Search This Blog

Saturday, March 9, 2013

LIVE MATCH CENTRE: YANGA 1 - 0 TOTO AFRICA FULL TIME







Dk 90+4 FULL TIME. YANGA 1-0 TOTO

Dk 90 Toto imefanya mabadiliko ametoka Musa Musa, ameingia Simba Boaz.

Dk 88 Kiiza anafunga bao lakini mwamuzi anakataa kwa kuwa ni off side.

Dk 85 Kiiza anaonekana anataka kufunga tu, kila mpira anaoupata hatulii nao anaupiga langoni kwa Toto.

Dk 82 Kiiza anakosa bao la wazi akiwa amebaki peke yake na kipa wa Toto.

Dk 78 GOOOO....! Nizar Khalfan anaipatia Yanga bao la kwanza akiunganisha krosi ya Kiiza. Mpira uliopigwa na Nizar ulimparaza kipa wa Toto, Ngwegwe na kutinga wavuni. YANGA 1-0 TOTO.

Dk 74 Kavumbagu anaonyeshwa kadi ya njano baada ya kumchezea vibaya Swita wa Toto. YANGA 0-0 TOTO

Dk 73 Yanga imefanya mabadiliko, ametoka Godfrey Taita ameingia Didier Kavumbagu.

Dk 67 RED CARD...! Eric Mlilo wa Toto anaonyeshwa kadi nyekundu baada ya kumchezea vibaya Msuva. Mlilo alikuwa na kadi ya njano awali, hivyo mwamuzi amemwonyesha kadi ya njano kisha nyekundu.

Dk 64 Yanga inafanya mabadiliko, ametoka Tegete ameingia Nizar Khalfan.

Dk 62 Toto imefanya mabadiliko, ametoka Chika Olugbe, ameingia Simba Boaz.

Dk 60 Toto imefanya mabadiliko, ametoka Severine Constantine, ameingia Heri Mohamed.

Dk 57 Msuva anakosa bao baada ya mpira wa kichwa alioupiga akiunga krosi ya Kiiza, kudakwa na kipa wa Toto, Eric Ngwegwe.

Dk 53 Mshika kibendera Abdallah Mkomwa wa Pwani anaipa Yanga penalti baada ya Msuva kupambana na beki Eric Kyaruzi wa Toto. Mwamuzi Andrew Shamba ameikataa penalti kwa kile kinachooneka kwamba beki wa Toto alicheza mpira na hakumgusa Msuva.

Dk 51 Jerry Tegete wa Yanga anakosa bao la wazi akishindwa kuunga vyema krosi ya Kiiza.

Dk 49 Katika kiungo leo hapa uwanjani kuna mchuano mkali kati ya Swita wa Toto na Niyonzima wa Yanga. YANGA 0-0 TOTO.

Dk 46 Hamis Kiiza anakosa bao la wazi baada ya kupewa pasi nzuri na Frank Domayo. Kiiza raia wa Uganda anajiangusha na kushindwa kupiga mpira.

Dk 45 KIPINDI CHA PILI KIMEANZA.

Dk 45 HALF TIME. YANGA 0-0 TOTO.

Dk 43 Swita wa Toto anamchezea rafu Haruna Niyonziama wa Yanga na anaonyeshwa kadi ya njano. Niyonzima anamvamia Swita baada ya kukerwa na rafu hiyo. Swita amewahi kuichezea Yanga.

Dk 39 Beki wa Toto, Evarist Maganga anagongana na Hamisi Kiiza wa Yanga na kuumia. Anatibiwa na kuendelea na mchezo.

Dk 33 Mbuyu Twite wa Yanga anayecheza kama beki wa kati leo, anamchezea vibaya Emmanuel Swita wa Toto.

Dk 30 Simon Msuva wa Yanga anapoteza mpira jirani na lango lake, Hamis Msafiri wa Toto anaunasa mpira na kupiga shuti kali linalotoka nje kidogo ya lango la Yanga.

Dk 25 Mpira ni kawaida mno, kila timu zinafanya makosa mepesi hasa wachezaji kupoteza mipira na pasi nyingi hazina macho.

Dk 20 David Luhende wa Yanga anamchezea rafu Musa Musa wa Toto. YANGA 0-0 TOTO

Dk 16 Hamis Kiiza anaifungia Yanga bao la kichwa akiunga krosi ya Godfrey Taita, lakini mwamuzi Andrew Shamba wa Pwani anakataa kwa kuwa mfungaji alimchezea vibaya kipa kabla ya kufunga.

Dk 7 Eric Mlilo wa Toto anamchezea rafu David Luhende wa Yanga.

Dk 5 Mpira bado haujatulia lakini Toto African ndiyo waliofika mara nne langoni kwa Yanga. Yanga imefika mara mbili langoni kwa Toto.

Dk 2 Uwanjani kuna mvua, mashabiki ni wachache na pitch inatereza kiasi japokuwa hali ya uwanja ni nzuri.

00 MPIRA UMEANZA!

Young Africans line-up to face Toto Africans today:
1.Ally Mustafa
2.Godfrey Taita
3.David Luhende
4.Mbuyu Twite
5.Kelvin Yondani
6.Athumani Idd
7.Saimon Msuva
8.Frank Domayo
9.Jerson Tegete
10.Hamis Kiiza
11.Haruna Niyonzima

Subs:
1.Said Mohamed
2.Shadrack Nsajigwa
3.Oscar Joshua
4.Omega Seme
5.Nizar Khalfani
6.Said Bahanuzi
7.Didier Kavumbagu

Toto Line Up: Eric Ngwegwe, Eric Mlilo, Robert Magadula (C), Eric Kyaruzi, Evarist Maganga, Hamis Msafiri, Severine Constantine, Emmanuel Swita, Chika Olugbe, Musa Musa na Mohamed Jingo.

Friday, March 8, 2013

IMEFAHAMIKA ALIYEMUWEKEA MALINZI PINGAMIZI UCHAGUZI WA TFF AMESOMA NA NYAMLANI NA MWENYEKITI WA KAMATI RUFAA ALIYEMUENGUA MALINZI


MGOMBEA nafasi ya urais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Athumani Nyamlani, Mwenyekiti wa Kamati ya Rufaa ya uchaguzi wa shirikisho hilo, Idd Mtiginjola pamoja na Agape Fue, wote ni wahitimu wa sheria kutoka Chuo Kikuu cha Tumaini Iringa, imefahamika.
Fue alitikisa duru za soka hapa nchini baada ya kumwekea pingamizi mgombea wa nafasi ya urais wa shirikisho hilo, Jamal Malinzi. Hata hivyo alipoulizwa kuhusu hilo, Mtiginjola alicheka kabla ya kukubali na kusema: "Kwani kuna tatizo gani, mbona hamniulizi kuhusu Wambura (Michael) ambaye niliwahi kusoma naye Mzumbe?"
Alisema vyuo vikuu nchini vinajulikana na kwamba ni ujinga na upuuzi kuzungumzia suala la yeye kusoma na mtu kwani mwenye akili timamu anajadili hoja na si mtu.
"Ni upuuzi kujadili watu, tujadili hoja iliyopo mezani, ukishaanza na hoja za aina hiyo hoja itakayofuata itakuwa ni ya ukabila, utahoji mbona huyu na huyu Wahaya, kitaaluma hiyo si sahihi,'' alisema.
Pamoja na kuweka pingamizi hilo Fue, aliyepata shahada ya Sheria ya Chuo Kikuu cha Tumaini Iringa mwaka 2005, alishindwa kutokea siku aliyotakiwa kuthibitisha pingamizi lake kwa Malinzi mbele ya kamati uchaguzi.
Kwa mujibu wa kanuni za uchaguzi wa TFF, mkata rufaa akishindwa kutokea basi pingamizi lake huwa batili.
Hata hivyo, Mwenyekiti wa Kamati ya Rufaa, Mtiginjola ambaye alisoma pamoja na Fue katika Chuo cha Tumaini na kumaliza naye mwaka 2005 aliamua kutumia rufaa hiyo kumwengua Malinzi kwenye kinyang'anyiro.
Kuenguliwa kwa Malinzi kulimfanya Athuman Nyamlani, ambaye pia alisoma shahada ya sheria Chuo Kikuu cha Tumaini Iringa, lakini akimaliza kabla ya Fue na Mtiginjolo kuwa mgombea pekee kwenye nafasi ya urais kitendo kilichozua mzozo mkubwa kutoka kwa wadau wa soka nchini.
Uchaguzi wa TFF ulipangwa kufanyika Februari 24 mwaka huu, lakini ukaahirishwa kutokana na Fifa kuingilia kati kabla ya Serikali kuifuata katiba mpya ya TFF iliyokuwa itumike kwenye uchaguzi huo.a

