Search This Blog

Sunday, April 6, 2014

YANGA YAITWANGA JKT RUVU 5-1, MGAMBO YAINYUKA COASTAL 2-1 MKWAKWANI, PRISONS, MTIBWA ZACHAPWA!!

Na Baraka Mpenja, Dar Es Salaam

GHARIKA!. Mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania bara wameshusha mvua kubwa ya mabao 5-1 dhidi ya JKT Ruvu katika mchezo wa ligi kuu soka Tanzania bara uliomalizika jioni ya leo  kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Yanga waliuanza mchezo kwa kasi na iliwachukua dakika 8 tu kutikisa nyavu za JKR Ruvu kupitia kwa winga wake machachari, Mrisho Khalfan Ngasa `Anko`.
Dakika ya 15 ya kipindi hicho, Ngasa alitia tena mpira kambani na kuandika bao la pili kwa wanajangwani waliokuwa na uchu wa ushindi.
JKT Ruvu wakiwa doro muda mrefu waliendelea kuoneshwa ufundi na Yanga na katika dakika ya 39 Mrundi, Didier Kavumbagu aliipatia Yanga bao la tatu kufuatia kutumia vyema pasi ya Mrisho Ngasa.
Bao hili lilifungwa kirahisi kwasababu mabeki wa JKT Ruvu walizembea kwa kudhani Kavumbagu ameotea.
Yanga waliendelea kushambulia na kutawala mchezo, lakini mpaka dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika, walikuwa mbele kwa mabao 3-0.
Kipindi cha pili Yanga walianza mpira kwa kulishambulia lango la wapinzani wao ambapo dakika ya 49 Mrisho Ngasa alifunga bao lake la tatu na `kukamilisha hat-trick` kwenye mchezo wa leo.
Dakika tatu baadaye, Hussein Javu aliandika bao la tano na kukamilisha karamu hiyo ya mabao.
JKT Ruvu walipata bao lao la kufutia machozi  katika dakika ya 82 kupitia kwa mshambuliaji wake, Idd Mbaga baada ya kupewa pasi nzuri na Damas Makwaya.
Baada ya mechi hii, Mrisho Ngasa alipewa mpira wake na kuudunda dunda uwanjani, huku mashabiki wa Yanga wakimshangilia nyota huyo.
Baada ya mchezo wa leo, Yanga wamefikisha pointi 49 katika nafasi ya pili baada ya kushuka dimbani mara 23.
Azam fc wanaendelea kuwa kileleni kwa tofauti ya pointi 4 na Yanga, lakini kizuri sasa timu hizi mbili zimelingana michezo.
Jumatano ijayo, timu zote mbili zitakuwa uwanjani, ambapo Yanga wataumana na Kagera Sugar uwanja wa Taifa, wakati Azam fc watakuwa wageni wa Ruvu Shooting uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.
Kwa ujumla Yanga walitawala mchezo wa leo ndani ya dakika zote 90.
JKT Ruvu walipoa sana na  kuonekana kukosa  mipango ya aina yoyote.
Toka mwanzo walikuwa wamezidiwa katika idara zote na kuwafanya Yanga kucheza kama watakavyo.
Si kawaida ya Kocha Fredy Felix Majeshi Baba Isaya Minziro kutulia muda mwingi pale timu yake inapofanya vibaya, lakini leo hii muda mwingi wa mchezo alitulia tuli.
Matokeo ya leo ni mabaya kwa Minziro kwani anaendelea kubakia nafasi ya 9 kwa pointi 28, huku wakibakiza mechi mbili tu.
Sasa watahitaji kushinda mechi zote mbili walizosaliwa nazo kibindoni ili kujinusuru kushuka daraja.
Kwa upande wa Yanga imewapa unafuu mkubwa katika harakati zao za kutetea ubingwa wao.
Yanga na Azam fc wanachuanoa kuwania ubingwa, na kila klabu inahitaji kushinda mechi zote ili kujiweka mazingira mazuri ya kutwaa taji.
