Search This Blog

Saturday, October 19, 2013

BREAKING NEWS: ADNAN JANUZAJ ASAINI MKATABA WA MIAKA MITANO WA KUENDELEA KUICHEZEA MAN UNITED


Friday, October 18, 2013

NANI MTANI JEMBE YATIKISA MITAA YA JIJI LA DAR

  • Mashabiki wa Simba na Yanga wapagawa
Mashabiki wa Simba na Yanga katika sehemu mbalimbali za jiji la Dar es salaam leo wamepokea kwa kishindo promosheni ya Nani Mtani Jembe inayoendeshwa na bia ya Kilimanjaro Premium Lager nchi nzima kwa siku 75 ili kuleta mwamko katika utani wa jadi kati ya mashabiki hao.
Kampeni hiyo ilipokelewa kwa kishindo baada ya wafanyakazi wanaoitangaza kampeni hiyo wakiwa na msafara wa magari kutembelea maeneo mbalimbali ya jiji hususani yale ambayo ni maarufu kwa kuwa na mashabiki au makundi maarufu ya ushabiki kama vile Wakali wa Terminal, Vuvuzela Tandale, nk pamoja na vijiwe na matawi ya Simba na Yanga na kutoa burudani na maelezo ya kushiriki pamoja na kuitambulisha rasmi mtaani kampeni hiyo ya aina yake.
Baadhi ya wafanyabiashara katika soko la Tandika wilaya ya Temeke walisema kuwa kampeni ya Nani Mtani Jembe imeleta mwamko mkubwa sana katika utani wa jadi uliopo kati ya mashabiki wa Simba na Yanga na pia wanaamini itasaidia kuwaleta karibu zaidi mashabiki pamoja na kuibua mashabiki wapya.
 “Jonathan Assey alisema “Nimeanza kushabikia Yanga tangu nikiwa na miaka 14 lakini sijawahi kuona tukio lolote kubwa la kusisimua namna hii ambalo ni mahususi kwa ajili ya mashabiki, hivyo nawashukuru Kilimanjaro Premium Lager kwa kutukumbuka sisi mashabiki na kutuletea hii kampeni”.
Meneja wa Bia ya hiyo, George Kavishe alisema jana kuwa katika shindano hilo Kilimanjaro inayozidhamini timu za Simba ya Yanga imetenga kiasi cha shilingi milioni 100 na kisha kuzigawanya kwa timu hizo ambapo kila timu inazo shilingi milioni 50 ambazo zinashindaniwa na mashabiki wao.

Kavishe alisema kuwa mashabikiwa Simba na Yanga wanatakiwa kushindana kwa kushiriki kwenye kampeni hiyo ili kuhakikisha kuwa timu mojawapo inapata fedha nyingi zaidi ya timu nyingine.

Akielezea namna ya kushiriki, Kavishe alisema kuwa mpaka kila timu imetengewa shilingi milioni 50 na kuwa mshiriki wa shindano hilo la Nani Mtani Jembe ambaye ni shabiki wa Simba au Yanga anachotakiwa kufanya ni kununua bia ya Kilimanjaro ambayo kwenye kizibo chake kuna namba ya kushiriki.
Alisema baada ya shabiki kununua bia ya Kilimanjaro na kuona namba ya kwenye kizibo, anachotakiwa kufanya ni kuchukua simu yake ya kiganjani na kuandika ujumbe mfupi wa maneno akianza na jina la timu anayoshabikia kisha anaandika namba iliyo kwenye kizibo na kuituma kwenye namba 15440.

Alisema baada ya shabiki kutuma namba hiyo, atakuwa amepunguza shilingi 1,000 kutoka kwa timu pinzani yaani ikiwa shabiki aliyetuma ujumbe huo ni wa Simba atakuwa amefanikiwa kupunguza shilingi 1,000 kutoka kwenye fungu la Yanga na ikiwa shabiki ni wa Yanga pia atakuwa amepunguza shilingi 1,000 kutoka kwa Simba.

Kwa mujibu wa Kavishe matokeo ya uwiano wa fedha zinavyopungua kutoka Simba au Yanga yatangazwa kila siku kuanzia leo Jumatatu hadi siku ya mwisho wa shindano hilo Desemba 14, mwaka huu.

Kavishe alisema kuwa mashabiki watakaoshiriki kwenye shindano hilo kila siku pia watanufaika kwa kuchaguliwa watu 400 watakaokuwa wametuma mara nyingi zaidi ambao pia watazawadiwa shilingi 5000 kila mmoja na kufanya kiasi cha fedha zinazokwenda kwa mashabiki kuwa shilingi milioni mbili kila wiki.
Mashabiki wanaweza kufatilia matokeo kila dakika kupitia tovuti maalum ya Nani Mtani Jembe ambayo ni https://cms.rasello.com/kili.



Mashabiki wa Simba na Yanga wakiwa wanacheza kwa furaha jana wakati wa maandamano maalum yaliyofanywa kuitangaza Nani Mtani Jembe inayoendeshwa na Kilimanjaro Premium Lager kwa mashabiki wa jiji la Dar es salaam. Msafara huo utatembelea maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es salaam kwa siku tatu kuitambulisha kampeni hiyo  na kutoa elimu namna ya kushiriki.


