kunakuwa na program endelevu ya mafunzo ya makocha, waamuzi na wataalam wa afya ya michezo ili kuongeza ufanisi wao katika kutekeleza majukumu yao kwa mujibu wa sheria na taratibu zinazoongoza mchezo wa soka nchini na pia waweze kufikia viwango vya kimataifa vilivyowekwa na Shirikisho la Soka Afrika (CAF) na Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA).
Pia Nyamlani anasema atahakikisha anaweka msisitizo katika kuhamasisha watu wanaopenda soka na wenye uwezo wajiunge na katika fani hizo jambo ambalo litaongeza idadi ya wataalam hao.
Sita: KUONGEZA UBORA WA LIGI KUU, LIGI DARAJA LA KWANZA, LIGI ZA WILAYA NA MIKOA.
Anasema michuano ya Ligi Daraja la Kwanza, Ligi za Wilaya, Mikoa na Ligi Kuu ni ngazi muhimu ya kukuza soka katika nchi yoyote. Ni imani yake kwamba ligi hizo zikiimarishwa kwa kushirikiana na viongozi wa soka wa wilaya, mikoa na bodi ya kusimamia uendeshwaji wa ligi kuu Tanzania itaweza itaweza kuinua ubora wa soka na kufikia viwango vya kimataifa na kuweza kuhimili ushindani wakati wote.
Nyamlani anasema atashirikiana na viongozi wa soka na vyama vya kitaalam ili kuweza kuboresha kanuni mbalimbali zitakazowawezesha wachezaji vijana kuwa wachezaji wa kulipwa. Vile vile Nyamlani anasema atasimamia ipasavyo suala la malipo kwa klabu na vituo vya kukuzia vipaji pindi wachezaji wao wanapouzwa au kupanda viwango na kuwa wachezaji wa kulipwa.
Saba: KUONGEZA IDADI YA MAWAKALA.
Nyamlani ana imani kwamba ili mpira wa Tanzania ukue kwa kasi ni lazima tuongeze idadi ya wachezaji wanaocheza soka la kulipwa nje ya nchi kwa kufanya hivyo ni lazima kuwa na mawakala wanaozingatia weledi na siyo uwakala wa kupeana kiholela huku wakishindwa kuuza hata mchezaji mmoja tangu mtu alipopewa kazi hiyo.
Nane: KUIMARISHA USHIRIKIANO WA SERIKALI NA TFF.
Nyamlani anasema atahakikisha anasimamia, kukuza na kuendeleza uhusiano uliopo sasa kati ya TFF na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa imani kwamba jambo hili ni muhimu kwa ustawi wa soka Tanzania kwa sababu ni ukweli soka kwa sasa ni ajira rasmi kwa vijana ambao ndiyo nguzo ya taifa.
Tisa: KUIMARISHA USHIRIKIANO WA TFF, CAF NA FIFA.
Nyamlani anasema atahakikisha kuwa anakuza na kuendeleza uhusiano mzuri uliopo kati ya TFF na CAF na FIFA ili kuongeza kasi ya ukuaji wa soka nchini kufikia viwango vya kimataifa kwa kutumia misaada mbalimbali ya kitaalam na kifedha inayotolewa na taasisi hizo kubwa Afrika na duniani.
NAAM, HIZO NDIZO SERA ZA NYAMLANI KAZI KWENU WAPIGA KURA!         

VIONGOZI WA VILABU VYA LIGI DARAJA LA KWANZA KUWENI MAKINI NA UCHAGUZI WA BODI YA LIGI,MNAPIGWA CHANGA LA MACHO.



Uchaguzi wa viongozi wa bodi ya ligi unataraji kufanyika leo, ila kuna ubabaishaji mkubwa kwenye mchakato huu wa uchaguzi na kama ingekuwa ni uwezo wangu basi ningelisimamisha zoezi hili mpaka pale taratibu zitakapofuatwa.

Bodi hiyo ya ligi ni chombo kinachoundwa kwa ajili ya kuvisimamia vilabu vya ligi kuu pamoja na vile vya ligi daraja la kwanza,cha ajabu ni kwamba  Raisi na makamu wa chombo hiki watachaguliwa na vilabu 14 vya ligi kuu tu huku vilabu 24 vya ligi daraja la kwanza vikiwachagua wajumbe wawili tu wa kuviwakilisha kwenye bodi hiyo.

