Search This Blog

Saturday, September 28, 2013

YANGA ILIVYOTAKATA UWANJA WA TAIFA KWA KUICHAPA RUVU SHOOTING 1-0


Wachezaji wa Yanga, Simon Msuva (kushoto), Nadir Haroub (Canavaro), wakiwania mpira katika lango la Ruvu Shooting, wakati wa mchezo wa Ligi kuu ya soka Tanzania bara uliofanyika leo kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam. Yanga imeshinda 1-0. (Picha na Francis Dande)
Simon Msuva (kushoto) 
 Mshambuliaji wa Yanga, Didier Kavumbagu akichuana na beki wa Ruvu Shooting, Shaban Suzan.
 Golikipa wa Ruvu Shooting, Abdul Seif akiokoa moja ya hatari zilizoelekezwa langoni mwake.
 Furaha ya ushindi......Wachezaji wa Yanga, wakishangilia balo lililofungwa na Mrisho Ngasa.
 Simon Msuva akichuana na beki wa Ruvu Shooting.
Mshambuliaji wa Yanga, Mrisho Ngasa akimtoka beki wa Ruvu Shooting, Stephano Mwasika. 
 Mshambuliaji wa Ruvu, Shooting, Ayoub Kitala akimiliki mpira huku akizongwa na mshambuliaji wa Yanga, Mrisho Ngasa. Kushoto ni Cosmas Lewis

LIVE MATCH CENTRE: VPL - YANGA SC 1 - 0 RUVU SHOOTING


Dk 90+3 FULL TIME! Yanga 1-0 Ruvu 

Dk 89 Kiiza anachezewa faulo nje kidogo ya lango la Ruvu. Twite anapiga faulo na Ruvu wanaokoa. 

Dk 86 SUB: Yanga imefanya mabadiliko ametoka Msuva ameingia Niza Khalfan. 

Dk 78 YELLOW CARD..! Suzan wa Ruvu anaonyeshwa kadi ya njano baada ya kubishana na mwamuzi. Yanga 1-0 Ruvu 

Dk 68 SUB: Ruvu wanafanya mabadiliko ametoka Ayoub Kitala ameingia Said Madega. 

Dk 65 Yanga wamebadilika na kumiliki mpira kwa kiasi kikubwa hasa baada ya kuingia Chuji. 

DDk 62 GOOOOO.....! Kiiza anaipatia Yanga bao la kwanza kwa tik-tak safi akiunganisha krosi safi ya Mrisho Ngassa. Yanga 1-0 Ruvu 

Dk 55 Lewis wa Ruvu anaumia baada ya kugongana na Mbuyu Twite. 

Dk 50 SUB: Yanga inafanya mabadiliko anatoka Domayo anaingia Athuman Idd Chuji. 

Dk 46 Elius Maguli wa Ruvu anakosa bao la wazi katika lango la Yanga mpira wa kichwa anaopiga unatoka nje. 

Yanga 0 - 0 Ruvu Shooting

Dk 45 KIPINDI CHA PILI KIMEANZA! 

Dk 45 HALF TIME! Yanga 0-0 Ruvu 

Dk 44 YELLOW CARD..! Ayoub Kitala wa Ruvu anaonyeshwa kadi ya njano kwa kumlalamikia mwamuzi kupita kiasi baada ya Suzan kumchezea rafu Kavumbagu. 

Dk 40 Jerome Lambele wa Ruvu anapiga shuti kali langoni kwa Yanga lakini mpira unatoka nje. Yanga 0-0 Ruvu

Dk 38 Kiiza wa Yanga anakosa bao la wazi akiwa amebaki na kipa wa Ruvu Abdul Seif. 

Dk 37 Yanga inapata kona lakini Ruvu wanaokoa. 

Dk 32 YELLOW CARD....! Kipa wa Yanga Ali Mustapha anaonyeshwa kadi ya njano kwa kuchelewa kuanza mpira. 

Dk 31 Niyonzima anamchezea rafu Cosmas Lewis wa Ruvu. Yanga bado hawaelewani. 

Dk 27 Yanga wamepoteana hawana mipango kama ya siku zote, lakini Ruvu wanashindwa kutumia udhaifu huo wa Yanga. 

Dk 21 Kavumbagu anakosa bao la wazi akishindwa kuunganisha krosi ya Simon Msuva. 

Dk 19 Niyonzima anaushika mpira alioanzishiwa na Ali Mustapha na Ruvu wanapata kona baada ya David Luhende kuutoa nje mpira. Yanga 0-0 Ruvu 

Dk 14 YELLOW CARD...! George Michael wa Ruvu anaonyeshwa kadi ya njano kwa kumsukuma Kavumbagu wa Yanga. 

Dk 11 Haruna Niyonzima anakosa bao la wazi akiwa ndani ya eneo la hatari la Ruvu kwa kushindwa kupiga mpira kwenye lango la Ruvu.  

Dk 6 Ruvu wanapata kona baada ya Cannavaro kuutoa nje mpira. Yanga wanaokoa kona hiyo. 

Dk 4 Yanga inapata kona baada ya Shaban Suzan kuutoa nje mpira. Kona inapigwa na Ruvu wanaokoa. 

Dk 1 Jerome Lambele wa Ruvu anamchezea rafu Haruna Niyonzima. 

Mpira ndio umeanza hapa uwanja wa Taifa kati ya Young Africans Vs Ruvu Shooting

KIKOSI CHA RUVU 
 Abdul Seif, Michael Pius, Stephano Mwasyika, George Michael, Shaban Suzan, Gidion David, Ayoub Kitala, Hassan Dilunga, Cosmas Lewis, Elius Maguli na Jerome Lambele. Sub: Godhar Misweko, Said Madega, Mangasin Mbonosi, Mau Bofu, Kulwa Mfaume, Said Dilunga na Juma Seif 'Kijiko'.