Azam fc wanahitaji kushinda mechi zote tatu ili kuwazuia Yanga kubeba mwari .
Hata hivyo kama Azam fc atashinda mechi mbili kati ya tatu alizosaliwa nazo na kufungwa moja, watafikisha pointi 59.
Wakati huo huo,  Yanga wakishinda mechi zote tatu walizosaliwa nazo watafikisha pointi 58 ambazo Azam fc atakuwa amevuka.
Kwahiyo Kama Azam fc atapata pointi 6 tu katika michezo mitatu iliyosalia,  rasmi Yanga watakuwa wamevuliwa ubingwa wao kwasababu hawataweza kufikisha pointi 59 hata kama watashinda kwa mabao 100 mechi zote.
Mchezo mwingine wa ligi kuu umepigwa katika dimba la CCM Mkwakwani jijini Tanga ambapo Coastal Union walioneshana kazi na Mgambo JKT.
Dakika 90 za mchezo huo zimemalizika kwa maafande wa Mgambo JKT kuendelea kujisafishia njia ya kubaki ligi kuu msimu huu baada ya kushinda mabao 2-1.
Ushindi wa Mgambo unakuwa sawa sawa na ule walioshinda dhidi ya Yanga mechi iliypita uwanja huo huo wa Mkwakwani.
Baada ya mchezo huo, Afisa habari wa Coastal Union, Hafidh Kido amesema kuwa mchezo ulikuwa wa kawaida sana, lakini Mgambo walipata nafasi mbili wakazitumia na wao wakapata moja na kuitumia.
“Sasa mambo yamekuwa magumu kwetu.  Mpaka sasa hatujafikisha pointi 30. Tumebakiza mechi ngumu na Kagera Sugar na JKT Ruvu. Tunakaa na wachezaji wetu ili kupanga mikakati ya kushinda michezo miwili iliyosalia. Ligi imekuwa ngumu , aaah! Naambiwa nao JKT Ruvu wamekula mabao 5-1”. Alisema Kido.
Kwa matokeo ya leo, Mgambo wanapanda hadi nafasi ya 10 na kuishusha Prisons baada ya kufikisha pointi 25 kibindoni, huku wakisaliwa na mechi mbili tu.
Wajelajela wamaendelea kuonja joto la jiwe baada ya kulala mabao 2-1 dhidi ya JKT Oljoro katika dimba la CCM Shk. Amri Abeid Kaluta jijini Arusha.
Matokoe hayo yanawafanya Prisons waporomoke kwa nafasi moja na sasa wanakalia nafasi ya 11 kwa pointi  22 baada ya kucheza mechi 24.
JKT Oljoro baada ya ushindi wa leo wamefikisha pointi 18 katika nafasi ya 13, lakini bado matumaini ya kubakia ligi kuu yanaonekana kuisha kabisa.
Ashanti United na Prisons zinafungana kwa  pointi , hivyo vita inaendelea baina yao na Mgambo JKT ambao angalau wamesogea mbele kwa pointi.
JKT Oljoro na Rhino Rangers wana asalimia kubwa ya kushuka daraja, huku Mgambo,  Ashanti na Prisons mmoja wapo akijiandaa kuungana nao.
Tayari timu tatu zimeshapandaligi kuu ambazo ni Stand United ya Shinyanga, Polisi Morogoro ya Morogoro na Ndanda fc ya Mtwara.
Mchezo mwingine ulipigwa dimba la Ali Hassain Mwinyi, ambapo Rhino Rangers wameona jua baada ya kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Mtibwa Sugar.
Kwa matokeo hayo, Rhino wanafikisha pointi 16 katika mechi 24 walizocheza, lakini wanaendelea kuburuza mkia.
Dhahiri inaonekana Rhino Rangers wameshashuka daraja msimu huu, kwani wamebakiwa na mechi mbili tu ambazo wakishinda zote watafikisha pointi 22 zilizopitwa na timu nyingine.

No comments:

Post a Comment