Search This Blog

Saturday, March 29, 2014

SIMBA SC YAIWINDA AZAM FC JUMAPILI, LOGA ATULIZA AKILI MABIBO!!

Na Baraka Mpenja , Dar es salaam

0712461976

SIMBA SC yenye matokeo mabovu kwasasa inaingia kambini  maeneo ya Mabibo jijini Dar es salaam kuandaa kikosi cha kuwavaa vinara wa ligi kuu soka Tanzania bara, wana Lambalamba, Azam fc siku ya jumapili uwanja wa Taifa.


Hiyo ni hatua ya Simba kuweka akili sawa ili kukwepa kipigo kwa mara nyingine baada ya kufumuliwa bao 1-0 na Wagosi wa Kaya, Coastal Union ya jijini Tanga mwishoni mwa wiki iliyopita.


Afisa habari wa Simba aliuambia mtandao huo kuwa uongozi wa Simba unasikitishwa na matokeo mabaya  wanayozidi kupata msimu huu licha ya kuwaweka wachezaji wao katika hali nzuri kuanzia mishahara, kambi na posho.


“Hakuna mchezaji mwenye tatizo na benchi la ufundi au uongozi. Wote wanalipwa vizuri mishahara na posho zao. Mengi yanazungumzwa kuwa hawalipwi, Si kweli, hakuna mchezaji anayeidai klabu”.


“Hata sisi hatuelewi kwanini tunapata matokeo mabovu. Hatuna jinsi, lazima tukubali ukweli kwasababu mpira unachezwa uwanjani. Lakini kuumia kuko palepale”. Alisema Asha.


Afisa habari huyo aliwaomba mashabiki wao kukubali na hali halisi inayotokea uwanjani, kwasababu kuna wakati mpira unawakataa wachezaji.


“Benchi la ufundi wanafanya kazi kubwa kuandaa kikosi chetu. Lakini tukiingia uwanjani mambo yanakuwa magumu. Ni upepo mbaya tu msimu huu. Tunajipanga kwa nguvu zote kushinda mechi zilizosalia.


Kuhusu mchezo wa jumapili dhidi ya Azam fc, Asha alisema itakuwa mechi ngumu kwao, lakini wanajiandaa kupata matokeo ili kuepuka kipigo ambacho kitawavunja moyo zaidi mashabiki wao.


Wakati hayo yakijiri kwa upande wa Simba sc, Azam fc wameendelea kufanya vizuri zaidi msimu huu kufuatia ushindi wa mabao 2-0 huko Tanga dhidi ya Mgambo JKT katikati ya wiki.


Afisa habari wa Azam fc, alisema kikosi cha Mcameroon, Joseph  Marius Omog kina nia ya kutwaa ubingwa msimu huu na sivinginevyo.


“Mechi zote ni ngumu kwetu. Tunawashukuru wachezaji wetu kwa kuelewa malengo ya Azam fc msimu huu”.


“Wamekuwa wakipigana sana uwanjani. Tunawaheshimu  Simba sc, lakini tunajiandaa kuwavaa kwa lengo la kutafuta pointi tatu”. Alisema Jafar.


Azam fc wamekuwa na safu nzuri ya ushambuliaji kutokana na mabao mengi wanayofunga kwa mechi za karibuni.


Wakati huo huo wataingia katika mchezo wa jumapili  wakiwa na kumbukumbu ya kuwafunga Simba sc mabao 2-1 mzunguko wa kwanza.

Kipindi hicho, Azam fc walikuwa chini ya kocha, Muingereza, Sterwat John Hall, wakati Simba walikuwa chini ya kocha wake, Abdallah Kibadeni `King Mputa`.


Itakuwa ni vita kali baina ya mabeki wa Simba sc, Haruna Shamte, Issa Rashid `Baba Ubaya` Joseph Owino, Donald Mosoti dhidi ya washambuliaji wa Azam fc John Bocco `Adebayor`, Kipre Tchetche.


Katikati Henry Joseph, Said Ndemla, Omary Salum, William Lucian ‘Gallas’  na Jonas Mkude watakuwa wanachuana na  Michael Bolou, Himid Mao, na Salum Abubakar `Sureboy`.


Erasto Edward Nyoni, Michael Gardiel, Aggrey Morris na David Mwantika,  watakuwa na kibarua kizito cha kuwazuia Haroun Chanongo, Amisi Tambwe na Ramadhani Singano ‘Messi’ ambao wanategemewa kupangwa siku hiyo.


Kocha wa Azam fc, Joseph Marius Omog amefanikiwa kuifanya Azam kuwa kileleni kwa kutofungwa mechi yoyote msimu huu.


Matajiri hao wa Bongo wameshuka dimbani mara 22 na kujikusanyia pointi 50 kileleni.


Dravko Logarusic, Kocha wa Simba sc, ameshindwa kuipa mafanikio Simba kama ilivyotarajia na mashabiki wake.


Simba inashika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi 36.

AZAM FC, YANGA, PENGO LA POINTI LIGI KUU KUBAKI 1 AU 4 JUMAPILI?

Na  Baraka Mpenja, Dar es salaam


0712461976


KITENDAWILI cha klabu gani itatwaa taji la ligi kuu soka Tanzania bara msimu huu hakichateguliwa kwasasa, na hapo kesho kutakuwa na  mechi muhimu kwa timu zinazopigiwa upatu  wa kutwaa ubingwa, Yanga na Azam fc.

Vinara Azam fc watakuwa uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam kukabiliana na kikosi cha Simba, wakati mabingwa watetezi, Young Africans watakuwa na kibarua kizito mbele ya wapiga kwata wa Mgambo JKT, kwenye uwanja wa CCM Mkwakwani, jijini Tanga.

Mechi ya Azam fc dhidi ya Simba sc itakuwa ngumu kwa klabu zote, lakini kwa Wana Lambalamba ina uzito wa hali ya juu katika mbio zao za kutwaa ubingwa.

Kama watapoteza mechi hiyo, halafu Yanga wakapata ushindi jijini Tanga, Azam watajiweka mazingira magumu zaidi ya kubeba mwari wao wa kwanza tangu waingie  ligi kuu msimu wa 2008/2009.

Yanga nao watatakiwa kuwa na mipango mizuri ya uwanjani dhidi ya Magambo kesho, kwasababu rekodi ya nyuma inaonesha wapinzani wao wamekuwa wagumu kufungwa Mkwakwani.

Hukutakuwa na sababu yoyote kwa kikosi cha Yanga kuwadharau Mgambo kwakuwa wapo katika mstari mwekundu wa kushuka daraja.

Maskari hawa wa  Jeshi la kujenga Taifa wanahitaji ushindi kwa nguvu zote kwasababu ndio matokeo pekee yanayowafaa kwasasa.