Msafara wa magari yakipita katika Barabara ya Kilwa jijini Dar es Salaam jana kuitangaza kampeni ya Nani Mtani Jembe inayowashindanisha mashabiki wa Simba na Yanga kuzipa shavu timu zao kupitia kampeni hiyo inayoendeshwa na Kilimanjaro Premium Lager. Msafara huo utatembelea maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es salaam kwa siku tatu.
Mbezi Joseph akimvalisha jezi ya Yanga shabiki wa Yanga Anastazia John (80) wa Mabibo nae alijitokeza kupokea msafara huu wa utambulisho wa Nani Mtani Jembe kwa mashabiki wa Dar.

EDO KUMWEMBE AJIUZULU RASMI USEMAJI WA COASTAL UNION.


ADNAN JANUZAJ: ANAMILIKIWA NA MAN UNITED, ANAFUKUZIWA NA ENGLAND...MTOTO WA WAKIMBIZI WA VITA KOSOVO ALIYEZALIWA BELGIUM


Mjadala unaohusu ni nchi gani ambayo Adnan Januzaj anapaswa kuchagua kuichezea umeshika hatamu nchini England kuliko sehemu nyingine yoyote. 


Wiki iliyopita kituo cha TV cha  Albania kilikuwa na mjadala kuhusu nyota huyo wa Manchester United katika kipindi walichokipa jina la Hero or Traitor (Shujaa au Msaliti), kwa mtazamo atakuwa shujaa akiichagua nchi hiyo au msaliti atakapoikacha na kuchagua sehemu nyingine.

Kinda hilo lenye miaka 18 ambaye amepata umaarufu mkubwa hivi karibuni baada ya kufunga mabao mawili ya ushindi wa klabu yake ya Man United, lipo kwenye presha ya kuamua nchi gani achague kuitumikia.

Alizaliwa Brussels - Belgium, Januzaj ni mtoto wa wazazi wa kutoka Kosovo na Albania ambao walikimbia mji wa Balkan-Kosovo kuepeukana na umaskini na ubaguzi wa kidini  ulioleta machafuko., jambo ambalo liliwakumba wanafamilia wengine wa ukoo wa Januzaj. Leo utafahamu historia yao kiundani.

Historia ambayo inaonyesha kwamba Januzaj anaweza kuichezea Belgium, Albania, Kosovo, Turkey au England, na mpaka leo Januzaj hajaweka wazi ni wapi jezi ya taifa gani angependelea kuivaa, hata baba yake Abedin nae amekuwa kimya.  


Wakala wa Januzaj, Dirk de Vriese, amesema hakuna mwanafamilia atakayezungumza lolote mpaka watakaposaini mkataba mpya na United, ingawa bado wapo kwenye mazungumzo huku vilabu vingine vikimtolea macho kinda hilo.

Inadhaniwa kwamba kama Kosovo ingekuwa inatambuliwa na FIFA - basi Januzaj angelichagua taifa hilo, lakini sasa inaaminika England ndio wana nafasi kubwa ya kumtwaa kiungo huyo.

 FA wanaamini hilo linawezekana na wameanza kuangalia kama uwezekano wa kumpatia passport ya UK itapelekea FIFA kubadili kanuni za uraia wa ukazi, inayotoa ruhusa kwa mchezaji aliyekaa ndani ya taifa moja miaka 5 mfululizo kulichezea taifa hilo.......


Januzaj, ni mtoto aliyelelewa kwenye misingi ya imani ya dini ya kiislam, yenye kufuata maadili ya dini hiyo.

Kuanzia kwa walimu wa zamani wa soka mpaka wa shuleni, hakuna kati yao mwenye jambo baya la kumzungumzia kinda hilo wala familia yake.  Hata Anderlecht, klabu ya soka kutoka jijini Brussels ambayo ilimpoteza mchezaji huyo akiwa na miaka 16 kwa kumuuza kwenda United kwa sababu sheria za Belgium zinakataza kuwapa mikataba ya kazi watoto chini ya umri wa miaka 18, bado inamtakia mambo ya kheri kijana huyo.

‘Hatuna furaha tumempoteza mchezaji kwa €300,000, ada ya uhamisho ambayo ilipangwa na FIFA, hivi sasa ana thamani ya   20 million,’ msemaji wa Anderlecht David Steegen alisema.

‘Alizaliwa Brussels, alisoma katika klabu yetu, ni mmoja wetu na inatusikitisha kuona hayupo nasi. Lakini tuna furaha Adnan anafanya vizuri. Ni kijana mzuri.’

Nchini Belgium kuna taarifa kwamba United ililipa kiasi cha ziada cha €200,000 kwa familia ya Januzaj na imewapa nyumba nzuri katika moja ya sehemu nzuri ndani ya jiji la Manchester ambapo mchezaji huyo anaishi na mama na baba yake.