BAADA YA KUVURUNDA LIGI KUU: KOCHA WA JKT AJIUZULU

KOCHA wa JKT Ruvu, Charles Kilinda ametangaza rasmi kujiuzulu kukinoa kikosi cha timu hiyo kutokana na kutofanya vizuri kwenye mechi zake za Ligi Kuu Tanzania Bara.
Kilinda amechukua uamuzi huo, baada ya timu hiyo, kufungwa mabao 2-0 na Kagera Sugar katika mchezo wa ligi uliopigwa Uwanja wa Azam, Chamazi juzi Alhamisi.
"Nafikiri ni muda mwafaka kuchukua uamuzi mgumu, kijiuzulu ili kuinusuru timu."
"Binafsi kwa uelewa wangu timu inapopata matokeo mabaya, kocha ndiye anayepaswa kuwajibika."
"Kwa hiyo nimeona ni vema na haki kuachia ngazi aje mtu mwingine kuokoa jahazi." alisema Kilinda ambaye amekinoa kikosi cha JKT Ruvu kwa miaka sita tangu 2007/13.
Kocha huyo alisema, baada ya kutangaza rasmi kujiuzulu kinachofuata kwa sasa ni kuandika barua uongozi wa timu kuthibitisha hilo.
"Najua kwa sasa watakuwa wanasikia habari hizi kwenye vyombo vya habari. Barua nitaiwakilisha wakati wowote kuanzia sasa." alisema Kilinda.


WACHEZAJI;
"Taarifa tumezipata. Kila mtu amesikitika. Binafsi nimeumia sana. Kocha alikuwa mtu mkarimu na mwenye upendo na kila mtu pasipo kubagua."
"Kubwa ambalo amelitamka kujiuzulu kwake ni matokeo mabaya ya timu." alisema Amosi Mgisa ambaye ni mshambuliaji wa JKT Ruvu.
'Nafikiri tunapaswa kuheshimu uamuzi wake. Ndilo suala ambalo limebaki kwa sasa."
"Kila mtu ameguswa na kueleza jinsi alivyopokea taarifa hizo. Lakini kwa sasa nafikiri ni wakati kuweka nguvu pamoja na kushinda mechi zilizosalia." alisema nahodha wa timu, Hussein Bunu.
Kabla ya Kilinda kubwaga manyanga aliwahi kutamka tangu ameanza kazi ya kufunda soka hakuwahi kuwa na msimu mbaya wa ligi kama huu.
JKT Ruvu ina pointi 19 sawa na mechi ambazo imecheza na kujiweka katika nafasi ya nne kutoka mkiani.
Maafande hao wanalazika kushinda mechi saba zilizobaki na kufikisha pointi 40 ambazo haziwezi kufikiwa na timu tatu za mwisho, African Lyon, Toto African na Polisi Moro.

SALUM MACHAKU: NASHANGAZWA NA SIMBA INAVYOFANYA VIBAYA

WINGA wa zamani wa Simba, Salum Machaku amesema anashangazwa na timu hiyo kufanya vibaya kwenye michezo yake mbalimbali hivi karibuni.
Machaku anayechezea Polisi Morogoro alisema Simba ina kikosi kizuri na benchi la ufundi limejaa watu makini, lakini wanashindwa kufanya vizuri.
"Sidhani kama benchi la ufundi ni baya kiasi hicho, labda kuna matatizo mengi ya ndani yanayoichanganya Simba.
Machaku ambaye akutaka kuzungumzia kwa undani juu ya hali ya klabu yake zamani, lakini anaamini kocha Mfaransa Patrick Liewing ni moja wa makocha bora ni hivyo anatakiwa kupewa nafasi zaidi kwenye kukinoa kikosi hicho.
Akizungumzia kikosi chake cha Polisi Morogoro winga huyo alisema kinachotakiwa sasa ni kuhakikisha wanashinda kila mechi ili waweze kujiweka katika mazingira mazuri ya kutoshuka daraja msimu huu.

HII NDIO MIFUMO YA TIMU ZOTE ZA LIGI KUU NA NA SABABU KWANINI MAKOCHA WANAITUMIA


KILA kocha wa soka ana falsafa yake ya ufundishaji, lengo likiwa kushinda kila mechi na kufikia malengo ambayo amejiwekea.

Pia, katika soka kuna mifumo mingi na tofauti ya uchezaji ambayo huendana sana na aina ya wachezaji wa timu husika.

Baadhi ya mifumo ambayo imezoeleka katika soka la sasa ni 4:4:2, 4:3:3 na 4:5:2.

Makala haya yanakuchambulia timu zote 14 zinashiriki Ligi Kuu Tanzania Bara na mifumo yake.

YANGA SC

Mfumo; 4:4:2
YANGA hucheza mfumo wa 4-4-2, lakini Mholanzi Ernie Brandts amekiri kuwa mambo yanapokuwa magumu hubadilika na kucheza 4-3-3.

"Kwa kawaida huwa tunacheza 4-4-2. Lakini mambo yanapoharibika tunalazimika kutumia fomesheni ya 4-3-3." Brandts anaeleza kuwa anapotumia mfumo wa 4-3-3 hushambulia zaidi kutokana nakucheza na washambuliaji watatu ambao ni Jerry Tegete, Said Bahanuzi na Himis Kiiza.

"Wakati tunapokuwa kwenye mfumo wetu wa 4-4-2 tunafanya yote kwa pamoja. Kushambulia na vile vile kujihami kufungwa kirahisi." anasema kocha huyo aliyevaa viatu vya Mbelgiji Tom Saintfiet aliyetupiwa virago na Yanga.

SIMBA SC

Mfumo; 4:3:3
MFARANSA Patrick Liewig ameeleza kuwa tangu ametua na kuanza kazi ya kukinoa kikosi cha Simba akichukua mikoba ya Mserbia Milovan Cirkovic ameona mfumo 4-3-3 ndio ambao Simba wameonyesha kufiti tofauti na 4-4-2.

"Nilipokabidhiwa timu nilijaribu kutumia mifumo tofauti. Lakini nafikiri 4-3-3 ni bora zaidi kwetu." anasema kocha huyo. Liewig anafafanua kuwa aina ya wachezaji ambayo wanaunda kikosi cha Simba ni sahihi kucheza mfumo wa 4-3-3 kuliko 4-4-2.

AZAM FC

Mfumo;4:3:3
MWINGEREZA Stewart Hall ambaye ni kocha mkuu wa timu hiyo amefichua kuwa hucheza 4-3-3, ingawa wakati mwingine hubadilika na kutumia 4-4-2.

"Mara kwa mara tunacheza 4-3-3, lakini wakati mwingine tunapaswa kubadilika kutokana na mpinzani wetu anavyocheza."

Stewart anaeleza kuwa anapobadilisha fomesheni hucheza 4-4-2.

"Kwa aina ya wachezaji ambao ninao kwa sasa, nafikiri mfumo sahihi kwetu kucheza ni 4-3-3." anasema kocha huyo aliyetemwa na kurejeshwa kwa

mara nyingine kukinoa kikosi hicho.

MTIBWA SUGAR

Mfumo; 4:5:1
MECKY Maxime ambaye ni kocha mkuu wa Mtibwa anasema hutumia mfumo wa 4:5:1, lakini wakati mwingine hubadilika na kucheza 4:3:2:1.

Mchezaji huyo wa zamani wa Mtibwa na Taifa Stars anaeleza kuwa lengo la kucheza 4-3-2-1 ni kutanua uwanja na kufanya mashambulizi mengi kusaka ushindi.

"Mara nyingi tunavyotumia mfumo wa 4-5-1. Tayari tumeshinda kwa hiyo tunataka kulinda ushindi wetu na kumiliki mpira." anasema kocha huyo.

COASTAL UNION

Mfumo; 4:3:3
KOCHA Mkuu, Hemed Morocco anasema hutumia mfumo 4-3-3 kwa lengo la kutanua Uwanja na kufanya mashambulizi yake kupitisha mipira pembeni ya uwanja.

"Nafikiri timu ambazo zinafanya vizuri duniani kwa sasa zinatumia zaidi mawinga wake kutengeneza ushindi. Pia, kwa aina ya wachezaji ambao ninao, nafikiri nalazimika kucheza 4-3-3." anasema Morocco aliyerithi mikoba ya Juma Mgunda aliyejiuzulu kukinoa kikosi hicho kwa shinikizo la wanachama na mashabiki wa mabingwa hao wa Ligi Kuu Bara 1988.

Coastal inawatumia mawinga wake wawili, Daniel Lyanga na Seleiman Kassim 'Selembe' ambao wana uwezo mkubwa pia wakufunga mabao.

JKT RUVU

Mfumo; 3:5:2
NI moja kati ya timu ambazo zinasifika kwa soka la pasi fupi na kushambulia kama nyuki. Soka la JKT Ruvu halitofautiani sana na la Kagera Sugar.

Kocha Charles Kilinda anasema hana mfumo maalum wakutumia isipokuwa hutegemea na timu ambayo anakabiliana nayo.

"Sina mfumo maalum wakutumia isipokuwa nacheza kulingana na mpinzani wangu anavyocheza na aina ya wachezaji wake."

Kilinda anafafanua kuwa mara nyingi hutumia mfumo wa 3-5-2, Pia, wakati mwingine hubadilika na kucheza 4-4-2.

KAGERA SUGAR

Mfumo; 4:4:2
MRANGE Kabange ambaye ni kocha msaidizi wa Kagera Sugar anasema kwa kipindi kirefu wamekuwa wakitumia mfumo wa 4-4-2.

"Ni mfumo ambao wachezaji wetu wameonyesha kuushika vizuri na kumudu tofauti na mifumo mingine tunapojaribu kucheza." anasema kocha huyo.

Kabange anafafanua maana ya kucheza mfumo huo ni timu iweze kucheza soka la pasi fupi.

"Falsafa yetu ni kucheza soka la pasi fupi. Kwa maana hiyo lazima tucheze tukiwa karibu. Mipira ya juu kwetu mwiko." anasisitiza.

RUVU SHOOTING

Mfumo; 4:5:1
KOCHA mkuu, Boniface Mkwasa anasema lengo lake kutumia mfumo huo ni kuiteka sehemu ya katikati ya Uwanja.

"Falsafa yangu kubwa ni kucheza na viungo watano katikati ya uwanja."

Mkwasa anasema anaamini akiweza kutawala sehemu ya kiungo inakuwa kazi rahisi kwa timu yake kujenga mashambulizi ya kusaka ushindi. Pia, anasema inapotokea timu yake imebanwa hubadilisha mfumo na kucheza 4-4-2.

OLJORO JKT

Mfumo; 4:2:3:1
KATIBU wa Oljoro, Alex Mwamgaya ambaye kwa sasa anashirikiana na kocha msaidizi, Fikiri Edward kukinoa kikosi hicho anasema timu hiyo anatumia mfumo wa 4-2-3-1.

"Nafikiri mfumo ambao tunatumia ni kwa ajili ya kujihami na vile vile kushambulia."

Mwamgaya anaeleza kuwa mabeki wanne na viungo wawili wakabaji kazi yao kubwa ni kuhakikisha timu hairuhusu bao kirahisi.

Anasema kazi ya viungo watatu ni kuunganisha timu kutoka nyuma na kwenda mbele kushambuliaji.

"Majukumu yao ni mawili, kutengeneza nafasi za kufunga na pia kufunga inapotokea nafasi."

TANZANIA PRISONS

Mfumo; 4:2:3:1
KOCHA mkuu, Jumanne Chale aliyeinoa African Lyon msimu uliopita, anasema wacheza mfumo wa 4-2-3-1.

"Lengo letu ni kuhakikisha hatufungwi kirahisi. Pia tunashambulia." Chale aliyerithi mikoba ya Stephen Matata aliyeipandisha timu hiyo Ligi Kuu msimu huu anaeleza kuwa mara nyingine hubadilika kutokana na timu anayokabiliana nayo.

"Wakati mwingine tulazimika kubadilika kulingana na mpinzani wetu."

Anasema anavyobadilika hucheza 4-4-2 na mara nyingine 4-3-3.

MGAMBO JKT

Mfumo; 5:3:2
KOCHA mkuu, Mohamed Kampira aliyerithi mikoba ya Stephen Matata anasema anatumia mfumo wa 5-3-2.
"Silaha yetu kubwa ni kushambulia na kurudi nyuma kwa pamoja kujilinda."

Kampira anaeleza kuwa lengo la kutumia fomesheni hiyo ni wasifungwe kirahisi, lakini timu yake ishambulie.

TOTO AFRICAN

Mfumo; 4:4:2
TANGU Toto imeanza kushiriki Ligi Kuu misimu mitatu iliyopita imekuwa ikitumia mfumo wa 4-4-2.

Kocha msaidizi, Athuman Bilali 'Bilo' anasema mfumo huo umekuwa rahisi kwao kulingana na aina ya wachezaji wanaounda timu hiyo.

"Kila mwalimu anatumia mfumo wake kulingana na aina ya wachezaji alionao." Bilo anaeleza ni vigumu leo ukaitaka Chelsea icheze kama Arsenal.

"Lazima kuwe na maandalizi. Huwezi kukurupuka usingizini na kubuni fomesheni. Leo tucheze 4-3-3, kesho 5-3-2." anasisitiza kocha huyo.

AFRICAN LYON

Mfumo; 4:4:2
MKURUGENZI wa Ufundi, Charles Otieno anasema timu hiyo inatumia mfumo wa 4-4-2. Lakini mambo yanapokuwa magumu hugeuka na kutumia 3-5-2.

"Fomesheni yetu ni 4-4-2, Lakini inapotokea kumeshikwa tunageuka na kutumia 3-5-2. Nafikiri kila mwalimu lengo lake ni kupata ushindi kila mechi."

Otieno anafafanua kuwa timu hiyo inapotumia mfumo wa 4-4-2 hushambulia na pia kujihami.

"Tunapogeuka na kucheza 3-5-2. Lengo letu huwa ni kushambulia kuliko kujilinda."

POLISI MORO

Mfumo; 4:4:2
KOCHA mpya, Adolf Rishard anasema tangu ameanza kazi ya kuinoa Polisi Moro anacheza katika mfumo wa 4-4-2.

"Mifumo ni mingi ya uchezaji, lakini inategemea sana na aina ya wachezaji ulionao." anasema kocha huyo aliyerithi mikoba ya John Simkoko aliyetupiwa virago na Polisi kushindwa kupata ushindi ngwe yote ya kwanza ya ligi.

Rishard anasema mfumo ambao anacheza ni 4-4-2 kulinga na aina ya wachezaji wanaounda timu yake.

"Kwa kiasi kikubwa fomesheni ya 4-4-2 imenipa mafanikio makubwa."

Polisi imeshinda mechi mbili za kwanza, mzunguko wa pili wa ligi dhidi ya Mtibwa Sugar na African Lyon ambapo imefikisha pointi 10.

TANZANIA VODACOM PREMIER LEAGUE: CHAGUA LIPI BAO KALI.

MIKAKATI YA KUENDELEZA MPIRA WA MIGUU KWA WANAWAKE




Utangulizi:
Awali ya yote napenda kuchukua nafasi hii kwa niaba ya kamati ya utendaji ya TWFA kuwashukuru wajumbe wa mkutano mkuu kwa kutupa ridhaa ya kuongoza chama kwa kipindi cha miaka minne.

Pia napenda kuchukua nafasi hii kuwashukuru wadau wote wa mpira wa miguu kwa kutuwezesha kufika hapa tulipo. Napenda niwashukuru wadau wote kwa ujumla wao na pia kuishukuru serikali kwa namna ya pekee zaidi kwa mchango wake ,na mashirika na makampuni ambayo yamekuwa karibu sana nasi NMB, SERENGETI, NSSF, PPF, na Bakheresa Group of Companies.