Cha kustaajabisha ni kwamba vilabu vya ligi daraja la kwanza havitashiriki kwenye mchakato wa kuwachagua raisi na makamu wa raisi wa bodi. Swali: kama vilabu vya ligi daraja la kwanza havitashirikishwa kwenye mchakato wa kuwachagua Raisi na makamu wake sasa iweje wawe viongozi wao?

Hili nalifananisha na mchakato wa uchaguzi mkuu wa nchi uwambie wakazi wa jimbo fulani wana haki ya kumchagua mbunge wao ila hawana haki ya kumchagua raisi na makamu wa nchi. Je kidemokrasia hili linawezekana ?.

Thursday, October 24, 2013

NURDIN BAKARI: TULIKOSA UMAKINI WA ‘MARKING’ TUKAFUNGWA NA YANGA



KIUNGO wa zamani wa Yanga anayechezea Rhino Rangers ya Tabora, Nurdin Bakari amesema kosa kubwa walilofanya katika mchezo wa jana na kufungwa mabao 3-0 na Yanga ni wachezaji wenzake kushindwa kuwakaba vyema wachezaji wa Yanga.
Nurdin amesema hata ukitazama mabao ya Yanga yalifungwa kutokana na uzembe wa mabeki wa timu yake kushindwa kuwakaba viungo na washambuliaji wa Yanga ambao kuna wakati walicheza wanavyotaka.

“Tumefungwa kutokana na poor marking (umakini mdogo wa kukaba), muda mwingi Yanga walikuwa wakicheza wanavyotaka na kupenya ngome yetu kirahisi. Lakini hili ni jambo la kawaida kwa timu hizi zinazokuwa zimepanda daraja kwa mara ya kwanza, nadhani baadaye mambo yanaweza kuwa mazuri na tutafanya vizuri zaidi,” alisema Nurdin.

Bao la kwanza la Yanga lilifungwa na Hamisi Kiiza dakika ya 12 akiunganisha vyema krosi ya Simon Msuva kutoka wingi ya kulia. Kiiza alifunga bao hilo akiwa katikati ya mabeki wa Rhino ambao ni Julius Masonga na Laslaus Mbogo ambaye amewahi kuichezea Yanga pia.

Bao la pili la Yanga lilifungwa na Frank Domayo dakika ya 72 akimalizia pasi nzuri ya Mrisho Ngassa akiwa ndani ya eneo la hatari la Rhino lakini mabeki hawakuweza kumkaba kiufasaha na kuweza kufunga kirahisi.
Yanga ilipata bao la tatu kupitia kwa Kiiza ambaye alimalizia vyema pasi ya Ngassa ambaye aliichambua safu ya ulinzi ya Rhino kutoka wingi ya kulia na kumpasia Kiiza aliyefunga kirahisi. 

Nurdin alienda mbali kwa kusema kuwa, kitu kingine kilichosababisha kipigo kwao ni kutokana kuwa na wachezaji wengi ambao hawana uzoefu wa kucheza Ligi Kuu ya Bara.
“Wachezaji wengi katika kikosi chetu hawana uzoefu wa kucheza ligi kuu, nadhani hilo nalo lilikuwa tatizo kwetu kuweza kuifunga na kuizuia Yanga kufunga nadhani tukikaa muda mrefu tunaweza kufanya vizuri zaidi,” alisema Nurdin.

BRANDTS AWAPOZA KAVUMBAGU, CANNAVARO, CHUJI NA BARTHEZ



BAADA ya kutowatumia wachezaji wake wanne wa kikosi cha kwanza katika mchezo wa jana dhidi ya Rhino Rangers, Kocha wa Yanga, Ernie Brandts amesema amelazimika kuwapumzisha wachezaji wanne wa kikosi cha kwanza kutokana na uchovu.
Katika mchezo dhidi ya Rhino Rangers Jumatano iliyopita, Brandts hakuwatumia wachezaji Didier Kavumbagu, Athuman Idd ‘Chuji’, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ na Ali Mustapha ‘Barthez’, lakini kikosi kilichoanza kiliweza kuibuka na ushindi wa mabao 3-0.
Tofauti ya Cannavaro na Barthez, Chuji na Kavumbagu wenyewe waliwekwa benchi lakini hawakuweza kupewa nafasi ya kucheza katika mchezo huo ulionekana kikosi cha Yanga kilichoanza kinaweza kuhimili vishindo vya Rhino.

