Search This Blog

Saturday, March 22, 2014

YANGA YAITUNGUA RHINO 3-0 TABORA, MBEYA CITY YAWAANGAMIZA JKT RUVU 2-0 CHAMAZI!!


Na Baraka Mpenjwa , Dar es salaam

0712461976 

LIGI kuu soka Tanzania bara imeendelea leo  kwa mitanange miwili ya vuta nikuvute iliyopigwa katika miji miwili tofauti hapa nchini.
Mabingwa watetezi wa ligi hiyo, Young African walialikwa na maafande wa JWTZ, Rhino Rangers kwenye uwanja wa Ally Hassan Mwinyi mjini Tabora.
Mbeya City walikuwa wageni wa JKT Ruvu wanaonolewa na kocha Fredy Ferlix Minziro, katika uwanja wa Azam Complex, uliopo Chamazi, nje kidogo ya jiji la  Dar es salaam.
Yanga waliuanza mchezo wa leo kwa lengo moja la kuibuka na ushindi ili kuwasogelea Azam fc kileleni.
Haikuwa rahisi kwao kuwafunga Rhino kwa dakika 28 za kwanza, lakini dakika ya 29, mshambuliaji aliyekalia benchi kwa muda mrefu, Jeryson Tegete aliandika bao la kuongoza.
Baada ya bao hilo, Yanga waliendelea kulisakama lango la Rhino ambapo mara kadhaa Tegete alijaribu kuzitafuta nyavu za wapinzani wao, lakini mabeki wa Rhino walikuwa makini.
Mpaka dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika, Yanga walitoka kifua mbele kwa bao 1-0.
Kipindi cha pili  kilianza kwa Yanga kuendelea kulishambulia lango la Rhino.
Dakika ya 68, Yanga walipata bao la pili baada ya mlinzi wa Rhino kujifunga wakati akijaribu kuokoa mpira wa winga machachari, Saimon Msuva.
Dakika ya 75, kocha Pluijm alimtoa Tegete na kumuingiza mshambuliaji Hussein Javu.
Hakika nyota ya Yanga iliendelea kung`ara ambapo dakika ya 90, Hussein Javu aliandika bao la tatu kwa Yanga na kulizamisha zaidi jahazi la Rhino.
Dakika 90 za mchezo huo zimemalizika kwa Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 3-0.
Safari ya Rhino Rangers kuelekea ligi daraja la kwanza imezidi kuiva kwasababu wamebakiwa na michezo minne tu.
Huko Azam complex, Chamazi, nje kidogo ya jijini la Dar es salaam, JKT Ruvu walikuwa wenyeji wa Mbeya City.
Mchezo huo umemalizika kwa wagonga nyundo wa Mbeya kuibuka na ushindi wa mabao 2-0.
Mabao yoye mawili ya Mbeya City yamefungwa na Saad Kipanga.
Kocha msaidizi wa Mbeya City, Maka Mwalwisyi ameuambia mtandao huu kuwa mechi ilikuwa nzuri, na walijitahidi kutumia nafasi walizotengeneza.
“JKT Ruvu walicheza vizuri. Sisi tulikuwa wazuri zaidi. Tumepata nafasi na kutumia. Mashabiji wetu wazidi kutuamini kwani safari ya ubingwa bado ipo”. Alisema Maka.
Kwa matokeo hayo, Mbeya City wanafikisha pointi 42 katika nafasi ya tatu, pointi moja nyuma ya Yanga wenye pointi 43 baada ya kushinda leo mabao 3-0 mjini Tabora.
Utofauti wa pointi moja unaonesha jinsi ambavyo timu za ligi kuu hasa za juu zinaendelea kupambana kutafuta taji msimu huu.
Ligi hiyo itaendelea kesho kwa mechi nne ambapo Simba itacheza na Coastal Union katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Azam itaoneshana kazi na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Azam Complex. Mechi hizo mbili zitakuwa ‘live’ kupitia Azam Tv.
 Mechi nyingine za kesho Jumapili ni Mgambo Shooting dhidi ya Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, wakati Ruvu Shooting na Ashanti United zitapimana ubavu kwenye Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.

WENGER ATIMIZA MECHI YA 1,000 NA KIPIGO KIZITO KUTOKA KWA CHELSEA - WAPIGWA 6-0


Mchezo wa 1,000 wa kocha Arsene Wenger umeisha kwa kipigo cha 6-0 kutoka Chelsea. Ushindi huo umemfanya Jose Mourinho aendelee kumtambia Wenger huku akiimarisha rekodi yake ya kutopoteza mechi katika dimba la Stamford Bridge katika mechi 76.

Pia ushindi wa 6-0 ndio mkubwa kabisa kwa Jose Mourinho tangu alipokuja katika ligi kuu ya England.

PRISONS YATEMA MKWARA KWA YANGA, WADAI MOTO WAO HAUZIMWI KWA PETROLI!!


