Search This Blog

Saturday, April 12, 2014

UFALME WA RAGE SIMBA WAFIKA KIKOMO, SWALI NANI KURITHI MIKOBA YAKE?, KAZI KWA WANACHAMA!!




Na Baraka Mpenja , Dar es salaam

0712461976

KWA MUDA mrefu mashabiki  na wanachama wa Simba sc wamekuwa wakiamini kuwa klabu yao imefika hapo ilipo kwasababu ya mwenyekiti wao Ismail Aden Rage kuongoza vibaya.
Rage amekuwa akisuguana na wanachama wake kwa muda mrefu, lakini sasa ameshatangaza kutogombea tena nafasi hiyo katika uchaguzi Mkuu unaotarajia kufanyika mei 4 mwaka huu.
Rage alitangaza maamuzi hayo machi 16 mwaka huu katika mkutano mkuu wa wanachama  ulioitishwa maalumu kwa ajili ya kufanya marekebisho wa katiba.
Kauli ya aina yake katika mkutano huo ilikuwa ile ya Rage kuwaita wanachama wa Simba ni  ‘mbumbumbu’
Kufuatia kauli hiyo, Rage, alilazimika kuwaomba radhi wanachama hao zaidi ya 571 waliohudhuria mkutano huyo uliofanyika kwenye Ukumbi wa Bwalo la Polisi, Oysterbay jijini Dar es Salaam.
“Napenda kuwaomba radhi wanachama wenzangu kutokana na nilivyosema tuache umbumbumbu, lakini sikuwa namaanisha kama wengi wenu mlivyoelewa,” alisema Rage.
Licha ya kusema hatagombea tena uongozi, Rage, alisema ataendelea kuwa mwanachama mwaminifu wa Simba na atatoa mchango wake ili kufanikisha maendeleo.
Ikumbukwe kuwa kabla ya kauli hiyo, Rage alishawahi kusema kauli za aina yake.
Mwezi machi mwaka jana aliwahi kuuita  mkutano wa wanachama walioaminika kuwa zaidi ya 600 ambao ulitangaza kumpindua madarakani  kuwa ni kama `kikao cha harusi`.
Pia novemba mwaka jana kamati ya utendaji ya Simba ilitangaza kumuondoa madarakani mwenyekiti wake, Ismail Aden Rage.
Kamati hiyo ilifikia uamuzi wa kumsimamisha Rage akiwa nje ya nchi  na kumtangaza aliyekuwa Kaimu Makamu Mwenyekiti, Joseph Itang’are ‘Mzee Kinesi’ kushika nafasi hiyo ya juu zaidi katika klabu hiyo.
Mzee Kinesi alisema walifikia maamuzi hayo kutokana na mwenyekiti huyo kwenda kinyume na makubaliano na Kamati ya Utendaji ya Simba.
Lakini baadaye ya mwanaume huyo kurudi alitamba kuwa yeye ni mwenyekiti halali wa Simba na kikao hicho kilikuwa kikao cha harusi.
Wakati anawasili uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mwalimu Nyerere kulikuwa na kundi kubwa la watu walioaminika kuwa wanachama wa Simba waliojitokeza kumlaki na kumshangilia kwa nguvu.
Kweli jamaa alirudi na baadaye TFF walitangaza kumtambua kuwa ndiye mwenyeki halali wa Simba, lakini wakamtaka aitishe mkutano wa dharura na kumpangia ajenda.
Rage aligoma na kusema yeye ndiye mwenye mamlaka ya kupanga ajenda za mkutano kwa mujibu wa katiba.
Yapo mengi ya kuyasema kuhusu Rage, lakini sasa ameshatangaza kung`atuka baada ya muda mrefu wa mvutano na viongozi wenzake pamoja na wanachama wa Simba.
 Baadhi ya wananachama wa Simba wanafikiria kuwa Rage ndiye mchawi wa klabu yao, hivyo kuondoka kwake ni jambo la heri.
Tarehe ya uchaguzi ilishatangazwa na tayari kamati ya uchaguzi ilishaundwa chini ya mwenyekiti wake, Dr. Damas Ndumabro ambaye ni mwanasheria kitaaluma.
Hata hivyo, Kamati ya uchaguzi ya klabu ya Simba imetangaza kuwa mchakato wa uchaguzi wa klabu hiyo utaweza kuendelea baada ya msajili wa vyama vya michezo kuipitisha rasimu ya katiba ya Simba iliyopelekwa hivi karibuni.

Mwenyekiti wa kamati hiyo Damas Ndumbaro alisema jana kuwa kamati yake ilikaa Alhamisi wiki hii na kujadili masuala mbalimbali kuhusiana na mchakato wa uchaguzi ambao awali ulipangwa kufanyika mapema mwezi ujao.

Mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi ya Simba Damas Ndumbaro amewataka
wanachama wa klabu ya Simba kuvuta subira hadi hapo msajili wa vyama
vya michezo atakaposaini rasimu ya katiba ndipo watakapo tangaza kuanza rasmi kwa harakati za kuwania nafasi mbalimbali ndani ya klabu
hiyo.
Haya sasa mambo yameshaiva ingawa bado rasimu ya katiba ikisubiriwa kusajiliwa.
Lakini cha msingi wakati unaoamini kuwa wa ufalme wa Rage kuiongoza Simba unaelekea ukingoni.
Wanachama wa Simba ndio wenye mamlaka kikatiba ya kuchagua kiongozi wao mkuu.
Ni wanachama hawa hawa waliomchagua Rage kwa kura nyingi, lakini walimkana baadaye na kuona hana maana kwa klabu.
Sasa swali la msingi kwa wanachama wa Simba, Rage anaondoka, nani wanadhani atakuwa mbadala wake?.
Nadhani wapo wengi watakaojitokeza kugombea nafasi ya mwenyekiti pamoja na wajumbe wa kamati ya utendaji.
Kuna watu wataomba kwa lengo la kuleta mabadiliko na kuifufua Simba ya miaka ya nyuma, lakini hata wachumia matumbo watakuwepo tu.
Unajua kila mtu anataka kazi fulani kwa sababu zake.
Simba ni chama kubwa, pesa zipo na ukitaka kula utakula sana kwasababu kumekosekana watu makini wa kufuatilia mahesabau ya klabu yao.
Si Simba tu, hata klabu nyingine kama Yanga kuna matatizo kama haya.
Wapo watu wanaoneemeka kuwepo katika klabu hizi na wanajulikana.
Walikuwa wa kawaida, lakini kupitia nafasi za uongozi wazipatazo, wanazidi kuwa watu maarufu kwa mkwanja.
Ukichunguza vyonza vya pesa zao utagundua ni pesa za mpira wazivunazo katika  klabu wanazozitawala.
Niliwahi kuongea na kiongozi mmoja wa chama cha juu cha soka, alinipa siri kuwa hakuna pesa nyepesi na za bure kama kwenye mpira.
Mazungumzo yetu yalikuwa ya kawaida tu na alisema kamwe nisiseme. Ni miaka mingi imepita na sasa si kiongozi tena.
Kama mtu anaingia kwa maslahi binafsi basi hana maana yoyote kwa Simba.
Ikumbukwe kuwa viongozi wetu wanakuwa na mtandao mkubwa sana.
Anapotoka huyu anataka amrithishe mtu ambaye wana mahusiano ya karibu ili waendele kuvuna mapato yasiyo halali.
Ni wakati wa wanachama wa Simba kuwapima watu watakaoomba kugombea nafasi za juu katika klabu hiyo.
Najua ni ngumu kuwajua kwa macho, lakini angalau wawatafiti wanaotarajia kuomba.
Ndani ya klabu yao, wapo walioonesha nia ingawa kwasasa hatuwezi kuwataja kwasababu mchakato bado.
Lakini wanajulikana na wanachama wanawajua vizuri tu. Na bahati nzuri walishaanza kuwapigia debe chini kwa chini.
Nawatahadhirisha Simba kutochagua kwa hasira za muda mrefu walizokuwa nazo juu ya Rage.
Najua lipo kundi kubwa lisilomuunga mkono Rage, hivyo kuondoka kwake kunawapa raha.
Lakini wasije wakachagua mtu kwa kufikiria raha ya kuondoka kwa Rage.
Kinachotakiwa ni kupima uwezo wa watu wanaoweza kuwafikisha mbali.
Najua Simba ina uchu wa mafanikio makubwa wakianza na kurejesha hadhi yao iliyopotea kuanzia uongozi na mambo ya uwanjani.
Wanahitaji mtu mwenye malengo makubwa, nia ya dhati ya kuikoa klabu hii hapa ilipo.
Watu wa aina ni wachache sana, hivyo lazima wanachama watumie muda wao kuwapima watu wanaotarajia kuomba nafasi ili mwisho wa siku wajue nani anafaa.
Wakati wa mabadiliko ndio huu, nafasi ya kubadii timu umefika.
Nafasi ndio hii, kama watakosea kufanya hivyo, watasubiri mpaka wakati mwingine uchaguzi utakapofika.
La sivyo wataendelea na sinema zao za kumpindua kiongozi, lakini mwisho wa siku wanaonekana hawana maana na vikao vyao kuitwa vikao vya harusi.
Ili kuirudisha Simba kwenye hadhi yake, wanachama fikirieni mara mbilimbili ili kupata watu sahihi.
Kwa msimu wa pili sasa, Simba sc inakosa mashindano ya kimataifa, kwasababu msimu huu wataishia nafasi ya nne au ya tano kama wakikosea hesabu zao  katika mechi mbili za mwisho.
Msimu huu wamevuna matokeo mabaya mno, na tatizo linaloonekana ni kwenye uongozi ambao kuna maamuzi ya msingi huamuriwa bila kuona mbali.
Pia kuna lawama za uongozi wa Rage kutowalipa wachezaji maslahi yao. Makocha nao hufukuzwa mara kwa mara.
Sasa mwisho wa haya ni mei 4, lakini wakikosea tu, majanga kama kawaida yataendelea.
Kila la kheri wanachama wa Simba sc katika harakati zenu za kuleta mapinduzi klabuni kwenu.

No comments:

Post a Comment