Mara baada ya mchezo huo, Brandts aliuambia mtandao huu kwamba, hakuwachezesha wachezaji hao kutokana na kutumika katika mechi nyingi za Yanga hivyo aliamua kuwapumzisha ili watumike katika mechi zinazofuata.
“Ni kweli sikuwapanga Chuji, Cannavaro na wengine ambao mmezoea kuwaona kikosi cha kwanza kutokana na kuwa wametumika sana hivyo niliamua kuwapumzisha ili niweze kuwatumia katika michezo ijayo na sikuwa na maana nyingine nje ya hiyo.

“Yanga imesajili zaidi ya wachezaji 25, hivyo kutowatumia wachezaji fulani wa kikosi cha kwanza, haina maana kwamba wapo katika adhabu au kuna jambo tofauti lililotokea naomba nieleweke hivyo, mtawaona katika mechi zijazo hao wachezaji wala msiwe na shaka,” alisema Brandts.

Kikosi cha jana cha Yanga kiliwakilishwa na Deogratius Munishi ‘Dida’, Juma Abdul, David Luhende, Mbuyu Twite, Kelvin Yondani, Rajab Zahir, Simon Msuva, Frank Domayo, Hamisi Kiiza, Mrisho Ngassa na Haruna Niyonzima.
Katika kikosi hicho, Brandts aliwafanyia mabadiliko Msuva na Luhende ambao nafasi zao zilichukuliwa na Oscar Joshua na Nizar Khalfan.  

Yanga ambayo sasa ina pointi 19 katika mechi 10 ilizocheza, Jumanne ijayo inatarajiwa kucheza na Mgambo JKT katika muendelezo wa ligi hiyo kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Yanga inashika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo yenye timu 14.

KIIZA AVUA KIATU CHA DHAHABU YANGA, ATAKA UBINGWA



Mshambuliaji wa Yanga, Hamisi Kiiza amesema hana mpango wa kuwania tuzo ya ufungaji bora yaani kiatu cha dhahabu katika Ligi Kuu ya Bara badala yake anajipanga kuhakikisha timu yake inatetea ubingwa wa ligi hiyo.
Kiiza ambaye hadi sasa amefunga mabao saba, ikiwa ni moja nyuma ya Amisi Tambwe wa Simba ambaye hadi sasa ameshafunga mabao manane.
Baada ya kufunga bao moja moja katika mechi dhidi ya Azam, JKT Ruvu na Kagera Sugar, Kiiza alifunga mabao mawili mawili katika mechi dhidi ya Simba na Rhino Rangers.
Akizunguma na mtandao huu jijini Dar es Salaam, Kiiza amesema licha ya kuwa na mabao saab hadi sasa, hana mpango wa kutolea macho nafasi ya ufungaji bora kwani anachofanya sasa ni kufunga mabao kwa ajili ya timu yake ili iweze kutwaa ubingwa.

“Kuwa mfungaji bora bila ya kutwaa ubingwa hakuna maana yoyote, badala yake mimi najipanga kuhakikisha nafunga mabao muhimu yatakayoiwezesha timu yangu kutwaa ubingwa. Ufungaji bora bila ubingwa unakuwa si lolote,” anasema Kiiza.
Kiiza raia wa Uganda amesema anafurahia akicheza na mchezaji yeyote katika nafasi ya ushambuliaji ndani ya Yanga kwani wote hufanya nao mazoezi na ndiyo maana ameweza kufunga akiwa na wachezaji tofauti tofauti.

Yanga ambayo sasa ina pointi 19 katika mechi 10 ilizocheza, Jumanne ijayo inatarajiwa kucheza na Mgambo JKT katika muendelezo wa ligi hiyo kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Yanga inashika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo yenye timu 14.