Tunaamini kabisa kuwa vyombo vya habari ni washirika wetu wakubwa katika kuendeleza mpira wa miguu wanawake. Napenda kuvishukuru vyombo vyote vya habari hapa nchini na hata vile vya nje vilivyoweza kutoa nafasi katika ujenzi wa mpira wa miguu wanawake.

 Maendeleo ya mpira
 Kutekeleza na kuendeleza mpango wa grassroot.

Kwa kushirikiana na Shirikisho la Mpira wa miguu Tanzania,Chama cha Mpira  wa Miguu wanawake  na vyama vya mikoa na wadau mbalimbali  tutaendelea kuendeleza mradi wa mpira wa miguu kwa watoto wa kike na wa kiume Grassroot programme.(umri wa miaka 06-12).kwa mwaka 2013 mradi huu utatekelezwa katika mikoa  mitano (5) mikoa hiyo ni  Tanga,Pwani.Mwanza,Mtwara na Lindi. Mradi huu unaendeshwa kupitia shule za msingi.Kwa mwaka 2012 Mradi huu umeendeshwa katika mkoa wa Dar es Salaam na  watoto wapatao 8766 (wasichana 4909 na wavulana 3857 ) na walimu 26 wameshirikishwa.

Mafunzo ,semina na makongamano
Kwa mwaka 2013 tunatengemea kuendesha mafunzo mbalimbali katika nyanja kuu nne za maendeleo ya mpira wa miguu yaani Utawala na uongozi,Ualimu(Ukocha)  Uamuzi na utabibu katika mpira wa miguu .Katika mwaka mwaka 2013 mafunzo yatafanyika zaidi katika nyanja ya uongozi ili kuwajengea stadi za uongozi viongozi wengi ambao wameingia madarakani katika chaguzi zilizofanyika kwa mwaka 2012/2013.Mafunzo ya utawala na uongozi yatafanyika katika mikoa nane:Dar es Salaam,Pwani,Morogoro,Mwanza,Musoma,Shinyanga,Kilimanjaro na Tanga.Katika mafunzo hayo baadhi ya washiriki watateuliwa kutokana na uwezo wao kwa kuzingatia vigezo vitakavyowekwa na watahudhuria semina itakayo andaliwa kwa kushirikiana na shirikisho la mpira wa miguu Tanzania.

Mafunzo kwa walimu katika ngazi mbalimbali na uratibu wa utekelezaji wa mafunzo yaliyofanyika yatapewa kipau mbele.

Mafunzo kwa waamuzi yatalenga zaidi kuibua vipaji vya watoto wa kike walioko mashuleni na wachezaji wanaomaliza/waliomaliza muda wao.Mafunzo yatafanyika kwa awamu mbili katika mkoa wa Dar es Salaam.

Madaktari  wa michezo  ni muhimu sana katika maendeleo ya mpira na afya za wachezaji kwa kushirikiana na vyombo husika mafunzo kwa mwaka 2013 yatafanyika kwa awamu mbili na yatafanyika katika mkoa wa Dar es Salaam. 
Wanahabari wenye uweledi katika mpira wa miguu wa wanawake ni chachu ya maendeleo ya mpira huo.Nafasi ya wanahabari ni kubwa katika kuendeleza mpira wa miguu ili kuwajengea ujuzi zaidi kutakuwa na mafunzo kwa wanahabari yatakayofanyika Dar es Salaam.

Uongozi na utawala bora
Maendeleo ya mpira wa miguu kwa wanawake yanahitaji viongozi bora na waliopewa ridhaa na vyombo husika.Chaguzi zimefanyika katika  mikoa 16 kati 25  ya mikoa ya Tanzania Bara. Pia tunahimiza mikoa ambayo haijafanya uchaguzi ifanye chaguzi mapema.  Mikoa hiyo ni: Dar es salaam, Mwanza, Kilimanjaro, Rukwa, Arusha, Geita, Simiyu, Njombe, Katavi na Mbeya.

Katika chaguzi hizo kuna baadhi nafasi zote hazikujazwa ni matumaini yetu kuwa  zitajazwa katika mikutano ijayo ya vyama husika.
Pia nichukue nafasi hii kuwahamasisha kina mama wengi wenye sifa kujitokeza kugombea nafasi mbalimbali katika vyama vya mikoa na taifa pale uchaguzi utakapoitishwa.

Mashindano
Mashindano mbalimbali ndio moyo wa mpira wa miguu bila mashindano  hakuna anayeweza kutambua  ubora na kiwango chakena pia ni kipimo cha maendeleo.
Kutakuwa na mashindano mbalimbali katika ngazi ya  mikoa,taifa na kimataifa.
Mashindano hayo pia yatahusisha shule za msingi na sekondari  na vyuo mbalimbali.Kwa kushirikiana na vyombo husika kutakuwa na ufuatiliaji wa karibu wa michezo ya UMISSETA toka ngazi ya mkoa hadi Taifa na kuwa na mpango endelevu wa kuwaendeleza wale wenye vipaji ambao wamechaguliwa /wanaweza kuchaguliwa kwenye timu za taifa.

Ligi itachezwa katika ngazi za mikoa na baadaye kuunda kombaini ya mkoa itakayoshiriki mashindano ya taifa.

Kwa mwaka 2013 tunatengemea mikoa kuchezesha ligi isiyopungua timu tano kwa mikoa 15 itakuwa na timu  10 na timu itaruhusiwa kusajili wachezaji 25 kwa mwaka 2013 tunatengemea watoto/wasichana  3750 kushiriki katika mpira wa miguu. Idadi hii ukizidisha mara nne unapata jumla ya wachezaji 15,000.Endapo tutakuwa na benki ya wachezaji hawa tutaweza kuunda timu bora za umri tofauti na zenye kiwango cha juu.

Pia mikoa inahimizwa kuanzisha mashindano mbalimbali yatakayoamsha ari kwa watoto wa kike na wasichana kushiriki katika mpira wa miguu.

Uratibu wa mikoa
Wajumbe wa kamati ya utendaji pamoja na  majukumu yao kama wajumbe watakuwa na jukumu la kuratibu shughuli za  maendeleo ya mpira wa miguu katika mikoa:Uratibu huo utakuwa kama ifuatavyo:
Rose Kissiwa
Makamu Mwenyekiti
Tabora, Dodoma, Rukwa, Kigoma, Pwani
Amina Karuma
Katibu
Lindi, Mtwara, Iringa, Njombe, Ruvuma
Zena Chande
Mjumbe
Dar es Salaam, Morogoro, Katavi, Shinyanga, Mbeya
Triphonia Temba
Mjumbe
Manyara, Arusha, Kilimanjaro, Tanga, Singida
Sophia Charles
Mjumbe
Mara, Kagera, Simiyu, Geita, Mwanza
Kwa mujibu wa katiba ya TWFA  ibara ya 37  inatoa nafasi kwa kamati ya utendaji kuunda kamati ndogo za kuendeleza mpira wa miguu wanawake kamati hizo ni kamati ya Fedha na mipango,kamati ya Ufundi,kamati ya ngingine itakayoonekana inafaa.Kamati ya utendaji kwa pamoja ilikubaliana kuunda kamati ya habari na masoko.
Kamati ya Fedha na Mipango
1.     Rose Kissiwa       - Mwenyekiti
2.     Evans Aveva
3.     Sophia Tigalyoma
4.     Sophia Mukama
5.     Asha Baraka
Kamati ya Ufundi
1.     Tryphonia Temba – Mwenyekiti
2.     Florence Ambonisye
3.     Miraji Fundi
4.     Dr. Leonia Kaijage
5.     Furaha Francis
6.     Richard Muhotoli
Kamati ya Habari na Masoko
1.     Zena Chande – Mwenyekiti
2.     Beatrice Mgaya
3.     Mohamed Mkangara
4.     Florian Kaijage
5.     Somoe Ng’itu

Masoko na Habari
Mpira wa miguu wanawake hauna udhamini na pia vyanzo rasmi vya kupata mapato.Kwa kupitia kamati ya habari na masoko ,tunaamini kutakuwa na mikakakti mbalimbali ya kuelimisha ,kuhamasisha wadau na watanzania wote kuwiwa na kujitoa kuendeleza mpira wa miguu .

