Search This Blog

Wednesday, January 15, 2014

OMBI LANGU LA “KIJINGA” KWA RAIS WA TFF.



Kheri ya mwaka mpya ndugu watanzania mahali popote mlipo.  Ujinga ni sehemu ya maisha na kila mwanadamu yawezekana ana mambo yake ya kijinga. Mimi natumia muda huu kuja na ombi langu la kijinga kwa raisi mpya wa TFF. Ehe, ngoja nisisahau, Natumia nafasi hii kuwapongeza wote mliopata nafasi ya kuingia katika chombo hiki cha kuendesha mpira wa miguu Tanzania (TFF), pongezi zangu zaidi zinakuja kwako Ndugu Jamal Malinzi “Tata Okaiyuka, Omukama Akwebembele”. Kabla sijaanza na kuwasilisha ombi hili naomba niongelee neno moja linaloitwa maadili, hii ni kwa sababu ombi langu la kijinga kwa siku ya leo linahusu neno “MAADILI”. Hivyo kabla ya ombi langu hili la KIJINGA kwa raisi Malinzi ni vyema nikaanza kutoa ufafanusu juu ya neno MAADILI. Kwakuwa tumefundishwa na kukaririshwa mambo mengi ya kimasomo kwa lugha ya kigeni bila sababu yoyote ile ya msingi nami naomba niendeleze kueleza hili neno “MAADILI” kwa lugha ya kigeni ya kingereza. Kwa lugha hii ya mapokeo, hili neno linaitwa “ethics”. Hivyo naanza kwa kulifafanua hili neno kama ifuatavyo:-
The word ethics is derived from the Greek word “ethos”, which means "character," and from the Latin word “mores”, which means "customs”. It has been defined as the rules of behavior pertaining to a particular class of human action. They relate to moral principles that control, influence or guide a person’s conduct or behavior so as to gain respect for him/herself.  (See Dr. Gerald Ndika, (2006): Judicial Ethics in Tanzania: A Paper presented at a Primary Courts’ Magistrates’ Seminar, IJA, Lushoto)
                                                                                                                 (Msisitizo ni wa kwangu).
As Socrates noted about ethics, "It is not just about any question, but about the way one should live, thus, ethics do not only benefit the client but also benefit of those belonging to the profession (See Plato, The Republic (A. Bloom, transl.), 1968, 352D ).
                                                                                                                 (Msisitizo ni wa Kwangu).
Ikumbukwe pia kuwa neno maadili (ethics) lina maana pana, haliishii tu kwenye kufuata matendo mema ya mwenyezi mungu au amri zake mwenyezi mungu, maadili kwa maana yake pana ni zaidi ya apo, maadili hujumuisha vitu vingi sana katika maisha. Hii imeelezwa vizuri na mwandishi Peter MacFarlane na namnukuu kama ifuatavyo:-
“….we should not use the term 'ethics' to mean only compliance with the Ten Commandments or other standards of common, basic morality…” (See Peter MacFarlane, The Importance of Ethics and the Application of Ethical Principles to the Legal Profession, Journal of South Pacific Law, Volume 13 issue 1, 2009).

Na pia ni vizuri kutambua kuwa sio lazima maadili ambayo mwanadamu anapaswa kuyafata lazima yawe yameandikwa mahala flani (ethics are not necessary to be codified). Kwa mfano kuna jamaa yangu alikuwa analalamika kuwa kuna Padre mmoja waga ananyoa fasheni/fashion, yaani ananyoa nywele kwa mitindo ya kisasa na pia anachonga “O”kwenye ndevu zake, akawa anasema huyu father/padre hana maadili kabisa, nami nilikubaliana naye kuwa kama kweli huyo padre ananyoa hivyo basi hana maadili ingawa hatujui kama kwenye taratibu zake za kitume amekatazwa kunyoa KIDUKU kama MOSE IYOBO,(WCB) na kuchonga ndevu kama NYOSI ELSAADAT wa F.M Academia. Sina uhakika na hilo.  Nikamdadisi kimakusudi huyu jamaa yangu muumini mzuri wa kanisa kwa kumuuliza kwanini sasa unalalamika kwani kunyoa hivyo ni kosa? Akanijibu, aha!, sasa mimi mtu aliyenyoa hivyo siwezi kuungama kwake(Wakatoliki mnaijua hii), kwanza namuona msela mwenzangu na heshima inapotea. Hapa nilipata somo, na kuelewa ambacho Mheshimiwa Ndika kama nilivyo mnukuu hapo juu kuwa maadili/ethics influence respect.(heshima).