Na Baraka Mpenja , Dar es salaam


MAAFANDE wa Jeshi la Magereza, Tanzania Prisons Maarufu  kwa jina la `Wajelajela` wamejichimbia mjini Morogoro kujiandaa na mechi yao ya  machi 26 mwaka huu katika dimba la Taifa jijini Dar es salaam dhidi ya mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania bara, Young African.
Katibu mkuu wa Prisons, Inspekta Sadick Jumbe amesema kuwa sababu ya kukaa Morogoro  kwa muda mrefu ni kutafuta mbinu mpya za kuwafunga Yanga wanaosifika kuwa na kikosi bora zaidi msimu huu.
“Jumatatu tunaondoka Morogoro kuja Dar es salaam, jumatano tunacheza na Yanga. Maandalizi yapo vizuri kabisa na tunakuja kufanya maajabu”. Alisema Jumbe.
Aidha aliongeza kuwa mechi iliyopita dhidi ya Kagera Sugar katika dimba la Kaitaba, mwamuzi aliwapendelea zaidi wenyeji wao.
“Tulifungwa 2-1. Lakini hatukufungwa na Kagera sugar. Tulifungwa na mwamuzi. Nawaomba TFF wawe makini katika upangaji wa marefa na kufuatilia maamuzi yao”. Alisema Jumbe.
Kueleka katika mchezo huo, Jumbe alisema Yanga ni wagumu zaidi wanapokuwa uwanja wa Taifa, lakini mzunguko huu wa pili Prisons wamekuwa bora zaidi.
“David Mwamwaja ni kocha mwenye historia nzuri. Baada ya kuchukua kikosi chetu kimekuwa bora zaidi. Sema kuna wakati waamuzi wanatuangusha kabisa. Kaitaba tulinyongwa sana”. Alisisitiza Jumbe.
Katibu huyo alisema moto wao ni mkali na kamwe hauzimwi kwa petrol, hivyo Yanga hata kama watakuwa uwanja wa Taifa, watahenyeshwa mwanzo hadi mwisho wa mechi.
“Tupo nafasi ya 10 kwa pointi 22 na tuna mchezo mkononi. Tunazitaka sana pointi tatu kutoka kwa Yanga. Hakika hatoki mtu na kipigo Taifa. Lazima kieleweke tu”. Alitamba Jumbe.
Mzunguko huu wa pili Prisons wameonekana kudhamiria kubakia ligi kuu kwani wamekuwa wakifanya vizuri zaidi.
Katika mechi ya mzunguko wa kwanza na Yanga uwanja wa Sokoine jijini Mbeya, timu hizo zilitoka suluhu ya bila kufungana,
Yanga wapo katika harakati za kutetea ubingwa wao msimu huu, wakati Prisons wanahitaji pointi ili kujinusuru kushuka daraja.
Kutokana na mazingira hayo, mechi hiyo ya jumatano wiki ijayo, itakuwa na changamoto kubwa kwa timu zote.
Matokeo ya ushindi yatakuwa na faida kubwa kwa Yanga, wakati huo huo kama Prisons watashinda, watazidi kujisafishia njia ya kubakika ligi kuu.

TABORA KWAWAKA MOTO, YANGA WATAMBA KUWAZIMA RHINO, MINZIRO AWAHOFIA MBEYA CITY LEO CHAMAZI!!


Na Baraka Mpenja , Dar es salaam


MABINGWA watetezi wa ligi kuu soka Tanzania bara, Young African  kwa mara nyingine leo jioni wanachanga karata zao katika uwanja wa Ally Hassan Mwinyi, Mjini Tabora dhidi ya wenyeji wao Rhino Rangers.
Viingilio katika mechi hiyo muhimu kwa timu zote mbili ni sh. 5,000 kwa jukwaa kuu na sh. 3,000 mzunguko.
Afisa habari wa Yanga, Baraka Kizuguto amezungumza kwa njia ya simu na mtandao huu kutoka Tabora na kueleza kuwa kikosi kipo salama na jana jioni kilifanya mazoezi tayari kwa kuwavaa Rhino  leo hii.
“Hakuna majeruhi mpaka sasa. Wachezaji wote wapo katika morali nzuri. Kwetu sisi michezo yote ni muhimu, tunajitahidi kufanya vizuri ili tuweze kutetea ubingwa wetu”. Alisema Kizuguto kutoka Tabora.
Kizuguto aliwataka mashabiki wa klabu hiyo kujitokeza katika mchezo wa leo kuiangalia timu yao katika mchezo wa tatu tangu watolewe katika michuano ya ligi ya mabingwa barani Afrika.
Yanga wanahitaji pointi tatu ili kurudisha hadhi yao ya kutetea ubingwa wao kwasababu si kazi nyepesi kuwachomoa Azam fc waliopo kileleni.
Mpaka sasa Yanga wamejikusanyia pointi 40 baada ya kushuka dimbani mara 19, wakati Azam fc wamecheza mechi 20 wakijikusanyia pointi 44 kileleni.
Mpaka sasa Azam fc wanabakia kuwa timu bora kwasababu hawajapoteza mchezo wowote ligi kuu.
Yanga walitolewa ligi ya mabingwa na Al Ahly kwa penati 4-3 jijini Alexndria nchini Misri machi 9 mwaka huu, na baada ya kurejea ligi kuu hawajashinda mchezo hata mmoja.
Walitoka suluhu na Mtibwa Sugar uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro, na katikati ya wiki walitoka sare ya 1-1 dhidi ya Azam fc.
Kwa vyovyote vile hawana cha kupoteza leo hii zaidi ya kutafuta ushindi ili kurudisha imani yao kwa mashabiki.
Itakuwa kazi kwa kocha mkuu, Mholanzi Hans Van Der Pluijm kutuliza akili yake kuwapanga vijana wake ili kuwalowesha Rhino nyumbani kwao.
Rhino kwa upande wao wanaonekana kukata tamaa kubaki ligi kuu kwasababu mpaka sasa wamebakiwa na mechi 5 tu ikiwemo ya leo.
Katika mechi 21 walizocheza, wameambulia pointi 13 tu na wanaburuza mkia mpaka sasa.
Kocha mkuu wa klabu hiyo, Jumanne Chale alisema wanajipanga kuibuka na ushindi katika mechi zote zilizosalia wakianzia na Yanga.
“Tumefanya vibaya na kujichimbia kaburi. Lakini mpira una matokeo ya ajabu. Tunaweza kushinda mechi zote na kujinusuru”. Alisema Chale.
Hata hivyo alionesha kuzungumza hayo akiwa hana matumaini kwasababu mechi alizosaliwa nazo ni ngumu zaidi kuanzia ya leo dhidi ya Yanga. 
Mbali na mchezo huo wa Tabora, nayo JKT Ruvu itakuwa mwenyeji wa Mbeya City katika mechi itakayochezwa leo, Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.
Kocha msaidizi wa Mbeya City, Maka Mwalwisyi ameuambia mtandao huu kuwa kikosi chao kipo salama isipokuwa mchezaji Richard Peter aliyepata majeruhi katika mchezo uliopita dhidi ya Rhino Rangers uwanja wa sokoine jijini Mbeya.
“Timu zote zinacheza kwa mitazamo miwili. Kuna timu zinahitaji ubingwa, kuna timu zinataka kukwepa kushuka daraja. Kwasababu hizi ushindani umekuwa mkubwa. Sisi tunafurahi kuona ushindani mkubwa ili bingwa apatikane kwa halali”.
“Tunawaheshimu JKT Ruvu, wapo katika wakati mgumu kwasasa. Tumejipanga kushindana na kuvuna pointi tatu muhimu”. Alisema Maka.
Maka aliwataka mashabiki wao kujitokeza kwa wingi Chamazi kwani kushinda leo kutawapa nguvu zaidi ya kujikita nafasi za juu.
Naye kocha wa JKT Ruvu, Fredy Felix Minziro alisema Mbeya City ni wazuri zaidi, hivyo wanakabiliwa na mechi ngumu zaidi.
“sisi tunahitaji pointi tatu, Mbeya City wanahitaji pointi tatu. Tunajua wazi kuwa wapinzani wetu ni wazuri, lakini kikosi chetu kipo katika hali nzuri na tunajipanga kuibuka na ushindi”. Alisema Minziro.
Ligi hiyo itaendelea keshokutwa (Jumapili) kwa mechi nne ambapo Simba itacheza na Coastal Union katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Azam itaoneshana kazi na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Azam Complex. Mechi hizo mbili zitakuwa ‘live’ kupitia Azam Tv.
 Mechi nyingine za Jumapili ni Mgambo Shooting dhidi ya Mtibwa Sugar kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga, wakati Ruvu Shooting na Ashanti United zitapimana ubavu kwenye Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.