YANGA KUICHIMBIA KABURI TOTO LAKE KESHO???

MICHUANO ya Ligi Kuu ya Vodacom kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Machi 9 mwaka huu) kwa mechi mbili ambapo vinara Yanga watakuwa wenyeji wa Toto Africans kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mwamuzi wa mechi hiyo namba 135 atakuwa Andrew Shamba kutoka Pwani akisaidiwa na Abdallah Mkomwa na Abdallah Rashid pia wote kutoka Pwani. Kamishna ni Salim Singano kutoka Tanga wakati Mtathmini wa waamuzi ni Alfred Lwiza.

Nayo Polisi Morogoro itakuwa mgeni wa Azam kwenye Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam. Azam katika mechi hiyo namba 136 na nyingine mbili zinazofuata itakuwa bila kocha wake Steward John Hall ambaye Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imemfungia mechi tatu.

Charles Komba kutoka Dodoma ndiye atakayekuwa Kamishna wa mechi hiyo namba 136 itakayochezeshwa na mwamuzi Simon Mberwa kutoka mkoani Pwani.

Ligi hiyo itaendelea tena keshokutwa (Machi 10 mwaka huu) ambapo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam utashuhudia mechi kati ya Simba na Coastal Union ya Tanga. Waamuzi wa mechi hiyo ni Martin Saanya akisaidiwa na Jesse Erasmo na Vicent Mlabu wote kutoka Morogoro.

RHINO, KANEMBWA ZASAKA TIKETI VPL
KINDUMBWENDUMBWE cha Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kinaendelea kesho (Machi 9 mwaka huu) katika makundi yote matatu, lakini macho na masikio ya washabiki wa mpira wa miguu yakiwa kwenye mechi za Rhino Rangers ya Tabora na Kanembwa JKT ya Kigoma.

Timu hizo ndizo ziko katika nafasi nzuri ya kupata tiketi ya kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu ujao kutoka kundi hilo la C. Tayari Mbeya City ya Mbeya na Ashanti United ya Dar es Salaam zimeshapata tiketi za kucheza VPL msimu ujao kutoka kundi A na B.

Rhino Rangers itaikaribisha Polisi Dodoma kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora, wakati Kanembwa JKT itakuwa mgeni wa Pamba kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Mechi nyingine za kundi C ni Mwadui vs Polisi Tabora (Kambarage, Shinyanga), na Morani vs Polisi Mara (Kiteto, Manyara). Mechi za kundi A ni Majimaji vs JKT Mlale (Majimaji, Songea), Mkamba Rangers vs Mbeya City (Sokoine, Mbeya) na Polisi Iringa vs Burkina Faso (Samora, Iringa).

Mshikeshike ya kundi B ni Ndanda vs Ashanti United (Nangwanda Sijaona, Mtwara), Villa Squad vs Green Warriors (Karume, Dar es Salaam), Polisi Dar vs Transit Camp (Mabatini, Mlandizi) wakati Tessema na Moro United zitacheza Machi 10 mwaka huu Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.

HUYU NDIYE MRITHI WA BONIFACE MKWASA TWIGA STARS

Rogasian Kaijage (wa kwanza kushoto aliyekaa) akiwa na kikosi cha timu TSC Academy
ROGASIAN Kaijage ameteuliwa kuwa kocha mpya wa timu ya taifa ya mpira wa miguu ya wanawake, Twiga Stars baada ya kocha wa zamani, Charles Boniface Mkwasa kujiuzulu katikati ya mwaka jana.

Mkwasa, ambaye alikuwa nyota wa Yanga na Taifa Stars, alijiengua kufundisha timu hiyo aliyoiongoza kwa muda mrefu, baada ya Twiga Stars kuondolewa katika kinyang’anyiro cha kuwania tiketi ya kucheza fainali za Afrika kwa Wanawake (AWC) zilizofanyika nchini Equatorial Guinea.

Twiga ilipata bao muhimu la ugenini jijini Addis Ababa ilipofungwa na wenyeji wao Ethiopia mabao 2-1, lakini ikiwa na matumaini ya kutumia vyema bao la ugenini ilijikuta ikilala bao 1-0 kwenye Uwanja wa Taifa katika mchezo wa marudiano na hivyo kukosa tiketi ya kurudi tena kwenye fainali hizo.

Kaijage ambaye kwa sasa anajihusisha na mradi wa vijana (grassroots) pamoja na programu nyingine za kukuza vipaji zilizo chini ya TFF, aliteuliwa na Kamati ya Ufundi ya TFF kufanya kazi hiyo na ameita kikosi cha Twiga Stars kwa mazoezi ya siku kumi kuanzia Machi 10 hadi 23 mwaka huu Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam.

Wachezaji walioitwa ni Amina Ally (Lord Barden), Asha Rashid (Mburahati Queens), Aziza Mwadini (Zanzibar), Esther Chabruma (Sayari), Esther Mayalla (TSC Academy), Etoe Mlenzi (JKT), Evelyn Sekikubo (Mbarahati Queens), Fatuma Bushiri (Simba Queens), Fatuma Mustafa (Sayari) na Fatuma Omari (Sayari).

Flora Kayanda (Tanzanite), Hamisa Athuman (Marsh Academy), Hellen Maduka (Bujora), Hellen Peter (JKT), Irene Ndibalema (TSC Academy), Maimuna Said (JKT), Mwajuma Abdallah (Tanzanite), Mwanaidi Tamba (Mburahati Queens), Mwanahamis Omari (Mburahati Queens) na Mwapewa Mtumwa (Sayari).

Nabila Ahmed (Marsh Academy), Nasiria Hashim (Zanzibar), Pulkeria Charaji (Sayari), Rukia Khamis (Sayari), Semeni Abeid (Tanzanite), Sharida Boniface (Makongo Sekondari), Sophia Mwasikili (Luleburgaz Gucu Spor, Uturuki), Theresa Yona (TSC Academy), Vumilia Maarifa (Evergreen) na Zena Khamis (Mburahati Queens).

TENGA SASA ATAKA KUMUONA WAZIRI WA MICHEZO MWENYEWE

RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga amemshukuru Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenela Mukangara kwa kukubali ombi la Shirikisho la kutaka kukutana naye kwa mazungumzo na kumsihi asitishe hatua anazodhamiria kuchukua hadi hapo kikao hicho kitakapofanyika.

Waziri Mukangara ameiagiza TFF kuitisha Mkutano Mkuu wa marekebisho ya katiba ifikapo tarehe 15 Aprili 2013 na Mkutano Mkuu wa Uchaguzi ifikapo tarehe 25 Mei 2013 na kwamba tamko la TFF kutekeleza maagizo hayo liwe limetolewa katika muda wa siku tano zinazoishia Jumatatu (Machi 11, 2013).

Katika barua pepe ambayo amemuandikia Waziri ambaye kwa sasa yuko nje ya nchi, Rais Tenga ameeleza kuwa alikwenda ofisini kwake tarehe 7 Machi 2013 kujaribu kumuona lakini akaambiwa amesafiri, hivyo kuomba kukutana na Katibu Mkuu wa Wizara, ambaye pia hakuwepo ofisini na hatimaye akakutana na Naibu Katibu Mkuu.

Katika barua hiyo pepe, Rais Tenga ameeleza madhumuni ya kutaka kuonana na Waziri Mukangara kuwa ni kwanza “kukushukuru kwa kukubali kuonana na ujumbe wa TFF ulioongozwa na mjumbe wetu wa Kamati ya Utendaji, Bw. Alex Mgongolwa, akiongozana na Katibu Mkuu wa TFF, Bw. Angetile Osiah, jana tarehe 6 Machi 2013.
“Kukushukuru kwa kukubali kukutana nasi tena siku ya tarehe 19 Machi, kwa ajili ya mazungumzo juu ya maagizo yako.
“Kukuarifu kuwa nimepokea maagizo yako uliyoyatoa jana kupitia kwa Mjumbe wetu wa Kamati ya Utendaji na kwa njia ya barua; na
“Kwa heshima na taadhima, kukuomba usitishe hatua yoyote ile unayodhamiria kuchukua hadi hapo tutakapokutana na kupata maelezo yetu, TFF, juu ya maamuzi na maagizo uliyoyatoa.”

