Search This Blog

Monday, January 13, 2014

SIKU 13 ZA MAPINDUZI CUP ZILIVYOIFUFUA SIMBA


 
na baraka mbolembole
Umeiona Simba SC ya sasa?, Ina nini kipya?, Nini kibaya? Nani aliongeza ubora wao wa sasa ?.
 Majibu utakuwa nayo wewe mwenyewe kama utakuwa umeitazama kiufundi timu hiyo katika michezo yake ya kombe la mapinduzi. Upande wangu naipongeza kamati ya michuano hiyo kwa kuendelea kuiboresha michuano kwa kualika timu zenye sifa sawa na zile za nyumbani kutoka nchi za jirani. Ni ngumu kuzipata timu kama AFC Leopard, URA, KCC, Tusker, Simba, Azam wakati kama huu timu hizo huwa na mambo mengi ya kufikiria, maandalizi ya ligi na huku nyingi zikiwa na mahesabu ya kuwapumzisha nyota wake muhimu waliokuwa katika timu za mataifa ya ukanda wa cecafa. Ila, tumeona kamati hiyo ikifanya jitihada na kluhakikisha si tu majina ya timu hizo yatakyuwepo bali vikosi halisi vya timu hizo bora za nchi za Kenya, Uganda na Tanzania, huku mabingwa wa Zanzibar KMKM, na washindi wa pili Chuoni wakiwa wamepata maandalizi mazuri na kujua wataanza vipi michuano ya kimataifa baadae mwezi ujao.

      SIMBA SI GOIGOI TENA?

Kabla ya mchezo wa fainali siku ya jumatatu, Simba ilikuwa imecheza
michezo mitano pasipo kuruhusu nyavu zao kuguswa. Ni kitu kizuri
ambacho si tu kimepunguza matatizo ya ngome yao, bali uimara wa safu
nzima ya ulinzi umepelekea timu hiyo kuwa imara kila idara, ukitoa
safu ya mashambulizi ambayo hakuna mshambuliaji aliyefunga bao, katika
eneo la kiungo timu hiyo imekuwa na kasi nzuri, mipango, utulivu na
umakini ambao umefanya mabao saba yote kufungwa na viungo. Uwepo wa Suleimani Matola, unaweza kuwa umeongeza ufundi, mbinu, na ufanisi kwa wachezaji wa idara hiyo kwa kuwa kocha huyo msaidizi ni mtu mwenye ufahamu mkubwa kuhusu nafasi hiyo. 

Wachezaji wameonekana kuamka upya na kuwa na hali, huku wale ambao
wanaokena kutokuwa fiti kimwili na kimchezo wakisugua benchi na
kuwapisha wenye usongo. Amri Kiemba alikuwa na kiwango kibovu katika
mzunguko wa kwa nza wa ligi kuu, hali hiyo ilipelekea timu kupungua makali kwa kuwa alikuwa ni mchezaji wa kutegemewa sana na aliyekuwa kama muhimili mpya wa timu baada ya kuamua kuingia katika mabadiliko baada ya kumalizika kwa msimu uliiopita,  Kiemba pia  alikosa nafasi wakati timu yake ilipoifunga Yanga katika mchezo wa hisani wiki tatu zilizopita.

 Amepandisha tena kiwango chake, akiwa amefunga mabao matatu katika michuano hiyo, kiwango cha juu cha Kiemba kimeweza kuhimarisha zaidi timu hiyo. Tatizo lake ni dogo tu nalo kutokuwa na kasi, ila ni mchezaji anayepitisha mipira ya hatari kwa wapinzani wake. Anajua njia ya kupitisha mipira. Simba si tu kuwa inanufaika na kiwango chake bali hata mashabiki wamekuwa wakiridhishwa na anachofanya kwa sasa. Ni mchezaji mzoefu
anayetegemewa kuwa muhimili wa timu, hatakiwi kujisahau tena. Kiemba
ni mfano mzuri kwa wachezaji wengine wazoefu kama Uhuru Suleiman,
Henry Joseph, Abdulhalim Humud, Nassoro Chollo, Haruna Shamte, Ramadhani Chombo, kuwa viwango vyao vizuri ndiyo vinaweza kuifanya Simba kuwa na makali zaidi.

