Search This Blog

Friday, March 8, 2013

YANGA KUICHIMBIA KABURI TOTO LAKE KESHO???

MICHUANO ya Ligi Kuu ya Vodacom kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Machi 9 mwaka huu) kwa mechi mbili ambapo vinara Yanga watakuwa wenyeji wa Toto Africans kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mwamuzi wa mechi hiyo namba 135 atakuwa Andrew Shamba kutoka Pwani akisaidiwa na Abdallah Mkomwa na Abdallah Rashid pia wote kutoka Pwani. Kamishna ni Salim Singano kutoka Tanga wakati Mtathmini wa waamuzi ni Alfred Lwiza.

Nayo Polisi Morogoro itakuwa mgeni wa Azam kwenye Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi, Dar es Salaam. Azam katika mechi hiyo namba 136 na nyingine mbili zinazofuata itakuwa bila kocha wake Steward John Hall ambaye Kamati ya Ligi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imemfungia mechi tatu.

Charles Komba kutoka Dodoma ndiye atakayekuwa Kamishna wa mechi hiyo namba 136 itakayochezeshwa na mwamuzi Simon Mberwa kutoka mkoani Pwani.

Ligi hiyo itaendelea tena keshokutwa (Machi 10 mwaka huu) ambapo Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam utashuhudia mechi kati ya Simba na Coastal Union ya Tanga. Waamuzi wa mechi hiyo ni Martin Saanya akisaidiwa na Jesse Erasmo na Vicent Mlabu wote kutoka Morogoro.

RHINO, KANEMBWA ZASAKA TIKETI VPL
KINDUMBWENDUMBWE cha Ligi Daraja la Kwanza (FDL) kinaendelea kesho (Machi 9 mwaka huu) katika makundi yote matatu, lakini macho na masikio ya washabiki wa mpira wa miguu yakiwa kwenye mechi za Rhino Rangers ya Tabora na Kanembwa JKT ya Kigoma.

Timu hizo ndizo ziko katika nafasi nzuri ya kupata tiketi ya kucheza Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu ujao kutoka kundi hilo la C. Tayari Mbeya City ya Mbeya na Ashanti United ya Dar es Salaam zimeshapata tiketi za kucheza VPL msimu ujao kutoka kundi A na B.

Rhino Rangers itaikaribisha Polisi Dodoma kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora, wakati Kanembwa JKT itakuwa mgeni wa Pamba kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.

Mechi nyingine za kundi C ni Mwadui vs Polisi Tabora (Kambarage, Shinyanga), na Morani vs Polisi Mara (Kiteto, Manyara). Mechi za kundi A ni Majimaji vs JKT Mlale (Majimaji, Songea), Mkamba Rangers vs Mbeya City (Sokoine, Mbeya) na Polisi Iringa vs Burkina Faso (Samora, Iringa).

Mshikeshike ya kundi B ni Ndanda vs Ashanti United (Nangwanda Sijaona, Mtwara), Villa Squad vs Green Warriors (Karume, Dar es Salaam), Polisi Dar vs Transit Camp (Mabatini, Mlandizi) wakati Tessema na Moro United zitacheza Machi 10 mwaka huu Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment