Search This Blog

Thursday, March 27, 2014

MVUA YA 5-0 KUTOKA KWA YANGA TAIFA YAWAVURUGA PRISONS, AZAM FC MWENDO MDUNDO, YAIPIGA VIDUDE VIWILI MGAMBO TANGA!!

GHARIKA!. Mabingwa watetezi wa ligi kuu soka Tanzania bara, Dar Young Africans wameishushia mvua ya mabao 5-0 Tanzania Prisons ya David Mwamwaja katika mchezo wa ligi kuu soka Tanzania bara uliomalizika jioni ya leo kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Iliwachukua dakika 20 tu Yanga kuandika bao la kuongoza kupitia kwa mshambuliaji wake wa kimatifa kutoka nchini Uganda, Emmanuel Okwi  baada ya kupiga shuti la chini chini kufuatia mpira wa adhabu ndogo uliotengwa nje kidogo ya eneo la hatari.
Yanga waliendelea kuutawala mchezo huo, na mnamo dakika ya 33, kocha mkuu wa klabu hiyo, Mholanzi, Hans Van Der Pluijm alifanya mabadiliko kwa kumtoa nje  mshambuliaji wake Jery Tegete na nafasi yake kuchukuliwa na Hussein Javu.
Kuingia kwa Javu kuliipa makali zaidi safu ya ushambuliaji ya Yanga ambao kwa dakika nyingi walicheza mpira kwa kujiamini.
Hata hivyo nyota ya Prisons ilionekana kufifia dakika ya 35 baada ya kukosa penati pekee kupitia kwa nahodha wake Lugano Mwangama.
Dakika mbili baadaye, Winga machachari, Mrisho Khalfan Ngassa `Anko` aliiandikia bao la pili Yanga kufuatia kazi nzuri iliyofanywa na Hussein Javu.
Mabao hayo mawili yalidumu mpaka dakika 45 za kipindi cha kwanza zinamalizika.
Kipindi cha pili, Yanga waliokuwa na uchu kwenye mchezo wa leo, waliingia kwa nguvu, lengo kikiwa ni kutafuta mabao mengi dhidi ya Prisons waliokuwa dhaifu leo hii.
Dakika ya 68 Mganda Hamis Friday Kiiza `Diego wa Kampala` aliiandikia Yanga bao la tatu na kuwanyanyua mashabiki waliofurika uwanjani leo.
Nyota ya Yanga ilionekana kusafishika zaidi kwani mnamo dakika ya 78 walipata bao la nne kwa njia ya penati  ambapo ilifungwa na nahodha wake Nadir Haroub `Canavaro`, lakini alishindwa kupiga kwa ufundi kama ile ya Misri dhidi ya Al Ahly.
Karamu ya mabao kwa Yanga ilihitimishwa dakika ya 88 ambapo kwa mara ya pili, Hamis Kiiza aliukwamisha mpira kimiani.
Kwa ujumla mchezo wa leo umechezwa zaidi upande mmoja kwa maana ya Yanga kutawala mpira katika idara zote.
Kadri dakika zilivyozidi kwenda, Yanga walionekana kuwa bora zaidi, huku Prisons wakionekana kupoteza matumaini.
Safu ya ushambuliaji ya Yanga leo hii ilikuwa makini zaidi, hivyo kupata mabao matano muhimu.
Kufuatia ushindi huo, Yanga wanafikisha pointi 46 baada ya kushuka dimbani mara 21.
Hata hivyo wanaendelea kusalia katika nafasi ya pili kutokana na matokeo yaliyopatikana huko CCM Mkwakwani, Jijini Tanga ambapo Vinara Azam fc wameshinda mabao 2-0 dhidi ya wenyeji wao Mgambo JKT.
Kwa matokeo hayo, Azam fc wamekamilisha mchezo wa 22 kwa kujikusanyia pointi 50 kileleni.
Kizuri zaidi, mpaka sasa hawajafungwa mchezo wowote, hivyo kuendelea kuwa timu bora kwa msimu huu wa 2013/2014.

Mabao ya Azam fc katika mchezo wa leo yalifungwa na nahodha wao John Raphael Bocco `Adebayor` katika dakika ya 60 ya mchezo huo.
Bao la pili lilitiwa kambani na Mganda, Brian Umony na kuwapa ushindi huo muhimu wana Lambalamba katika harakati zao kuwania ubingwa.
Katika mchezo huo, Mgambo JKT walicheza vizuri, lakini kilichowaathiri ni ubora wa wapinzani wao.
Waliweza kumaliza dakika 45 bila kufungwa, ila kipindi cha pili waliruhusu nyavu zao kutikishwa mara mbili.
Mgambo wanazidi kujiweka katika mazingira magumu ya kusalia ligi kuu msimu huu.
Baada ya kuchapwa leo wamebakia nafasi yao ya 11 wakiwa wameshuka dimbani mara 22 na kujikusanyia pointi 19 kibindoni.
Wakati wakihenyeka kujaribu  kubakika ligi kuu, machi 30 mwaka huu watakuwa wenyeji wa  Yanga katika dimba la Mkwakwani jijini Tanga.
Hiyo itakuwa mechi ngumu zaidi kwao, kwasababu Yanga wanahitaji pointi kwa nguvu zote ili kuweza kutetea ubingwa wao.
Kupata ushindi, lazima waweke mipango mizuri ili kuhakikisha wanawazuia Yanga wenye kasi kubwa mechi hizi za mwisho.
Kwa upande wa Prisons, matokeo ya leo yamekuwa mabaya zaidi na wanabakia nafasi yao ya 10 kwa pointi 22 baada ya kushuka dimbani mara 22.
Machi 30 mwaka huu watakabiliana na mahasimu wao katika dimba la CCM Sokoine jijini Mbeya.
Hiyo itakuwa mechi nyingine ngumu zaidi kwa Prisons kwasababu Mbeya City wapo katika harakati za kusaka nafasi tatu za juu.
Azam fc baada ya mchezo wa leo, watakuwa na kibarua kizito mwishoni mwa wiki hii dhidi ya Simba sc uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.
Kwa namna moja unaweza kusema mchezo huo utaamua hatima ya Azam fc msimu huu katika mbio zake za kuwania ubingwa.
Kama watafanikiwa kuwafunga Simba  siku hiyo, basi wataendelea kuwasumbua Yanga  katika harakati zao za kutetea ubingwa wao.
Mechi ya Dar es salaam itakuwa na mvuto mkubwa kutokana na sababu kubwa mbili;
Mosi; Simba sc watakuwa wanapambana na aibu ya kufungwa tena baada ya kichapo kutoka kwa Coastal Union mwishoni mwa wiki iliyopita.
Bila shaka kocha mkuu, Dravko Logarusic anaandaa kikosi chake vizuri ili kuwapunguzia machungu mashabiki wa Simba waliokosa raha msimu huu.
Pili; Azam fc watapambana kwa nguvu zote ili kuvuna pointi tatu na kujiweka mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa.
Kwasababu kama watapoteza mechi hiyo na Yanga kupata matokeo ya ushindi Tanga  itakuwa hatari zaidi kwao.

No comments:

Post a Comment