Tenga, ambaye ni mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu la Afrika (CAF) aliondoka jana (Machi 7 mwaka huu) kwenda Marrakech, Morocco kuhudhuria kikao cha kamati hiyo na pia Mkutano Mkuu wa CAF ambao umepangwa kufanyika Machi 10 mwaka huu ukihusisha pia ajenda ya uchaguzi wa rais.

Thursday, March 7, 2013

MABAO YA HARUNA NIYONZIMA YAMUACHA MDOMO WAZI KOCHA WAKE: NA HUU NDIO UMUHIMU WA MABAO YA KAVUMBAGU NA NIYONZIMA KWA YANGA

KOCHA wa Yanga, Mdachi Ernie Brandts ametamka kuwa mabao mawili aliyofunga Niyonzima katika mechi mbili za ligi kati ya Azam FC na Kagera Sugar Uwanja wa Taifa ni mazuri na hayana mfano.

"Ni magoli mazuri. Pia, ni muhimu kwetu. Tumevuna pointi sita ambazo zimetuweka kileleni na pointi 42." alisema Brandts.
 

Kocha huyo alisema; "Nafikiri yamekuja wakati mwafaka tukiwa katika mbio za kuwania ubingwa wa ligi."
 

Kwa upande wake, Niyonzima alisema siri kubwa ya staili ya mabao aliyofunga akiwa nje ya eneo la penalti ni mazoezi.
"Mara nyingi nimekuwa nikijifua mazoezini kupiga mashuti na kufunga nikiwa mbali na lango. Nafikiri hiyo ndiyo siri yangu kubwa." alisema Niyonzima ambaye anachezeshwa nafasi ya winga wa kushoto.

Mabao yake na Kavumbagu
KWA taarifa yako ukae ukijua, kati ya mabao tisa ambayo Kavumbagu amefunga, Yanga imenufaika na pointi mbili pekee. Tofauti na mabao mawili aliyofunga Haruna Niyonzima. Yanga imenufaika na pointi sita katika mabao mawili ya Niyonzima aliyofunga katika mchezo wa Azam na Kagera.
 

Endapo Kavumbagu angegoma kufunga mabao hayo, bado Yanga ingepeta kilele na pointi 40 kibindoni na kuiacha Azam FC nafasi ya pili na pointi zake 36.
Lakini Niyonzima angesusa kufunga mabao hayo, Yanga ingekuwa na pointi 36 sawa na Azam FC.
 

 Kwa akili ya kawaida, itakuwia vigumu sana kuamini. Lakini huo ndio ukweli wa mambo yenyewe.
 

Huwezi kuamini kwa akili ya haraka. Lakini hiyo ndio hali halisi ya mambo.Kavumbagu amefunga mabao hayo katika mechi nane ambazo Yanga ilishinda zaidi ya bao moja.
 

Kwa kawaida ushindi wa aina yoyote ile unaipa timu husika pointi tatu. Hali hiyo imefanya mchango wa Kavumbagu kuoneka mdogo tofauti na idadi ya mabao yake aliyofunga.

Ubingwa wa Ligi
KATIKA hali ya kushangaza, nyota huyo amefunguka na kutamka maneno mazito kuwa endapo Yanga itashindwa kunyakua ubingwa wa ligi msimu huu ataondoka zake.
 

"Kuna malengo ambayo nilijiwekea. Kwa hiyo kama yatashindwa kutimia sina budi kuondoka na kusaka timu nyingine."
 

Mnyarwanda huyo alisema wakati anajiunga na Yanga alitamka ataisaidia timu hiyo kutwaa taji la ligi na kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika.
 

"Naweza kujivunia tumetwaa Kombe la Kagame mwaka jana. Lakini kiu yangu kubwa kwa sasa ni taji la ligi."  alisema kiungo huyo.
 

Hata hivyo, itakuwa vigumu kwa Niyonzima kutimka Yanga endapo itashindwa kutimiza malengo yake kutwaa taji la ligi kutokana na mkataba wake kumalizika mwaka 2015.

YANGA VS TOTO: BARTHEZ HALI TETE ASHINDWA KUFANYA MAZOEZI NA YANGA

KIPA wa Yanga, Ally Mustapha 'Barthez' ameshindwa kufanya mazoezi na wenzake leo kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya tumbo. 

Yanga inajiwinda na mchezo wake wa ligi dhidi ya Toto African ya Mwanza utakaopigwa Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam. Daktari wa Yanga, Nassor Matuzya alisema jana asubuhi, baada ya mazoezi ya timu hiyo, Uwanja wa Bora Kijitonyama, Dar es Salaam;
 

"Barthez ameshindwa kufanya mazoezi na wenzake leo kutokana na kusumbuliwa na maumivu ya tumbo." Matuzya alisema; "Vipimo vimeonyesha chakula alichokula juzi usiku ndicho kimemsababishia hali hiyo.

"Kwa sasa hali yake inaendelea vizuri. Natarajia kesho atajiunga na wenzake kuanza mazoezi."
 

Hata hivyo, daktari huyo alisema hawezi kuweka wazi kuwa atakuwepo katika mchezo wa Jumamosi. "Siwezi kuweka asilimia 100 kuwa Barthez atakuwa fiti kucheza dhidi ya Toto. Nafikiri tusubiri hiyo kesho."
 

Pia, beki wa kulia Juma Abdul na kiungo Nurdin Bakari walishindwa kufanya mazoezi na wenzao kutokana na kuwa majeruhi.
 

"Nurdin anasumbuliwa na goti kama ilivyo kwa Abdul. Kwa sasa hali zao zinaendelea vizuri. Lakini nafikiri kuanzia kesho watajiunga na wenzao kuanza mazoezi."

BEKI YANGA LADISALUS MBOGO KUFANYIWA UPASUAJI

BEKI wa Yanga, Ladisalus Mbogo anatarajia kufanyiwa upasuaji Machi 12, mwaka huu katika hospitali ya Mwananyamala.
Kwa mujibu wa daktari wa timu hiyo, Nassor Matuzya alisema jana jijini Dar es Salaam kuwa beki hiyo atafanyiwa upasuaji huo kuondoa uvimbe kwenye shavu lake la kushoto.
“Upasuaji wake utafanyika kwenye hospitali ya Mwananyamala, Jumanne ya wiki ijayo."
Matuzya alisema; "Vipimo vyake alivyofanyiwa katika hospitali ya Muhimbili na madaktari bingwa vimetoka."
"Tuliamua kushirikiana na madaktari wa Muhimbili ili kujiridhisha zaidi kama hapatakuwa na madhara, baada ya kumpasua."
Alisema; “Upasuaji huu umekuja baada ya Mbogo kutueleza kuwa hafurahishwi na hali ya tatizo hilo,”
Mbogo ambaye alijiunga na Yanga msimu huu akitokea Toto African ya Mwanza alisema; "Hali hii nimekuwa nayo tangu utoto wangu. Nitashukuru endapo upasuaji utakwenda vizuri na kupona."
Pia, aliwashukuru viongozi wa Yanga kumsaidia kutibu tatizo lake bila kusukumwa.
"Nafikiri tatizo hili nimekuwa nalo muda mrefu. Sina budi kuwashukuru viongozi wangu kujitolea kunitibu. Nadhani ni jambo zuri na la kuigwa katika jamii." alisema beki huyo aliyeichezea Yanga kwa dakika 19 kwenye michuano ya Kombe la Kagame mwaka jana.

ITS OFFICIAL KABURU AJIUZULU UMAKAMU UENYEKITI SIMBA SC - HANS POPE NAE ABWAGA MANYANGA


Hatimaye makamu mwenyekiti wa klabu ya Simba Godfrey Nyange Kaburu ametangaza rasmi kujiuzulu nafasi yake kwenye klabu ya Simba mapema leo.

Taarifa rasmi kutoka kwenye uongozi wa Simba ambazo mtandao huu umezipata ni kwamba Kaburu leo ametuma barua pepe kwenda kwa mwenyekiti wa klabu ya Simba Mh.Aden Rage akimuelezea maamuzi yake ya kujivua madaraka ya kuitumikia Simba kutokana mgawanyiko mkubwa uliopo kwenye uongozi wa klabu hiyo.