David Steegen, bado anakiri kwamba Anderlecht iliwafanyia klabu ya RWDM Brussels FC kitu ambacho United ilikuja kuwafanyia miaka minne baadae. RWDM ni klabu iliyokuwa ndani ya eneo ambalo familia ya Januzaj ilikuwa ikiishi pembezoni mwa jiji la  Brussels - Mzee Abedin Januzaj alikuwa akimchukua mwanae Adnan na kumpeleka mazoezini baada ya kutoka alipokuwa akifanya kazi katika kampuni ya Chevrolet-Opel dealership ambapo alikuwa akifanya kazi kama mhasibu.

‘Tuliona mapema kwamba Adnan angekuwa mchezaji mzuri,' anasema Jean-Paul Pira, ambaye ndio mwalimu wa timu ya watoto chini ya miaka minne katika klabu ya RWDM. ‘Hakuwa mchezaji mkubwa sana - alikuwa sio mwenye nguvu sana - lakini uwezo wake wa kiufundi ulikuwa hauelezeki, haukuwa wa kawaida. Katika mchezo mmoja wa under 10 nakumbuka alifunga mabao 16 au 17 katika ushindi wa 22-0.'

Pira pia anamkumbuka baba yake Adnan. ‘Siku zote alikuwa mtulivu na mwenye kumsapoti mwanae, lakini hakuwahi kumsifia namna alivyocheza vizuri.’

RWDM FC haikupokea hata senti tano kutoka Anderlecht. ‘Zero!’ alisema Pira. Lakini tena, bado timu hiyo ina mapenzi na Januzaj.

Abdel Jaichi ambaye alikuwa mwalimu wa michezo wa Januzaj katika shule ya Athenee Royal De Jette iliyopo katika kitongoji cha Koekelberg kwa miaka minne ana furaha kubwa na mafanikio ya Januzaj. Alimfundisha Januzaj tangu alipokuwa na miaka 12 mpaka alipohamia Manchester akiwa na miaka 16. 'Alikuwa ni kijana mtulivu mwenye heshima ambaye alikuwa mfano mzuri kwa wenzake. Alikuwa na bidii sana katika masomo na michezo’.

‘Adnan alikuwa mchezaji bora na mwenye kipaji kuliko wenzie shuleni lakini hakuwa mbinafsi,' alisema Jaichi. ‘Alikuwa akicheza na kuwatesa sana mabeki na kujaribu kutumia nafasi alizopata kufunga mabao. Lakini pia hakuwa na shida kwenye masomo yake.’

Sir Alex Ferguson alimzungumzia Januzaj kama ‘a beautifully balanced player’, wakatik kocha wa timu ya vijana ya Anderlecht  - Yannick Ferrera - amemfananisha na Johan Cruyff. Pia imefahamika kwamba amezaliwa siku moja na Cristiano Ronaldo na Neymar: February 5.

Wengi wanasema baba yake Januzaj ndio nguzo kuu ya kipaji hicho, mmojawapo ni mchezaji mwenzie wa Anderlecht Michael Heylen, ambaye kwa sasa yupo Courtrai, alisema: ‘Januzaj ni mchezaji ambaye mwenye kipaji kikubwa ambacho nimewahi kukishuhudia na kucheza nae. Alikuwa na kasi na mwenye uwezo wa kuchambua mabeki na kuwapita.
‘Lakini ikiwa Adnan alipocheza vibaya, baba yake alimuweka chini na kumkosoa na kumuelekeza pamoja na kumtia moyo wa kuongeza juhudi. Muda mwingine alikuwa mkali sana na ungeweza  kumuona Adnan akilia. Lakini nilikuwa najua kwamba Baba yake alikuwa anajua nini anafanya. Alimfundisha mwanae namna ya kupambana na hilo limemsaidia katika kujij


Wakati baba yake Januzaj Abedin alipoichukua familia yake na kukimbia Kosovo, baadhi ya ndugu zake waliingia jeshini kupigania uhuru wao dhidi ya waserbia.

Lakini mpaka sasa mahusiano yao bado ni imara sana, huku kila anapopata mapumziko Januzaj, ambaye anaongea kialbania vizuri sana hutembelea nchi hiyo kwa wiki kadhaa, eneo ambalo lipo katika milima inayotenganisha Kosovo na Serbia pamoja na Montenegro.

Wakati kama huo utamkuta Januzaj akicheza soka na ndugu zake wakiwemo binamu na baba zake wadogo. Lakini ndugu zake hao wanakumbuka maisha magumu waliyopitia wakati vita iliyosababishwa na ubaguzi wa kidini, kikabila baina ya Albania na Kosoro.

Mtoto mkubwa kati familia ya watoto sita, Abedin alikuwa akitegemewa na familia yake baada ya baba yake Idriz, mfanyakazi wa kiwanda cha nguo, kuanza kuumwa ugonjwa wa kansa. Lakini huku kukiwa na uwezekano wa kulazimishwa kujiunga na jeshi liliotawaliwa na waserbia la Yugoslav ili kupigana vita huko Bosnia, Abedin aliamua kuondoka kwenda  Belgium mwaka 1992.