Tanzania imekuwa ni nchi amabayo maadili yanaporomoka kwa kasi ya ajabu sana, watu wanaweza kutembea makalio yako nje, hawa ni jinsia zote, Rushwa ipo idara zote(waulize vijana wa wacheza mpira mkoa wa Dar-es-Salaam wanavyoombwaga rushwa hili wachaguliwe katika timu za mikoa yao), waulize vijana wanaofanya applications za kazi, n.k. Nchi hii imejaa majanga na wananchi wengi washavurugwa kiasi cha kutosha.(Asante Snura Mushi kwa maneneo mazuri ya Kiswahili). Watanzania wenzangu yote mnayajua, hapa tatizo kubwa ni kukosa maadili.
Tuachane na porojo hizi, maana mimi tatizo langu mpaka nalalamikia rushwa ni kutaka kupata kila kitu kwa “ubwete”(Asante kwa neno hili Dr MacRegan Kipara-Alex Chalamila wa O.K) kumbe lazima utoe kitu. Turudi kwenye mada hii ya kuhusu neno maadili, hapo juu mheshimimiwa Gerald Ndika pamoja na mambo mengine anasema kuwa maadili husaidia mtu kupata heshima(tafsiri isiyo rasimi). Mwanafalsafa (sio mwana FA mwanamuziki aliyeimba Bila Kukunja Goti), akha! namuongelea Plato(Aristocles), mwanafalsafa wa Kigiriki ambaye aliwahi kusema kama nilivyomnukuu hapo juu kwamba kuwa na maadili si kwa faida ya mteja bali hata kwa mhusika katika fani husika. Yaani kama ni mcheza mpira si kwa faida ya timu yako bali ni kwa faida yako pia. Kwamfano kama ukienda kucheza ndondo YOMBO(katika fainali ya mwenyekiti wa mtaa) na ukaumizwa hasara si kwa YANGA tu, bali pia kwako kwani nafasi yako ya kucheza uwanjani inaweza kuchukuliwa na mchezaji uliyekuwa unamuweka benchi na ukipona husiweze kuichukua tena, na kama ni ndoto ya kwenda nje basi inaweza kuishia hapo. Hila ukijitunza vizuri faida si kwa klabu yako tu bali kwako pia, yawezekana nawe MOSE KATUMBI akakupeleka TP MAZEMBE, ni kweli klabu yako itapata hela ya mauzo(Ingawa najua hela ya mauzo ya wachezaji wetu waga hatujui inaendaga kwenye benki account ya nani, wanachama na mashabiki wa Simba ni mashaidi kwa hili) nawe pia kama mchezaji mshahara mzuri itakuwa haki yako.
Kukosa maadili ni pamoja na kuchukua hela ya mauzo ya mchezaji bila klabu yake kujua, kucheza kwa dharau huku ukituliza mpira kwa makalio ukimungoja beki umpige tobo, pia ni pamoja na kukataa kukaa na wenzako baada ya kufanyiwa mabadiliko na ukaondoka moja kwa moja, ni mengi tu tena kama nilivyotangulia kusema hapo juu si yote yataandikwa katika document moja, mengine hayaandikwi.