Taarifa kutoka Tanga zinaeleza kuwa kocha mkuu wa Young Africans,  Mholanzi Hans Van der Pluijm amewasifia vijana wake kwa kumuelewa vizuri na kushika vilivyo mafunzo yake.

Sababu kubwa inayotumiwa na  Pluijm ni matunda yaliyoanza kuonekana katika michezo miwili iliyopita kwa timu kuweza kujikusanyia pointi 6 na magoli nane ya kufunga, huku safu ya ulinzi ikizuia timu pinzani kuziona nyavu zao.

Kweli hayo ni mafanikio kwa klabu hususani wakati huu muhimu kwao kutetea ubingwa.

Lakini kesho Yanga watatakiwa kuingia kwa tahadhari kubwa dhidi ya Mgambo JKT.

Kocha msaidizi wa Mgambo JKT, Moka Shaban Dihimba aliueleza mtandao huu kuwa matokeo ya kufungwa mabao 2-0 na Azam fc jumatano yamezidi kuwafanya wawe na kazi kubwa ya kupambana kubakika ligi kuu.

“Tumefungwa na Azam fc. Hii imetupeleka mazingira mengine magumu zaidi  kwa wakati huu. Tunafahamu ugumu wa mechi ijayo dhidi ya Yanga. Hakika tumekaa chini na kuandaa mikakati ya kutofungwa na mabingwa hao watetezi”. Alisema Moka.

Si rahisi kujua mikakati ya Mgambo kuelekea mchezo huo, lakini kwa asilimia kubwa itakuwa mikakati ya ndani ya uwanja ambayo itaonekana hadharani Mkwakwani hapo kesho.

Wataalamu wanasema timu inayowania ubingwa ikikutana na timu inayokwepa mkasi wa kushuka daraja, mechi inakuwa ngumu zaidi.

Hivyo Yanga wanatakiwa kujipanga kwa kutumia uzoefu wao na ukongwe wa wachezaji wao kupata matokeo hapo kesho.

Hakuna cha muhimu zaidi kwa Yanga, ushindi pekee ndio itakuwa silaha yao katika mbio za kutetea ubingwa wao.

Ukiyatazama majina mawili ya Yanga na Mgambo JKT, hayana ufanano kabisa.

Yanga ni timu kubwa, kongwe, yenye wachezaji wakubwa na mashabiki lukuki, hivyo wanapewa asilimia kubwa ya kupata matokeo mazuri.

Lakini mpira huwa una mambo yake, si ajabu kuona Mgambo wanashinda kirahisi mchezo wa kesho.

Kwa mazingira ya timu zote mbili, ushindani utakuwa mkubwa, na itawalazimu wachezaji wa timu zote kuwa makini kutumia nafasi zao.

Yanga wapo nafasi ya pili kwa pointi 46 baada ya kucheza mechi 21.

Kama watashinda kesho watafikisha  pointi 49 katika nafasi hiyo hiyo ya pili, bila kujali matokeo ya Azam fc yatakuwaje.

Wachezaji waliopo jijini Tanga  ni Magolikipa: Juma Kaseja na Ally Mustafa "Barthez"

Walinzi: Mbuyu Twite, Juma Abdul, Oscar Joshua, David Luhende, Kelvin Yondani na Nadir Haroub "Cannavaro".

Viungo: Frank Domayo, Hassan Dilunga, Haruna Niyonzima, Nizar Khalfani na Athuman Idd "Chuji"

Washambuliaji: Emmanuel Okwi, Mrisho Ngasa, Saimon Msuva, Didier Kavumbagu, Jerson Tegete, Hamisi Kizza na Hussein Javu.

Kwa mechi ya Dar es salaam, timu zote mbili, Azam fc na Simba zimeonekana kuogopana.

AZAM FC kupitia kwa katibu wake mkuu, Nassor Idrisa ‘Father’ imesema mechi dhidi ya Simba SC Jumapili itakuwa ngumu kwa sababu wapinzani wao bado ni timu bora na watataka kurejesha heshima baada ya kucheza mechi tano bila kushinda.
“Simba SC ni moja ya timu bora msimu huu, haipo kwenye mbio za ubingwa kwa sababu ya bahati tu, lakini si kama ni timu mbaya. Kumbuka tulikuwa na Simba SC katika Kombe la Mapinduzi mapema mwaka huu, sisi tukatolewa Nusu Fainali, wao wakaingia Fainali,”alisema Father.

Kwa upande wa Simba sc, Afisa habari wake, Asha Muhaji alisema kuwa wanaiheshimu zaidi Azam fc kwasababu msimu huu imekuwa na kikosi bora ambacho hakijafungwa hata mechi moja.

“Mechi itakuwa ngumu sana. Wapinzani wetu wako bora na wamepata matokeo mazuri kuliko sisi. Lakini haina maana kuwa hatuwezi kufanya vizuri. Tumejiandaa kwa lolote na malengo yetu ni kutafuta ushindi”. Alisema Asha.

Mechi hii itakuwa na umuhimu mkubwa kwa Azam fc kwasababu inaweza kuamua hatima yao endapo Yanga atashinda Mkwakwani.

Kama wataibuka na ushindi dhidi ya kikosi cha Dravko Logarusic itakuwa faida kubwa kwasabu wataendelea kuweka pengo  la pointi 4 baina yao na Yanga, hata kama Pluijm atawaongoza wanajangwani kushinda.

Kama Azam watapoteza, Yanga atawasogelea zaidi kileleni na kutofautiana kwa pointi moja tu, kitu  ambacho kitakuwa hatari zaidi.

Kocha wa Azam fc, Mcameroon, Joseph Marius Omog anatakiwa kutuliza kichwa chake hapo kesho kwasababu Simba hawatakubali kufungwa kirahisi.

Japokuwa mengi yanasemwa kuwa Simba wapo tayari kuwapa ushindi Azam fc, lakini si Yanga aprili 19, Omog na kikosi chake wasibweteke kwa maneno hayo ya mitaani.

Hatudhani kama benchi la ufundi la Simba linaweza kuwa na mawazo mabovu kiasi hicho.

Lazima wataingia kutafuta ushindi, kwasababu kufungwa tena kwa mara ya pili uwanja wa Taifa, itakuwa fedheha kwao na watawaumiza zaidi mashabiki wao.

Simba sc hawapo katika mbio za ubingwa, lakini si sababu ya kukubali kupoteza mechi kirahisi.

Azam fc wajiandae kupambana, ila nao Simba sc lazima wajipange zaidi kukabiliana na vinara hao kutokana na ubora wa kikosi chao.

Kwa matokeo ya uwanjani, Azam fc ni bora zaidi ya Simba, hivyo Loga lazima atulize akili yake.

Mechini nyingine za kesho ni baina ya Mbeya City  fc dhidi ya Tanzania Prisons , uwanja wa Sokoine jijini Mbeya.