Wakati huo baba yake mdogo Abedin, Januz, tayari alikuwa kashafungwa kwa miaka 15 kwa kushiriki katika harakati za kuomba uhuru kutoka kwa Yugoslavia ambayo sasa ni  Kosovo. Baadae mdogo wake, Shemsedin, alienda kujiunga na Januz katika jeshi la kupigania uhuru wa Albania.

Shemsedin, ambaye kwa sasa hana ajira yoyote akihangaika kwa hali na mali kuisadia familia yake ya mke na watoto wawili, anaeleza namna Abedin alivyokimbia ukandamizi wa Waserbia lakini kutafuta namna atakvyoweza kuisadia familia yao kwa kutuma fedha nyumbani. ‘Baba yangu alifariki miaka miwili baadae hivyo  Abedin akawa ndio kichwa cha familia,' alisema.

Mke wa Abedin na mama yake Adnan, Ganimete Sadikaj, pia alikuwa mmoja ya wahanga wa ukandamizi. Alizaliwa kwenye moja ya familia za kitajiri huko Istog, familia ya Sadikajs ilikuwa inaonekana tishio na utawala wa Yugoslav baada ya vita vya pili vya dunia. Walilazimika kuondoka Kosovo na kwenda kuishi Uturuki. 


Familia hiyo mwishoni ikahamia Belgium ambapo babu yake Adnan, Alija, alikuwa ameanzisha biashara zake huko na hatimaye mama na baba yake Adnan walipokutana na kuanzisha familia na matokeo ndio kinda hili linalotawala vyombo vya habari ulimwenguni.


MBEYA CITY, JKT RUVU UWANJANI VPL




Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inaendelea kutimua vumbo kesho (Oktoba 19 mwaka huu) kwa mechi tano huku Mbeya City ikiikaribisha JKT Ruvu kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Mechi nyingine zitakuwa kati ya Oljoro JKT na Azam (Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha), Mtibwa Sugar na Mgambo Shooting (Uwanja wa Manungu, Turiani), Ashanti United na Ruvu Shooting (Azam Complex Chamazi, Dar es Salaam) na Kagera Sugar dhidi ya Coastal Union (Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba).

Wakati huo huo, Ligiu Daraja la Kwanza (FDL) nayo inaendelea katika viwanja nane kesho (Oktoba 19 mwaka huu) huku Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam ukiwa mwenyeji wa mchezo kati ya African Lyon na Friends Rangers.

Nayo Villa Squad itacheza na Green Warriors katika Uwanja wa Mabatini, Mlandizi, Polisi Morogoro na Kimondo (Uwanja wa Jamhuri, Morogoro), Lipuli na Kurugenzi (Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora mjini Iringa) na Mkamba Rangers dhidi ya Majimaji (Uwanja wa CCM Mkamba, Morogoro).

Toto Africans na Mwadui (Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza), Polisi Dodoma na Polisi Tabora (Uwanja wa Jamhuri, Dodoma), wakati Polisi Mara na pamba zitacheza kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma.

COUNTDOWN TO DAR DERBY: MAGARI MAALUMU TU MECHI YA SIMBA, YANGA



Magari yenye shughuli maalumu tu ndiyo yatakayoruhusiwa kuingia uwanja wakati wa mechi ya Simba na Yanga itakayochezwa keshokutwa (Jumapili) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mechi itaanza saa 10 kamili jioni, na kila timu inaruhusiwa kuingia na magari matatu tu; gari la timu na mengine mawili ya viongozi. Ukaguzi wa kuingia uwanjani ni kwa watu wote, kwani utaratibu huo si wa kumdhalilisha mtu bali lengo lake ni kuhakikisha usalama.

Vilevile watu hawataruhusiwa kuingia uwanjani na mifuko ya aina yoyote ikiwemo mabegi, isipokuwa kwa waandishi wa habari wanaotumia mabegi hayo kwa ajili ya kubebea kamera zao. Pia hakuna wafanyabishara watakaoruhusiwa kufanya biashara katika maeneo yanayozunguka uwanja.

Kwa washabiki watakaokuwa katika mazingira ya kuwa kero kwa wenzao wakiwemo walevi hawataruhusiwa kuingia uwanjani, pamoja na wale wenye silaha kama bastola ambapo wakikamatwa wafikishwa polisi na baadaye kufunguliwa mashtaka kortini.

Barabara ya Uwanja wa Taifa itafungwa kuanzia saa 2 asubuhi upande wa Chang’ombe, hivyo washabiki wanatakiwa kununua tiketi zao mapema kesho (Jumamosi) ambapo zitaanza kuuzwa katika vituo mbalimbali kuanzia saa 4 asubuhi.

Vituo hivyo ni mgahawa wa City Sports Lounge, Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala, Uwanja wa Uhuru, mgahawa wa Brake Point uliopo Kijitonyama na BMM Salon iliyoko Sinza Madukani.

KAMATI YA UCHAGUZI YATANGAZA WAGOMBEA TFF

 Jamal Malinzi-Uraisi


 Athumani Nyamlani-Uraisi

Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imetangaza orodha ya mwisho ya wagombea wa uchaguzi wa TFF na wa Bodi ya Ligi (TPL Board) utakaofanyika baadaye mwezi huu.