KIKOSI CHA YANGA KINACHOANZA LEO

1.Ally Mustapha 'Barthez' - 1
2.Mbuyu Twite - 6
3.David Luhende - 3
4.Kelvin Yondani 'Cotton' - 5
5.Nadir Haroub 'Cannavaro' - 23
6.Frank Domayo 'Chumvi' - 18
7.Saimon Msuva - 27
8.Haruna Niyonzima - 8
9.Didier Kavumbagu - 7
10.Hamis Kiiza 'Diego'- 20
11.Mrisho Ngassa - 17


Subs:
1.Deogratius Munishi 'Dida' - 30
2.Juma Abdul - 12
3.Oscar Joshua - 4
4.Athuman Idd 'Chuji ' - 24
5.Nizar Khalfani - 16
6.Said Bahanuzi - 11
7.Jerson Tegete - 10

SEMINA YA KAMATA FURSA TWENDZETU KWA VIJANA YAFANYIKA LEO JIJINI MWANZA


 
 Naibu Waziri wa Nishati na Madini,Mh Stephen Masele akizungumza mada iliyohusu fursa mbalimbali zinazopatikana kwenye nishati na madini ndani ya semina ya kamata fursa twendzetu,iliyofanyika mapema leo ndani ya ukumbi wa Gold Crest.
  Naibu Waziri wa Nishati na Madini,Mh Stephen Masele akimtambulisha mmiliki wa hotel kubwa ya kitalii hapa jijini Mwanza, Gold Crest,Bwa.Mathias Erasto,ambaye pia ni mchimbaji mdogo wa madini,aliyajipatia fursa mbalimbali na kuzitumia ipasavyo na kufikia hapo alipo kimafanikio.
 Mkuu wa Wilaya ya Iramba mkoani Singida,Mh.Yahaya Nawanda akizungumzia mada yake iliyohusu suala la ufugaji,hasa kuku wilayani mwake,ambapo pia amewataka vijana kuitumia fursa ya ufugaji wa aina yoyote katika suala zima la kujiletea maendeleo kwa namna moja ama nyingine badala ya kusubiri Serikali iwafanyie ama iwaletee kila kitu hapo walipo.
Naibu Waziri wa Mawasiliano,Sayansi na Teknolojia,Mh Januari Makamba akizungumza kwenye mada yake iliyohusu masuala mbalimbali, kuhusiana na Fursa ya kuongeza thamani na kutengeneza jina,sambamba na fursa ya matumizi ya Teknolojia mbele ya maelfu ya vijana waliojitokeza kwa wingi mapema leo kwenye semina ya kamata fursa twendzzetu,iliyofanyika leo,ndani ya ukumbi Gold Crest,jijini Mwanza.
 Sehemu ya wakazi wa mji wa Mwanza waliojitokeza kwa wingi mapema leo kwenye semina ya kamata fursa twendzetu,wakifuatilia yaliyokuwa yakijiri ukumbini humo,ambapo mada mbalimbali zilikuwa zikizungumzwa. 
  Mmoja wa wasanii wa bongofleva,Nikki Wa Pili akizungumza kwenye semina ya kamata fursa twendzetu.
 Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya Maxcom inayouza bidhaa yake ijulikanayo kama Max Malipo,Bwa.Juma Rajab akizungumzia kuhusiana na fursa ya bidhaa yake ya Max Malipo inavyoweza kuisadia jamii kwa namna moja ama nyingine.
Baadhi Washiriki wakifuatilia.
Mmoja wa waigizaji mahiri wa filamu hapa nchini Elizabeth Michael akijulikana zaidi kwa la kisanii kama Lulu akiwasili kwenye semina ya kamata fursa Twendzetu,ndani ya ukumbi Gold Crest,jijini Mwanza asubuhi hii,ambapo pia atazungumzia mambo kadhaa mbalimbali kwenye semina hiyo,ambayo itawakutanisha Naibu Waziri wa Mawasiliano,Sayansi na Teknolojia,Mh Januari Makamba,Mbunge wa jimbo la Kigoma Kaskazini na watoa mada wengine mbalimbali

Mkurugenzi  Mtendaji wa Benki ya Wanawake Tanzania (TWB),Bi.Magreth Chacha alipokuwa akiwasili kwenye  semina ya kamata fursa Twendzetu,ndani ya ukumbi Gold Crest,jijini Mwanza asubuhi hii.

Naibu Waziri wa Mawasiliano,Sayansi na Teknolojia,Mh Januari Makamba akiwa ameambatana na Naibu Waziri wa Nishati na Madini,Mh Stephen Masele (mwenye miwani) akisalimiana na Mkurugenzi wa Benki ya Wanawake Tanzania (TWB),Bi.Magreth Chacha walipokuwa wakiwasili kwenye  semina ya kamata fursa Twendzetu,ndani ya ukumbi Gold Crest,jijini Mwanza asubuhi hii,pichani kati ni Mkurugenzi wa vipindi na uzalishaji Clouds Media Group,Bwa.Ruge Mutahaba.

Baadhi ya Wakazi wa mji wa Mwanza na vitongoji vyake wakiwa wamejitokeza kwa wingi kwenye  semina ya kamata fursa Twendzetu,ndani ya ukumbi Gold Crest,jijini Mwanza asubuhi hii. 
 Sehemu ya meza kuu.

YANGA VS RUVU SHOOTING: MRISHO NGASSA KUIBEBA AMA KUIPONZA YANGA?

Yanga ina zaidi ya mwezi bila kushinda mechi yoyote. Sare nne mfululizo zilizokuwa zikionekana matope ziligeuka nafuu baada ya kipigo kutoka kwa Azam kilichowafanya wajikute wakiambulia pointi sita tu kati ya kumi na tano katika mechi tano za msimu mpya wa ligi kuu.

Gumzo kubwa kuelekea pambano la leo ni kurudi dimbani kwa Mrisho Ngassa. Ngassa anarudi Jangwani kwa mara ya Kwanza baada ya kuwa 'utumwani' Azam na Simba kwa misimu mitatu iliyopita. Anarudi uwanjani baada ya kutumikia adhabu ya mechi sita kwa kusajili timu mbili, Simba na Yanga. Macho na masikio yatakuwa kwake hasa baada ya kugonga vichwa vya habari kwa takriban wiki nzima kuelekea pambano la leo. Unaweza kufananisha sakata lake na lile la Liverpool na Suarez.

Suarez alirudi Uwanjani baada ya kutumikia adhabu ya mechi kumi lakini alishindwa kuiokoa klabu yake. Liverpool ilijikuta ikiambulia kipigo mbele ya Manchester United. Je,Ngassa ataweza kufanya kile alichoshindwa kufanya Suarez Jumatano? Yanga watalia ama kucheka na urejeo wake?

Msemaji wa Ruvu Shooting, Masau Bwire ametamba kuwatonesha vidonda Yanga. Amesema ' Yanga ni majeruhi wenye vidonda...tunataka kuwajeruhi zaidi kwa kuvitonesha hivyo vidonda".

Yanga wanakabiliwa na mechi ngumu baada ya pambano la leo, wataikaribisha Mtibwa Sugar kisha kuwafuata Kagera Sugar huko Kaitaba kabla ya kupambana na watani wao wa jadi, Simba. Ikumbukwe katika msimu uliopita, Yanga waliondoka nane tu kati ya kumi na nane katika mechi sita dhidi ya timu hizo tatu, Simba, Kagera na Mtibwa. Kuteleza kwenye mechi ya leo inaweza kuwa ishara ya kuuweka rehani ubingwa wao.

