Search This Blog

Tuesday, April 8, 2014

MAJANGA AZAM FC, BRYSON RAPHAEL KUWAKOSA RUVU SHOOTING KESHO!!

Kutoka kushoto Makinda Franco, Bryson Raphael na Aishi Salum
Na Baraka Mpenja, Dar Es salaam
WANA Lambalamba, Azam fc wataikosa huduma ya mchezaji wao chipukizi Bryson Raphael katika mchezo wake wa kesho wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya Ruvu Shooting Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani.

Meneja wa Azam FC, Jemadari Said ameiambia Tovuti ya klabu hiyo kuwa mchezaji  huyo amerejea kutoka Kenya alipokwenda kuichezea timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes akiwa anachechemea kwa maumivu ya kifundo cha mguu.
Jemadari alisema  hilo ni pigo kwa timu kwa sababu huyo ni miongoni mwa wachezaji muhimu, lakini kocha Mcameroon, Joseph Marius Omog atalazimika kumuondoa mchezaji huyo katika programu yake ya kesho.
Wachezaji wengine ambao wataukosa mchezo wa kesho ni Samih Haji Nuhu, Joseph Kimwaga, Ismail Gambo ‘Kussi Jr’, Farid Mussa na Ibrahim Mwaipopo ambao wote ni majeruhi kwa muda mrefu sasa.
Mpaka sasa Azam fc wapo kileleni kwa pointi 53, pointi 4 mbele ya mabingwa watetezi, Dar Young Africans.
Mchezo wa kesho utakuwa muhimu kwa kocha mkuu Mcameroon,Omog katika harakati zake za kuwapatia Azam fc ubingwa wao wa kwanza tangu wapande ligi kuu msimu wa 2008/2009.
Azam fc wamebakiza mechi 3 tu kufunga pazia la ligi kuu. Na katika mechi hizo wanahitaji kushinda mbili na kuwavua Yanga ubingwa.
Nao wapinzani wakubwa wa Azam fc, Young Africans watawakabili Kagera Sugar katika mchezo muhimu utakaopigwa kesho uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Ligi hiyo itaingia raundi ya 25 Aprili 12 na 13 mwaka huu ambapo timu zote 14 zitakuwa viwanjani. Aprili 12 mwaka huu itakuwa Mtibwa Sugar vs Ruvu Shooting (Manungu, Morogoro), Coastal Union vs JKT Ruvu (Mkwakwani, Tanga), na Tanzania Prisons vs Rhino Rangers (Sokoine, Mbeya).

Aprili 13 mwaka huu ni Mgambo Shooting vs Kagera Sugar (Mkwakwani, Tanga), Simba vs Ashanti United (Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam), Mbeya City vs Azam (Sokoine, Mbeya) na Oljoro vs Yanga (Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha).
Wakati huo huo Azam fc wamesema beki wao wa pembeni ,  Samih Hajji Nuhu ameshawasili leo hii katika hospitali ya Vincent Palloci mjini Cape Town, Afrika Kusini tayari kuingia kufanyiwa upasuaji na Mtaalamu, Dk Nicholas. 

No comments:

Post a Comment