Search This Blog

Monday, March 31, 2014

NGASSA AENDELEA KUONGOZA KWA UFUNGAJI AFRIKA: AL AHLY YAVULIWA UBINGWA NA WAARAB WENZIE

AL Ahly ya Misri juzi Jumamosi usiku ilivuliwa taji la Ligi ya Mabingwa Afrika baada ya kuchapwa mabao 3-2 na Al-Ahly Beghazi ya Libya, lakini Mrisho Ngassa wa Yanga anaendelea kuongoza kwa ufungaji (mabao sita) katika michuano hiyo licha ya kuwa timu yake ilishatolewa mashindanoni.
Mafarao hao ambao pia ni mabingwa wa Super Cup, wametolewa kwa jumla ya mabao 4-2 baada ya kukubali pia kipigo cha bao 1-0 katika mechi ya kwanza iliyochezwa Libya. Al-Ahly ilifuzu kwenye raundi ya pili ya michuano hiyo baada ya kuiondoa Yanga kwa penalti.
Katika mechi nyingine zilizochezwa juzi Jumamosi, bao pekee la mshambuliaji wa TP Mazembe, Mbwana Samatta, ambaye huichezea pia timu ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars, lilitosha kuipeleka mbele klabu yake hiyo ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo na sasa iko robo fainali.
Mazembe ambayo imefuzu kwa faida ya bao la ugenini, iliifunga Sewe Sports ya Ivory Coast bao 1-0 baada ya wapinzani wao awali kushinda mabao 2-1 mjini Abidjan wiki moja iliyotangulia.
Mechi nyingine zilizopigwa siku hiyo As Vita Club ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo iliitoa Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini kwa mabao 3-2 huku CS Sfaxien ya Morroco ikiiondosha Horoya ya Guinea kwa jumla ya mabao 3-0.
Mechi nyingine za ligi hiyo zilitarajiwa kucheza usiku jana Jumapili  ambapo klabu pekee ya ukanda wa Cecafa iliyosalia, Al-Hilal ya Sudan ilikuwa icheze ugenini na AC Léopards, AS Real Bamako itaikaribisha Espérance de Tunis, Zamalek ilikuwa wageni wa Nkana ya Zambia na ES Sétif ilikaribisha Coton Sport.
Source: Mwananchi

No comments:

Post a Comment