Search This Blog

Monday, May 27, 2013

MAKALA: KWANINI RADAMEL FALCAO ANAKWENDA MONACO? MKATABA ALIOSAINI AKIWA KINDA UNAMFANYA AWE MTUMWA

Kwa umeshasikia kwamba Radamel Falcao anaelekea Monaco. Kulikuwa na tetesi nyingi  Manchester United, Chelsea, Real Madrid na timu nyingine - sasa kwanini ameishia kwenda Monaco?

Jibu ni kwa sababu ya kitu kinachoitwa "third-party ownership" (umiliki wa sehemu tatu) unaomhusisha Radamel Falcao. Kulikuwa na hali kama hii kwenye sajili wa Hulk alipohamia Zenit.

Third-party ownership ni nini?
 Ni umiliki wa haki za kiuchumi za mchezaji zinazomilikiwa na wakala/kampuni/taasisi.

Kuelezea hili inabidi kuangalia mifano ya nyuma na kuona ni namna gani "third party ownership" inavyofanya kazi. Ambao wanafuatilia ligi ya England tayari watakuwa wameshakutana na kitu hiki huko nyuma wakati Carlos Tevez na Javier Mascherano walipojiunga na West Ham United. Hapa ilikuwa mastaa wawili wa kutoka Argentina wakijiunga na klabu ya London ambao walikuwa wanahangaika kubaki kwenye ligi kuu. Utata wa usajili wachezaji hawa wawili ulipelekea West Ham kuwalipa fidia ya £18M  Sheffield United, na hatimaye FA kupiga marufuku third party ownership.

Lakini third party ownership bado ipo na inaendelea kufanyika kwenye bara la ulaya. Inatumika zaidi wachezaji wa Amerika ya Kusini kuhajihakikishia kwenda kucheza Ulaya. Jinsi inavyofanya kazi ni pale wakala/kampuni/taasisi inaponunua haki usajili za mchezaji anayechipukia. Hili linafanyika muda mwingine wakati mchezaji akiwa kwenye klabu, au muda mwingine wakati wa usajili.

Kwa mfano: Kuna mchezaji mmoja mwenye miaka 16 huko Amerika ya kusini atafuatwa na wakala na kuambiwa kama kama nahitaji msaada kwenye masuala ya masoko na kuweza kupenya kwenda kucheza ulaya. Dili za namna hii kawaida huwa zinahusisha suala la kumlipa mshahara mzuri mchezaji, kumtafutia wakala mzuri, management nzuri, mikataba ya matangazo n.k. Ikiwa mchezaji anapokubali, mmiliki wa 3 (third party owner) ataenda kwenye klabu iliyomsajili na kufanya makubaliano ya kununua haki za mchezaji za usajili - aidha zote au nusu.

Mchezaji huyu sasa atakuwa kwenye mikono ya utawala wa timu na umiliki wa third party ownership group, ambao watakuwa wanamuongoza kwenye kila jambo linalohusiana na kazi yake ya soka kutokea hapo. Hilo kawaida huhusisha kumlipa mshahara mkubwa juu ya ule anauolipwa na klabu yake, kumtafutia masoko kwenye vilabu vingine ili kujulikana zaidi, nk.

Namna nyingine ambayo third-party ownership inavyofanya kazi ni pale wakala/kampuni/taasisi inapolipa ada ya uhamisho ya mchezaji. Kwa mfano Porto wanataka kumsaini mchezaji kutoka Brazil lakini hawana fedha za kufanikisha jambo hilo, basi watawafuata wakala/kampuni/taasisi kwa ajili ya kuwezeshwa kifedha kwa dili ya kugawana 50-60% za haki za usajili wa mchezaji husika.
   
Wakala/kampuni/taasisi itawekeza kwa kila kitu kwa mchezaji ikiwa na tumaini kwamba mchezaji kwa muda fulani huko mbele atakuja kuimarika kiuchezaji, kuwa star, na watamuuza kwa gharama kubwa .

Baadhi ya mifano: Tevez na Mascherano waliwekwa kwenye klabu ya West Ham na wawekezaji kwa kuweza kuwapa utambulisho mkubwa kwenye soka la ulaya. Hilo lilifanya kazi kwa wachezaji wote wawili - Liverpool walimsaini Mascherano( kwa kununua haki zote za mchezaji kutoka kwa wewekezaji) na Manchester City hatimaye wakaweza kununua haki zote za Tevez - Manchester United hawakuwa wamenunua haki za usajili za Tevez.



Turudi kwa Falcao. Alinunuliwa na third-party ownership group kwenye usajili wake wa kwenda Porto. Wawekezaji walinunua zaidi ya 55% ya haki zake za usajili, walilipa mshahara alipokuwa Porto na baadae wakamuhamishia Atletico kwa dhumuni la mwishowe wamuuze Real Madrid. Wakati Falcao akiwa Atletico, wawekezaji walikuwa wanalipa karibia mshahara wake wote na huku wakifanya kazi ya kumtafutia matangazo ya biashara na pia kutafuta timu tajiri yenye uwezo wa kumnunua ili warudishe fedha zao na faida kubwa juu.

Takwimu za kifedha za Porto zinaonyesha yafuatayo kuhusu uhamisho wa Falcao::
Kuuzwa kwa 60% ya haki za kiuchumi za mchezaji kwa kampuni ya  Natland Financieringsmaatschappij B.V., mwezi July 2009, kwa kiasi cha fedha kinachokadiriwa kufikia 1,500,000 Euro, (manunuzi yamefanyika chini ya mchakato wa umiliki wa 40% za haki za usajili wa Falcao)
Pia kuna kipengele kingine kinachosema kwamba Porto waliwauzia 5% nyingine za Falcao, pia kuna kipengele kingine kinachosema kwamba third party wana ruhusa ya kununua asilimia nyingine 10.

