Search This Blog

Wednesday, February 13, 2013

JERRY TEGETE IS ON FIRE APIGA 2 - YANGA IKIZIDI KUJIKITA KILELENI - YAIPIGA AFRICAN LYON 4-0, COAST YARAMBISHWA SUKARI NA KAGERA SUGAR

KLABU ya soka ya Yanga imeendeleza mauaji katika Ligi Kuu ya Bara baada ya leo kuitandika African Lyon mabao 4-0 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
 
Kwa ushindi huo, Yanga imefikisha pointi 36 na kuzidi kujikita kileleni mwa ligi hiyo, wakati Lyon nayo imezidi kudidimia mkiani mwa ligi hiyo.
 
Straika Jerry Tegete ndiye aliyekuwa kinara wa mchezo huo baada ya kufunga mabao mawili katika mchezo huo licha ya kukosa kadhaa katika kipindi cha kwanza.
 
Tegete alifunga bao la kwanza dakika ya 21 kwa kichwa akiunganisha krosi safi ya beki wa kushoto David Luhende aliyepanda kuongeza nguvu ya mashambulizi.
 
Baada ya bao hilo, Lyon walizinduka na kulishambulia kwa kasi lango la Yanga lakini washambuliaji wake wakiongozwa na Ike Bright hawakuweza kuleta madhara Zaidi katika lango la Yanga.
 
Dakika ya 42, Tegete aliifungia Yanga bao la pili kwa kisigino mpira aliopigiwa na winga Simon Msuva ambaye aliisumbua vilivyo ngome ya Lyon iliyokuwa ikiongozwa na Obinna Salamusasa. Mabao hayo yalidumu hadi mapumziko.
 
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi huku kila timu ikijaribu kushambulia lango la mwenzake lakini walikuwa ni Yanga waliofanikiwa kupata penalti dakika ya 46 baada ya beki wa Lyon kuunawa mpira ndani ya eneo la hatari. Hamis Kiiza alipiga penalti hiyo lakini kipa wa Lyon, Abdul Seif aliidaka.
 
Baada ya penalty hiyo, Yanga ilizidisha mashambulizi huku ikiwa imetawala kiungo na kufanikiwa kupata penalti nyingine dakika ya 69. Penalti hiyo ilikuja baada ya beki Salamusasa kuunawa mpira ndani ya eneo la hatari. Straika Didier Kavumbagu alipiga penalti hiyo kuiandikia Yanga bao la tatu dakika ya 69.
 
Kocha wa Yanga, Ernie Brandts alifanya mabadiliko kwa kumtoa Kiiza na kumuingiza kiungo Nizar Khalfan ambaye dakika ya 80 aliifungia Yanga bao la nne kwa shuti kali.
 
Nizar alifunga bao hilo akiunganisha krosi safi ya Said Bahanuzi kutoka wingi ya kushoto.
 
Dakika ya 90, mwamuzi Martin Saanya alimuonyesha kadi nyekundu beki Yusuf Mlipili wa Lyon baada ya kumchezea vibaya kiungo wa Yanga, Haruna Niyonzima.
Hadi mwisho wa mchezo, Yanga 4-0 Lyon.
 
Katika michezo mingine ya ligi hiyo iliyochezwa leo, JKT Mgambo imeifunga Oljoro JKT mabao 2-0, Kagera Sugar imeifunga Coastal Union bao 1-0, Toto African imetoka sare ya mabao 2-2 dhidi ya Polisi Moro na Mtibwa Sugar imetoka suluhu na Ruvu Shooting.

No comments:

Post a Comment