SOURCE: LONESTRIKERTZ

MWINYI KAZIMOTO NA UBORA WA LIGI YA TIMU SITA HUKO QATAR

Licha ya kuwa wanasoka wa Tanzania wamekuwa wazito kuvuka mipaka kucheza soka la kulipwa, hali ni tofauti unapoongelea Uarabuni. Ni kweli kuwa milango ya kucheza soka la kulipwa bado ni migumu kufunguka jambo lilojidhibitisha kwa mara nyingine msimu huu ambapo ni wachezaji wawili tu, Kapombe na Kazimoto walioweza kuvuka mipaka baada ya kumalizika kwa ligi kuu. Hata katika uhamisho wa wachezaji hao wa Simba jambo lilojidhihirisha ni ugumu wa uuzwaji wa wachezaji wetu. Kwa lugha nyepesi ambayo hata wakala aliyesimamia uhamisho wa Kapombe alikiri na kuitumia ni kuwa ' wachezaji wetu bado ni bidhaa isiyouzika kimataifa'.

Ugumu wa uhamisho wa Kapombe unajulikana kwa wote wanaofuatila kandanda la nchi hii na kama si jicho zuri la biashara na akili za kujiongezea kutoka kwa wakala wake pamoja na viongozi wa Simba hakuna shaka chipukizi huyo ilikuwa arudi kwenye mpira wa Temeke. Bidhaa yetu, yaani wachezaji wetu bado ni bidhaa isiyo na thamani kwenye soka la kimataifa. Hata ligi ya Afrika Kusini ni ngumu kwetu.

Nirudi kwenye suala la Kazimoto, kiungo wa timu ya taifa ambaye wengi tunaamini ni moja ya viungo waliobarikiwa vipaji vya hali ya juu. Licha ya kipaji chake na umahiri alionesha uwanjani katika jezi za Simba na Taifa Stars ukweli unabaki kuwa Kazimoto hakufanikiwa kupata timu ya ligi kuu Qatar. Hakufanikiwa kuvishawishi vilabu vya ligi kuu Qatar na kuangukia ligi ya pili yenye timu sita tu. Ndio, timu sita! Wakati nchini tunalia kuwa udhaifu wa ligi yetu unachangiwa na uchache wa vilabu, Kazimoto yupo kwenye ligi ya timu sita. Tujiulize amepiga hatua, ameganda au amerudi nyuma?

Kiuchumi, yaani maslahi yake binafsi hakuna shaka kuwa amepiga hatua. Bila shaka anaweka kibindoni kitita kikubwa zaidi ya kile alichokuwa anapata Msimbazi. Kutoka JKT Ruvu kwenye mshahara wa laki na sabini, kujaa Simba hadi Qatar ni hatua kubwa kiuchumi. Inawezekana hakuna sifuri iliyoongezeka kwenye mshahara wake lakini ni lazima kuna namba kubwa zimeongezeka,hilo halina shaka hasa kwa nchi yenye uchumi mzuri kama Qatar.

Hata Simba, licha ya usiri na mkanganyo ( Bonyeza Hapa kusoma Makala inayochambua mkanganyo wa malipo ya Uhamisho wa Kazimoto) kwenye malipo bado wamefaidika kiuchumi. Bingwa wa ligi nchini anapewa takriban dola elfu hamsini ambazo zinakaribiana na kiasi walichopokea Simba kwenye uhamisho wa Kazimoto. Yaani ni sawa na kusema hata Simba wakikosa ubingwa msimu huu ni kama wameshapata zawadi ya ubingwa kutokana na mauzo ya Kazimoto. Kiuchumi ni bao zuri kwa Simba na Kazimoto, wote wamefanya biashara.

Swala la maendeleo binafsi na mchango kwa taifa wa mchezaji wa kulipwa Uarabuni ni tata kidogo na wengi tutatofautiana, wengine tutasema ni hatua mbele ilhali wengine watasisitiza ni hatua kurudi nyuma. Pia kuna wachache wanaweza kuwa wanaamini hakuna hatua aliyopiga, yaani kiushindani wa ligi yupo pale pale.

Kutokana na viwango vya wachezaji wengi kuonekana kuporomoka baada ya kwenda Uarabuni kuna kasumba iliyojengeka kuwa ligi za Uarabuni ni dhaifu. Tena hoja ya udhaifu huo inapigwa jeki na wingi wa Wachezaji wa Tanzania waliopata fursa ya kucheza Uarabuni kulinganisha na mabara mengine. Kauli za kuwa hakuna anayeshindwa majaribio ligi za Uarabuni zinaipa nguvu zaidi hoja ya kuwa ligi yetu ni bora kuliko ligi nyingi za Uarabuni.

Nakumbuka kauli ya kocha wa zamani wa Yanga, mkongomani Raul Shungu baada ya kumtazama Waziri Mahadhi aliporejea nchini kutoka Uarabuni. Shungu alitikisa kichwa kama vile aamini kisha akatamka ' Mahadhi amenepa hadi kichwa! Mpira wote umepotea miguuni..." Waziri Mahadhi aliyerudi nchini si yule aliyeondoka huku akiwaacha mashabiki na kumbukumbu za Mendita hasa kwa soka alilopiga kwenye michuano ya Castle Cup...walioangalia mechi ya Taifa Stars dhidi ya Simba wa Kongo kwenye Castle Cup pale Arusha watakuwa wana kumbukumbu nzuri. Waziri Mahadhi ni mfano mmoja kati ya mingi ya wachezaji waliotimkia Uarabuni na kurejea makapi. Hata Ghana wanalia na Asamoah Gyan kukimbilia Uarabuni licha kuwa huwezi kulinganisha ligi aliyotoka Gyan na aliyotoka Kazimoto.

Kazimoto yupo kwenye ligi ya timu sita tena si ligi kuu, tujiulize kapiga hatua mbele kiuchezaji au ni hatua kurudi nyuma? Ligi ya daraja la pili Qatar ni bora kuliko ya kwetu? Nizar Khalfan na Danny Mrwanda baada ya kwenda Kuwait walirudi vipi? Je, ni kweli Nizar aliyetoka Kuwait si yule aliyekuwa hapa akiwatungua makipa kwa mikwaju ya masafa marefu? Kazimoto aliyeondoka nchini akipiga pasi za uhakika atarudi vipi? Ligi yenye pesa lakini ushindani wa timu sita tu utamkuza au kumshusha kiwango? Yaani msimu mzima kama asipokaa benchi na kuepuka majeruhi Kazimoto atacheza mechi 11 za ligi.

Pia tusisahau, kitakwimu ligi kuu ya Qatar iko juu yetu. Ina makocha wa kimataifa haswa, wakufunzi waliodhibisha ubora wao kwenye dunia ya Kwanza kisoka na kiuchumi. Hakuna shana kuwa Qatar wanatuzidi vitu vitatu kati ya vinne vinavyotakiwa kukatika ukuzaji wa soka, ubora wa vifaa,walimu, na viwanja. Naamini kuwa tunawazidi jambo la nne, yaani vipaji. Mtu akikuzidi kwenye vitu vitatu na wewe ukamzidi kimoja mnaweza kulingana? Wenzetu wana vifaa bora, viwanja safi na walimu bora tunaweza kuwazidi kweli? Kipaji ni sehemu ndogo tu ya mchezaji, wengine wamediriki kusema ni aslimia 10% tu ya mchezaji bora. Tutawezaje kusema ligi yetu ni bora kwa misingi ya vipaji tu?