EL CLASSICO: BALE VS NEYMAR NANI AMEKUWA USAJILI MZURI NDANI YA VILABU VYA BARCA NA REAL MADRID


Usajili wao katika vilabu vya Real Madrid na FC Barcelona wakati wa dirisha kubwa la usajili lilopita ndio ulitingisha zaidi vyombo vya habari duniani - Neymar alijiunga FC Barcelona na Gareth Bale alienda Real Madrid.

Wakati tukielekea kushuhudia El Classico wikiendi hii, ebu tutazame nani kati yao hawa wachezaji wawili amekuwa ndio usajili mzuri ndani ya vilabu hivi vikubwa duniani.

Bale alianza msimu kwa wakati mgumu sana kwa kuwa na majeruhi ya mara kwa mara, Neymar alianza vizuri ingawa nae hapa katikati alipata majeruhi kwa wiki kadhaa ila amerudi.

Katika mechi ya kwanza ya El Classico Neymar alitoka anacheka, Bale na timu yake walitoka kwenye dimba la Camp Nou baada ya kufungwa. Real Madrid wakiwa kileleni kwa tofauti ya pointi 4 - mechi ya wikiendi dhidi ya FC Barcelona inaweza kuamua bingwa wa La Liga msimu huu.

Tukielekea kwenye mchezo huo ni vizuri tutazame nani baina ya Gareth Bale na Neymar - wachezaji wenye umri mdogo waliosajiliwa kwa fedha nyingi - yupi kati yao amekuwa bora zaidi ya mwenzake katika msimu wao wa kwanza ndani ya vilabu vyao.

Kitakwimu Gareth Bale amemzidi Neymar. Bale amefunga mabao 14 katika mechi 27, yakiwemo manne katika Champions League. Neymar amefunga mabao 10 katika mechi 28, matatu katika Champions League. Pia Bale ameshatoa pasi za magoli 14 wakati Neymar amefanikiwa kutoa 11.

Baadhi wanaweza kusema takwimu zinaweza zisitoe uhalisia wa mambo, lakini namba hazidanganyi na kwenye hili unaweza kabisa kuona kwamba Bale amekuwa usajili zaidi kuliko Neymar.

Wakati Neymar amekuwa akihangaika kuunda safu nzuri ya mashambulizi na Messi, Bale amekuwa mwiba mchungu kwa timu pinzani akiisaidia Madrid kukamata kilele cha La Liga kwa ushirikiano mzuri alionao na Ronaldo pamoja na Karim Benzema.

CHELSEA VS ARSENAL: WENGER HAJAWAHI KUMFUNGA MOURINHO - LEO ANATIMIZA MECHI 1000, JE ATAIVUNJA REKODI YA KUTOPOTEZA MECHI 75 YA MOURINHO DARAJANI


Arsene Wenger anatimiza mechi ya 1,000 leo katika mchezo dhidi ya timu ambayo inafundishwa na kocha ambaye Wenger hajawahi kumfunga hata mara moja - Jose Mourinho.

Wenger akiwa na Arsenal amekutana mara 10 na Chelsea inayofundishwa na Mourinho, katika mara hizo zote Wenger hajaambulia ushindi hata mmoja, zaidi ya sare 5 na vipigo vitano.

Mourinho na rekodi bora ya katika uwanja wa nyumbani Stamford Bridge - hajapoteza mechi hata moja kati ya 75 Chelsea ilizocheza uwanjani hapo chini ya Mourinho.

Kuelekea mchezo wa leo Je rekodi ya Mourinho itaendelea, au Wenger atatimiza mechi ya 1,000 na ushindi dhidi ya kocha aliyemdharau kwa kumuita 'bingwa wa kufeli'?

Jibu litapatikana majira ya 9 kwa saa za Afrika Mashariki wakati mahasimu wa jiji la London watakapokutana kukata mzizi wa fitna.

NINI MAONI YAKO KUHUSU HALI YA MAN UNITED BAADA YA VAN PERSIE KUTANGAZWA KUIKOSA MANCHESTER DERBY PAMOJA NA ROBO FAINALI VS BAYERN MUNICH

Mshambuliaji wa klabu ya Manchester United Robin van Persie ameripotiwa kwamba amepata majeruhi ya goti baada ya kuumia katika mchezo wa raundi ya pili wa hatua ya 16 ya ligi ya mabingwa wa ulaya dhidi ya Olympiakos uliopigwa katika dimba la Old Trafford, jumatano wiki hii.

Van Persie ambaye alifunga hat trick iliyoipeleka Man United hatua ya robo fainali alitolewa nje na machela katika mchezo huo katika dakika za mwisho za huo, na leo hii baada ya kufanyiwa vipimo kiundani imegundulika amepata majeruhi yatakayomuweka nje kwa muda wa wiki 4-6.

Kwa maana hiyo mdachi huyo ataukosa mchezo dhidi ya Manchester City pamoja na mchezo wa kwanza wa robo fainali ya UCL dhidi ya Bayern Munich, hivyo kuiachia timu yake pigo zito.