 Wanatakiwa nao kujibidiisha zaidi na kufanya mazoezi ya kutosha ili kwenda sambamba na wachezaji vijana walio katika viwango vya juu. Kwa sasa Simba imekluwa ikinufaika na viwango vya makinda kama Ramadhani Singano, Jonas MKude, Haruna Chanongo, William Lucian, Issa Rashid, Edward Christopher, Said Ndemla hyuku wakisubiri kuwa fiti kwa vijana kama Ibrahim Twaha na Abdallah Seseme, bila shaka kuwa kikosi kilichoshindwa kuunganishwa ndani na nje ya uwanja na makocha, Abdallah Kibadeni na Jamhuri Kiwelo kinaweza kuvuka ratiba ya michezo migumu, mwezi februari watakapokwenda, Morogoro, Tanga, na Mbeya kucheza na timu za Mtibwa Sugar, JKT Oljoro, na Mbeya City. Timu inatakiwa kuimarishwa zaidi na viwango vya wachezaji wazoefu na kundi la kina Joseph linatosha kurejesha imani ya mashabiki kuwa Simba inaweza kuondoka katika nafasi waliyomaliza msimu uliopita, Nafasi ya tatu.

    SAFU YA ULINZI

Timu imara huanza kujengwa nyuma, golikipa mzuri ni yule ambaye
anaweza kujipanga na kujiongeza mwenyewe, kuwapanga vizuri walinzi
wake, kuokoa mipira isiingie golini, kucheza mipira ya krosi, kona, na faulo. Tatizo kubwa lililoiporomosha Simba katika duru la kwanza lilianzia golini. Abel Dhaira alishindwa kujiongoza na akajikuta akijipanga vibaya. Uwepo wa Ivo Mapunda na Yaw Berko umesaidia umakini katika ngome ya Simba, sisemi hivi kwa kuwa hawajaruhusu mabao katika siku za karibuni, bali ni kutokana na viwango vyao wanavyovionyesha kwa sasa. Ni wazoefu na ni makipa wanaojipanga vizuri, wataruhusu mabao ila si kwa namna ilivyokuwa  wakati wa Dhaira, ambaye alionesha udhaifu hata katika kyucheza mipira ya krosi na kona japo alikuwa na umbo la kutosha. 

Walinzi wa pembeni, Shamte na Lucian ambao wametumika katika michuano ya mapinduzi upande wa kulia, Issa Rashid katika upande wa kushoto wamejitahidi kupunguza mianya ya kuruhusu upigwaji wa krosi katika lango lao, ila bado wanasumbuliwa na kukosa umakini kwa muda wote. WAmejitahidi kusonga mbele, japo si kwa kiwango cha kuridhisha. Wanatakiwa kucheza kama ilivyokuwa wakati wa Said Sued na Nurdin Bakari, na si wanavyocheza sasa.


        KAZI YA MAKOCHA, LOGA NA SELE

Ili kupata hamasa kutoka kwa wachezaji kocha yoyote anahitajika kuwa
na hamasa hiyo yeye mwenyewe. Kuwa na matarajio ya kufanikisha mipango mikubwa, kama kocha husaidia kwani hali hiyo huwaingia wachezaji pia. Baada ya kufanikiwa kuiongoza Simba bila kushindwa hadi sasa, kocha Zdravko Logarusic ameonesha kuwa na njaa ya mafanikio na hali hiyo ipo pia kwa msaidizi wake, Matola na kwa wachezaji wake pia. Mechi dhidi ya Yanga, Leopards, KCC, KMKM, Chuoni si kipimo kwa ajili ya mafanikio ya siku za baadae. Ila tayari Simba imeonekana kuwa na utulivu zaidi, mipango zaidi na kuwa na makocha ambao wanahitaji kufanikiwa kila mara. Kuwa bora kunaletwa na matokeo bora, endapo Simba itashindwa kupata ushindi hakuna atayeona ubora wa makocha wao. Ndiyo maana Kibadeni na Julio waliondolewa. Itategemea na upande utakaoangukia, ila kwangu hadi sasa naitazama Simba kwa jicho la timu inayoweza kutwaa ubingwa msimu huu. 

Wachezaji wanatakiwa kufanya kazi kwa bidii yeye mwenyewe na
kuzingatia mazoezi wanayofundishwa ili kuinua na kuhimarisha viwango
vyao. Kitendo cha Logarusic na Matola kubadili mwelekeo wa Simba,
hakishangazi sana kwa kuwa wameonekana kusimamia wanachotaka.  Makocha hao wanajaribu kuiinua tena Simba kutoka timu goigoi hadi kushinda mfululizo katika muda wa wiki tatu, kutokana na umakini wao katika kila jambo. Hawana wachezaji wazuri sana, lakini wamejitahidi kufanya kila mchezaji kujua jukumu lake kwa uhakika.  Muda, ni jambo muhimu. Utaongea hapo baadae, hakika siku 13 za mapinduzi cup zimeirudisha upya Simba, ngoja tuisubiri katika ligi.

No comments:

Post a Comment