SOURCE: LONESTRIKERTZ.BLOGSPORT.COM

Friday, September 27, 2013

MAKALA: WAZUNGU WAMESHINDWA, KIBADENI AMEWEZA


KOCHA mkuu wa klabu ya Simba, Abdallah Kibaden inaelekea amejiuliza “makocha wazungu wanaweza wana nini, na makocha wazawa wanashindwa wana nini?”
Msimu uliopita, akiwa kocha mkuu wa klabu ya Kagera Sugar ya Bukoba alihakikisha inazichapa klabu za Simba ya Yanga ambazo zilikuwa zinanolewa na makocha wazungu katika Ligi Kuu ya Bara.
Msimu huu, Kibaden aliitosa Kagera Sugar akaingia mkataba na Simba. Klabu hiyo na nyingine inazoshiriki Ligi Kuu zinafanya vizuri tofauti na zile zinazofundishwa na wageni au makocha wa Kizungu.
Simba ndiyo inaongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 11, ikifuatiwa na JKT Ruvu iliyo chini ya mzawa Mbwana Makata yenye pointi tisa.
Hadi mzunguko wa tano Jumapili iliyopita, timu zinazonolewa na makocha wageni zinaonekana kuchechemea. Azam FC iliyo chini ya Mwingereza, Stewart Hall ipo nafasi ya tatu ikiwa na pointi tisa huku Kagera Sugar inayonolewa na Mganda Jackson Mayanja ikiwa nafasi ya sita na pointi nane.
Mabingwa watetezi wa ligi hiyo, Yanga chini ya Ernie Brandts raia wa Uholanzi, ipo nafasi ya nane ikiwa na pointi sita. Timu zote hizo zimecheza michezo mitano.
Kwa muda mrefu Simba ilikuwa chini ya makocha wa kigeni hasa wazungu kutoka nchi mbalimbali za Ulaya, wa mwisho wa kigeni alikuwa raia wa Ufaransa, Patrick Liewig.
Simba haikuwa katika kiwango chake chini ya kigeni hasa kuanzia miaka hii ya 2000, na hata mwaka huu ilipoachana na Liewig haikuwa katika kiwango cha kuridhisha.
Ukimwacha Patrick Phiri wa Zambia aliyewahi kuipa ubingwa klabu hiyo yenye maskani yake Mtaa wa Msimbazi, Dar es Salaam, makocha wengine kama Neider dos Santos (Brazil), Nielsen Elias (Brazil), Krasmir Benzinski (Bulgaria), Milovan Cirkovic na Liewig hawakuwa na matokeo ya uhakika japokuwa timu ilikuwa ikipata ushindi na hata ubingwa.
Hata makocha wageni waliofanikiwa katika kikosi hicho, mara nyingi wasaidizi wao walikuwa wazawa kama Amri Said, Kibadeni na Jamhuri Kihwelo ‘Julio’. Kazi kubwa ya wazawa ni kuwa kiunganishi kati ya kocha na wachezaji.
Kitu kinachoitafuna Simba inayoundwa na wachezaji wengi chipukizi, ni saikolojia. Vijana wengi wanaonekana kucheza vizuri, lakini bado hawajiamini wawapo uwanjani.
Hilo huwa jukumu la kocha na benchi zima la ufundi (wasaidizi hasa), lakini kwa vile benchi la ufundi linadhibitiwa na wazawa Kibadeni na Julio, inawawia rahisi kuzungumza nao kwa Kiswahili kuwaweka sawa vijana hao ambao sasa wanafanya vizuri. Ukiwachanganya na wazoefu kama Hamisi Tambwe, Henry Joseph na Amri Kiemba, Simba sasa ipo moto.
Inapotokea kocha wa kigeni akawa na jukumu moja tu la kufundisha timu na kurudi hotelini, huku akiwa hana muda wa kutazama hali za kisaikolojia za wachezaji wake huku akishindwa kujua matatizo ya wapiganaji wake, mambo huwa tofauti uwanjani.
Itazame Yanga sasa, inaonekana moto uwanjani kutokana na kuwa na wachezaji wengi wazoefu huku uwepo wa kocha msaidizi Fred Minziro ukisaidia kuwaweka sawa kisaikolojia wachezaji wote.
Katika miaka ya 2000, Yanga imewahi kufundishwa na Jack Chamangwana (Malawi), Milutin Sredojevic ‘Micho’, Dusan Kondic, Kosta Papic (wote Serbia), Sam Timbe (Uganda), Tom Saintfiet (Ubelgiji) na Brandts raia wa Uholanzi ambaye hadi sasa anainoa timu hiyo.
Mara nyingi makocha wote hao wamepata mafanikio kutokana na usaidizi wa karibu na makocha wazawa. Na mbaya zaidi makocha hao wazawa wengi wao wana elimu ama zinazolingana au zinazokaribiana na zile za makocha wa kigeni.
Tatizo linaloikabiri Simba inapokuwa na makocha wa kigeni ni lile lile lililopo kwa makocha wa Yanga. Tena mbaya zaidi kwa timu hizi, ni kuwa na lundo la wachezaji ambao lugha ya Kiingereza inakuwa tatizo kwao.
Ukichanganya kocha wa kigeni kutokuwa na mazoea ya kutazama hali ya kisaikolojia kwa wachezaji ambao hawana msingi wa kufundishwa, halafu tatizo la lugha likihusika hapo timu lazima itayumba hata kama inakuwa na mwalimu mwenye ujuzi mwingi.
Makocha hawa wa kigeni hasa wasiofahamu lugha ya Kiswahili, hupenda kuwatumia wazawa kama wakalimani, hapo ndipo tatizo linapotokea. Katika hali ya kawaida, tafsiri inaweza kuwa tatizo, kile anachomaanisha kocha si kinachowafikia wachezaji.
Tazama Azam ikiwa chini ya Hall, bila ya ushindi wa mechi ya wikiendi iliyopita dhidi ya Yanga, mambo yangekuwa tofauti. Ana kikosi kilichosheheni wachezaji kutoka sehemu kubwa ya Afrika lakini mambo bado ni magumu.
Kuwa na wachezaji bora kunasaidia kutengeneza timu bora. Azam yenye wachezaji bora ama wachezaji hawauelewi mfumo au haukubaliki. Pia mambo mengine nje ya uwanja yanachangia hasa kutokana na tabia ya misimamo ya kocha.
Aidha, kuna matatizo katika mfumo wetu wa soka. Kuna wakati mchezaji anafika Yanga au Simba bado anafundishwa namna ya kukokota mpira. Kwa nini? Sababu ni kwamba walisajiliwa si kwa ubora bali ‘kufanikiwa’ kuzifunga Simba na Yanga na ghafla anateuliwa Taifa Stars.
Kibaden anajua udhaifu wa mfumo, anajua kuurekebisha. Hata hivyo, mfumo wa uongozi Simba na Yanga unawapenda akina Kibaden klabu ikichacha au ikiwa haipo kwenye mashindano ya kimataifa. Wakati mwingine klabu zetu huona ufahari kuwa na makocha wa kigeni hata kama hawaongezi thamani yoyote katika Ligi Kuu ya Bara.