Nini maoni yako kuhusu kukosekana kwa Van Persie katika kikosi cha United hasa katika kipindi hiki kigumu cha mwishoni mwa msimu?

Friday, March 21, 2014

NADIR HAROUB, AMEJIIMARISHA NA KUIMAIRISHA SAFU YA ULINZI YA YANGA SC



Na Baraka MbolemboleMchezaji anatakiwa kupiga hatua siku zote katika uchezaji wake.
Unapopewa jukumu kama nahodha wa timu, linakuwa ni jambo la changamoto nyingine na linachangia kumfanya mchezaji kuwa bora, na ni kitu ambacho kinaweza kumfanya mchezaji kubadilika katika uchezaji wake kiujumla. 
Kama nahodha unakuwa na kiwango kisichobadilika, hasa katika
kupandisha kiwango cha uchezaji, watu watakusema kwa namna
wanavyotaka.

Kiwango cha sasa cha nahodha wa timu ya Yanga SC, Nadir Haroub kimeonekana kuimarika na kupanda. Wakati, Yanga ilipocheza michezo miwili dhidi ya Al Ahly ya Misri, katika ligi ya mabingwa Afrika, mapema mwezi huu na kuruhusu bao moja katika muda wa dakika 180, safu ya ulinzi ilionekana kucheza kwa umakini mkubwa huku, Nadir na Kelvin Yondan wameonekana kucheza kwa maelewano mazuri.

Unapobadilishiwa mtu wa kucheza nao kama beki wakati mwingine
linapelekea mchezaji kupata wakati mgumu kutokana na mazoea ambayo mara nyingi hujenga uimara wa beki kama safu muhimu ya timu. 
Nadir, amekuwa akicheza sambamba na Kelvin kwa msimu wa pilisasa, lakini kiwango chao wakicheza pamoja katika michezo dhidi ya Mtibwa Sugar na Azam FC, na namna ubadilikaji wa walinzi mchezo ni mzuri tofauti na walivyokuwa wakicheza katika siku za nyuma.

Hakuna kitu kigeni katika soka. Wakati mwingine mchezaji unatakiwa kuzoea kucheza tofauti na mchezo uliouzoea kutokana na msaidizi wako anavyokuwa akitimiza majukumu yake. Nadir ameonekana kupunguza makosa yake ya kuondoka mara kwa mara katika eneo lake la muhimu, kwa kuachana na stahili yake ya kucheza kwa kumfuata mshambuliaji wa timu
pinzani. 
Kama, Namba Tano, Nadir anatakiwa kucheza kwa kuwaongoza
wasaidizi wake huku yeye akicheza kwa kusahihisha makosa yanayokuwa yanafanywa na wenzake.

Katika umri wa miaka 31 sasa, mchezaji huyo ameonekana kutulia chini ya kocha, Hans. Kuwa nahodha inasaidia kujenga mtazamo wa ushindi muda wote kwa mchezaji. 
Kama unakuwa nahodha na huna sifa hizo si kitu kizuri, Nadir ni mchezaji mwenye usongo wa kupata ushindi uwanjani.

Wakati mwingine beki unapitwa na timu inafungwa, ni kitu ch
a kawaida. Lakini ni lazima kufanya jitihada kuzuia hilo kadri
iwezekanavyo. 
Mlinzi makini ni yule anayetazama mambo yaliyo muhimu na kuyazingatia, si vizuri kusikiliza sana yale yanayokuwa yakisemwa juu yako unapokuwa mchezaji.

Unapocheza vizuri watu wakakusifia inamfanya mchezaji ajisikie
vizuri, lakini ukisemwa vibaya unatakiwa kuwa na umakini wa ziada ili kutofanya makosa zaidi. 
Nadir, amecheza na walinzi wengi wa kati katika klabu yake tangu aliposajiliwa mwaka 2007. Lulanga Mapunda, Wisdom Ndlovu,Isack Boakey, Chacha Marwa, Ibrahimu Job, Mbuyu Twite,
ila kiwango chake cha sasa akicheza na Kelvin kinaonesha kuimarika na kupevuka kiuchezaji. Ni wakati mzuri sasa kwa upande wake, na timu yake pia.

Nadir, ametokea kujiamini sana, kupunguza papara, kuondosha mipira inayoingia katika maeneo yao ya hatari, amekuwa akiwapanga wenzake na yeye binafsi katika mchezo, jambo ambalo limemfanya kucheza akiwa huru na kujiamini. 
Kama watazidi kuboresha mahusiano yao ya kiuchezaji na
Kelvin, Nadir atacheza kwa muda mrefu katika timu hiyo kawaida.
Lakini ni lazima kufanya jitihada kuzuia hilo kadri iwezekanavyo.
Mlinzi makini ni yule anayetazama mambo yaliyo muhimu na kuyazingatia

Si vizuri kusikiliza sana yale yanayokuwa yakisemwa juu yako unapokuwa mchezaji. Unapocheza vizuri watu wakakusifia inamfanya mchezaji ajisikie vizuri, lakini ukisemwa vibaya unatakiwa kuwa na umakini wa ziada ili kutofanya makosa zaidi. 

Nadir, amecheza na walinzi wengi wa kati katika klabu yake tangu aliposajiliwa mwaka 2007. 
Lulanga Mapunda, Wisdom Ndlovu,Isack Boakey, Chacha Marwa, Ibrahimu Job, Mbuyu Twite, ila kiwango chake cha sasa akicheza na Kelvin kinaonesha kuimarika na kupevuka kiuchezaji. Ni wakati mzuri sasa kwa upande wake, na timu yake pia. Ukuta wa Yanga umeimarika sasa, na kiwango cha Nadir kinapelekea safu nzima ya ulinzi kucheza kwa mpangilio na umakini wa kuepuka makosa yasiyo na ulazima.

KIKOSI KAZI KUSHUGHULIKIA TIKETI ZA ELEKTRONIKI - TFF NA CRDB WAJIPANGA NAMNA YA KUMALIZA TATIZO

(Picha kwa hisani ya Saleh Ally)
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na benki ya CRDB zimeunda kikosi kazi (task force) kwa ajili ya kushughulikia matumizi ya tiketi za elektroniki ambayo yalisimamishwa kutoka na changamoto mbalimbali zilizokuwa zimejitokeza.