Uchaguzi wa Bodi ya TPL utafanyika Oktoba 25 mwaka huu wakati ule wa TFF utafanyika Oktoba 27 mwaka huu. Kampeni kwa ajili ya uchaguzi wa TPL Board na ule wa TFF zimeanza leo (Oktoba 18 mwaka huu)  zitamalizika siku moja kabla ya uchaguzi saa 10 kamili alasiri.

Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Hamidu Mbwezeleni amewataja wagombea kwa upande wa TPL Board kugombea uenyekiti ni Hamad Yahya Juma (Mtibwa Sugar), Makamu Mwenyekiti ni Said Muhammad Said Abeid (Azam). Wanaowania ujumbe wa Bodi ya Uendeshaji ni Kazimoto Miraji Muzo (Pamba) na Omary Khatibu Mwindadi (Mwadui).

Wagombea kwenye uchaguzi wa TFF ni Athuman Jumanne Nyamlani na Jamal Emily Malinzi (Rais), Imani Omari Madega, Ramadhan Omar Nassib na Wallace Karia (Makamu wa Rais).

Kwa upande wa wajumbe wa Kamati ya Utendaji ni Kalilo Samson (Kanda namba 1- Geita na Kagera), Jumbe Odessa Magati, Mugisha Galibona, Samwel Nyalla na Vedastus Lufano (Kanda namba 2- Mara na Mwanza), Epaphra Swai na Mbasha Matutu (Kanda namba 3- Shinyanga na Simiyu).

Ali Mtumwa, Elley Simon Mbise na Omar Walii Ali (Kanda namba 4- Arusha na Manyara), Ahmed Idd Mgoyi na Yusuf Hamis Kitumbo (Kanda namba 5- Kigoma na Tabora), Ayubu Nyaulingo na Blassy Mghube Kiondo (Kanda namba 6- Katavi na Rukwa), Ayoub Shaibu Nyenzi, David Samson Lugenge, John Exavery Kiteve, Lusekelo Elias Mwanjala (Kanda namba 7- Iringa na Mbeya).

James Patrick Mhagama na Stanley William Lugenge (Kanda namba 8- Njombe na Ruvuma), Athuman Kingombe Kambi, Francis Kumba Ndulane na Zafarani Mzee Damoder (Kanda namba 9- Lindi na Mtwara), Hussein Zuberi Mwamba, Stewart Ernest Masima, Charles Komba (Kanda namba 10- Dodoma na Singida), Farid Nahdi, Geofrey Irick Nyange, Juma Abbas Pinto, Riziki Juma Majala) na Twahil Twaha Njoki (Kanda namba 11- Morogoro na Pwani).

Davis Elisa Mosha, Khalid Abdallah Mohamed (Kanda namba 12- Kilimanjaro na Pwani), Alex Crispine Kamuzelya, Kidao Wilfred Mzigama, Muhsin Said Balhabou na Omary Isack Abdulkadir (Kanda namba 13- Dar es Salaam).

Mbwezeleni amewataka wagombea kufanya kampeni bila kukashfu wenzao, kwani Kanuni ya Uchaguzi za TFF toleo la 2013 inatoa fursa kwa Kamati ya Uchaguzi kuwaondoa wagombea wa aina hiyo kwenye uchaguzi.

BREAKING NEWS! HAMIDU MBWEZELENI AMKATA TENA DAUDA UCHAGUZI WA TFF!


MAKALA: HADITHI YA UWANJA SIMBA YAHAMIA YANGA

Na Elius Kambili

MWENYEKITI wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage aliposema hivi karibuni kuwa “Kama serikali imeweza kujenga uwanja wa kisasa (wa taifa) kwa muda wa miaka 50, iweje mimi niweze ndani ya miaka miwili?” alimaanisha uwanja alioahidi kuujenga sasa haiwezekani.

Rage alitoa ahadi hiyo alipoingia madarakani Mei, 2010. Aliahidi kuendeleza mchakato wa ujenzi wa uwanja huo, eneo Bunju, Dar es Salaam.

Lakini kwa kauli hiyo mpya ilimaanisha Simba haiwezi kujenga uwanja wake kwa sasa. Macho na masikio ya wadau wa soka yalielekezwa kwa watani wao Yanga, klabu iliyofikia hatua hata ya kuonyesha michoro ya uwanja na kuunda kamati maalum kwa ajili ya ujenzi huo.

Yanga walikuja na wazo hilo mwaka 2010 kwamba itajenga uwanja wa kisasa katika eneo la Jangwani yalipo makao makuu ya timu hiyo makutano ya mitaa ya Jangwani na Twiga.

Novemba mwaka jana klabu hiyo iliingia mkataba wa awali na kampuni ya Beijing Constructions Engineering Group (T) Limited (BCEG) kuhusu ujenzi wa uwanja wa kisasa.