MRISHO NGASSA: NAWALIPA SIMBA MWENYEWE NIRUDI KUITUMIKIA KLABU YANGU YA YANGA"


Mshambuliaji wa Yanga na timu ya Taifa (Taifa Stars), Mrisho Ngassa ameamua kulipa mwenyewe deni lake la Sh45 milioni anazotakiwa kuilipa klabu ya Simba baada ya kuhukumiwa na Shirikisho la Soka nchini (TFF).
Awali Ngassa alikuwa ameweka ‘ngumu’ kulipa fedha hizo na kuzua tafrani kwa mashabiki na wanachama wa Yanga kuhusiana na adhabu yake ya kulipa fidia iliyotolewa na Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi ya Wachezaji ya TFF.
Kamati hiyo ilimfungia Ngassa kucheza mechi sita, adhabu ambayo amekwisha itumikia na kilichobakia sasa ni kulipa fedha hizo ili aweze kucheza mechi za Ligi Kuu ya Tanzania Bara.
Pamoja na Ngassa kuonyesha juhudi kubwa mazoezini, sakata la ulipaji wa fedha hizo lilizua tafrani nyingine huku uongozi ukitaka kulipa fedha hizo, lakini kwa masharti ya kuongeza mkataba mwingine.
Hali hiyo ilizua maswali mengi kutokana na ukweli kuwa muda wa kuingia mkataba kwa mujibu wa taratibu za TFF ulikuwa umekwisha na suala hilo lingeweza kufanikiwa wakati wa dirisha dogo la usajili.
Baada ya kukaa kimya cha muda mrefu, Ngassa ameamua kutangaza waziwazi kuwa atalipa fedha hizo  alizochukua kutoka Simba  na faini ambayo Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi ya Wachezaji iliyoamua. Kamati hiyo ilimtaka Ngassa kulipa fidia ya asilimia 50 ya fedha Sh30 milioni alizochukua kutoka Simba.
Ngassa alisema kuwa ameamua kutoa fedha hizo kutoka katika vitega uchumi vyake na amefanya hivyo kwa sababu suala hilo linamhusu yeye huku klabu yake ya Yanga ikiadhibiwa pasipo sababu.
“Nina magari na biashara zangu, nitalipa fedha hizo na nitarejea Jumamosi kucheza mechi yangu ya kwanza ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara dhidi ya Ruvu Shooting, mpira ni kazi yangu na hili nimelifanya kutokana na mapenzi yangu ya dhati na Yanga,” alisema Ngassa.
Alisema kuwa hajisikii vizuri kukaa nje ya uwanja huku akiamini kuwa kipaji chake kinapotea. “Nimekaa nje, sikuwa na raha, sasa narejea kwa nguvu zote ili kuendeleza gurudumu la Yanga, mawazo yangu ya kucheza nje ya nchi kwa sasa nimeyafuta na hasa baada ya kupata ushauri kutoka kwa marafiki zangu, nawaomba radhi mashabiki na wanachama wa Yanga,” alisema Ngassa.
source: mwananchi newspaper

TUNAWAENDELEZAJE WACHEZAJI WETU WANAOIBUKA KWA MTINDO WA WAYNE ROONEY?



Na Baraka Mbolembole 
Miaka 11 iliyopita soka la Uingereza lilimpokea mchezaji ‘ wa aina yake’, wakati timu ya Everton ikicheza na Arsenal katika mchezo wa ligi kuu, mwanzoni mwa msimu wa 2002/ 03. Alikuwa ni kijana wa miaka 16 ambaye kocha David Moyes ( wakati huo) alimuinua katika bechi la wachezaji wa akiba, na kwenda kufunga ‘ bao kali la mkwaju wa mbali’, Everton ikashinda mchezo huo kwa mabao 2-1, lakini habari kubwa ilikuwa ni Wayne, alikuwa ni mchezaji kijana zaidi kuwahi kufunga bao katika historia ya ligi kuu ( wakati huo).

‘ PELE mweupe’ alifikia hatua ya kufananishwa hivyo kutokana na kile alichokionesha uwanjani. Ni mmoja wa wachezaji bora ‘ namba kumi’ anayeweza kucheza katika mfumo wowote na kutoa matunda. Mtaalamu wa mashuti ya mbali ( kabla hajaumia sehemu ya enka yake mara mbili) Rooney angeweza kufunga bao hata akiwa umbali wa mita 30, anaweza kufunga akitokea pembeni, iwe upande wa kulia au kushoto, pia anakuwa hatari zaidi katika eneo la ushambuliaji wa kati. Alijiunga na Everton wakati akiwa mtoto mdogo, na akapandishwa katika kikosi cha wakubwa na kuwa mchezaji wa kulipwa, 2002. Akatumia misimu miwili katika klabu hiyo ya ‘Mersyside’ kabla ya kujiunga na Manchester United, wakati wa majira ya kiangazi, 2004.
Kuanzia hapo ameweza kushinda mataji matano ya ligi kuu England, taji moja la Mabingwa wa Ulaya, lingine moja la Klabu bingwa ya dunia, huku akiwa na medali mbili za ushindi wa pili katika ligi ya mabingwa Ulaya na mbili za ligi kuu England, na mapema mwezi huu aliifungia United bao la 201 na kuwa mfungaji bora wanne wa muda wote katika timu hiyo ya Old Trafford. Akiwa na medali nyingine za ushindi wa vikombe vya FA, Capital One, Ngao ya Jamii na tuzo nyingi binafsi ambazo amezipata akiwa na United.
Katika ngazi ya soka la Kimataifa, Wayne alianza kuichezea England, mwaka 2003 na hadi sasa ameicheza jumla ya michezo 84 na kuifungia mabao 36, akiwa karibu kuvunja rekodi ya muda wote ya ufungaji katika kikosi cha ‘ The three l.ions’, mabao manne nyuma ya Michael Owen, aliyefunga mabao 40, na 13 nyuma ya kinara Bobby Charlton ambaye alifunga mabao 49. Aliweka rekodi ya mchezaji mdogo zaidi kuiwakilisha England ( kabla ya Theo Walcott) kuvunja rekodi hiyo, ni ni mchezaji mdogo zaidi kufikisha michezo 50 ya kimataifa kwa upande wa England. Rooney aliweka redi ya mfungaji bora zaidi kijana katika historia ya michuano ya Euro. Alifanya hivyo mwaka 2004 katika michuano iliyopigwa nchini Ureno. Wayne ni mshindi binafsi, akiwa tuzo tano za mchezaji bora wa mwezi wa ligi kuu, sambamba na Steven Gerrard, wawili hao ndiyo wenye rekodi ya kutwaa tuzo hiyo mara nyingi zaidi. Rooney msindi wa tuzo ya mchezaji bora wa mwaka mara mbili ( 2008, 2009) Ameshiriki mara tano katika tuzo ya mwanasoka bora wa dunia. Na ameiwakilisha England mara mbili katika fainali za kombe la dunia, 2006 na 2010, pia amecheza fainali mbili ya Euro, 2004 na 2012.