Kwa mujibu wa chanzo cha habari Kaburu ameelezea kwamba kamati ya utendaji imegawanyika na ufa uliopo hautoi nafasi nzuri kwake kuitumikia vizuri Simba, akisema ni moja ya sababu ya timu yao ya Simba kutofanya vizuri katika michuano mbalimbali inayoshiriki.

Pia Kaburu amesema amechukua maamuzi hayo ni njia mojawapo ya kuwajibika kama kiongozi kutokana mambo kutokwenda vizuri hali ambayo imesabababisha kutukanwa na kupigiwa kelele nyingi na wanachama na wapenzi wa Simba SC Mwenyekiti. Hivyo ameamua kujiuzulu kupisha wanachama wengine wa Simba waweze kuliongoza jahazi la klabu hiyo.


Katika hatua nyingine mwenyekti wa kamati ya usajili na mjumbe ya kamati ya utendaji Zacharia Hans Pope nae ametangaza kujiuzulu kwenye nafasi zote alizokuwa akishikilia Simba.

Pia kwenye taarifa yake ya kujiuzulu Pope amesema mgawanyiko uliopo kwenye uongozi ndio chanzo cha kujiuzulu kwake katika kuitumikia Simba kupitia nafasi za uongozi alizokuwa nazo kwa takribani miaka 3.

Wednesday, March 6, 2013

THE SITE IS UNDER MAINTANANCE: TUTARUDI HEWANI SOON


TUPO KWENYE MATENGENEZO YA KUREKEBISHA MTANDAO HUU - TUTARUDI KWENYE HALI YA KAWAIDA HIVI KARIBUNI. ASANTE

HATIMAYE TFF YAUFYATA: SERIKALI YAIAGIZA KUANDAA MKUTANO MKUU KUFANYA MAREKEBISHO YA KATIBA NDANI YA SIKU 40 NA KUANDAA UCHAGUZI MKUU UPYA

 Taarifa za ndani kutoka kwenye chanzo cha kuaminika ni kwamba kikao cha serikali kupitia wizara ya habari na michezo na shirikisho la soka nchini kuzungumza juu ya suala la serikali kuondoa usajili wa katiba mpya ya TFF kimeishia kwa serikali kuliagiza shirikisho hilo kuwataarifu wanachama juu ya mkutano mkuu ndani ya siku 5 zijazo, na kuandaa mkutano wa kufanya mabadiliko ya katiba katika kipindi cha siku 40 zijazo kutoka leo.

Kwenye kikao hicho TFF iliwakilishwa na Katibu Mkuu Angetile Osiah, mwanasheria Alex Mgongolwa, na Mkurugenzi wa ufundi wa TFF Sunday Kayuni - taarifa za kutoka ndani ya kikao hicho zinasema kwamba TFF ilionekana haikufuata taratibu za kufanya marekebisho ya katiba na hivyo serikali ikafikia maamuzi ya kuwaagiza waandae mkutano mkuu wa wanachama wote wa TFF ili kukidhi matakwa ya kufanya marekebisho ya katiba.

Pia baada ya kufanyika kwa mkutano mkuu, serikali imeagiza uchaguzi mkuu wa shirikisho hilo ufanyike katika kipindi cha siku 40 baada ya mkutano mkuu kufanyika.

CRISTIANO RONALDO ANAWEZA AMERICAN FOOTBALL - AKIRI REGGIE BUSH

Katika kusherehekea kutimiza miaka 28 ya kuzaliwa kwake siku ya jumamosi iliyopita, mchezaji wa timu ya mchezo american football Red Bull Reggie Bush alipewa ofa ya kwenda kuangalia El classico nchini Spain kati ya Real Madrid na Barcelona.

Real Madrid wakashinda 2-1 kwenye uwanja wao wa nyumbani Santiago Bernebeu, lakini walishindwa kumzuia Messi asifunge goli ake la 39 kwenye La Liga. Raggie Bush anakiri alishangazwa na uwezo wa mchezaji huyo kiargentina namna anavyofanya uone mchezo wa soka ni rahisi.

Lakini alipoulizwa na mchezaji gani kwenye el classico anaweza kwenda kucheza kwenye American Football, Reggie alisema bila shaka ni Cristiano Ronaldo, "Ni kweli Ronaldo anaweza kucheza NFL, Ni mrefu wa kimo 6'1", 6'2", na anakimbia sana. Itakuwa jambo la kuvutia kumuona Ronaldo akipambana kwenye NFL, paia mie kama ningepata nafasi ya kucheza soka ningependa kuwa Ronaldo na kucheza nafasi ya ushambuliaji."

Reggie Bush na Cristiano Ronaldo wana historia ya kuvutia kidogo pamoja, wote wamewahi kuwa na mahusiano na mwanadada Kim Kardashian.

Tuesday, March 5, 2013

MAN UNITED VS REAL MADRID: VITU VITANO (5) VINAVYOWEZA KUAMUA MECHI LEO

Manchester United wanaikaribisha  Real Madrid leo jumanne katika mechi ambayo inaaminika itakuwa kubwa kuliko zote katika raundi ya 16 bora ya ligi ya mabingwa wa ulaya. 

Real Madrid hivi karibuni wameshinda mara mbili mfululizo dhidi ya mahasimu wao Barcelona, lakini wanasubiriwa na mtihani mwingine mgumu leo pale Old Trafford.

Kikosi cha Sir Alex Ferguson kiliweza kulazimsisha sare ya  1-1 wiki tatu zilizopita kwenye uwanja wa Bernabeu, hivyo Mourinho na Madrid yake leo itakuwa na kazi kushambulia zaidi ili kuweka hai matumaini ya kupita.

Hivyo inamaamisha leo hii kutakuwa na vita kubwa sana katika washambuliaji wa Madrid dhidi ya walinzi wa lango la United. Lakini vita haitokuwa hiyo tu - hivi ni vitu vitano vingine vitakavyoamua nani katika ya magwiji hawa wa soka barani ulaya anaendlea kwenye hatua ya robo fainali.


ANGEL DE MARIA VS MABEKI WA UNITED
Angel Di Maria, muargentina aliye kwenye fomu nzuri sasa hivi, amekuwa akipangwa kwenye kila mechi muhimu wakati Madrid wakitumia mfumo wa kuchezesha washambuliaji watatu. Akiwa anahama kutoka winga moja mpaka nyingine kuhakikisha Madrid inatamba.

Katika mechi ya kwanza wiki tatu zilizopita, Di Maria alitoa krosi safi iliyomfikia Ronaldo na kuwa goli - krosi ikitokea upande wa kushoto ambao ndio Ronaldo anaanzaga kwenye mechi.

Di Maria na Ronaldo wanaweza kuwa upande wowote wa uwanja muda wowote. Ronaldo kwa hakika atatolewa macho zaidi, lakini Di Maria na krosi zake, uharaka na ujuzi wa kupenya yeye mwenye au mipira yake unaweza ukawa hatari kubwa kwa upande wa Man United.

Wapinzani wa Di Maria watakuwa mabeki wa pembeni wa United Evra na Rafael, na ikiwa Di Maria atacheza vizuri sana kwa hakika hali haitokuwa salama langoni mwa Mashetani wekundu. Ni mmoja ya watu wanaoweza kuamua mechi hii.


VIUNGO WA ULINZI WA MADRID VS WASHAMBULIAJI WA UNITED
Kuna taarifa kwamba Ferguson anaweza asimuanzishe Wayne Rooney leo hii, inaweza ikawa kweli au ni mbinu tu za mscotland huyo kuwachanganya Real Madrid.Vyovyote itakavyokuwa leo, tunafahamu kwamba Real Madrid hawapaswi kuruhusu nyavu zao kuguswa usiku wa leo. Kuruhusu goli hasa mapema itamaanisha inabidi wacheze sana na kufunga mabao mawili ili kuweza kupita. Hivyo ushirikiano mzuri wa beki ya madrid utakuwa mchango muhimu sana. Walinzi wa kati na viungo wakabaji wanapaswa kuwa makini zaidi.
 
Mjerumani Sami Khedira mhispania Xabi Alonso mara nyingi huwa wanaanza pamoja na wanatengeneza ushirikiano mzuri sana kama viungo wa ulinzi mbele ya ukuta. Kazi yao na kuwalinda walizni wanne wa nyumana kuunganisha safu ya ulinzi na ushambuliaji. Pamoja na uwezo wake wa kuzuia, Alonso anatambulika kwa pasi znuri na zenye maana.
 
