Search This Blog

Saturday, April 12, 2014

`BAI BAI` RHINO LIGI KUU, YAPIGWA 4-3 NA PRISONS, RASMI MINZIRO AIOKOA JKT RUVU KUSHUKA DARAJA, YAITANDIKA 1-0 COASTAL MKWAKWANI!

Maafande wa Rhino Rangers kutoka Tabora


Na Baraka Mpenja, Dar es salaam


RASMI Maafande wa jeshi la wananchi Tanzania (JWTZ), Rhino Rangers kutoka mkoani Tabora wamejihakikishia kushuka daraja msimu huu wa ligi kuu soka Tanzania bara.

Hii inatokana na kupokea kipigo cha mabao 4-3 kutoka kwa maafande wa Tanzania Prisons kwenye uwanja wa Sokoine jijini Mbeya jioni hii.

Matokeo haya yanawafanya Rhino waendelee kuwa mkiani kwa pointi 16 tu baada ya kucheza mechi 25. Hata  kama watashinda mchezo wa mwisho haina maana kwao.

Mchezo wa leo  ulikuwa mgumu zaidi kwa Prisons kwasababu walikuwa wanasaka pointi tatu ili angalau kujinusuru kushuka daraja.

Kwa upande wa Rhino walishakata tamaa siku nyingi, lakini leo hii walikuwa wanajidhatiti angalau kushinda mechi mbili walizosaliwa nazo.

Baada ya kupoteza mechi hii, rasmi jahazi la Rhino limeshazama  na kinachofuata ni kujiandaa kukamilisha ratiba na kuungana na timu za daraja la kwanza ili maisha mengine yaendelee.

Katibu mkuu wa Tanzania Prisons, Insepekta Sadick Jumbe ameueleza mtandao huu kuwa mchezo wa leo ulikuwa mgumu kwao, lakini vijana waliingia kwa nguvu zote kuhakikisha wanaibuka na pointi tatu.

“Unajua huu ulikuwa mchezo wa kuwashusha rasmi Rhino, walipambana na kuufanya mchezo uwe na mvutoi”.

“Lakini wasingekwepa kipigo kwasababu hatukuwa na sababu ya kupoteza mechi ya tatu mfululizo wakati tunajua tuko katika wakati mgumu”. Alisema Jumbe.

Katibu huyo aliongeza kuwa baada ya mechi ya leo wanasubiri matokeo ya mechi ya kesho baina ya wekundu wa Msimbazi Simba na Ashanti United katika dimba la Taifa jijini Dar es salaam.

“Kama Ashanti United watafungwa mechi ya kesho, basi tukikutana Morogoro aprili 19 watalazimika kutufanga mabao 10 kama wanataka kubaki ligi kuu”.

 Imani yetu ni kubwa na tunawaambia mashabiki wetu kuwa wasiwe na wasiwasi”. Aliongeza Jumbe.

Kwa matokeo hayo, Prisons wamefikisha pointi 25 kwa kucheza mechi 25 na kupanda nafasi ya 10 , huku wakiwashusha Mgambo JKT waliokuwa nafasi hiyo kwa pointi 25.

Mgambo wanashuka mpaka nafasi ya 11 wakiwa na pointi 25 kama Prisons, lakini wastani wa mabao ya kufunga na kufungwa unawafanya maafande hawa wa Tanga kuwa chini ya Wajelajela.

Mechi nyingine imechezwa katika dimba CCM Mkwakwani jijini Tanga ambapo Coastal Union waliwakaribisha maafande wa JKT Ruvu.

Mechi hiyo imemalizika kwa JKT Ruvu ya kocha Fredy Felix Minziro kuibuka na ushindi wa bao 1-0.

Kwa matokeo hayo, JKT Ruvu wamefikisha pointi 31 na kupanda nafasi mbili kutoka ya 9 waliyokuwepo kabla ya mechi ya leo mpaka nafasi ya 7.

JKT Ruvu wamewashuka Mtibwa Sugar waliokuwa nafasi ya 7 mpaka ya 8 kwa pointi zao 30, huku Coastal Union wao wakiendelea kukalia nafasi ya 9 kwa pointi 29.

Mpaka hapo Minziro amefanikisha malengo yake kwasababu alipatiwa timu kwa matarajio ya kuinusuru isishuke daraja msimu huu.

Baada ya mechi hiyo, Kocha Minziro amefurahishwa na matokeo hayo huku akiwapongeza vijana wake kwa kupambana na kupata bao moja muhimu.

“Mechi ilikuwa ngumu, lakini nawashukuru sana wachezaji wangu kwa kujituma”.

“ Malengo yangu ilikuwa ni kuinusuru timu isishuke daraja. Nadhani sasa nimefanikiwa na nitajipanga kwa msimu ujao”. Alisema Minziro.

Kwa upande wa Coastal Union, afisa habari wa klabu hiyo, Hafidh Kido amesema kuwa timu yao imecheza vibaya na kupoteza mchezo, lakini ndio matokeo ya soka.

“Hakika vijana wametuangusha leo.Wamecheza chini ya kiwango”.

“ Yote kwa yote JKT Ruvu walikuwa  katika nafasi ya hatari na ndio maana walichezwa kwa nguvu na kutufunga. Tunajiandaa kwa mechi ya mwisho dhidi ya Kagera Sugar hapa Mkwakwani”. Alisema Kido.

No comments:

Post a Comment