YUPO WAPI HERRY MORRIS? NAOMBENI REKODI YAKE YA UCHEZAJI 
Ninakumbuka wakati ule Rooney akichomoza katika klabu ya Everton, nchini Tanzania katika timu ya Tanzania Prison ilikuwa na rundo la wachezaji bora, kuanzia kwa Dixon Osward, Samson Mwamanda, Osward Morris na wengineo, kiburudisho kilikuwa wakati mpira ukiwa katika miguu ya kiungo Primus Kasonso, Misango Magae ‘ Diego wa Mbeya’, au kwa mshambuliaji kinda wakati huo, Herry Morris ( mdogo wake na Osward) Morris alikuwa mfungaji mwenye kipaji hasa cha kufunga, aliweza kufunga akitokea kulia, kushoto au katikati, alikuwa akitega na kuivunja ‘ mitego ya offside’ na akatamba kwa staili yake ya kufunga mabao ya kuvutia. Achana na Morris, katika timu ya CDA ya Dodoma kulikuwa na mshambuliaji mmoja hivi, Dominick Meshaki, aliwafunga Simba, Yanga popote pale alikuwa na mashuti, uwezo wa kumili mpira na kasi ambayo mshambuliaji anatakiwa kuwa nayo, katika timu ya Mtibwa kulikuwa na Nicco Nyagawa, kuna mtu anaweza kusema Nicco hakuwa bora sana kama mchezaji wa kiungo lakini wakati yupo Mtibwa alipata uzoefu kutoka kwa kina Monja Liseki, Thomass Masamaki ( marehemu), na kinda mwenzake Abuu Mkangwa, Nicco alikuwa na shabaha hasa, kipaji kizuri cha ufungaji na mchezaji mwenye nidhamu muda wote. Hawa ni wachache tu kati ya wengi ambao hawakutamba kwa muda mrefu na kupotea.
KWA NINI ROONEY YUPO HERRY HAYUPO 
Tumekuwa tukiwatumia wachezaji wetu kama ‘ nguo tu’ . Wakati nikichezea timu ya Burkina Faso ya Morogoro, 2008 nilipata bahati ya kukutana na mmoja wa wachezaji wa Prisons ambao walikuwa ni sehemu ya wachezaji wa kikosi cha Herry. Niliwahi kumuuliza ni kwa nini hawakuweza kutwaa ubingwa wa Bara, 2002 wakati nafasi ilikuwa ni yao. Prisons wakati huo ilikuwa ikihitaji sare tu ili kuwa mabingwa lakini wakapigwa mabao 4-1 na Yanga ambao hawakuwa na nafasi wakatwaa ubingwa mbele yao. Aliniambia kwa uwazi kuwa tatizo lilikuwa ni kuwepo kwa watu wa Yanga katika timu yao. Aliniambia wakati Yanga ikipata bao la tatu, aliyekuwa kocha wa Prisons wakati huo, alitaka kushangilia kutokana na mapenzi yake kwa Yanga. Ila akajikaza, ‘ wajanja’ walikuwa tayari wameshtukia, wakajifanya hawajui, timu ilikuwa ikicheza vibaya uwanjani, wachezaji waliokuwa wakitegemewa walikuwa katika benchi na wale ambao walikuwa na msaada wa wastani kwa msimu mzima walikuwa ndani ya uwanja. Wakapigwa bao la nne, kwa maelezo ya mchezaji huyu ambaye alikuwa katika bechi wakati huo, ni kwamba kocha wao ( Prisons,) alikwenda katika moja ya vyoo vya uwanjani hapo na kujifungia ndani . Unafikiri alipatwa na haja, hapana. “ Watu walimkuta anashangilia kwa kurukaruka chooni” . Unajua ukiwa mbali sana na wahusika wa mpira wetu unaweza kufikiri muda wowote timu zetu zitacheza fainali ya vilabu Afrika na pengine kutwaa taji hilo ‘ ambalo ni ndoto isiyokuwepo kwa wenye dhamana ya kuviongoza vilabu vyetu’.

Hata mimi naunga mkono, Simba kwanza, Yanga kwanza, nyingine zifuatie. Ila inakuwaje kocha ambaye anakuwa na nafasi ya kutwaa ubingwa wa nchi na kung’arisha ‘ CV’ yake anaingia katika mkumbo wa kupanga kikosi ‘ kibovu’ katika mchezo muhimu ili timu anayoishabikia itwae taji. Bahati mbaya hali hii imekuwa ikifanywa na wale wenye mapenzi na Simba au Yanga, siyo mapenzi ya maendeleo hapana, bali kulinda nyazifa zao katika klabu zao.

Kumekuwa na ahadi ambazo baadhi ya wachezaji wa timu ‘ ndogo’ ambazo zinakuwa na nafasi ya kufanya vizuri katika ligi na pengine kutwaa ubingwa kuahidiwa kusajiliwa na timu kubwa kama ‘ tu wataregeza’ ili timu zao zifungwe na timu kubwa. Rejea kuhusu Prisons, na baadae Moro United, 2005 kuna rundo la wachezaji waliisiwa kuziumiza timu hizo kwa sababu ya kupata nafasi katika timu zetu kubwa. Kumbuka wachezaji wangapi walikwenda Yanga kutoka Prisons, 2002 na waliotoka Moro United kwenda Yanga, 2005. Hapa hatuwaendelezi wachezaji wetu vijana zaidi ya kuwashusha thamani.

“ Fabio ( Capello) mimi ni kichaa, nimetoka kutumia kiasi kikubwa cha pesa kumsajili mchezaji yosso” ni maneno ya Sir Alex Ferguson alipokutana na kocha Fabio Capello wakati wa upangaji wa makundi ya ligi ya mabingwa, agosti, 2004 jijini Lyon, Ufaransa. Ferguson alikuwa ametoka kumsaini Rooney kwa ada ya uhamisho euro 25 million ambayo ilifikia hadi euro 27 million na pamoja na matatizo yake yote ya kinadhamu fergie aliweza kumfanya Rooney kuwa mchezaji bora. Alimsimamia na kumuongoza hata alipokuwa akisumbuliwa na mambo ya nje ya uwanja, ulevi, ufuksa na mambo ambayo wakati Fulani yalitishia usalama wa kipaji chake, bado Fergie alimthamini na kutambua umuhimu wa Rooney.