TFF na CRDB zimefanya kikao cha pamoja jana (Machi 20 mwaka huu) kuhusu masuala ya tiketi za elektroniki na kukubaliana kuunda kikosi kazi hicho kwa ajili ya uboreshaji matumizi ya mfumo huo.

Kikosi kazi hicho kitakuwa na wajumbe kutoka TFF na CRDB. Kwa upande wa TFF wajumbe wake ni Mkurugenzi wa Sheria na Uanachama, Evodius Mtawala, Ofisa Habari na Mawasiliano, Boniface Wambura na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Ligi Kuu Tanzania (TPLB), Silas Mwakibinga.

Rais wa TFF, Jamal Malinzi ametoa shukrani za kipekee kwa Mkurugenzi Mtendaji wa benki ya CRDB, Dr. Charles Kimei ambaye alihudhuria binafsi kwenye kikao akiongoza timu yake.


Malinzi amesema ni imani ya TFF kuwa mfumo wa tiketi za elektroniki ndiyo mkombozi wa ulinzi wa mapato milangoni, na anaamini kwa pamoja TFF na CRDB zitafanikisha matumizi hayo ya tiketi za elektroniki.

YANGA KUCHANGA KARATA TENA TABORA, MBEYA CITY WAINYATIA JKT RUVU, AZAM FC KUSUBIRI KWA HAMU MATOKEO!!


Na Baraka Mpenja, Dar es salaam


MABINGWA watetezi wa ligi kuu soka Tanzana bara, Young Africans leo jioni wanatarajia kufanya mazoezi katika uwanja wa Ally Hassan Mwinyi , mjini Tabora kujiwinda na mchezo wa kesho dhidi ya wenyeji, Rhino Rangers.

Yanga waliwasili mjini Tabora jana usiku wakiwa na tafakuri nzito ya kutafuta pointi tatu muhimu ili kuwasogelea Azam fc waliopo kileleni katika msimamo wa ligi.

Mpaka sasa Yangaa wapo nafasi ya pili wakiwa na pointi 40 baada ya kucheza mechi 19, wakati Azam fc wameshajikusanyia pointi 44 kileleni kwa kushuka dimbani mara 20.

Timu hizi mbili zilitoka sare ya bao 1-1 jumatano ya wiki hii katika mchezo uliochezwa uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Hata hivyo, Azam fc walionekana kuwa bora zaidi kwani kwa dakika 20 za mwisho walicheza wakiwa pungufu kufuatia beki wake wa kulia, Erasto Edward Nyoni kutolewa nje kwa kadi nyekundu kwasababu ya kutoa lugha chafu kwa mwamuzi.

Azam fc hawajafungwa mechi hata moja msimu huu, na malengo yao ni kutwaa ubingwa.

Kocha wa Yanga, Mholanzi, Hans Van Der Pluijm baada ya mechi ya jumatano  alisema anajipanga kufanya vizuri mechi ya kesho na nyingine zote zilizosalia.

Kushinda kwa Yanga hapo kesho kutawafanya warudishe hadhi yao ya kutetea ubingwa msimu huu,

Wakati Yanga wakihitaji ushindi ili kujiweka mazingira mazuri ya kutwaa taji, wenyeji wao, Rhino wanahangaika kukwepa mkasi wa kushuka daraja.

Kikosi hicho cha kocha Jumanne Chale mpaka sasa kinaburuza mkia kwa kujikusanyia pointi 13 kufuatia kushuka dimbani mara 21.

Rhino wamebakiza mechi 5 ambazo wanahitaji kushinda zote ili kurejesha matumaini, japokuwa inaonekana kuwa ndoto.

Kwa hesabu za haraka, maafande hawa wa JWTZ kama vile wameshashuka daraja, ingawa mpira wa miguu huwa hauendi kwa hesabu rahisi kiasi hiki.

Kama Rhino watashinda kesho na mechi nyingine zote zilizobaki, basi wanaweza kufikisha point 28 ambazo pengine zitaweza kuwaokoa.

Kushinda mechi zote itakuwa ngumu hasa kwa kuanzia na kipute cha  kesho dhidi ya Yanga wenye uhitaji mkubwa wa Pointi kwasasa.

Mechi nyingine yenye msisimko hapo kesho ni baina ya JKT Ruvu dhidi ya Mbeya City katika uwanja wa Azam Complex, Chamazi.

Mechi hii ni muhimu kwa timu zote kwani JKT Ruvu wapo katika harakati za kukwepa kushuka daraja.

Kwasasa kocha wake, Fredy Felix Minziro hana cha kupoteza zaidi ya kutafuta ushindi. Hivyo wataingia uwanjani kwa nguvu zote.

Haitakuwa kazi nyepesi kwa Minziro kupata matokeo mazuri hapo kesho, kwasababu Mbeya City wanahitaji zaidi pointi ili kujikita katika nafasi za juu.

Mpaka sasa Mbeya City wapo nafasi ya tatu kwa pointi 39, hivyo wakishinda kesho watafikisha pointi ­42.

Kupanda nafasi itategemeana na matokeo ya Tabora ambapo Yanga watakuwa na kibarua na Rhino.

Kama Yanga atashindwa kupata matokeo ya ushindi na Mbeya City atashinda, basi wanajangwani watazidi kujiweka mazingira hatari zaidi kwasababu wataporomoka kwa nafasi moja.

Ligi kuu itaendelea tena siku ya jumapili, ambapo uwanja wa Taifa, Simba SC watakuwa wenyeji wa Coastal Union .
Hiyo itakuwa mechi ngumu kwa timu zote kwasababu kocha wa Simba, Dravko Logarusic hahitaji kuona anapata matokeo mabaya kwa mara nyingine.

Loga ataingia akiwa na presha kubwa nyuma yake kutokana na ukweli kuwa Simba haijawa katika ubora wake wa siku za nyuma.

Mpaka sasa Mnyama yupo nafasi ya nne kwa pointi 36 kibindoni na ameshuka dimbani mara 21.

Nao Coastal Union hawataki kufungwa tena ukizingatia wikiendi iliyopita walifungwa mabao 4-0 na Azam fc uwanja wa Azam complex Chamazi.

Nao vinara wa ligi hiyo, Azam fc watakuwa nyumbani kwao Azam complex kuumana na JKT Oljoro.

