Search This Blog

Friday, September 23, 2011

YEW BERKO NA NIYONZIMA NDIO MAPROO WANAOKULA MISHAHARA KIHALALI YANGA

Mchezaji Athuman Iddi 'Chuji' amesema hakuna kiungo mzalendo wa kumzidi kiwango chake ndani ya Simba na Yanga huku akiwasifu Haruna Niyonzima na Yaw Berko kuwa ndio wachezaji pekee wa kigeni waliostahili kusajiliwa na Jangwani wala sio wengine wanaolipwa mamilioni.

Chuji aliachwa na Simba na kutimkia Villa Squad kabla ya TFF kumzuia kucheza Ligi Kuu na sasa yuko mtaani akifanya shughuli zake ingawa ametangaza kwamba atarudi uwanjani kwenye dirisha dogo.

"Ukiangalia namba ambazo mimi nilikuwa nacheza Simba na Yanga sasa hivi zimeshikwa na wachezaji wa kigeni, hiyo inamaanisha kwamba hakuna mzalendo yeyote wa kunifikia."
"Waliopo wameshindwa kuhimili vishindo ndio maana wamebadilishwa namba na wengine wako benchi, Yanga nafasi yangu imechukuliwa na Niyonzima 'Fabregas' na Simba yupo Patrick Mafisango ambao wote ni raia wa Rwanda,"alisema Chuji ambaye yupo Kinondoni, Dar es Salaam ingawa muda mwingi kwa sasa anaishi Tanga.

Kiungo huyo wa zamani wa Taifa Stars, hakusita kuwapongeza nyota wawili waliosajiliwa na Yanga ndio wachezaji kigeni wanaokula mshahara kihalali.

"Yanga imesajili wachezaji watano wa kigeni, lakini ni wawili tu wanaokula mshahara kihalali kutokana na msaada wao kwa timu, ambao ni Haruna (Rwanda) na Berko (Ghana), hao wachezaji wanaisaidia sana Yanga na unaona kweli ni watu wanaofanya kazi tofauti na wenzao."

"Haruna akicheza kiungo kinatulia sana na hata Berko unaona kwamba kweli huyu ni kipa hata kama timu haifanyi vizuri, lakini hao wengine hawana jipya, kuna wachezaji wengi sana wa Tanzania waliokuwa wanaweza kucheza sehemu zao,"alisisitiza Chuji.

Wachezaji wengine wa kigeni wa Yanga ambao Chuji haridhiki na uwezo wao tofauti na wanavyokuzwa na mashabiki ni Hamis Kiiza wa Uganda, Kenneth Asamoah wa Ghana na Davis Mwape wa Zambia.

Habari za ndani zinasema kuwa mchezaji huyo amefanya mazungumzo na Coastal Union ingawa bado hawajafikia muafaka na huenda akasaini wakati wa dirisha dogo la Desemba na kurudi uwanjani.

No comments:

Post a Comment