Khedira na Alonso ni wazuri sana kwenye eneo hilo, lakini United wana washambuliaji hatari. Machaguo kama Robin Van Persie, Rooney, Danny Welbeck na Chicharito.

Wikiendi iliyopita, Shinji Kagawa alifunga hat-trick katika ushindi wa United 4-0 dhidi ya Norwich City. Pia kuna winga wazuri kama vile Nani, Ashley Young na Valencia ambao kama wanakutana safu ya ulinzi isiyokuwa imara wanaweza wakaleta madhara makubwa.


MICHEAL CARRICK VS OZIL
Cristiano Ronaldo, Robin van Persie na wafungaji wengine wanaweza kuwa wanatajwa sana kwenye vyombo vya habari. Japokuwa viungo wanaweza kuwa waamuzi wa hii mechi.

Mjerumani Mesut Ozil usiku zote huwa anacheza kama kiungo mchezashaji wa Real Madrid, akicheza nyuma ya Karim Benzema au Gonzalo Higuain. Au iwe tofauti meneja Jose Mourinho achague kumpanga Kaka  au Luka Modric kuanza, lakini ishara zote leo zinaonyesha Ozil ataanza kwenye mechi leo.

Mpinzani wake mkuu atakuwa kiungo aliye kwenye fomu msimu wa United Micheal Carrick, ambaye hucheza nyuma kidogo ya kiungo cha United huku akicheza part kubwa ushambuliaji wa United.

Ozil inawezekana akawa anaonekana bora zaidi kwenye levo ya kimataifa zaidi ya Carrick, lakini mchango wa muingereza Carrick kwenye timu ya United hasa msimu huu umekuwa muhimu sana. Upinzania baina ya wawili hawa unaweza ukaaamua mechi.


MBINU(FERGIE VS MOURINHO)
Kocha wa Manchester United Sir Alex Ferguson na wa  Real Madrid Jose Mourinho wamekuwa na upinzani mkali sana tangu Mourinho alipokuwa Chelsea. Sasa hivi japokuwa ni marafiki, lakini wawili hawa hawajaacha upinzani wao, na wote bado wanatajwa kuwa amkocha bora duniani. 

Babu Ferguson aliiwezesha United kupata sare wiki tatu zilizopita. Matokeo ambayo yanamaanisha Real Madrid watacheza mchezo wa kushambulia sana leo Old Trafford. Hilo litafanya kuwepo na ushindani wa mbinu kali za soka baina ya wawli hawa na mabenchi yao ya ufundi.

Pia kutakuwa na vita baina ya wawili hawa kwenye mstari wa uwanja kama ambavyo wote wanajulikana wazuri wa kuhamasisha maamuzi kutoka kwa marefa.
CRISTIANO RONALDO
 BBC Sport, kupitia mwandishi wa kihispania Andy West walitoa makala ya namna ya kumzuia Cristiano Ronaldo yenye maneno zaidi ya 800.
Badhi ya maneno hayo yalikuwa haya:
 "Wanachotakiwa kufanya United ni kuzuia Ronaldo asipige shuti na mguu wake wa kulia, au kushoto, au kuwa wa mwisho kufikia na krosi kwenye eneo la hatari. Wajitahidi kutokutoa faulo karibia na eneo la hatari, au kumuachia nafasi yoyote Ronaldo kuweza kukabiliana na ukuta."
Kama ambavyo inavyoonekana kufanyika kwa haya yote ni vigumu karibia na kutowezekana, ukweli unaweza ukawa unatisha zaidi kwa United. Ronaldo, ambaye aliichezea United kwa kipindi cha miaka 6, amefunga mabao 37 kwenye mashindano yote msimu huu. Anapokuwa kwenye fomu, ni vigumu sana kumzuia kihalali pasipo kucheza madhambi.

Kama alivyoonesha kwenye mechi ya kwanza, Ronaldo ni hatari hewani. Lakini wote tunafahamu moja ya vitu vinavyomtofautisha Ronaldo na wengine yeye ni hatari kwenye eneo lolote la uwanja.

Na kuifanya hali kuwa mbaya zaidi kwa United ni majeruhi ya mlinzi Phil Jones, ambaye hatocheza leo kwa mujibu wa kocha Sir Alex Ferguson.

Kizuizi kikubwa cha ushindi wa United leo kwa hakika ni mtoto wao wenyewe waliowauzia maadui zao kwa £80millioni - Cristiano Ronaldo.T

LIPI BAO KALI : NIYONZIMA Vs KAGERA & ROONEY Vs NORWICH CITY, NIYONZIMA Vs AZAM FC

HARUNA NIYONZIMA ( YANGA VS KAGERA SUGAR ) WAYNE ROONEY ( MAN UTD VS NORWICH CITY ) HARUNA NIYONZIMA ( YANGA VS AZAM FC )

PETER CECH AMTETEA ABRAMOVICH - AWAULIZA ARSENAL KAMA WANGEKUWA TAYARI KUFUNDISHWA NA MAKOCHA 10 NA KUSHINDA MAKOMBE?

Huku kukiwa na hatari ya kupoteza ajira kwa kocha Rafael Benitez kwenye klabu ya Chelsea, golikipa Peter Cech ameamua kuweka mtazamo wake kwenye mlengo chanya kuhusu mmiliki wa klabu hiyo Roman Abramovich na tabia yake ya kutokuwa mvumilivu na makocha pindi timu inapofanya vibaya. 

Akizungumza na The Guardian alisema: 
"Unaweza ukazungumza mengi kuhusiana na hili suala, lakini pia katika kipindi hicho hicho tumeshinda kama au pungufu ya Manchester United," alisema. "United wamekuwa na kocha mmoja, sie tumekuwa nao nane, na tumeshinda makombe sawa, wameshinda champions league hata sie tumeshinda. Kuna vitu vingi chanya tumepata
          "Arsenal wamekuwa na kocha mmoja na ni muda mrefu hawajashinda hata kikombe    kimoja. Labda uwaulize wenyewe kama wangekuwa radhi kuwa na makocha 10 na makombe sita, sijui wangejibu nini lakini nadhani kila klabu ina namna yake ya kufanya kazi zake."


HATMA YA AFRICAN LYON LIGI KUU KUJULIKANA CHAMAZI KESHO

HATMA ya African Lyon kuendelea kushika mkia au la kwenye Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inajulikana kesho wakati itakapokuwa mwenyeji wa Ruvu Shooting kwenye Uwanja Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam.

Lyon yenye pointi 13 kutokana na mechi 19 inabidi iifunge Ruvu Shooting kama inataka kuirejesha mkiani Toto African yenye pointi 14. Kama kweli inazitaka pointi zote tatu itabidi ifanye kazi mbele ya Ruvu Shooting inayotiwa makali na Kocha Charles Boniface Mkwasa.

Hiyo itakuwa mechi ya 18 kwa Ruvu Shooting inayoshika nafasi ya saba ikiwa na pointi 26 ikitanguliwa na vinara wa ligi hiyo Yanga, Azam, Simba, Coastal Union, Kagera Sugar na Mtibwa Sugar yenye pointi 28 ikinolewa na nahodha wa zamani wa Taifa Stars, Mecky Maxime.

Mechi hiyo namba 139 itachezeshwa na mwamuzi Amon Paul kutoka Musoma wakati wasaidizi ni Anold Bugado wa Singida na Milambo Tshikungu kutoka Mbeya. Mwamuzi wa mezani atakuwa Shafii Mohamed wa Dar es Salaam.

Nayo Tanzania Prisons ya Jumanne Chale itakuwa mgeni wa Oljoro JKT katika mechi itakayochezwa Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid jijini Arusha wakati Mgambo Shooting itaoneshana kazi na Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.

Keshokutwa (Machi 7 mwaka huu) Uwanja wa Azam Complex jijini Dar es Salaam utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya JKT Ruvu ya Kocha Charles Kilinda na Kagera Sugar.

Ligi hiyo itaendelea tena Jumamosi ya Machi 9 mwaka huu kwa mechi mbili; Yanga vs Toto Africans (Uwanja wa Taifa), na Azam vs Polisi Morogoro (Azam Complex, Chamazi).