Kagera Sugar watakuwa nyumbani kuwakaribisha Ruvu Shooting katika dimba la Kaitaba, mjini Bukoba, mkoani Kagera.

Mtibwa Sugar watakuwa Manungu Complex kuumana na wagosi wa Kaya, Coastal Union ya Tanga.

Nao maafande wa JKT Ruvu watakuwa Azam Complex kuoneshana kazi na maafande wa JWTZ, Rhino Rangers kutoka mkoani Tabora.B

Friday, March 28, 2014

PICHA YA SIKU: BANGO NA NDEGE ITAKAYOPITA JUU YA PAA LA OLD TRAFFORD KESHO


MECHI YA AZAM, SIMBA YAWA GUMZO DAR, MBEYA MAMBO TOFAUTI, KILA KONA MBEYA CITY VS PRISONS JUMAPILI!!


Na Baraka Mpenja  Dar es salaam

WAKATI jijini Dar es saalam pambano la jumapili la ligi kuu soka Tanzania bara baina ya vinara  Azam fc dhidi ya  wekundu wa Msimbazi, Simba sc likizidi kuwa gumzo, jijini Mbeya hali ni tofauti kabisa ambapo kila kona ya jiji mashabiki wanazungumzia mechi  ya mahasimu  wawili, Mbeya City fc na Tanzania Prisons.
Timu hizo zenya makazi yake jijini Mbeya maarufu kama `Jiji la Kijani` zitakutana kwenye  mechi  huo utakaopigwa  uwanja wa CCM kumbukumbu ya Sokoine.
Mbeya City wataingia wakiwa na kumbukumbu ya kuwalaza Wajelajela mabao 2-0 katika mchezo wa mzunguko wa kwanza mwaka jana.
Kocha msadizi wa Mbeya City, Maka Mwalwisyi alisema mchezo huo utakuwa na mvuto wa aina yake kwasababu utazikutanisha timu mbili zilizosimama maeneo tofauti katika msimamo wa ligi kuu msimu huu.
“Sisi tunapigana kuutafuta ubingwa, wao wanapigana kujinasua kushuka daraja. Si kwamba Prisons ni timu mbovu, isipokuwa ndivyo maisha ya soka yalivyo”.
“Wamekosa nafasi ya juu na sasa wanapigania kukwepa kushuka daraja. Lakini mchezo utakuwa mgumu kwasababu wachezaji wa timu zote wanafahamiana vizuri”. Alisema Maka.
Maka aliongeza kuwa wamefanya maandalizi mazuri zaidi na sasa wapo hatua za mwisho wakiwa na matarajio ya kupata pointi tatu muhimu dhidi ya Prisons.
“Tmejiandaa kwa michezo 26 ya ligi kuu. Kila mechi ni muhimu kwetu. Cha msingi mashabiki wetu ambao ni wachezaji wa 12, tunawaomba wajitokeze kwa wingi siku hiyo”. Alisema Maka.
Wakati Mbeya City wakiwa na kumbukumbu ya kushinda 2-0 mechi iliyopita dhidi ya JKT Ruvu uwanja wa Azam Complex,  Chamazi, Prisons wanaugulia machungu ya kufungwa mabao 5-0 na Yanga uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam katikati ya wiki.
Katibu mkuu wa Prisons, Inspekta Sadick Jumbe alisema kuwa wamekubali kufungwa na Yanga kwasababu ni timu kubwa yenye uchu wa kutafuta matokeo kwa ajili ya kutetea ubingwa.
“Timu ya Yanga na sisi ilikuwa sawa na ngumu kati ya Tyson dhidi ya Matumla. Hawa wenzetu wanauhitaji ubingwa kwa nguvu zote, hivyo hawana mchezo.. Tumepigwa 5-0. Kuna wenzetu tunaofanana nao, hao tutafia uwanjani”. Alisema Jumbe.
Akizungumzia mchezo wa jumapili, Jumbe alisema wanaenda kulipa kisasi cha kufungwa mabao 2-0  mzunguko wa kwanza na wakishindwa sana watawafunga  Mbeya City 3-0.
“Utakuwa mchezo wenye ushindani mkubwa sana. Sisi tutaingia pale kutafuta pointi tatu kwa nguvu.  Mungu bado yupo nasisi. Mgambo wamepoteza na tumebakia nafasi yetu ya 10, lazima tushindane ”.
“Kwanza watu wengi wataingia uwanjani, pili vijana wana ari kubwa. Itakuwa mechi ngumu, lakini ushindi lazima”. Alisema Jumbe.
Pia aliongeza kuwa Mbeya City wasahau kushika nafasi ya pili au ubingwa kwa msimu huu kwasababu  nafasi hizo zinapiganiwa na  klabu za Yanga na Azam fc.
“Wenzetu wanasema wanataka ubingwa. Tuongee tu ukweli, nafasi ya pili au ya kwanza kwa msimu hu si rahisi kwao. Lakini wakifanikiwa ni jambo jema na sisi tunawaombea wafanikiwe”. Alisema Jumbe.
Ugumu wa mechi hiyo unajengwa katika mazingira ya timu hizi mbili katika msimamo.
Mbeya City  wanawania ubingwa wakiwa  nafasi ya 3 kwa kujisanyia  pointi 42 kibindoni, huku juu yao wakiwemo Yanga wenye pointi 46, na nafasi ya kwanza wapo Azam fc kwa pointi 50.
Prisons wao wanapambana kushuka daraja wakiwa na pointi 22 katika nafasi ya 10.
Hivyo ushindi  kwa timu zote  una maana kubwa na lazima makocha wajidhatiti kuhakikisha wanafanikiwa kuibuka na pointi tatu.
Faida kubwa kwa Mbeya City ni kujikusanyia mashabiki wengi zaidi ya Prisons jijini Mbeya na nje ya jiji.
Kikosi cha Juma Mwambusi kimekuwa na mvuto kwa mashabiki wengi kutokana na kufanya vizuri zaidi msimu huu ambao ni wakwanza kwao

KASEBA NA MASHALI WAPIMA UZITO KUPIGANA JUMAMOSI MARCH 29 PTA SABASABA


Bondia Japhert Kaseba akipima uzito kwa ajili ya mpambano wake wa ubingwa na Thomasi mashali kushoto mpambano utakaofanyika PTA Sabasaba siku ya jumamosi march 29 picha na www.superdboxingcoach.blogspot.com
Mabondia Thomasi Mashali kushoto na Japhert Kaseba wakiwa na mkanda ambao wataugombania katika ukumbi wa PTA sabasaba siku ya jumamosi picha nawww.superdboxingcoach.blogspot.com

Promota wa mpambano huo Ally Mwazoa akizungumza mbele ya waandishi wa habari
Mabondia Alani Kamote wa Tanga kushoto pamoja na Karage Suba wakiwa na mkanda watakaougombania kesho kwenye ukumbi wa PTA Sabasaba picha nawww.superdboxingcoach.blogspot.com
Ally Mwazoa akisisitita jambo

BLATTER NA PLATINI WAHOJIWA KUHUSU UHALALI WA QATAR KUPEWA UENYEJI KOMBE LA DUNIA




Maafisa wa Fifa akiwemo Rais wa chama hicho,Sepp Blatter na Michel Platini wamehojiwa kuhusu uhalali wa mkataba wa kuandaa michuano ya Kombe la dunia mwaka 2018 na 2022 kwa Urusi na Qatar.

