Search This Blog

Saturday, September 28, 2013

YANGA VS RUVU SHOOTING: MRISHO NGASSA KUIBEBA AMA KUIPONZA YANGA?

Yanga ina zaidi ya mwezi bila kushinda mechi yoyote. Sare nne mfululizo zilizokuwa zikionekana matope ziligeuka nafuu baada ya kipigo kutoka kwa Azam kilichowafanya wajikute wakiambulia pointi sita tu kati ya kumi na tano katika mechi tano za msimu mpya wa ligi kuu.

Gumzo kubwa kuelekea pambano la leo ni kurudi dimbani kwa Mrisho Ngassa. Ngassa anarudi Jangwani kwa mara ya Kwanza baada ya kuwa 'utumwani' Azam na Simba kwa misimu mitatu iliyopita. Anarudi uwanjani baada ya kutumikia adhabu ya mechi sita kwa kusajili timu mbili, Simba na Yanga. Macho na masikio yatakuwa kwake hasa baada ya kugonga vichwa vya habari kwa takriban wiki nzima kuelekea pambano la leo. Unaweza kufananisha sakata lake na lile la Liverpool na Suarez.

Suarez alirudi Uwanjani baada ya kutumikia adhabu ya mechi kumi lakini alishindwa kuiokoa klabu yake. Liverpool ilijikuta ikiambulia kipigo mbele ya Manchester United. Je,Ngassa ataweza kufanya kile alichoshindwa kufanya Suarez Jumatano? Yanga watalia ama kucheka na urejeo wake?

Msemaji wa Ruvu Shooting, Masau Bwire ametamba kuwatonesha vidonda Yanga. Amesema ' Yanga ni majeruhi wenye vidonda...tunataka kuwajeruhi zaidi kwa kuvitonesha hivyo vidonda".

Yanga wanakabiliwa na mechi ngumu baada ya pambano la leo, wataikaribisha Mtibwa Sugar kisha kuwafuata Kagera Sugar huko Kaitaba kabla ya kupambana na watani wao wa jadi, Simba. Ikumbukwe katika msimu uliopita, Yanga waliondoka nane tu kati ya kumi na nane katika mechi sita dhidi ya timu hizo tatu, Simba, Kagera na Mtibwa. Kuteleza kwenye mechi ya leo inaweza kuwa ishara ya kuuweka rehani ubingwa wao.

SOURCE: LONESTRIKERTZ

No comments:

Post a Comment