Search This Blog

Monday, March 31, 2014

JAMHURI, MKWAKWANI, SOKOINE VIMEGEUKA VIWANJA VIGUMU KWA SIMBA NA YANGA


Na baraka Mbolembole

Hakuna, Simba, hakuna Yanga, iliyopata ushindi katika viwanja vya Mkwakwani, Tanga, Sokoine, Mbeya na Jamhuri, Morogoro?. Je, kuna siri gani kwa klabu kubwa za Simba na Yanga kushindwa kupata ushindi katika michezo mitano mitano kwa kila timu msimu huu?.

Yanga na Simba wameambulia pointi moja kila mmoja katika uwanja wa Mkwakwani. Simba ililazimisha suluhu-tasa dhidi ya Coastal Union (kumbuka Coastal, wameifunga Simba katika duru la pili ndani ya uwanja wa Taifa), na wakachapwa bao 1-0 na Mgambo JKT, katika duru la pili (kumbuka Simba iliibugiza Mgambo mabao 6-0 katika duru la kwanza).

Yanga pia waliambulia suluhu dhidi ya Coastal katika mzunguko wa pili (kumbuka Coastal ilisawazisha dhidi ya Yanga katika mzungo wa kwanza na kupata sare ya bao 1-1 katika uwanja wa Taifa), na jana wamechapwa na Mgambo mabao 2-1 ( kumbuka Yanga waliifunga Mgambo mabao 3-0 katika duru la kwanza ndani ya uwanja wa Taifa).

Yanga walikuwa timu ya kwanza kubwa kwenda kucheza katika uwanja wa Sokoine, Mbeya. Ni wakati ule ligi ikiwa bado ' mbichi' na ratiba ilikuwa inawapeleka dhidi ya timu za Mbeya City na Tanzania Prisons, walifanikiwa kupata sare ya bao 1-1 katika kila mchezo ( kumbuka Yanga waliifunga City bao 1-0 huku timu hiyo ya Mbeya ikicheza kwa zaidi ya
dakika 40 wakiwa pungufu.

Pia waliifunga Prisons mabao 5-0 wiki iliyopita, katika michezo ya
mzunguko wa pili ndani ya uwanja wa Taifa). Simba walianza kucheza uwanja wa Taifa dhidi ya timu hizo za Mbeya. Ililazimishwa sare na City, baada ya timu hiyo kusawazisha mabao mawili na kupata sare ya mabao 2-2, baadae wakaifunga Prisons mabao 3-1. Safari zao mbili katika uwanja wa Sokoine, zilishuhudia wakiambulia pointi mbili.
Walilazimisha sare ya bao 1-1 dhidi ya City, kisha suluhu-tasa mbele ya Prisons...

Mtibwa Sugar timu pekee kutoka mkoani Morogoro msimu huu, imekuwa si kali. Ilifungwa mabao 2-0 na Simba katika duru la kwanza, kisha wakachapwa tena mabao kama hayo na Yanga katika uwanja wa Taifa.
Lakini timu hiyo inayotumia uwanja wa Jamhuri dhidi ya mechi za Simba na Yanga kama uwanja wao wa nyumbani, ilikuwa ngangari na kuvibana vigogo hao wa soka nchini na kulazimisha sare katika michezo yote ya mzunguko miwili ya ya duru la pili dhidi ya timu hizo kubwa za Dar es Salaam.

Mtibwa haijafungwa na Simba na Yanga kwa misimu mitatu mfululizo katika uwanja wa Jamhuri, Morogoro. Na wakati timu za Polisi Morogoro (yenye rekodi ya kuibania Simba katika uwanja wa Jamhuri), Ndanda FC ya Mtwara na moja kati ya timu za Toto Africans ya Mwanza na Lipuli ya Iringa ikitarajiwa kupanda daraja ni wazi timu za Simba na Yanga zitakutana na matokeo magumu zaidi katika viwanja vya ugenini msimu ujao.

Nang'wanda sijaona, utakuwa uwanja wa nyumbani wa Ndanda FC, na tatari umekuwa na kumbukumbu mbaya kwa vigogo hao wakati ule ukiwa unatumiwa na timu ya Bandari ya Mtwata. CCM Kirumba si uwanja mzuri kwa Simba, na Samora, Iringa si salama kwa Yanga. 
Je, Simba na Yanga wajipange vipi? Kwanza ni kutumia muda wao mwingi kuhakikisha wanapata data za wachezaji bora wenye asili ya Dar es Salaam, na hapo wanaweza kutengeneza msingi wa timu zao wakitumia wachezaji waliozaliwa na historia ya klabu zao.

Kufanya usajili wa gharama kubwa kwa kusajili wachezaji kutoka
ng'ambo, bado hakujawahi kuleta mafanikio yoyote na funzo kubwa ambalo lipo ni kuwa wachezaji wazawa wapo wengi wenye uwezo wa kuleta mafanikio ni namna tu ya kutengeneza kikosi inavyokuwa. 
Simba ilifuzu nane bora ya klabu barani Afrika huku wakiwa na mchezaji mmoja tu kutoka ng'ambo na Yanga waliwahi kuondolewa katika raundi ya kwanza klabu bingwa wakiwa na wamesajili wachezaji kumi wa kigeni. 
Wachezaji hao mara zote usajili wao umekuwa kamari kubwa na haina matunda yoyote. Sasa ni wakati wa timu kusukwa kupitia historia na tamaduni za wachezaji husika. Eti, Okwi alikuwa mzuri Simba, tumsajili sisi.... Haina faida tena.
0714 08 43 08

1 comment:

  1. Hoja hizi ni za mtu asiyejua mpira.Sio lazima ukimsajili Okwi basi ushinde kila mechi kwani bado kuna vigezo vingine vinavyoweza kuamua matokeo ya mchezo.Kikubwea ni kuangalia hizo timu zinazotoa upinzani kwa Yanga na Simba kwenye viwanja vya mkwakwani,jamhuri na sokoine huwa zinaishia wapi mwishoni mwa ligi?Kumbuka hata Chelsea,Manchester United,Real Madrid,Man City n.k zinzofanya usajili wa gharama kubwa na kufanya maandalizi makubwa bado huwa zinafungwa na timu zinzoshuka daraja lakini bado zinaendelea kaufanya usajili wa gharama kwa kuwa ndiyo hadhi yao waliyofikia.Huwezi ukawa na kipato cha kukuwezesha kula vizuri halafu ukaendelea kula vibaya ili kuwafurahisha wapuuzi fulani

    ReplyDelete