Kwa nini wachezaji wetu hawadumu kwa muda mrefu. Hata Ulaya wapo wa auina hiyo, lakini bado wachezaji wakorofi kama Nigel De Jong, Mario Balotelli, Joey Barton wanaendelea kuthaminiwa na makocha wa timu zao. Wanajaribu kuwasimamia kwa mambo mengi kubwa wakitaka kupata kile walichonacho ili kuwasaidia katika kuwaweka salama kazini mwao. Lakini sisi tuna matatizo mengi. Wachezaji wenyewe hawana imani. Hawaamini kama kuwa wakati kiwango kinaweza kushuka na kupanda tena, hawaamini kama kuna kuumia katika soka. Wao wanapopata majeraha ya mara kwa mara hufikiri kuwa wamerogwa. Vipi Owen alirogwa na nani? Phillipo Inzaghi je, vipi kwa Ricardo Kaka’? Imani inasaidia. Katika soka ni lazima kuwe na ratiba ya kumpumzika, kutembea na kufanya kazi.

Tatizo linguine ni viongozi kushindwa kuwasimamia wachezaji vijna, viongozi namaanisha kuanzia katika benchi la ufundi hadi ule wa juu, kama tunakuwa tunawaona wachezaji wa nje walio na tabia mbaya wanadumu katika soka kwa kipindi kirefu bila shaka wana wasimamizi wazuri wa ndani ya uwanja. Wako wapi kina Abuu Ramadhani, Omari Matutta, Julius Mrope, Yussuph Soka, na wengine? Karibu Joseph Kimwaga katika soka la Tanzania, mchezo wako umezungukwa na Simba, Yanga kila mahali, wanaweza kukutumia wanavyotaka kama hautakuwa makini, ila ukipata msimamizi mzuri unaweza kucheza kwa muda mrefu kama Wayne Rooney, ana miaka 11 katika soka la kulipwa na umri wa miaka 28 tu. Kama kocha wa Prisons, 2002 hakutaka kuona timu yake ikichukua ubingwa mbele ya Yanga, kama Ivo Mapunda, Shadrack Nsajigwa, Wazir Mahadhi, na Lulanga Mapunda walikosda ubingwa wakiwa Moro United, 2005 baada ya kukosa pointi 15 katika michezo 15 ya raundi ya pili, wakati walimaliza raundi ya kwanza wakiwa na pointi 45 baada ya kushinda michezo yote, basi nitaendelea kuweka kete yangu kwa Simba au Yanga. Kila mahali zipo hadi katika mifuko na mioyo ya wachezaji wa timu nyingine, ila Wayne ni motto wa ‘ Mersyside’ anatangaza kipaji chake na kufanya kazi akiwa Manchester. Herry Morris aliondoka na rekodi ‘ mbovu kabisa katika soka, tunawatazama vijana wa sasa wenye majina ‘ mazito’ katika masikio yao, na midomo ya mashabiki wa klabu zao. Daima Rooney alishindwa kufanana na Pele, nap engine sifa za kuitwa ‘ Pele mweupe’ hakustahili kupewa ila atabaki Wayne Rooney, mwenye kipaji, usongo wa mataji na kiu ya mafaniko. Sijui ni vipi kwa Ramnadhani Singano ‘ Messi’. Rooney tayari ana mabao 201 OT.... 0714 08 43 08

HATIMAYE LEWANDOWSKI KUSAINI BAYERN MUNICH MWEZI JANUARY - MWENYEWE ATHIBITISHA


Mshambuliaji wa Borussia Dortmund Robert Lewandowski amethibitisha rasmi kwamba atasaini mkataba wa kwanza wa makubaliano wa kujiunga na Bayern Munich katika soko la usajili la mwezi wa  January kisha kujiunga na mabavaria mara tu mkataba wake utakapoisha mwishoni mwa msimu huu.


Baada ya tetesi za muda mrefu kuhusu mshambuliaji huyu wa kipoland, hatimaye hivi sasa ipo wazi Pep Guardiola atamuongeza mshambuliaji katika kikosi chake  2014.

Kwa mara ya kwanza mchezaji amekiri kwamba atajiunga na Bayern mwishoni mwa msimu wakati alipokuwa akihojiwa na Sport 1, alisema: ‘Ndio, nathibithisha nitahamia Bayern kwa sababu sasa hivi nikasaini mkataba wa makubaliano.’

Thursday, September 26, 2013

KAMATI YA MAADILI YASHINDWA KUWAADHIBU SHAFFIH DAUDA NA WENZAKE - LAKINI WAONDOLEWA KWENYE UCHAGUZI. KULIKONI????



KAMATI YA MAADILI TFF YATANGAZA UAMUZI
Kamati ya Maadili ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imetangaza hukumu ya mashauri nane yaliyowasilishwa mbele yake kwa kumsafisha mlalamikiwa mmoja, kutowaadhibu zaidi washtakiwa sita na kuahirisha kusikiliza shauri moja baada ya mlalamikiwa kutokuwepo.

Riziki Juma Majala, ambaye ni Katibu wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Pwani (COREFA) ndiye pekee aliyesafishwa na Kamati ya Maadili dhidi ya mashtaka ya kutoa kauli zilizosababisha kufunguliwa kwa kesi dhidi ya TFF.

Vilevile Kamati imesita kuwachukulia hatua Shafii Dauda, Nazarius Kilungeja, Wilfred Kidao, Omar Isaak Abdulkadir na Kamwanga Tambwe kutokana na kuridhika kuwa wameshaadhibiwa kwa kuenguliwa kwenye uchaguzi, hivyo hawawezi kuadhibiwa mara mbili.

Pia imesema haiwezi kumuadhibu Richard Julius Rukambura, aliyeshtakiwa kwa kukiuka Katiba ya TFF kwa kosa la kufungua kesi mahakamani, baada ya kubaini kuwa si mwanafamilia wa TFF kutokana na kuenguliwa kwenye uchaguzi.

Hoja hiyo pia ilitumika kutomchukulia hatua Dauda na mwamuzi wa zamani Omar Abdulkadir kwa hoja kuwa walipoteza sifa za kuwa wanafamilia wa TFF baada ya kuenguliwa kwenye uchaguzi na Kamati ya Uchaguzi.

Shauri la Omary Mussa Mkwaruro la tuhuma za kutumia cheti cha elimu kisichotambuliwa na mamlaka husika, limeahirishwa kutokana na Mlalamikiwa kutowasilisha utetezi wake, hivyo Kamati imeagiza Sekretarieti kuwasiliana naye ili awasilishe maelezo yake.

Watu hao walifikishwa mbele ya Kamati ya Maadili baada ya kujitokeza kuwania nafasi mbalimbali za uongozi wa TFF na baada ya usaili walibainika kuwa na matatizo ya kimaadili, hivyo ili iamue juu ya hadhi yao katika familia ya mpira wa miguu kwa kuwachukulia hatua au kuwaweka huru.
Katika hukumu iliyotolewa leo (Septemba 26 mwaka huu), Kamati ya Maadili imeeleza kuwa Majala hakiuka Kanuni za Maadili kwa kuwa vielelezo vilivyowasilishwa na TFF vinaonyesha kuwa klabu ya Kiluvya United imesajiliwa na Serikali na vyama wanachama wa TFF.

Kuhusu Rukambura, ambaye alilalamikiwa kwa kuipeleka TFF kwenye mahakama ya kiraia, hivyo kukiuka Kanuni ya 73 (3) (b) ya Kanuni za Maadili, Kamati imesema ushahidi uliowasilishwa na TFF hauonyeshi kama mgombea ni mwanafamilia wa TFF; alishaondolewa katika uchaguzi na hivyo si kati ya wagombea na hivyo mikono ya Kamati kufungwa kwa mujibu wa kanuni ya pili ya Kanuni za Maadili.

Kamati pia imeeleza kuwa Kanuni ya 73 (3) ambayo ingepaswa kutumika kumchukulia hatua, chimbuko lake ni Ibara ya 75 ya Katiba ya TFF ambayo inawalenga wanachama tu na hivyo kuamua kuwa malalamiko hayo hayana mashiko na kwani Rukambura alishapoteza sifa za kuwa mwanafamilia na hivyo kushindwa kumchukulia hatua.

Kidao alishtakiwa kwa kosa la kumiliki nyaraka za Kamati ya Utendaji kinyume na taratibu na pia kuwasilisha malalamiko yake Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) bila ya kufuata taratibu, lakini Kamati imesema kwa vile mlalamikiwa ameenguliwa kwenye uchaguzi, anatumikia adhabu ya kinidhamu na hivyo haiwezi kumuadhibu mara mbili.

Kuhusu Shafii Dauda, Kamati imesema malalamiko dhidi yake hayana mashiko kwa kuwa si mwanafamilia wa TFF na kwamba lalamiko dhidi yake linatupiliwa mbali kwa kuwa tayari ameshaondolewa kwenye uchaguzi kutokana na kosa la kinidhamu.

Kamati iliona hakukuwa na haja ya kushughulikia mashauri dhidi ya Nazarius Kilungeja, ambaye alishtakiwa kwa kukaidi maagizo ya vyombo halali vya TFF, na Kamwanga Tambwe kwa kuwa tayari wawili hao wanatumikia adhabu ya kufungiwa na Kamati ya Nidhamu.

HATIMAYE YANGA YAWALIPA NSAJIGWA NA MWASIKA DENI LA ZAIDI YA MIL 15


Baada ya vuta ni kuvute huku ikitishiwa kulimwa adhabu na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), klabu Yanga imekubali matokeo na kumalizana na wachezaji wake wa zamani, Stephano Mwasika na Shadrack Nsajigwa ‘Fusso’ waliokuwa wakiidai klabu hiyo zaidi ya Sh15 Milioni.
Wachezaji hao walikuwa wanaidai Yanga fedha hizo kutokana na malimbikizo ya ada ya usajili, ambapo uongozi wa klabu hiyo ulikuwa ukiwapiga danadana kuwalipa wakati walipokuwa waikiitumikia.
Kutokana na hali hiyo wachezaji hao baada ya kuachwa na klabu hiyo katika usajili wake wa msimu huu waliamua kuishtaki Yanga ili iweze kuishinikiza na kuwalipa haki zao.
Nsajigwa, alikuwa akiidai Yanga kiasi cha Sh 9 milioni wakati Mwasika ambaye sasa anaitumika Ruvu Shooting alikuwa akiidai Yanga Sh 6.5 milioni.
Katibu Mkuu wa Yanga, Lawrence Mwalusako ameliambia gazeti hili jana kuwa wamemalizana na wachezaji hao siku tatu zilizopita.
Alisema Yanga haikuwa na nia ya kuwadhulumu wachezaji hao isipokuwa malipo yao yalichelewa kutokana na kuwepo kwa sababu mbalimbali za kiutawala.
“Tumemalizana nao, lakini ni vema ukawauliza na wenyewe kwa uhakika zaidi,” alisema Mwalusako.
Hata hivyo Nsajigwa alipouliwa alikubali kuwa tayari wamemalizana na klabu hiyo tangu siku ya Jumatatu na sasa hana kitu chochote anachoidai klabu hiyo.
SOURCE: MWANANCHI

TIMU ZA WIZARA YA HABARI ZAANZA KWA KUTOA VIPIGO SHIMIWI

Wachezaji wa Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo wakiwa wamembeba Naibu katibu Mkuu wa Wizara hiyo Profesa Ole Sante Gabriel kusherehekea ushindi walioupata timu za kuvuta kamba za wizara hiy 
Mshambuliaji wa timu ya mpira wa pete Hadija Jaha akijiandaa kutoa pasi kwa mwenzake wakati walipokutana na timu ya Wizara ya Maji. Wizara ya Habari ilishinda kwa alama 19 kwa 15.

Kiungo wa timu ya mpira wa pete ya Wazara ya Habari Flora Mwakasala akijiandaa kutoa pasi kwa mshambuliaji wa timu hiyo Grace Kinga

Kiungo wa timu ya mpira wa miguu ya Wizara ya Habari Mbozi Katala akimtoka beki wa timu ya Wizara ya Maji wakati timu hizo zilipokutana katika mshindano ya SHIMIWI.Habari ilishindwa kwa 1-0.
Wachezaji wa timu ya kuvuta kamba ya Wanawake ya Wizara ya Habari wakiivuta timu ya Afrika Mashariki (haipo pichani) katika mchezo wa mashindano ya SHIMIWI Septemba 22.

Wachezaji wa timu ya kuvuta kamba ya Wanawake ya Wizara ya Habari wakiivuta timu ya Afrika Mashariki (haipo pichani) katika mchezo wa mashindano ya SHIMIWI Septemba 22.

Nahodha wa timu ya soka ya Wizara ya Habari Carlos Mlinda akiongoza wenzake kusalimiana na wachezaji wa timu ya Wizara ya Maji wakati walipokutana katika ya kwanza ya mashindano ya SHIMIWI.

Wachezaji wa timu ya kuvuta kamba ya Wanaume ya Wizara ya Habari wakiivuta timu ya Afrika Mashariki (haipo pichani) katika mchezo wa mashindano ya SHIMIWI Septemba 22.

Kikosi cha mpira wa miguu cha Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo. 
Kikosi cha mpira wa pete cha Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo.