Search This Blog

Saturday, December 7, 2013

WANACHAMA SIMBA KUTINGA BUNGENI JUMANNE.


WANACHAMA wa klabu ya Simba wanaompinga Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ismail Aden Rage wataelekea mjini Dodoma Jumanne kwa ajili ya kuonana na Spika wa Bunge hilo, Anna Makinda kuelezea namna Mwenyekiti huyo anavyovunja Katiba ya klabu hiyo.
Awali wanachama hao walipanga kuondoka leo kwenda Dodoma ili kesho Jumatatu waonane na spika lakini wamehairisha kutokana na kesho kuangukia siku ya Uhuru ambapo watu awaendi makazini.
Akizungumza jijini Dar es Salaam kwa niaba ya  wanachama wenzake, Katibu wa tawi la mzambalauni, Daniel Kamna mwenye kadi ya uwanachama wa klabu hiyo namba 100, alisema kuwa lengo lao wanataka kufikisha matatizo ya Rage kwenye klabu hiyo kwa wabunge  hili wamshauri kuachia madaraka klabuni hapo.
"juzi tulimpa siku mbili awe amejiuzulu..., lakini ameonekana kuwa mkaidi na kiburi, sasa sisi msimamo wetu uko pale pale tumeshajipanga na tumewasiliana na wabunge wanachama wa klabu yetuambao wametualika bungeni na tutaondoka hapa Jumanne ili siku inayofuata asubuhi tuingine bungeni," alisema Kamna.
Alisema kuwa mwenyekiti wao huyo ameonyesha jeuri na kutowasikiliza wanachama waliomuweka madarakani na badala yake amekuwa na maamuzi ya peke yake yasiyokuwa na faida kwa klabu hiyo.
Kamna alisema moja ya jambo ambalo limewashangaza ni kitendo cha Mwenyekiti huyo alipokutana na mmiliki wa klabu ya Sunderland ya Uingereza mapema mwaka huu ambapo badala ya kuomba msaada kwa ajili ya klabu (Rage) aliomba msaada kwa jili ya jimbo lake la Tabora mjini.
"Sasa mtu kama huyo klabuni kwetu wa nini, ameonyesha kuweka masrai yake binafsi mbele badala ya Simba kwanza," aliongezea kusema Kamna.
Alisema kuwa Simba inawanachama na mashabiki wabunge ambao aliwataja baadhi yao kuwa ni Makongoro Mahanga, Zitto Kabwe, Iddi Azan na Mussa Azan Zungu ambao watafanikisha wao wanachama kuingia bungeni siku hiyo ya Jumatano.
"Unajua uwezi kuingia bungeni bila kuwa na mwaliko maalum kutoka kwa aidha mbunge au kiongozi mwingine pale bungeni, tayari tumepata mwaliko na tunajiandaa na safari," aliongezea kusema Kamna.
Alisema kuwa hawana ugomvi na Rage ila wanapingana naye baada ya kuonyesha vitenda vya wazi vya kuvunja katiba ya klabu hiyo hivyo wanataka ajiuzulu na kuwaachia Simba yao.
Hata hivyo alipotafutwa Rage kwa njia ya simu kuzungumzia kauri hiyo ya wanachama, simu yake ya mkononi haikuwa ikipatikana.
Klabu ya Simba ipo kwenye mvutano mkubwa wa kiuongozi katika kipindi hiki ambacho timu nyingi zipo kwenye maandalizi kwa ajili mzunguko wa pili wa ligi kuu.
Wanachama na baadhi ya wajumbe wa kamati ya utendaji wa klabu hiyo wanamtaka Mwenyekiti wao Rage ajiuzulu kwa madai ya kushindwa kufuata katiba ya klabu hiyo.

1 comment:

  1. Nadhan uendeshaji wa vilabu vya mpira kwa njia ya wanachama ufike mwishe wanachama wawe washabiki tu.

    Sababu kwa namna ya wanachana hata weledi haueshimiki, kila mtu anasema la kwake, wakufunzi wanaingiliwa katika program zao, Siasa nazo zinatawala.

    kama nitapata nafasi ya kuongoza club kama simba au yanga nitakachofanya ni kuiuza team kwa watu wachache ili mabadiliko ya kisoka yawe mepesi.

    ReplyDelete