Mechi hiyo ni muhimu kwa Oljoro kwani wapo hatarini kushuka daraja msimu huu, hivyo hawana cha kutafuta zaidi ya pointi tatu kwao.

Lakini utakuwa muhimu zaidi kwa Azam fc, kwani kushinda kwao kutawafanya kuwa katika mazingira mazuri ya kubeba ndoo ya ubingwa kwa mara ya kwanza.

Azam fc wakishinda watazidi kusogelea ubingwa, lakini wakishindwa kupata matokeo mazuri, Yanga wakashinda Tabora, basi watakuwa wamejitia hatiani.
Ruvu Shooting watakuwa wenyeji wa Ashanti United Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.

BREAKING NEWS: MAN UNITED YAPANGWA NA BAYERN MUNICH ROBO FAINALI CHAMPIONS LEAGUE


Barcelona v Atletico Madrid
Real Madrid v Borussia Dortmund

Paris St Germain v Chelsea

Manchester United v Bayern Munich

Mechi kuchezwa April 1/2 and April 8/9

R.I.P NGAPASA ' KEKE BOY ' MAPUNDA,LEO UMETIMIZA MIAKA MINNE TANGU ULIPOTUTOKA GHAFLA.


Thursday, March 20, 2014

DAUDA TV :MHESHIMIWA BALOZI WA BRAZIL NCHINI TANZANIA FRANCISCO LUZ AZUNGUMZIA MAANDALIZI YA KOMBE LA DUNIA.

DAUDA TV: MAGOLI YA MCHEZO WA AZAM NA YANGA.

DWIGHT YORKE: MAN UNITED INAWEZA KUZIFUNGA ATLETICO, PSG AU DORTMUND - NISINGEPENDA TUPANGWE NA BARCA, REAL AU BAYERN

H

REAL MADRID HAWAJAPOTEZA MECHI KATIKA KIPINDI CHA MIEZI 5 ILIYOPITA - JE BARCA WATAIVUNA REKODI HIYO KWENYE EL CLASSICO WIKIENDI HII?

Real Madrid C.F. hawajapoteza mechi hata moja katika kipindi cha miezi 5 iliyopita - FC Barcelona ndio timu ya mwisho kuifunga Real Madrid. Wiki hii timu hizo zinakutana katika El Classico - unadhani Barca wataivunja rekodi ya kutokufungwa kwa Real Madrid?

BAO LA KAVUMBAGU DHIDI YA AZAM LAMUUA SHABIKI WA YANGA SC

SHABIKI wa Timu ya Yanga SC, Deodatus Isaya Lusinde, mkazi wa Kipunguni A, amefariki dunia leo baada ya kuanguka ghafla wakati akishangilia bao la Yanga lililofungwa na Didier Kavumbagu katika dakika ya 14 kipindi cha kwanza.
Marehemu amepoteza maisha akiwa chumba cha matibabu mara baada ya kuwekewa mashine ya oksijeni na taarifa kuhusu kifo cha shabiki huyo zimethibitishwa na mmoja wa madaktari aliyemhudumia akiwa uwanjani kabla ya mauti kumfika, Nassor Matuzya.
Bwana Isaya alikuwa Meneja wa Bar ya Rose Hill iliyopo Segerea jijini Dar. Ameacha mke aitwaye, Rose William Lusinde ambaye ni askari magereza.
Marehemu amekutwa na mauti hayo wakati wa mechi ya Ligi Kuu Tanzania Bara, kati ya timu yake ya Yanga na Azam, mchezo uliomalizika kwa sare ya bao 1-1.
Mungu ailaze roho ya mwanamichezo, Deodatus Isaya Lusinde mahali pema peponi. AMEN!

MAN UNITED VS WEST HAM: SAM ALLARDYCE ANAKUTANA NA MWANAFUNZI WAKE MOYES ALIYEMTOA SCOTLAND NA KUMLETA ENGLAND


Zikiwa zimebakia siku kadhaa kabla ya mechi ya West Ham United vs Manchester United wikiendi hii, kocha wa West Ham  Sam Allardyce, ametoa historia ya kuvutia kuhusu yeye na David Moyes.
Allardyce anasema mwaka 1993, wakati akiwa kocha wa timu ya vijana ya Preston, alienda kumuangalia Moyes akiichezea Dunfermline dhidi ya Falkirk ili aone uwezo wake kama anafaa kusajiliwa, na alitumwa na kocha mkuu wa timu ya Preston John Beck.

Na pamoja Moyes kuonyeshwa kadi nyekundu kwa kushika mpira makusudi katika kipindi cha kwanza dakika ya 38, Allardyce aliridhishwa na uwezo wake na akampelekea ripoti nzuri kocha mkuu Beck.
Moyes alipokuwa akiichezea Preston ambayo Allardyce alikuwa kocha msaidizi
Moyes hatimaye alihamia Preston, na baada ya mechi 159 mscotish huyo akawa kocha wa timu hiyo, lakini alikosa nafasi ya kupanda ligi kuu ya England baada ya kufungwa kwenye play-offs na Everton mnamo 2002.
Kuelekea mchezo ambao utawakutanisha Allardyce na Moyes wakati United itakapoifuata West Ham Upton Park, kocha wa West Ham anakumbuka alivyomuona Moyes mara ya kwanza. 
Allardyce alisema: 'Alitolewa kwa kadi nyekundu baada ya dakika ya 38 za mchezo. Niliendesha gari mpaka Scotland,  John Beck alinituma nikamtazame. 
'Lakini ndani ya hizo dakika 38 nilijua kwamba angefaa kuitumikia Preston." 

KWA MILIMA HII ILIYOBAKI, YANGA, AZAM FC, SIMBA, MBEYA CITY NANI KUTWAA TAJI LIGI KUU MSIMU HUU?



Na Baraka Mpenja , Dar es salaam


KINYANG`ANYIRO cha ubingwa wa ligi kuu soka Tanzania bara msimu wa 2013/2014, bado kinabaki kuwa kitendawili kwa timu zilizopo juu katika msimamo.

Sare ya bao 1-1 jana uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam baina ya vinara Azam fc dhidi ya Yanga imezidi kuweka mazingira magumu kwa mabingwa watetezi, Young African.

Katika mchezo huo  uliovuta hisia za mashabiki, Yanga walikuwa wa kwanza kufunga bao kipindi cha kwanza kupitia kwa Didier Kavumbagu, lakini Azam fc walisawazisha dakika za lala salama kupitia kwa kinda, Kevin Friday.

Hiyo ilikuwa mechi ya 19 kwa Yanga, wakati kwa Azam fc ilikuwa ya  20, huku wakijikusanyia pointi 44, wakati Wanajangwani wakivuna pointi 40 katika nafasi ya pili.

Yanga SC wamebakiza mechi 7, wakati Azam fc wamebakiza mitanange  6.

Wikiendi hii timu zote zitashuka dimbani. Yanga watasafiri mpaka mkoani Tabora kuwafuata maafande wa Rhino Rangers, wakati jumapili machi 23, Azam fc watawakaribisha JKT Oljoro,  uwanja wa Azam Complex Chamazi.

Rhino Rangers ndio wanaoburuza mkia katika msimamo wakiwa wameshacheza mechi 21 na kujikusanyia pointi 13 tu kibindoni.

Kwa asilimia kubwa, maafande hawa wa Tabora, wameshachungulia kushuka daraja na inawezekana hakuna muujiza wa kubaki ligi kuu msimu huu kwasababu ya mazingira yao.

Mchezo dhidi ya Yanga utakuwa mkali endapo bado Rhino wanahitaji ushindi.

Lakini imani yao imeshuka na wanacheza bora liende na wameshapoteza matumanini ya kuendelea kucheza ligi kuu.

Pointi 13 kwa mechi 21 ni chache sana, zinahitajika nguvu za ziada kushinda mechi zote 5 walizobakiza, hapo sasa tunaweza kuzungumza mengine.

Yanga wataingia uwanjani wakiwa ma matokeo ya sare ya jana na suluhu ya Mtibwa Sugar wiki iliyopita uwanja wa Jamhuri.

Yanga sc hawajafanya vizuri mechi zao mbili tangu watolewe na Al Ahly ligi ya mabingwa kwa penati 4-3, machi 9 mwaka huu, jijini Alexndria,  hivyo hawana cha kuwaza zaidi ya ushindi.

Kama watashindwa kupata ushindi katika mchezo huo, watakuwa wanazidi kuweka rehani ubingwa wao msimu huu.

Kwa maana hiyo, kocha mkuu wa Yanga, Hans Van Der Pluijm lazima awaeleze vijana wake umuhimu wa mechi ya jumamosi endapo wanahitaji ketetea taji lao.

Wakati Yanga wakiwa kwenye mawazo mazito juu ya mchezo huo, wapinzani wao, Azam fc watakuwa wanasubiria matokeo ili kujipanga kwa mchezo wa kesho yake.

JKT Oljoro  waliopoteza matumanini ya kusalia ligi kuu msimu , wataingia kuwavaa Azam fc ambao hawajapoteza mchezo mpaka sasa kwa lengo la kutafuta pointi tatu.

Mechi za karibuni zinaonesha kuwa Azam fc wamekuwa bora zaidi katika uwanja wao kwasababu  wanagawa dozi kubwa kwa wapinzani.

Mechi iliyopita waliwafunga Coastal Union mabao 4-0, hivyo JKT Oljoro wasipokuwa makini watachezea kipigo.

Endapo Azam fc watashinda mechi hiyo, watazidi kujikita zaidi kileleni, nao Yanga wakishinda watandelea kuwa wa pili.

Matokeo ya sare au suluhu hayatakuwa mazuri kwa Yanga, kwasababu Mbeya City waliopo nafasi ya tatu nao watacheza na JKT Ruvu jumamosi uwanja wa Chamazi.

Kama Yanga hawatashinda na Mbeya City wakapata matokeo ya ushindi, basi Yanga watashuka nafasi ya tatu.

Hata kama watatoa sare au suluhu mjini Tabora, bado Yanga watabaki nafasi ya tatu, kwani Mbeya City watakuwa wamefikisha pointi 42, Yanga 41.

Kama Yanga watashinda na Mbeya City watashinda, basi nafasi za pili na tatu zitabaki kama zilivyo.

Matokeo yoyote ya Yanga na Mbeya City hayatakuwa na athari kwa Azam fc katika nafasi ya kwanza, isipokuwa watasogelewa kwa pointi.

Wakati Yanga na Azam fc wakichunao vikali kusaka ubingwa, mechi zilizosalia kwa timu zote ni kama zifuatazo;

Yanga wamebakiza mechi dhidi ya Rhino Rangers itakayochezwa machi 22 mwaka huu uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora.

Baada ya hapo atakuwa na mechi dhidi ya Tanzania Prisons uwanja wa Taifa.

Ugumu wa mechi hizi mbili unatokana na mazingira ya Prisons na Rhino kwa sasa.
Hawataki kushuka daraja, zaidi Prisons wamedhamiria kubakia lihi kuu kuliko Rhino wanaoonekana kukata tamaa.

Haitakuwa kazi nyepesi kwa Yanga kuwafunga wajelajela hao uwanja wa Taifa, jijini Dar es salaam.

Mechi nyingine zilizosalia kwa Yanga ni dhidi ya Mgambo JKT, Uwanja wa Mkwakwani Tanga.

Hii pia itakuwa na changamoto kubwa kwasababu Mgambo wanajinusuru kushuka daraja msimu huu.

Pia Yanga wamebakiza  mechi dhidi ya Kager Sugar, Uwanja wa Taifa, mechi dhidi ya JKT Oljoro, jijini Arusha, mechi na JKT Ruvu uwanja wa Taifa.

April 19 mwaka huu Yanga watafunga msimu kwa kuvaana na Simba sc uwanja wa Taifa.

Katika mechi saba zilizosalia kwa Yanga, mechi mbili pekee ndizo atakutana na timu zilizopo salama msimu huu na zinahitaji nafasi nne za juu.

Kagera Sugar mpaka sasa wana uhakika wa kusalia ligi kuu pamoja na Simba sc ambao wanasaka nafasi za juu.

Mechi nyingine zote, Yanga atakutana na timu zinazopambana kukwepa mkasi wa kushuka daraja. Hivyo lazima ajiandae kwa nguvu zote kwasababu kukamiana kutakuwepo.

Kila timu inahitaji kupata ushindi bila kujali inakutana na timu kubwa au ndogo.

Kocha wa Yanga , Mholanzi, Hans Van Der Pluijm akisaidiwa na Charles Mkwasa wanahitaji  kutuliza sana akili zao kuelekea mechi hizo.

Azam fc amebakiza mechi sita ambazo ni dhidi ya JKT Oljoro, Mgambo, Ruvu shooting, JKT Ruvu, Mbeya City na Simba sc.

Mechi dhidi yaMbeya City itakayopigwa sokoine Mbeya, itakuwa ngumu zaidi kwa Azam fc kulingana na rekodi ya Mbeya City katika uwanja wake.

Mbeya City hawajawahi kufungwa kwao, hivyo lazima Azam fc wajiandae kama wanataka kuvunja rekodi hii.

Pia Mbeya City wanasaka ubingwa wa kwanza kama ilivyo kwa Azam fc. Tofauti ni umri katika ligi. Azam fc waliingia 2008/2009, Mbeya City waliingia 2013/2014.

Azam fc ameshakuwa makamu bingwa kwa zaidi ya misimu miwili, wakati Mbeya City ndio kwanza wanaanza kutafuta mafanikio.

Mechi hii itakuwa ngumu kwa timu zote mbili, matokeo yatategemea jinsi makocha wote wawili, Juma Mwambusi wa Mbeya City na Mcameroon, Joseph Marius  Omog wa Azam fc wamejipangaje.

Pia mechi dhidi ya Simba sc itakuwa mlima mwingine kwa Azam fc kwasababu Simba hawatakuwa na chakupoteza zaidi ya kusaka ushindi.

Kwa mazingira ya mechi za Azam fc, itakuwa ngumu kwake kupata ushindi kwenye baadhi ya mechi kwasababu wapinzani wake wanahitaji kujiweka vizuri katika msimamo.

Simba na Mbeya City wanawania nafasi za juu. Ruvu Shhoting anatafuta nafasi nzuri pia.

Mgambo, JKT Ruvu, JKT Oljoro wapo katika hatihati ya kukwepa kushuka daraja, hivyo mechi zao zitakuwa ngumu zaidi kutokana na kukutana na timu ambayo inaongoza ligi.

Haitakuwa kazi nyepesi kwa Azam fc kuibuka na ushindi katika mechi hizi, lakini kama watajiandaa vizuri basi wataweza kuvuna ushindi na kujihakikishia kutwaa ubingwa msimu huu.

Ligi ya mwaka huu imekuwa na changamoto kubwa kutokana na timu kubwa za Simba na Yaga kushindwa kufua dafu kwa Azam fc na Mbeya City.

Misimu ya nyuma, mpaka sasa ilikuwa rahisi kubashiri bingwa, na wakati mwingine timu ilikuwa inatangaza ubingwa kabla ya mechi tatu au nne.

Kwa msimu huu jambo hilo limebaki kuwa ndoto, ubingwa utaonekana mechi za mwisho, kwani mpaka sasa mbio bado zipo wazi kwa klabu zaidi ya moja.

Katika soka, hii ni hatua nzuri kwasababu inadhirisha zimekuweo timu zaidi ya mbili zenye ubora wa juu, tofauti na miaka ya nyuma iliyokuwa na ufalme wa Simba na Yanga.

Tuzidi kusubiri ili kuona nani ataibuka kidume katika nafasi nne za juu.

SALUM MADADI - BOSI MPYA WA UFUNDI TFF


Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limemteua Salum Madadi kuwa Mkurugenzi wake mpya wa Ufundi.

Uteuzi huo umefanya na Kamati ya Utendaji katika kikao chake cha dharura kilichofanyika jana (Machi 19 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

Kabla ya uteuzi, Madadi alikuwa akikaimu nafasi hiyo tangu Januari mwaka huu baada ya Mkurugenzi wa Ufundi aliyekuwepo kumaliza mkataba wake Desemba 31 mwaka jana.

Madadi mwenye leseni A ya ukocha ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) ni kocha mwenye uzoezi wa zaidi ya miaka 30 ambapo alianza kufundisha mpira wa miguu mwaka 1980 katika klabu ya Maji SC ya Lindi.

Ana elimu ya sekondari aliyoipata katika shule ya Chidya na diploma ya ukocha wa mpira wa miguu aliyoipata nchini Ujerumani. Pia ni Mkufunzi wa makocha wa CAF, na alijiunga na TFF mwaka 2006 akiwa Ofisa Maendeleo.

Alikuwa Kocha wa Taifa Stars mwaka 2000. Mbali ya Maji SC, amewahi kufundisha timu za Nyota Nyekundu, Ushirika ya Moshi, Simba, Shangani ya Zanzibar, Malindi ya Zanzibar, Cardif ya Mtwara na Kariakoo ya Lindi.


Pia amewahi kuwa mjumbe wa Kamati ya Ufundi ya Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).

SIMBA NA YANGA WAPIGWA FAINI YA MILLIONI 25 KWA VURUGU KWENYE YA AL AHLY

Klabu za Yanga na Simba zimeagizwa kulipa jumla ya sh. milioni 25 kutokana na uharibifu wa viti na vurugu zilizofanywa na washabiki wao kwenye mechi ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya Yanga na Al Ahly ya Misri iliyochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Yanga italipa sh. milioni 15 ambayo ni gharama ya uharibifu wa viti uliofanywa na washabiki kwenye mechi hiyo. Pia imepigwa faini ya sh. milioni tano kutokana na vurugu za washabiki wake. Nayo Simba imepigwa faini ya sh. milioni tano kutokana na washabiki wake kuhusika katika vurugu hizo.
Uamuzi huo umefanywa na Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) katika kikao chake cha dharura kilichofanyika jana (Machi 19 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.


Tunatoa onyo kwa washabiki wa mpira wa miguu kujiepusha na vurugu viwanjani ikiwemo uharibifu wa miundombinu mbalimbali ya viwanja ikiwepo viti, na tutachukua hatua kali zaidi kwa klabu na washabiki wake iwapo vitendo hivyo vitajitokeza tena.

KIBONZO: NAMNA YA TIMU PINZANI ZINAVYOOMBA KUKUTANA NA MAN UNITED ROBO FAINALI UCL