Search This Blog

Tuesday, April 1, 2014

KOCHA OLJORO AFICHUA SIRI TIMU ZA MAJESHI KUBORONGA LIGI KUU, MAOFISA WA JUU WAKUMBATIA `MAGALASA`!!


WAKATI ligi kuu soka Tanzania bara inaelekea ukingoni, huku Azam fc wakipigiwa upatu wa kutwaa taji lao la kwanza tangu wapande msimu wa  2008/2009, timu za majeshi zimekumbwa na balaa la kufanya vibaya na kuwashangaza wengi.

Kati ya timu sita (6) za majeshi, maafande wa Ruvu Shooting  pekee ndio wapo katika mikono salama ya kubakia ligi kuu msimu huu wakifuatiwa kwa mbali na JKT Ruvu.

Ruvu Shooting  chini ya kocha Mkenya, Tom Alex Olaba, wapo nafasi ya 6 baada ya kushuka dimbani mara 23 na kujikusanyia pointi 32, wakati JKT Ruvu  ya kocha Fredy Minziro ndio timu ya jeshi inayofuatia kwa kufanya vizuri.

JKT Ruvu imecheza mechi 23 na kukusanya mzigo wa pointi 28 katika nafasi ya 9 ya msimamo wa ligi kuu.
Timu nyingine nne ambazo ni maafande wa jeshi la Magereza,  Tanzania Prisons, maafande wa Jeshi la kujenga Taifa wa Mgambo JKT, JKT Oljoro na wanajeshi wa Jeshi la wananchi, (JWTZ), Rhino Rangers zipo katika mstari mwekundu wa kushuka daraja.

Katika timu zote za jeshi, Rhino Rangers ndio imetia fora kufanya vibaya baada ya kushuka dimbani mara 23 na kujikusanyia pointi 13 mkiani.

Kwa ugumu wa mechi tatu zilizosalia kwa klabu ya Rhino,  ambapo mbili itakuwa nyumbani dhidi ya Mtibwa Sugar na Ruvu Shooting, huku moja akisafiri hadi jijini Mbeya kuumana na Tanzania Prisons, inaonesha wazi kuwa wameipa mkono wa `baibai` ligi kuu Tanzania bara.

Dhahiri kabisa,  wapenzi wa soka mkoani Tabora mwakani wataukosa uhondo wa mechi za ligi kuu baada ya kuonjeshwa msimu huu.

Timu nyingine ambayo ipo katika hatari zaidi ya kushuka daraja ni JKT Oljoro ambayo ipo nafasi ya 13 baada ya kushuka dimbani mara 23 na kujikusanyia pointi 15 tu.

Oljoro wamebakiza mechi tatu za nyumbani dhidi ya Prisons, Yanga na Mtibwa Sugar.

Mechi hizo zitakuwa ngumu zaidi kutokana na mazingira ya timu zote, hasa Yanga na Prisons.

Mtibwa hawana cha kupoteza msimu huu kwasababu hawawezi kutafuta nafasi tatu za juu wala kushuka daraja, hivyo mchezo hautakuwa na nguvu sana.

Lakini kimbembe ni mechi dhidi ya Yanga ambao ni washindani wa Azam fc katika mbio za ubingwa mwaka huu.

Mechi dhidi ya Prisons itakuwa ngumu kutokana na mazingira ya Wajelajela ambao watakuwa wakisaka pointi tatu ili kukwepa mkasi wa kushuka daraja.

Kwa upande wa Mgambo JKT angalau wamefufua matumaini ya kubakika ligi kuu baada ya kuwafunga Yanga mabao 2-1 wikiendi iliyopita katika dimba la CCM Mkwakwani, jijini Tanga.

Sasa Mgambo wapo nafasi ya 11 baada ya kushuka dimbani mara 23 na kujikusanyia pointi 22, huku juu yake wakiwemo Prisons wenye pointi 22 kwa kucheza mechi 23, lakini wana wastani mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa.

Kwa nafasi waliyopo Mgambo , kama watatumia vizuri wembe wake uliowanyoa Yanga SC,  katika mechi tatu walizobakiza dhidi ya Coastal Union, Kagera Sugar (zote Mkwakwani) na Mbeya City uwanja wa sokoine, wanaweza kubakia ligi kuu.
Haitakuwa rahisi kwa Mgambo kushinda Mbeya kwasababu Mbeya City wanawania nafasi mbili za juu.

Coastal Union na Mtibwa Sugar hawana uwezo wa kutwaa ubingwa wala kushuka nafasi, hivyo `Presha` ya mechi hizo mbili haitakuwa kubwa sana.

Kuna timu nyingi za majeshi katika michuano ya ligi kuu, lakini kupata mafanikio imekuwa ngumu kwao.

Katika mahojiano maalumu na mtandao huu , aliyekuwa kocha msaidizi wa JKT Oljoro na kutimuliwa  pamoja na bosi wake Mbwana Makata, Mwalimu Riziki Shawa amebainisha baadhi ya siri za timu za majeshi kufanya vibaya;

Riziki alisema aina ya wachezaji wanaotumiwa na timu za mejeshi,  wengi wao ni wabovu, huku upatikanaji wa wanandinga hao ikiwa mbovu zaidi.