Rais wa Fifa, Blatter na Platini wa shirikisho la soka barani ulaya Uefa, walishiriki katika mchakato huo mwezi Desemba mwaka 2010.

Mkuu wa kitengo cha upelelezi ndani ya Fifa anafanya uchunguzi namna ambavyo mchakato huo ulifanyika.

Jumla ya Wajumbe 13 kati ya 24 waliokuwa kwenye kamati wamekuwa wakihojiwa kuhusu sakata hilo.

Baadhi ya walioshiriki kupiga kura wamestaafu huku wengine wakiwa wanatumikia adhabu ya kufungiwa halikadhalika kushinikizwa kuacha kazi baada ya kukutwa na hatia ya kuvunja sheria ya Fifa.

Hatua hii haina uhusiano na uchunguzi uliofanywa na gazeti la Daily Telegraph kuhusu maafisa wa zamani wa Fifa, Mohamed Bin Hammam na Jack Warner wanaohusishwa na utoaji wa mkataba wa kuhodhi mashindano ya Kombe la dunia kwa Urusi mwaka 2018 na Qatar mwaka 2022.

Juma hili, gazeti hilo limeeleza kuwa shirika la upelelezi FBI linachunguza malipo yanayodaiwa kutolewa na Kampuni ya Bin Hammam kwa Warner na Watoto wake muda mfupi baada ya zoezi la upigaji kura kukamilika.

HATIMAYE MASHABIKI WASIOMTAKA MOYES KUPITISHA NDEGE JUU YA PAA LA OLD TRAFFORD ITAKAYOBEBA UJUMBE WA KUMTAKA KOCHA HUYO AONDOKE

Mashabiki wa Manchester United wanaochukizwa na mwenendo wa timu yao chini ya uongozi wa David Moyes wamefanikiwa kupata ndege itakayopita juu ya paa la uwanja wa Old Trafford jumamosi hii - huku ndege hiyo ikiwa imebeba bango la ‘Moyes Out’.
Ndege hiyo imepangwa kupita juu ya paa la OT kwa dakika 10 kabla ya mchezo kuanza na baadae kwa dakika 5 na wakati wa mchezo dhidi ya Aston Villa.
Kundi la mashabiki hao tayari limethibitisha kwamba kesho ndege hiyo yenye bango la  “Wrong One: Moyes Out.”
Bango hilo ni kinyume ya lile walilotaka kulishusha kutoka kwenye jukwaa la Stretford End linalosomeka  ‘Chosen One’.

TAKWIMU YA SIKU: LUIS SUAREZ ANAHITAJI MABAO 4 KUVUNJA REKODI YA RONALDO NA SHEARER EPL

Luis Suarez anahitaji magoli (4) tuu ili aweze kuvunja rekodi ya Alan Shearer na Christiano Ronaldo ya kufunga magoli (31) katika msimu mmoja wa premier league record wenye mechi 38..

KUELEKEA DAR ES SALAAM DERBY: SIMBA TUMPELEKE DALALI NA MO INDIA ILI KUIKOMBOA TIMU YETU


Unamfahamu mtu anaitwa Mohamed Dewji aka "MO"? Na vipi huyu anaeitwa Hassan Dalali aka "FIELD MARSHAL" je, unamfahamu? Bila shaka jibu ni ndio. Basi tunachotakiwa kukifanya wanachama wa Simba ifikapo May 4 ni kuwapandisha ndege hawa jamaa na kuwapeleka India, kule ambapo kuna madaktari bingwa wa upasuaji. Tuwape kazi jopo la madaktari bingwa wa upasuaji ya kumpasua Mo kichwa na kuchukua akili zake kisha wakazihamishia kwa Hassan Dalali, au wampasue Field Marshal Hassan Dalali kifua na kuchukua moyo wake na kuuhamishia ktk kifua cha Mohamed Dewji, kisha tupate mtu mmoja mwenye akili za Mo na moyo wa Dalali, atakaetuongoza ktk kipindi cha miaka minne ijayo. Unajua kwanini tunapaswa kufanya hivi?

Unaikumbuka Simba iliyokuwa chini ya udhamini wa Mohamed Enterprises Tanzania Limited? Simba ile iliyokuwa inavaa jezi zilizoandikwa METL kifuani, mwanzoni kabisa mwa miaka ya 2000? Hii ndio Simba bora kabisa niliyowahi kuishuhudia mimi ktk maisha yangu. 
Ilikuwa Simba hatari zaidi kuwahi kutokea kuacha ile ya akina Masatu mwanzoni mwa miaka ya tisini wakati huo nikiwa kinda na akili ndio zinaanza kutambua soka ni kitu gani. 

Simba hii iliyokuwa chini ya Mohamed Enterprises ilikuwa balaa, hapa bongo ilipewa jina la "SIMBA DOZI" maana ilikuwa mtu akipona sana ni 3 na ndio Simba iliyotingisha Africa baada ya kuiadabisha Zamalek nyumbani kwao na kuwavua ubingwa wa klabu bingwa Africa, ktk wakati ambao fitna za kiarabu ndio zilikuwa ktk kiwango cha juu kabisa. 

Pesa na akili za Mohammed Dewji zilikuwa zikitumika vyema wakati ule lkn mmiliki huyu wa kampuni ya METL hakuridhika na hali ya timu nje ya uwanja, alitaka timu iondokane na mfumo tegemezi wa ufadhili na badala yake timu iwe na uwezo wa kujiendesha yenyewe na kuwa na mipango endelevu kama program nzuri za vijana na kuwa na vitega uchumi pamoja na uwanja. Lkn wapuuzi wachache wasiokuwa na akili waliokuwa ktk system walimpinga kwa nguvu zote. 
Jamaa alikasirika kuona watu hawana mwelekeo na wanapinga mipango mizuri ya maendeleo, hatimaye akaamua kuondoka zake na kuwaacha na mauzauza yao. Huwezi amini ila ni ukweli usiopingika kuwa tangu kuondoka kwa Mohamed Dewji pale Simba, timu ilipoteza mwelekeo na mpaka leo bado tunahangaika tu na hakuna cha maana.

Hapo katikati kabla ya kuja mwanasiasa Ismail Aden Rage takribani miaka minne iliyopita, alipita mzee wangu 'Field Marshal' Hassan Dalali. Huyu mzee hakufanikiwa sana lakini walau afadhali kuliko wote waliopita baada ya Mo kuondoka na bora zaidi ya huyu mwanasiasa anaejiita msomi lakini ndio katuvurugia kabisa timu yetu. Chini ya mzee Dalali umoja wa wanamsimbazi uliopotea kwa muda mrefu ulirejea na tukasahau kabisa misuguano ya kipuuzi ya wenyewe kwa wenyewe. Ndani ya uwanja timu haikuwa mbaya sana hatukufungwa hovyohovyo kama ilivyo sasa, na ktk miaka minne ya Dalali hakuna mwaka tuliokosa kikombe na miaka yote ya Dalali tulikuwemo katika mashindano ya kimataifa. Ila mzee wangu Hassan Dalali alifeli sana katika maendeleo ya timu nje ya uwanja.

Uchaguzi unaokuja Simba tunakiwa tumpate mtu mwenye akili za Mohammed Dewji na moyo wa Hassan Dalali ili timu yetu ipige hatua na kuwa na maendeleo nje na ndani ya uwanja. Kiukweli hatuhitaji tena mwanasiasa na wala hatuhitaji mtu mwenye fedha kuiongoza Simba, bali mwenye akili za maendeleo kama alivyo "MO' na mwenye moyo wa kuitumikia club na kuleta umoja miongoni mwetu kama alivyo "FIELD MARSHAL". Na hii ndio sababu ya kuwapeleka India watu hawa ili wakaunganishwe na tupate mtu mmoja aliekamilika atakaetupeleka ktk kilele cha mafanikio.

Severin Machila Mwanakijiji

Thursday, March 27, 2014

TFF YAANZA KUENDELEZA UWANJA WA TANGA.


NSSF MEDIA CUP KUANZA KUTIMUA VUMBI MACHI 29

Meneja Kiongozi Idara ya Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eunice Chiume akizungumza wakati swa hafla ya kukabidhi vifaa kwa timu zinazoshiriki mashindano ya NSSF Media Cup yanayotarajiwa kuanza rasmi Machi 29. 
 Meneja Kiongozi Idara ya Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eunice Chiume akizungumza wakati swa hafla ya kukabidhi vifaa kwa timu zinazoshiriki mashindano ya NSSF Media Cup yanayotarajiwa kuanza rasmi Machi 29.
 Meneja Kiongozi Idara ya Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eunice Chiume akimkabidhi vifaa vya michezo, mwakilishi wa timu ya Star Tv, Tom chilala kwa ajili ya mashindano ya NSSF CUP yanayotarajiwa kuanza Machi 29.
Baadhi ya vifaa vilivyotolewa kwa timu shiriki katika michuano ya NSSF Media Cup.
 Meneja Kiongozi Idara ya Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eunice Chiume (kushoto), akimkabidhi vifaa vya michezo, mwakilishi wa Kampuni ya Free Media Ltd, wachapishaji wa magazeti ya Tanzania Daima na Sayari, Francis Dande kwa ajili ya mashindano ya NSSF MEDIA CUP yanayotarajiwa kuanza Machi 29. 


 Meneja Kiongozi Idara ya Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eunice Chiume (kushoto), akimkabidhi vifaa vya michezo mwikilishi wa Jambo Leo, Julius Kihampa.
 Antony Siame, mwakilishi wa gazeti la Raia Mwema akipokea vifaa vya michezo kutoka kwa  Meneja Kiongozi Idara ya Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Eunice Chiume (kushoto).

Na Mwandishi Wetu

JUMLA ya sh. millioni 19 zimetolewa na Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), ikiwa ni fedha taslimu zitakazotolewa kwa washindi mbalimbali wa michezo ya NSSF MEDIA CUP 2014 itakayoanza Machi 29.

Akizungumza jijini Dar es Salaam, Meneja Kiongozi wa Idara ya Uhusiano na Huduma kwa Wateja wa Shirika hilo, Eunice Chiume, alisema kuwa maandalizi ya michuano hiyo imekamilika na kwa upande wa mpira wa miguu mshindi wa kwanza atapata Tshs. 4,500,000, mshindi wa pili atapata Tshs.3,500,000 na watatu atapata Tshs. 2,000,000.

Aidha alisema, kwa upande wa mpira wa Pete mshindi wa kwanza atazawadiwaTshs. 4,000,000, mshindi wa pili  Tshs.3,500,000 na mshindi wa tatu atazawadiwa Tshs. 2,000,000 taslimu.

“Wachezaji bora wa mashindano haya  kwa upande wa mpira wa miguu na pete wote wata zawadiwa kila mmoja Tshs 350,000 ili kuongeza hamasa  katika michezo hiyo” alisema Chiumea.

Alisema kuwa, mashindano hayo yatashindaniwa kwa njia ya mtoano kwa mechi za mpira wa miguu na pete, yatashirikisha  timu 20 za mpira wa miguu na 18 za mpira wa  pete kutoka vyombo vya habari  vya jiji la Dar es Salaam na Zanzibar.

“Timu zitakazoshiriki kwenye mashindano  hayo ni IPP, Free Media , BTL, New Habari, Mwananchi, Uhuru, Habari  Zanzibar, Tumaini Media, Star TV na TBC ambapo kilele cha michuano hiyo iatkuwa tarehe 12 April mwaka huu ambapo mwenyeji wake ni NSSF” alisema.

Alieleza kuwa, mbali ya timu alizozitaja pia kuna timu nyingine ambazo zipo katika michuano hiyo ikiwa ni TSN, Mlimani, Radio Maria, Wizara ya Habari, Global Publishers, Jambo Leo,  Raia Mwema na Azam  TV ambapo mechi zote zitafanyika uwanja wa DUCE-Chang’ombe na TCC–Club na fainali kufanyika hapo.

Michuano ya NSSF Media Cup 2014, imetimiza miaka 11 tangu kuanzishwa na inakwenda sambamba na sherehe za miaka 50 ya NSSF na pia mika 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

Michuano ya mwaka huu ikifanyika katika sherehe hizo kubwa mbili ndio yenye idadi ya timu zinazoshiriki kuliko mwaka mwingine tangu michuano hiyo ianze mwaka 2004.

Michuano hii ilianzishwa mwaka 2004 kwa kuzishirikisha timu 8 mpaka sasa timu zinazoshiriki zimefikia timu 20 wakati mpira wa Pete timu zimeongezeka kutoka 7, miaka mitano iliyopita tangu  mchezo huu ulipozinduliwa kwenye mashindano ya NSSF Media Cup. 

PICHA YA SIKU!


KAGERA SUGAR WAIKOMALIA NAFASI YA KIBADENI, WAGOMA KUWA WATANO MSIMU HUU!!

Na Baraka Mpenja,Dar es salaam

0712461976 au 0764302956

WASHINDI wa nafasi ya nne  msimu uliopita wa ligi kuu soka Tanzania bara, Kagera Sugar  wenye makazi yao  Kaitaba , Mjini Bukoba, mkoani Kagera hawajakata tamaa kuisaka nafasi ya tatu au nne msimu huu.

Murage Kabange, kocha msaidizi wa Kagera Sugar amesema kuwa katika mechi tano walizobakiza wamejiandaa kupata ushindi ili kutetea nafasi yao ya nne au kupata ya tatu.

“Mwaka jana tuliishia nafasi ya nne. Msimu huu tumekuwa na majeruhi wengi. Kikubwa kwasasa tunajipanga kuibuka na ushindi katika michezo yote iliyosalia”.

“Malengo yetu ilikuwa ni kutwaa ubingwa au kushika nafasi ya pili. Kushuka nafasi ya nne hatukutarajia. Lakini kutokana na matatizo ya kikosi chetu, sasa tunaiwinda nafasi ya tatu au kusalia nafasi ya nne kama mwaka jana”. Alisema Kabange.

Kocha huyo alisema maandalizi yao kuelekea mchezo wa jumapili dhidi ya Ruvu Shooting katika uwanja wa Kaitaba yanakwenda barabara,hivyo wana matumaini ya kufanya vizuri.
“Tunanoa makali ya safu ya ushambuliaji ili kuipa makali. Pia tunarekebisha kasoro zilizopo safu  ya kiungo na ulinzi. 
Tunatarajia kufanya vizuri dhidi ya Ruvu Shooting”. Alisema Kabange.

Akizungumzia mechi tano zilizosalia, Kabange alisema wanahitaji kujiandaa kwa umakini mkubwa kwasababu kuna ushindani wa hali ya juu.

“Hukuna mechi nyepesi hata kidogo. Tunacheza na Ruvu Shooting jumapili. Baada ya hapo tutawasubiri Simba nyumbani. Mechi hizi kwanza ukiziangalia zitakuwa ngumu, lakini tunafanya maandalizi mazuri”. Aliongeza Kabange.

Mbali na mechi hizo mbili, Kagera Sugar pia wamebakiza  kiporo kimoja dhidi ya Yanga aprili 9 mwaka huu uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Baada ya mechi hiyo, watasafiri mpaka Tanga kuwavaa Mgambo JKT uwanja wa Mkwakwani aprili 13 mwaka huu.
Kibarua chao cha  mwisho ni aprili 19 dhidi ya Coastal Union uwanja wa CCM Mkwakwani, jijini Tanga.

Mpaka sasa, Kagera Sugar wameshuka dimbani mara 21 na kujikusanyia pointi 32 katika nafasi ya 5.

Mbele yao wapo wekundu wa Msimbazi Simba ambao wameshuka dimbani mara 22 na kujikusanyia pointi 36 katika nafasi ya nne.

YANGA: UKIZEMBEA MAZOEZINI UTASUGUA BENCHI, INGIZO LA TEGETE, JAVU SABABU NI KIWANGO BORA!!


LAZIMA ukomae!.  Hukuna mchezaji mwenye namba ya kudumu katika kikosi cha mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania bara, Dar Young Africans msimu huu.

Kocha msaidizi wa klabu hiyo, Charles Boniface Mkwasa `Master` ameuambia mtandao huu kuwa mabadiliko ya wachezaji yanayofanywa katika kikosi chao yanatokana na ubora wa wachezaji katika mazoezi.

“Sisi hatujali wewe ni nani. Hutuwezi kumpanga mtu kwasababu labda ana kitu fulani. Nidhamu ya mazoezi  na kuonesha kiwango ndio sababu ya kupangwa katika mechi. Mabadiliko kwetu ni kitu cha kawaida”. Alisema Mkwasa.

Mkwasa alisema ingizo la Jery Tegete na Hussein Javu kwenye kikosi chao katika mechi mbili zilizopita kumetokana na kuonesha kiwango kizuri wakati wa maandalizi na si vinginevyo.
Tegete na Hussein Javu wameonesha kurudi mchezoni na kuwa mwiba mkali kwa wapinzani, huku Didier Kavumbagu aliyeonekana kuwa chaguo la kwanza akishindwa kuanza.
Aidha, Mkwasa alisema kila mdau anayefuatilia michezo ya ligi kuu, lazima anaelewa kuwa ushindani uliopo katika nafasi za juu ni mkubwa zaidi ya misimu kadhaa nyuma.

“Kila timu imejidhatiti. Kupata ushindi ni lazima ziwepo jitihada za wachezaji kitimu na binafsi. Nafasi tatu za juu zimekuwa ngumu na lazima ujipange”. Alisema Mkwasa.

Mkwasa aliongeza kuwa timu zinazokwepa kushuka daraja zimekuwa na changamoto kubwa katika ushindani, hivyo  kama timu iliyopo nafasi nzuri ikashindwa kujipanga, ni kazi ngumu kupata ushindi.

Mkwasa aliyekuwa kocha mkuu wa Ruvu Shooting mzunguko wa kwanza, alisema kuwa kwasasa wanajiandaa na mchezo wa machi 30 (Jumapili) dhidi ya MgamboJKT, kwenye uwanja wa CCM Mkwakwani, Jijini Tanga.

“Kila mechi ni ngumu kwetu. Ndio maana vijana wetu tunawaambiwa wajiandae kwa kila kitu kitakachotokea uwanjani. Tunakutana na timu inayotoka kufungwa mabao 2-0”.

 “Tunajua hawatakubali kufungwa kwa mara pili, watahangaika sana, lakini mwisho wa siku wajue kuwa Yanga ni timu bora zaidi na kongwe, lazima wakubali kufungwa”. Alisema Mkwasa.

Mkwasa aliwashukuru mashabiki wao kwa kuendelea kujitokeza kwa wingi  katika michezo yao na aliwaomba kuendelea kuwaunga mkono zaidi ili kufanikisha malengo yao ya kutwaa ubingwa.
“Mpira bila mashabiki si mpira tena. Nasema tena na tena, shukurani sana mashabiki wetu kwa kuwa karibu na timu”. Alisema Mkwasa.

Mechi ya jumapili, itakuwa mechi ngumu zaidi kwa Mgambo kwasababu kupoteza tena baada ya kipigo cha 2-0 kutoka kwa Azam fc, itakuwa kujipalia mkaa.

Yanga wataingia katika mechi hiyo ya 22 msimu huu wakiwa na pointi 46 katika nafasi ya pili, huku vinara Azam fc wenye pointi 50 kileleni watakuwa na kibarua dhidi ya Simba sc uwanja wa Taifa.

Baada ya kutoka Tanga, aprili 6 mwaka huu, Yanga itacheza dhidi  ya  JKT Ruvu Uwanja wa Taifa.

Aprili 9, Yanga wataikaribisha Kagera Sugar katika dimba la Taifa jijini Dar es saalam.

Aprili 13 katika dimba la Sh. Amri Kaluta Abeid jijini Arusha, Yanga watakuwa wageni wa  vibonde, JKT Oljoro.

Mechi ya mwisho kwa Yanga itakuwa aprili 19 mwaka huu ambapo watakabiliana na mahasimu wao, Simba Sc.

MWANASHERIA SALEHE NJAA KUIONGOZA KAMATI YA MAADILI YA YANGA.


'THE CLASS OF 92' WAKIONGOZWA NA BECKHAM NA GARY NEVILLE WARIPOTIWA KUTUMIWA NA FAMILIA YA KIFALME YA QATARI KATIKA UNUNUZI WA MANCHESTER UNITED


Ripoti kutoka kwenye vyombo vya habari mbalimbali zinasema kwamba David Beckham na wachezaji wenzie waliokuwa wanaunda kikosi cha Man United mwaka 1992 kwa kushirikiana na kampuni ya kutoka nchini Qatar wapo katika harakati za kuinunua Manchester United. 
Hata hivyo United wamekanusha taarifa kwamba wamiliki wa timu hiyo Familia ya Malcom Glazers imepoteza hamu ya kuendelea kuimiliki timu hiyo na sasa wanataka kuiuza.  
Lakini mapema jana iliripotiwa kwamba David Beckham, Gary na Phil Neville, Ryan Giggs, Nicky Butt, na Paul Scholes, wamekuwa wakitumika na familia ya kifalme ya Qatar katika mpango huo wa kuinunua United. 
The Glazers - ambao wanaimiliki United kwa 90% - wamekuwa wakiripotiwa kutaka kuiuza timu hiyo, huku mmoja wa watu wa karibu wa familia hiyo akikaririwa akisema kwamba "kila mtu anajua klabu inauzwa".
The Sun inaripoti kwamba familia ya kifalme ya Qatar imekuwa na mawasiliano na Glazers kuhusiana na dili la kuinunua timu hiyo lakini kikwazo kimekuwa kwenye bei. 
Pia inasemekana Gary Neville - ambaye amefungua Cafe Football na Giggs mwaka 2013 - ndio mtu aliye nyuma ya wazo hilo. 

BAYERN MUNICH YA GUARDIOLA INAWEKA REKODI NA KUZIVUNJA YENYEWE


Bayern Munich wameshinda mechi 10 za mwisho walizocheza ugenini katika ligi. Rekodi iliyokuwepo ilikuwa mechi 9 - waliiweka wenyewe msimu uliopita.

Bayern wameshinda mechi 19 kwenye ligi - hii ni rekodi mpya ya Bundesliga. Rekodi ya nyuma huko ilikuwa ushindi wa mechi 15, rekodi hii waliiweka Bayern wenyewe mwaka 2005.

The Bavarians wamefunga magoli mawili au zaidi katika mechi zao 19 walizoshinda - hii ni rekodi mpya kwenye ligi.

Huu ni ubingwa 24 Bayern Munich wa Bundesliga - rekodi mpya pia.

Boss wa Bayern Pep Guardiola alishinda makombe 14 katika miaka miaka yake minne ndani ya FC Barcelona, na sasa anaweza kushinda matano ndani ya msimu wake wa kwanza na Bayern.

Guardiola hajapoteza mchezo wowte wa ligi tangu alipoanza kuifundisha timu hiyo - pia kwa ujumla Bayern hawajafungwa katika Bundesliga ndani ya miezi 18.

SUAREZ NA STURRIDGE WAWEKA REKODI MPYA LIVERPOOL


Luis Suarez ndio mfungaji bora wa ligi kuu ya England, akiwa na magoli 28, anahitaji goli moja tu kuweka rekodi ya kuwa mfungaji aliyefunga mabao mengi zaidi kwa Liverpool katika msimu mmoja wa Premier League.

Luis Suarez amefunga kila baada 80 kwa wastani katika Premier league msimu huu.

Suarez mpaka sasa ametoa assists 12 - nyingi kuliko mchezaji yoyote katika Premier League msimu huu. 

Kwa pamoja - Daniel Sturridge na Suarez wameka rekodi ya kuwa washambuliaji wa Liverpool wa kwanza katika kipindi cha miaka 50 kuweza kufikisha mabao zaidi ya 40 ndani ya msimu mmoja wa ligi kuu ya England. 

YANGA, AZAM FC KUWANIA UBINGWA SHUGHULI PEVU, MZANI WA MECHI ZAO WATOFAUTIANA!!


Na Baraka Mpenja , Dar es salaam

0712461976 au 0764302956

YANGA sc wanachuana vikali na Azam fc katika mbio za kuwania mwari wa ligi kuu soka Tanzania bara msimu huu.
Mpaka sasa mbio za ubingwa ni wazi na hakuna anayeweza kutabiri nani anaweza kubeba taji.
Mbeya City nao wanafuata nyuma yao  wakiwa na dhamira ya kutwaa ubingwa au kushika nafasi tatu za juu katika msimamo.
Simba sc wameachwa mbali na hawazungumzwi kabisa katika kinyang`anyiro cha ubingwa.
Baada ya Yanga kuibuka na ushindi wa mabao 5-0 dhidi ya Tanzania Prisons, `Wajelajela`  uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam na Azam fc kushinda mabao 2-0 dhidi ya Mgambo JKT uwanja wa Mkwakwani Tanga, nafasi mbili za juu zimeonekana kuwa na ushindani mkubwa.
Kinachosubiriwa kwasasa ni timu moja kupoteza mchezo ili kuiruhusu nyingine kusogea juu zaidi.
Mpaka sasa Yanga wameshuka dimbani mara 21 na kujikusanyia pointi 46, huku Vinara Azam fc wakiwa wamecheza mechi 22 na kujikusanyia pointi 50.
Yanga wana mechi moja ya kiporo dhidi ya Kagera Sugar aprili 9 mwaka huu uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Wakati timu hizi zikipigana kufa na kupona kuwania ubingwa, mechi zifuatazo zimebakia kwa kila klabu.
Ukiangalia uzito wa mechi zenyewe, pengine wale wataalamu wa kubashiri matokeo ndio  wakati wao.
Kuna wakati soka linatabiriwa.  Huwa ni bahati tu kwa wale wanaopatia utabiri, lakini mara nyingi matokeo ya mpira wa miguu hupatikana ndani ya dakika 90.
Sababu inayotumiwa na watabiri wengi ni ubora wa vikosi vya timu zitakazocheza, kuanzia mchezaji mmoja mmoja na timu kwa ujumla.
Ila mpira wa miguu huwa unaleta matokeo tafauti. Unaweza kuwa na timu bora na ukapoteza.
Azam fc wamebakiza mechi 4,  huku mabingwa watetezi, Yanga wakibakiza mechi 5.
Machi 30 mwaka huu, Azam fc watakuwa wenyeji wa Simba katika dimba la Taifa.
Mechi hii inatazamiwa kuwa ngumu kwa timu zote kutokana  na mazingira ya timu zote.
Simba sc hawana matumaini ya kutwaa ubingwa, lakini yawezekana wakaingia uwanjani kushindaa  ili kulinda heshima.
Ukiwasikia mashabiki wa Simba sc, wanakiri kabisa kuwa hawana ujanja msimu huu, lakini bora kutoa pointi  tatu kwa Azam fc jumamosi, ila si kwa Yanga aprili 19.
Sidhani kama benchi la ufundi nalo lina mawazo kama hayo. Bila shaka kocha Dravko Logarusic ataingia kwa nia ya kupata matokeo ya ushindi.
Joseph Marius Omog , kocha wa Azam fc ataingia kwa wembe ule ule anaotumia kuzinyoa klabu za ligi kuu.
Kwanza ataingia kulinda rekodi yao ya kutofungwa msimu huu katika mechi 22 walizocheza, lakini ataweka mkazo zaidi katika ushindi kwa kuvuna pointi tatu muhimu.
Kupoteza mechi au kutoa sare hayatakuwa matokeo salama kwa Azam fc , kwasababu Yanga atakuwa Tanga kukabiliana na Mgambo JKT.
Mechi nyingine iliyobakia kwa Azam fc ni aprili 6 mwaka huu uwanja wa Mabatini mkoani Pwani ambapo watakabiliana na Ruvu Shooting ya mkoani humo.
Hii mechi itakuwa muhimu zaidi kwa Azam fc, kwasababu wapinzani wao hawana cha kupoteza.
Hawawazi kushuka daraja wala kutwaa ubingwa. Hivyo `presha` itakuwa kwa Azam fc kutegemeana na matokeo ya Yanga.
Aprili 13, Azam fc watasafiri mpaka jijini Mbeya kuwafuata Mbeya city FC katika uwanja wa Sokoine jijini humo.
Hii dhahiri shahiri itakuwa mechi ngumu zaidi kwa Azam fc kwani Mbeya City ni washindani wao.
Haitakuwa kazi nyepesi kupata matokeo ya ushindi mbele ya wagonga nyundo hao wa Mbeya,  kwasababu hawana rekodi ya kupoteza mchezo nyumbani kwao.
Baada ya kutoka Mbeya, Azam fc watarudi Chamazi kupambana na JKT Ruvu ya Fredy Felix Minziro.
Ugumu wa mechi hii utatokana na matokeo ambayo JKT Ruvu watakuwa nayo mkononi katika mechi nyingine watakazocheza kabla ya kipute hicho.
JKT Ruvu Wapo katika hatari ya kushuka daraja.  Kama kufikia siku ya mechi dhidi ya Azam watakuwa wanahitaji pointi ili kujisalimisha, basi mchezo utakuwa mgumu kwa timu zote mbili.
Kama Azam fc watakuwa wamefanya vizuri katika mechi nyingine zote, bila shaka watakuwa wapo hatua ya mwisho kutangaza ubingwa wao wa kwanza tangu wapande ligi kuu msimu wa 2008/2009.
Kwa upande wa Yanga, machi 30 watakuwa ugenini kuwakabili Mgambo JKT katika uwanja wa CCM Mkwakwani, Tanga.
Hii itakuwa mechi ngumu zaidi kwa Mgambo kwasababu kupoteza tena baada ya kipigo cha 2-0 kutoka kwa Azam fc, itakuwa ni kujichimbia kaburi wenyewe.
Hakuna ufanano wa majina na ukongwe katika ligi kati ya Yanga na Mgambo.Pia timu hizi zina wachezaji wa aina tofauti.
Yanga wanaweza kupewa kura ya ushindi siku hiyo, lakini soka linachezwa uwanjani kwa dakika 90.
Baada ya kutoka Tanga, aprili 6 mwaka huu, wanajangwani watakutana na wapigania kukwepa kushuka daraja wengine msimu huu, JKT Ruvu.
Ugumu wa mechi hiyo utatokana na mazingira ya JKT Ruvu.
Yanga msimu huu wameshusha vipondo vikubwa kwa timu nyingi za majeshi.
Bila shaka kipigo cha mabao 7-0 walichokula Ruvu Shooting na cha mabao 5-0 walichoambulia Prisons vinatosha kukubaliana na hilo.
JKT Ruvu watahitaji kujipanga kwani kwa wakati huo Yanga watakuwa hawana cha kutafuta zaidi ya ushindi ili kutetea ubingwa wao.
Aprili 9, Yanga wataikaribisha Kagera Sugar katika dimba la Taifa jijini Dar es saalam.
 Kagera wamekuwa washindani katika ligi kwa misimu kadhaa, lakini msimu huu mambo hayajawa barabara.
Si Kagera Sugar ya mwaka jana chini ya Abdallah Kibadeni `King Mputa`. Imekuwa ya kawaida sana.  Ila huwezi kuwanyima kura ya kuwaharibia Yanga.
Aprili 13 katika dimba la Sh. Amri Kaluta Abeid jijini Arusha, Yanga watakuwa na vibonde, JKT Oljoro.
Mpaka kufikia siku hiyo hatima ya Oljoro kubaki au kushuka itakuwa imefahamika.
Kama watakuwa wameshakata tiketi ya kushuka daraja, basi kuna uwezekano wa kuwa mechi nyepesi kwa Yaga kwasababu Oljoro watakuwa hawana cha kufanya zaidi ya kuendelea na safari yao ya kuporomoka.
Mzinga wa mwisho kwa Yanga utakuwa aprili 19 mwaka huu ambapo watakabiliana na mahasimu wao, Simba Sc.
Hii ni mechi ambayo huwezi kuitabiri kwa kuangali ubora wa vikosi kuanzia mchezaji mmoja mmoja.
Utayakubali haya ukikumbuka mechi ya mzunguko wa kwanza ya mabao 3-3, halafu ile ya `Nani Mtani Jembe` ya 3-1.
Katika mechi hizi mbili, nje ya uwanja, Yanga walikuwa wanaonekana kuwa na uwezo mkubwa wa kuwafunga Simba sc. Lakini haikuwa hivyo.
Kwa maana hiyo, usemi wa mechi ya Simba na Yanga haitabiriki, bado una nafasi katika mchezo huu.
Pia inawezekana mchezo huu  ukaamua bingwa wa msimu huu, endapo Azam fc watakuwa na matokeo mazuri au Mbeya City.