Search This Blog

Friday, October 21, 2011

WAZIRI: ZANZIBAR HAIWEZI KUWA MWANACHAMA WA FIFA


Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi wameambiwa kwamba Zanzibar imepoteza hadhi ya utaifa wake Aprili 26, mwaka 1964 ilipojiunga na Tanganyika na kuzaliwa kwa taifa jipya la Tanzania na hivyo haina sifa ya dola na haiwezi kuwa mwanachama wa FIFA.

Waziri wa Habari, Utangazaji, Michezo na Utalii, Abdillahi Jihadi Hassan alisema hayo katika Baraza la Wawakilishi wakati akijibu swali aliloulizwa na mwakilishi wa jimbo la RAHALEO Nassor Salim Ali aliyetaka kujua hatma ya Zanzibar katika kujiunga na shirikisho la soka la kimataifa FIFA.

“Suala la Zanzibar kupata uanachama wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) kwa sasa limegonga mwamba....naomba wajumbe mfahamu hivyo kwa sababu Zanzibar imepoteza hadhi ya utaifa wake katika mwaka 1964 April 26 ilipojiunga na Tanganyika na kuzaliwa kwa taifa jipya la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema Jihadi.

Alisema njia pekee ya kujaribu tena kujiunga na FIFA ni kutumia mchakato unaokuja wa marekebisho ya katiba kulielezea suala hilo kwa umakini zaidi.

Jihadi alisema suala la uanachama wa Fifa linaonekana zaidi kuwa na sura ya kisiasa kuliko michezo.

Alisema juhudi mbali mbali zilifanyika ikiwemo vyama vya soka nchini pamoja na Baraza la michezo la Taifa kutoa baraka zake kwa Zanzibar kupata uanachama wa FIFA lakini ilishindikana.

Waziri huyo alitumia nafasi hiyo kutoa ufafanuzi zaidi baada ya kikao kilichopita cha bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2011-2012 kuwaambia wajumbe kwamba yapo matumaini makubwa ya Zanzibar kupata uanachama wa FIFA huku akijitayarisha kufanya safari kuonana na rais wa FIFA Sept Blatter.

No comments:

Post a Comment