“Wachezaji ambao ni raia,  siku zote wanacheza kwa kujituma. Lakini timu za majeshi zina sheria zake. Wachezaji wengi wanatoka jeshini bila kujali ubora wao. Pia wanajeshi wanapata mishahara kwa kazi yao, hivyo wanaridhika na kucheza mpira bila Malengo”.

“Hata kiutaalum, wachezaji wa jeshi wanatumia nguvu zaidi badala ya maarifa. Kuwafundisha ni kazi kubwa na wanapokutana na wachezaji wa kawaida waliojengwa katika mfumo wa soka, wanashindwa kabisa kucheza vizuri”. Alisema Riziki.

Kocha huyo alitaja sababu nyingine kuwa ni undugu;  ambapo baadhi ya wachezaji wanasajiliwa na wakubwa wa jeshi kwa kujuana bila kuangalia viwango vyao.

“Kuna wachezaji wanaonekana wachezaji,  lakini si wachezaji. Utakuta bosi wako analazimisha mchezaji fulani asajiliwe. Kocha unajua kabisa hana uwezo, inabidi ukubali ili kulinda kibarua chako”.

 “Mimi naweka bayana, kama wanataka kufanikiwa lazima waheshimu benchi la ufundi. Kumwingilia kocha katika kazi yake ni kuleta matatizo. Katibu mkuu anataka kuwa kocha, unaacha  kazi kubwa kama hiyo na kutaka kuwa kocha wakati hana taaluma”. Alifafanua Riziki.

Riziki aliendelea kumwaga siri za timu za jeshi na kusema sababu nyingine ni kukataliwa kwa mapendekezo ya makocha.

“Kocha unapendekeza wachezaji,  lakini wanakataa. Sisi makocha,  ligi inapoendelea tunaona wachezaji wa kuwasajili, unapopeleka majina,  wao wanakataa. Utakuta siku zinaenda na hujapata wachezaji. Unapoanza kambi wachezaji wanajituma, lakini unakuwa umechelewa”.

“Kuna wakati unaweza kuletewa wachezaji ishirini wa jeshi, katikati orodha hiyo unakuta wazuri ni kumi tu. Na wewe umepewa nafasi ya kutafuta wachezaji watano, sasa unawezaje kufanya mambo kwa wakati wakati wanakataa baadhi ya mapendekezo”. Aliongeza Riziki.

Pia alitaja sababu nyingine kuwa ni utovu wa nidhamu kwa  baadhi ya wachezaji wengi wa jeshi.

“Ukiwapa mapumziko ya miezi miwili, utakuta wanafanya mambo ya ajabu akiwemo ulevi na kujihusisha na mambo ya ngono. Wanapoteza nguvu nyingi na wakirudi wanakuwa wabovu kupita maelezo”. Alibainisha Riziki.

Akizungumzia kufukuzwa kwa makocha katika timu za majeshi, Riziki alisema  viongozi wengi wa juu jeshini hawajui mpira na wanadhani unachezwa tu bila kanuni na kujali wachezaji kimaslahi.

“Unapokuwa mwalimu unakuwa na msimamo wako. Sasa jeshini mambo mengi ni amri, unapopinga tu waliyoamua unakuwa huna chako”.

“Kuna makundi mawili ya wachezaji, wapo wanajeshi na raia. Ifikapo mwisho wa mwezi, wachezaji wa jeshi wanalipwa mishahara yao na raia wanayumbishwa. Sisi walimu tunajua umuhimu wa kumlipa posho na mshahara mchezaji. Lakini ukihoji unaonekana mbaya”.

“Utakuta mchezaji anapata mshahara tarehe 15 ya mwezi mwingine, ukizingatia ana familia nyumbani. Muda mwingi anakuwa na mawazo, lakini unapohoji unaonekana jeuri. Sasa kuna mpira gani hapo?”. Alihoji Riziki.

Pia kocha huyo aligusia suala la ripoti ya benchi la ufundi baada ya msimu kuisha ambapo alisema makocha wanaandaa ripoti yao na kueleza wazi kuwa wachezaji kadhaa wameshuka kiwango, lakini kwakuwa viongozi wa juu ndio waliofanya mpango wa kuwasajili kwa undugu, wanalazimika kuwalinda.

“Unawapa ripoti wanaikalia. Wanaanza kuwaza kutafuta mwalimu mwingine kwasababu wakikubali mapendekezo yenu, wachezaji wao wataondolewa”

 Kocha huyo alimalizia kwa kuwaasa viongozi wa jeshi, maofisi wa jeshi kuwaacha makocha wafanye kazi yao kama wanataka kufanikiwa.

 Lakini kama wataendelea kwa mfumo huo na kukumbatia madhaifu haya, watabakia kuwa wa kupanda na kushuka daraja.

No comments:

Post a Comment