Katika makubaliano hayo, ujenzi wa uwanja huo ulipangwa kuanza Juni mwaka huu baada ya tathmini mbalimbali kufanyika ikiwezo za kiufundi na kiuchumi. Makubalino hayo ya awali yaliyosainiwa Novemba 23, 2012.

Yanga ilitakiwa kupata na kuwa na eneo la kutosheleza malengo ya mradi, kupata ushauri mzuri, michoro mizuri na mkandarasi mzuri wa mradi na pia kupata na kutenga fedha za kukamilisha usanifu na ujenzi wa mradi.

Kwa upande wa BCEG wajibu wao ni kuwa na utaalamu na uzoefu wa kutosha. BCEG ikafanya tathmini na kuchora ramani ya ujenzi wa uwanja huo. Kazi hiyo ilikamilika Aprili mwaka huu yaani miezi mitatu kabla ya kuanza kwa ujenzi wa uwanja huo. BCEG ilikabidhi ramani tatu kwa Yanga ili wachague moja tu.

Wakati akikabidhi ramani za ujenzi wa uwanja huo, Meneja Msaidizi wa BCEG, David Zhang Chengwei aliweka wazi kwamba, ni jukumu la Yanga kuamua aina ya uwanja inaouhitaji, kulingana na uwezo wao wa kipesa, ingawa vyote ni vya kisasa.

Gharama za ujenzi wa uwanja A ilielezwa ni dola milioni 50, pamoja na ofisi, ukumbi wa mikutano, maduka, maegesho na sehemu ya mazoezi (gym). Uwanja B gharama zake ni dola milioni 40, huku ule C gharama zikiwa ni dola milioni 30, ingawa vyote vina mahitaji muhimu.

Kwa mujibu wa ramani hizo, Uwanja A ambao ni wa kufunikwa juu, utakuwa na uwezo wa kubeba watazamaji 50,000, Uwanja B watazamaji 40,000, na Uwanja C utakaokuwa umefunikwa jukwaa kuu pekee utaingiza watazamaji 30,000 walioketi.

Yanga ina kiwanja chenye ukubwa wa heka 3.59 eneo la Jangwani. Kiwanja hiki kina hati miliki kwa miaka 99 toka mwaka 1972 na katika eneo hilo, klabu ilifanikiwa kujenga uwanja wa mpira wa Kaunda na Jengo la klabu la ghorofa tatu.

Jengo hilo lilijengwa kwa ufadhili mkubwa wa Rais wa Kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani Karume na michango ya wanachama na wapenzi wa klabu. Kwa kutambua udogo wa eneo lake, Novemba mwaka jana klabu hiyo iliandika barua kwa Manispaa ya Ilala na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ili kuomba nyongeza ya eneo.

Mjumbe wa Bodi ya Wadhamini Yanga, ambaye pia mwenyekiti wa kamati ya ujenzi wa uwanja huo, Francis Kifukwe Septemba 30 mwaka huu aliomba msaada kwa mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam juu ya suala hilo baada ya kuona barua hizo hazijajibiwa.

Kifukwe pia alionyesha ramani kwa waandishi wa habari kwa kusema ndani ya eneo la heka tatu la Yanga, kuna kipande cha eneo hilo kilichoingiliwa na wananchi. Wananchi hao wavamizi wanatakiwa kuhama ili kutoa nafasi ya ujenzi huo. Yanga imechagua kujenga uwanja B utakaoweza kubeba watazamaji 40,000.

Ukitazama hapo kuna maswali mengi ambayo majibu yake ni kizungumkuti kwani ukianza na hoja ya kuongeza eneo inaonekana wazi utata utatawala kwani bado wizara haionekani kuwa na jibu zuri kwa Yanga kupewa eneo la ziada kutoka viwanja vya wazi vya Jangawani. Pia kuna ugumu wa kuwaondoa watu wanaodaiwa kuvamia uwanja wa Yanga.

Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali, mamlaka husika ilionekana hazikuwa na taarifa na barua zilizoandikwa na Yanga kuhusu ongezeko la eneo lakini kitendo cha Kifukwe kukataa kusema njia mbadala ya ujenzi huo kama maombi yao yatagonga mwamba ni kama anasema uwanja huo hauwezi kujengwa.

Kifukwe alishindwa kueleza ‘plan B’ ya Yanga wasipopata eneo la nyongeza; pia hakuweka wazi zitakapopatikana dola milioni 40 kwa ujenzi huku tayari kukiwa na taarifa kwamba benki mbalimbali zina wasiwasi wa kukopesha klabu za Simba na Yanga kwa kuogopa kupoteza wateja.

Benki zinaogopa kupoteza wateja endapo Yanga au Simba zitashindwa kulipa mikopo na mali zao kupigwa mnada huku wateja wao wakiwa miongoni mwa wanachama wa klabu hizo.

Pia eneo la Jangwani ni bonde kubwa huku eneo la Yanga likianzia eneo la juu, hivyo tuta linalosemwa na Kifukwe kwamba litawekwa linaweza kuwa la kihistoria Afrika Mashariki na Kati.