Kitu kama hichi kilitokea kwamba Porto walikuwa wanamiliki 45% ya haki za Hulk.
Falcao akiwa Jorge Mendes pamoja Maradona
Kitu kingine cha kuvutia kuhusu umiliki wa Falcao. Kundi la kibiashara Doyen Sports ambayo ipo chini ya umiliki wa Jorge Mendes (maarufu kama wakala wa Cristiano Ronaldo, ambaye ndiye wakala anayeongoza kwa dili za third party.) pamoja na Peter Kenyon (CEO wa zamani wa Man United na mwenyekiti wa zamani wa Chelsea).
Katika mtandao wao wana ukurasa maalum wa Falcao pia unaweza ukaona wachezaji wengine walio chini yao. Falcao, kama ilivyokuwa kwa Hulk,akaishia kwenye hali ambayo fedha nyingi ziliwekezwa kwenye jina lake kiasi kwamba itahitaji fedha nyingi sana kwa wewekezaji kupata faida ya uwekezaji wao. Walikuwa wanalipa mshahara wake kwa misimu kadhaa, waliwapa Atletico fedha fulani ili kuwawezesha kujiendesha na wakapata udhamini wa jezi kama marejesho ya uwekezaji wao.
Falcao aliishia kujiunga na Atletico kwa ada ya uhamisho wa 40M  - japokuwa Atletico walisema msimu wa nyuma kwamba itabidi wauze wachezaji ili kuweza kupata  220M euro za deni la kodi wanalodaiwa na serikali ya Spain. Ikaja kugundulika kwamba lilikuwa dili la 20 + 20M kwa pande zote mbili klabu na akina Mendes. Mwanzoni Atletico walikubali kulipa kwa vipande 20m yao kwa Porto - wakachelewa kulipa sehemu ya kwanza ya deni na wakaishia kutoa 2.5m na kupelekea Porto kutishia kuwashtaki na kuwapeleka FIFA. Mwishowe 18M za upande wa Atletico zikalipwa na kampuni ya Doylen na hatimaye asilimia 60 za Falcao zikawa mikononi mwa kampuni hiyo. Pia imekuja kuonekana wakati Falcao akiwa na Atletico, Doylen walichukua asilimia nyingine za Falcao baada ya kuwalipia deni lao kwa Porto, kitu ambacho kilipelekea Doylen kuchukua mkataba wa udhamini wa jezi. Namna yoyote, wakawa na shea nyingi kwenye haki za Falcao na Atletico wakawa hawana msemo wowote juu ya mchezaji. Mwishowe inaonekana kama tu ilikuwa suala la mkopo kwa Atletico kutokana na kuwa na hisa chache katika haki za usajili za mchezaji.

Raisi wa Atletico Madrid alikuwa akisistiza mara kwa mara kwamba wanammiliki Falcao kwa asilimia zote, lakini jambo hilo halikuwa ukweli.

Falcao yupo kwenye mkataba wa kulipwa 10M euro kwa mwaka, na kutokana na kulipa mshahara huo wawekezaji wakataka kupata 60M euro katika ada ya uhamisho. Bei hii ikaviondoa vilabu vingi vilivokuwa vikimtaka mchezaji huyo. Atletico hawakuwa na mamlaka ya kuamua ni wapi Falcao aende.

Vilabu vya PSG, Monaco, Real Madrid, Chelsea na City vilikuwa vikimtaka. City kwa sasa hawafanyi uwekezaji mkubwa kwenye usajili. PSG tayari wana washambualiaji wa kutosha. Real Madrid hawakuwa tayari kulipa 60M za usajili + 50M za mshahara wa miaka 5. Chelsea walikuwa tayari kulipa  60M lakini mshahara wa 10M baada ya kodi ulikuwa ni mgumu kuutimiza. Pia Chelsea walikuwa wanashindwa kumnunua mchezaji huyo moja kwa moja kutoka kwa third-party owner - kitu ambacho kiliwaondoa Man United pia kwenye mbio za kusaka saini ya Falcao. Hivyo walihitaji uwepo wa hali ya kama ilivyokuwa wakati wakimsajili David Luiz.

David Luiz alikuwa mchezaji ambaye alikuwa na mkataba na third-party owner hivyo wakati Chelsea wanataka kumnunua iliwalazimu Benfica kununua haki zote za David Luiz kwa asilimia 100 ili kuwauzia Chelsea na kuepeuka sheria ya kukataza biashara ya kununua mchezaji kutoka third-party owner iliyopo nchini England.

Kwa sababu zote zilizotajwa ikabakia klabu moja tu: Monaco. Wana 60M za kuwalipa wawekezaji pia wanazo za 10M mshahara wa mwaka baada ya kodi.

Mwishowe Falcao anazungushwa kwenye vilabu tofauti barani ulaya na wawekezaji wake kwa lengo la kutafuta faida. Yeye mwenyewe hana kauli kwenye kuamua ni wapi anataka kwenda kucheza kwa sababu ya mkataba aliosaini wakati akiwa kidan unamfunga.
IMEANDALIWA NA AIDAN SEIF CHARLIE 

No comments:

Post a Comment