Tanzania imekuwa kichwa cha mwendawazimu katika nyanja mbalimbali za kimichezo, iwe riadha, kikapu, mpira wa miguu, n.k, tatizo kubwa kama nilivyotangulia kusema ni kukosa maadili. Aliyeshinda mkanda wa kimataifa wa ngumi(ingawa watanzania kama kawaida yao walisema ni mkanda feki) nasikia kidogo ndoa yake ivunjike baada ya kuanza ulevi, akashindwa kujiandaa kwa ajili ya mapambano mengine, na kuna kipindi akaenda nje ya nchi kupigana bila hata kocha wake kujua yote hii ni kukosa maadili.  Kuna mifano mingi tu katika hili, kila mtu mwenye akili timamu anayajua na ana yake moyoni.
Tukija katika mpira wa miguu hapo ndo usiseme, makocha na wachezaji wengi hawafati maadili ya mchezo huu pendwa hapa nchini.  Ndugu Jamal Malinzi ulitoa ahadi nyingi zenye malengo ya kuinua mpira wa Tanzania na wapiga kura (wajumbe) kwa niaba ya watanzania wakaridhia kukupa wewe kiti cha urais wa TFF. Tayari umeanza kazi ukiwa na timu mpya kabisa baada ya kuzivunja kamati zote alizoacha Ndugu Leodgar Tenga, naamini ni kwa nia nzuri tu(ingawa kuna malalamiko ju ya hilo). Baada ya kuzivunja kamati, ndugu Malinzi  uliunda timu ya jopo la makocha wa mpira wa miguu kujadili nini kifanyike kuitoa Tanzania hapa lipo kwenda hatua nyingine mbele kwa maendeleo ya mpira. Hivi katika ripoti yao pamoja na mambo mengine waliweza kuandika kuwa kukosa maadili ni chanzo cha sisi Tanzania kushindwa kusonga mbele katika mchezo wa soka? Basi kama halikusemwa kwenye ripoti basi nami ngoja nichangie kuwa chukua yote walioleza katika ripoti hila na hili la maadili nakuomba uliweke, we ukiulizwa limetoka wapi sema ni mtanzania mmoja tu mwenye kuupenda huu mchezo. Si ulisema kila mtanzania anao wajibu katika kuliinua soka letu? Nami ndo mchango wangu ingawa najua ni ngumu kusoma hili andiko.
Ndugu Malinzi kama ujuavyo kila kitu hili kufanikiwa lazima ushiriakiano wa dhati kutoka kwa wadau/stakeholders uwe juu, waweza kuwa na mipango mizuri lakini ukakosa ushirikiano, ni mbaya zaidi unapokosa ushirikiano kutoka kwa watu ambao mipango inayo pangwa ni kwa ajili yao, yaani kukosa support kutoka kwa targeted group. Yaani pale walengwa wakiyaacha maadili ya kazi yao. Hapa ni kama baba unalipa gharama kubwa ya ada kwa ajili ya mwanao, unampeleka shule nzuri yenye kila kitu lakini yeye hataki kusoma, lazima kama mzazi malengo yako na ndoto zako kumuona mwanao akiwa msomi mzuri zitashindwa kutimia.
OMBI LA KIJINGA.
Ndugu Malinzi wakati Rais aliyekutangulia anaingia madarakani aliletwa kocha wa kigeni, wote unawajua na mpaka sasa bado  timu ya taifa ipo chini ya kocha wa kigeni, saivi tunaye Kim Poulsen na baadhi ya wanachama wako, yaani vilabu, wanao makocha wa kigeni( Simba, Yanga, Azam,na nyinginezo ni mfano katika hili).  Rais wa sasa wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania amegharimikia kocha wa Timu ya Taifa, wafadhili na wamiliki wa vilabu nao wamefanya vivyo hivyo kwa timu zao.
Sasa makocha wa kigeni wenye ngozi nyeupe na nyeusi tumewazoea hapa Tanzania, saivi twaweza kujua ufanisi wao na ukanjanja wao,  Pia Tanzania sasa tunao makocha wazawa wenye vyeti vizuri (wengine wamepata Leseni B ya CAF hivi majuzi). Hivyo suala la makocha walau twaweza sema uko akuna shida sana.