Mwisho

'' KAMA RIHANNA AKINITAKA SIWEZI KUMKATAA''- DANIEL STURRIDGE

Mshambuliaji wa klabu ya Liverpool Daniel Sturridge amefichua hisia zake kwa nyota wa muziki wa Pop Rihanna . Katika Interview moja aliyoifanya kwenye jarida la rapa wa marekani Jay Z, Sturridge alizungumzia usajili wake toka Chelsea kwenda Liverpool na pia maisha yake ya Mapenzi na zaidi alizungumza kumhusu Rihanna . Soma maneno yake hapa.
 http://www.soccerreport.com/sturridge-i-wouldnt-say-no-to-rihanna/

COUNTDOWN DAR DERBY: NAIPENDA SIMBA, SHABIKI WA YANGA NA BARAKA MBOLEMBOLE



 Baraka Mbolembole 
Vinara wa ligi kuu Tanzania Bara, Simba SC watakuwa uwanjani siku ya jumapili ijayo katika uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuwakabili mabingwa watetezi na mahasimu wao wa soka nchini Yanga SC, katika mchezo wa raundi ya tisa. Timu zote zinatumia uwanja wa Taifa kama uwanja wao wa nyumbani, ila katika mchezo ujao Yanga watakuwa wageni, na Simba watakuwa timu mwenyeji.
Simba wapo juu ya Yanga kwa tofauiti ya pointi tatu, na wanaweza kuongeza pengo hadi kufikia tofauti ya pointi sita ebdapo watapata ushindi. Katika michezo nane iliyopita, Simba imekusanya pointi 18, huku wapinzani wao wakiwa na pointi 15 katika nafasi ya nne ya msimamo.
         ZILIPOTOKA
Simba iliifuinga timu ya Tanzania Prisons wiki iliyopita kwa bao 1-0, wakati mahasimu wao Yanga walipata ushindi wa ugenini dhidi ya Kagera Sugar, mjini Bukoba waliposhinda kwa mabao 2-1.
          OKTOBA 20
Yanga wanapewa nafasi kubwa ya ushindi katika mchezo huo kwa kulinganisha aina ya wachezaji wa pande zote mbili na kuwachambua katika makaratasi. Kwa ubora wa mtazamo Yanga wnaoneka kuwa na pointi katika hili, kwa kuwa wamekuanya wachezaji ' wa bei mbaya' katika kikosi chao ukilinganisha na wale wa Simba. Lakini hiko si kigezo sahihi cha kuwapa ' pointi' mbele ya Simba, ukizingatia tayari walionja radha ya kichapo waluipocheza na Azam FC, huku Simba wakifanya vizuri na kuwa timu ambayo haijapoteza mchezo wowote hadi sasa.
        MBINU ZA MCHEZO
Mara zote Simba wamekuwa watala wa eneo la katikati ya uwanja, pindi wakicheza na Yanga. Wana wachezaji ambao wanaweza kucheza katika mfumo wa 4-4-2, au ule wa 4-3-3 kwa usahihi, mifumo hii imekuwa ni mizuri kwao katika michezo ya ' DAR- PACHA' kwa kipindi kirefu sasa. Ila kuelekea mchezo wa jumapili hii inaonekana kuna hatari ya timu hiyo ' kupotea' mchezoni na kutoa utawala kwa timu ya Yanga ambayo pia inauwezo wa kusoma mifumo ya timu pinzani na kuivuruga wakitumia wachezaji wao wa ' kazi'
Kocha wa Simba, Abdallah Kibadeni kwa wiki nzima amekuwa akijinasibu kwa atashinda, wakati yule wa Yanga, Ernest Brandts amekuwa bize kuhakikisha wachezaji wao wanaongeza kiwango chao cha uchezaji, umakini, na nidhamu. Kumekuwa na tetesi kuwa makocha Kibadeni na msaidizi wake Jamhuri Kiwelo, kuingia katika tofauti na baadhi ya wachezaji wa timu yao.
Ila sikupendezwa na namna alivyokuwa bize kuongelea mambo hayo nje ya timu, makocha hao hawakujali ni sehemu gani nzuri ya kukaa na kuzungumzia mambo yao ya ndani, ilikuwa ni kazi ya msemaji wao Ezekiel Kamwaga kukanusha au kukubali kuhusiana na habari za kuwepo kwa ugomvi kati ya kocha na baadhi ya wachezaji muhimu. Wakati muda umekaribia kufika na kila kitu kuwa hadharani, makocha hao watakuwa wakikuna vichwa na kutazama ni namna gani wanaweza kuleta ' heshima'.
Nassoro Masoud, Issa Rashid hawa watakuwa walinzi wa pembeni wa Simba katika mchezo huo, japo anaweza kuingia Haruna Shamte upande wa kushoto kama, Kibadeni ataamua kucheza kamari ili kujaribu kuwadhibiti washambuliaji wa pembeni wa Yanga, Mrisho Ngassa na Saimon Msuva.