Ndugu Malinzi sasa mimi nakuja rasimi baada ya porojo nyingi na ombi langu la “KIJINGA”, ni hivi,  kama Raisi Jakaya Mrisho Kikwete alileta kocha wa kigeni kwa lengo la kuinua mpira wetu basi nakuomba nawe saivi jiandae kumuomba raisi ajaye atuletee kwa gharama ya serikali mchezaji walau mmoja wa kigeni aje kufundisha wachezaji wetu kuishi kama wana taaluma wa mpira/ yaani kuishi kiprofessional. Hivi serikali haiwezi kumlipa hata Thiery Henry akaja akafanya kazi hii? Si inaonekana hivi karibuni ataacha kucheza mpira huko aliko Marekani? Serikali yetu haishindwi, wewe waconvice tu watakuelewa.  Au wamlete anayecheza saivi ulaya kwa mfano Chiek Tiote, tena huyu mwafrika mwenzetu aje afanye hi kazi. Inawezekana kweli? Hapana, Hili ombi limekaa kijinga sana maana hakuna mchezaji wa kulipwa toka ulaya ataacha mihela aje kufundisha maadili Tanzania. Haitawezekana, labda tumtafute aliyestaafu kucheza mpira aje kufundisha haya, tuwaombe Airtel wamlete Fortune si kastaafu kambumbu Yule aje akae mwaka. Achana na hiyo, nimekumbuka, Stewart Hall( Kocha wa Zamani wa AZAM AFC) kapewa Academy nina imani kati ya mambo atakayo fundisha ni kuishi kiprofessional kwa kufuata maadili na miiko ya kiuchezaji. Asante Mungu, nina imani wachezaji wataokulia kwenye hii academy watakuwa maprofessional wa ukweli. Ila mpaka tuje tuvune uko ni muda mrefu sana, ila atasidia.
Swali ni kwa hawa ambao saivi bado wanacheza, na bado wana miaka mingi mbele kucheza mpira na lengo lako Ndugu Jamal Malinzi ni kuona Tanzania ikishiriki mashindano ya kimataifa kwa mafanikio. Sasa naona bado ombi langu la KIJINGA niendelee nalo, ni hivi naomba aletwe mtu ambaye atawanusuru hawa wachezaji wetu hili nao angalau waishi kiprofessional. Maisha ya wachezaji wetu na mienendo yao inatia shaka kama lengo lako ndugu rais wa TFF litatimia. Haiwezekani kufikia malengo yako mkuu wa TFF kama leo hii mchezaji wa ligi kuu anaishi kama mpiga debe wa stand kisa eti hasionekane anajidai, mchezaji anakaa kijiweni na masela wakipuliza naye anapuliza hapo hapo, mchezaji anacheza ndondo bila kujali afya yake, ni mengi bwana hata nawe unayajua.
Kwa mfano ulio hai, mchezaji unacheza AZAM F.C (Timu yenye kila kitu katika soka la bongo) na wewe pia ni kiungo wa kutumainiwa wa Taifa Stars na Kilimanjaro Stars na majuzi kati umepewa tuzo ya mchezaji bora wa mechi kati ya Kilimanjaro Stars na Zambia kwenye mashindano ya chalenji leo hii unaonekana kwenye ligi ya diwani tena una siku moja umetoka mapinduzi cup Zanzibar.
Hujui tu ulivyoniumiza, Naikumbuka sana hela yangu niliyoitumia kununua kifurushi (MB) niangalie kwenye internet highlights za mechi zenu mkiwa Zanzibar, nilitaka nikuangalie ulivyokuwa unatembea katikati ya uwanja. Ilikuwa lazima niingie gharama kukuona wewe supa star, kukuona pasi zako murua, kukuona unavyosababisha goli alilofunga Himid Mao.
Yaani wewe niliamini hili mtu aenjoy mambo yako ya uwanjani lazima aingie gharama/alipie aende Taifa, Chamazi, au afuatane na Azam ikiwa inaenda mikoani au aifuate Timu ya Taifa au alipie kwa wenye vibanda vya mpira akuone na aje asimulie wale waliokosa mia tano ya kulipia, aweke na uongo mwingi huku akitukuza kipaji chako.  Wewe ni si mtu wa mchezo bwana, kama Waingereza wanamtukuza Lampard wakati hakufikii kipaji cha kuuchezea mpira kwanini nasis tusikutukuze?