Yanga wana kawaida yao ya kuimaliza mechi yoyote ngumu wakitokea pembeni ya uwanja, Ngassa ni mchezaji mjanja, mnyumbulifu, ana kasi, chenga, na maarifa ya kufunga ama kutoa pasi, na uwepo wa Msuva upande mwingine wa uwanja naona kabisa kulikuwepo na fasi ya Henrry Joseph katika eneo la kiungo la Simba. Jonas Mkude ni kiungo mzuri sikatai ila bado ana mengi ya kujifunza ili kuingia katika kundi la viungo bora nchini, ana shambulia vizuri, ndiyo maana tayari ana mabao matatu katika michezo saba aliyocheza, ila si mzuri katika kucheza mipita ya ' tackling' . Hivyo uwepo wa Joseph ambaye ni mzuri katika vyote hivyo vingeweza kumfanya Mkude kuwa na nguvu ya kuisukuma timu mbele na ,kuicheza huku wakiwa na jukumu la kuwasaidia walinzi wao wa pembeni wakati wakiwa wanashambuliwa.
Mtu, mwingine muhimu kwa Simba katika eneo hili la kati ni Amri Kiemba, alicheza vibaya katika mchezo wa mwisho wa watano hao wa jadi, Mei 18, mwaka huu na katika siku za karibuni amekuwa akionesha kiwango cha chini. Kiemba amecheza michezo nane ya timu yake na hajafunga bao lolote kitu ambacho kilimfanya kocha wake kumuweka benchi katika mchezo uliopita. Ila anaweza kucheza vizuri siku ya jumapili na kuisadia Simba kwa kuwa Simba hadi sasa haina mbadala wa nafasi yake. Mechi ambazo Kiemba ameshindwa kuongoza eneo la kiungo Simba ilibaki ikimtegemea Haruna Chanongo, na hapo wakawa wanacheza na kutegemea upande wao wa kulia ili kupata mabao, bila shaka Chanongo anaweza kumsumbua mlinzi wa kushoto wa  Yanga David Luhende ila na wasiwasi kuwa anaweza kutumia muda mwingi kumsadia Chollo ili kumzima Ngassa, kama Yanga wataongoza mchezo.
Kiemba, anauwezo wa kukaa na mpira na kupiga pasi nzuri za mwisho huku rekodi yake ya ufungaji ikiwa ni nzuri pia Simba inaweza kunufaika na vitu alivyo navyo na kujaribu kuwazima ' viungo- wahamasishaji' Athuman Idd ' Chiji' na Haruna Niyonzima, ambao waliweza kutawa eneo la katikati. Yanga hawana safu kali sana ya mashambulizi, ila wana washambuliaji wa ' mechi kubwa', Hamis Kizza na Didier Kavumbagu wanaweza kuwaumiza kwa mara nyingi Simba endapo watarusu krosi, na pasi za kunyeza, sina shaka na uwezo wa Joseph Owino, huyu ni mlinzi kiongozi wa wenzake mchezo, ila uwepo wa washambuliaji wenye kariba ya Kizza na Kavu, utakuwa mtihani mkubwa kwao. Wanaweza kuibuka muda wowote mchezo na kuimaliza mechi kama walivyofanya Mei 18
Amis Tambwe, Chanongo kwa pamoja wamefunga mabao 11 katika michezo nane iliyopita, mabao manne pungufu yaliyofungwa na timu ya Yanga. Tambwe amekua akinufaika na uwepo wa Bertam Mombeki ambaye amekuwa akiwapa wakati mgumu walinzi wa timu pinzani, Mombeki hutumia umbo lake kumiliki kila mpira unaopigwa katika eneo lao, ni mzuri kwa mipira ya chini na ni hatari zaidi kwa ile ya juu, Tambwe yeye amekuwa ni bingwa wa kukaa katika maeneo ya hatari na kutumia kila nafasi anayoipata kwa umakini mkubwa, ni mzuri katika mipira ya ' kuunganisha', ana jua ni wapi goli lilipo, ila mara zote hutegemea timu yake kucheza na kuongoza mchezo. Endapo Simba watamili mchezo Tambwe atafunga mara mbili, kwa kuwa sijaona bado ubora wa sasa wa Nadir Haroub na Kelvin Yondan, bado wapo katika kujiweka sawa na wamekuwa wakipoteana mara kwa mara, ila Mbuyu Twite anaweza kuwasaidia kwa kuwasogeza Simba nyuma ili kuwafanya wawe bize na kukaba.
   NANI MSHINDI

Abel Dhaira na Ally Mustapha wote wameonesha udhaifu katika maeneo yao, Dhaira amefungwa mabao matano na Mustapha amefungwa nane. Kushina au kufungwa kwa timu zao kutagemea na kikla mmoja kupandisha kiwango chake cha uchezaji wa mipira iliyokufa, ushapu wa kuzungumza na kuitokea mipira. Atayayekuwa anatematema sana bila shaka ataimamiha timu yake. Naipenda Simba, Shabiki wa Yanga.....Dakika tisini za kukumbwa ' Mimi naikumbuka ile ya marehemu Mutesa, akiaina fulani ya muziki katika moja ya kona za uwanja wa Taifa huku akionesha ishara ya mkono juu'

   0714 08 43 08