Nilitamani nikutane nawe kwa bahati kwenye moja wapo ya SHOPPING MALL yoyote hapa Dar ukifanya shopping nikuombe tupige wote picha na unisainie mahali popote ningeona panafaa kwa muda huo, nikirudi mtaani nianze kutangaza kuwa leo nimekuona na ukakubali kuoiga name picha, au umetia sahihi kwenye shati langu jeupe. Mbona wangenikoma jamani, duh, kumbe niliingia cha kike, sivyo ulivyo nilikuwa naota ndoto ya KIJINGA.
Niliumia sana na kukereka nilipokuona mtaani kwetu tena si kwa bahati mbaya, yaani ukiwa umedhamiria kuja kucheza ndondo. Nilikusogelea ghafla ile hamu ya kukuona ikaisha maana sikutegemea kukuona maeneo yale, na thamani yako kwangu kama shabiki wako ikaisha pale, mbaya zaidi pale watu/mashabiki walivyokuwa wanakutukana matusi. Najua kutukanwa na mashabiki kwa mchezaji ni jambo la kawaida, lakini linakuwa la ajabu pale mchezaji wa kariba yako unapotukanwa na mashabiki wa mbagala kuu wakati ulipaswa kutukanwa na mashabiki wa timu za ligi kuu. Tena kwa uwezo wako uwanjani wewe unapaswa kuzomewa na mashabiki wa Ajax cape town, TP Mazembe, na nyinginezo toka nchi kama Dernmark, Ufaransa, Sweeden, n.k, maana ungekuwa umefanya hesabu hii ndogo (miiko + maadili=Kujitambua), wewe ungekuwa unacheza ligi za huko. Baada ya dakika tisini kwenye ule uwanja wa mchanga wenye vipimo vya kubuni ile thamani niliyokuwa nakupa iliisha ghafla, na siko peke yangu wapo wengine wengi. Wewe si mtu wa kuonekana sehemu zile ukicheza mpira wa ushindani, hapana kijana mwenzangu, hapana.
Inasikitisha sana wachezaji wetu wapendwa hamjitambui, hivi mnajua hao mnaotaka kuwaridhisha (masela wa kitaa) waga wanawacheka pale mnaposhindwa kujieleza mbele ya vyombo vya habari, wanasema ati hamjui kingereza. Sasa hutajuaje jinsi ya kuongea na vyombo vya habari wakati muda wote wewe ni ndondo tu, vijiweni na glossary za kitaa.  Mkihojiwa na waandishi wa kitanzana mnasema mna ndoto ya kucheza ulaya, kweli?  Hapana, nayo ni ndoto ya KIJINGA. Hiyo ndoto inaanza kutimilika kuanzia kwako, kwanza jiweke kiprofessional then mengine yatafuata. Leo hii watanzania tunamuona DIAMOND PLATNUMZ anavyong’ara kimuziki, na akikwambia anataka siku awe kama P-Square au Usher kwanini usikubali na kumuombea kwa Mungu afike huko, yeye kajiweka kiprofessional, wadada wakimuona wanadata, wanaomba awasainie mpaka kwenye mashati yao ya shule, hawajali. Huyu ni mtu anayejitambua anafanya nini (achana na isues zingine za upande wa pili mnazojua juu yake, hata Ashley Cole, Ronaldinho, na Rolnaldo wote kwenye hiyo sector hawajambo). Mimi nikisikia katoa video ya wimbo nakimbilia YOU TUBE kuona kafanya nini PLATNUMZ.  Kamuulize PLATNUMZ kajifunzia wapi kuongea na vyombo vya habari? Nani kamfundisha English? Tulimuona wakati amekaribishwa BBA alichokifanya, tuliduwaa, MAGAZETI pendwa yakaandika sijui kafundishwa na naniii!!! Sawa, ata kama alijifunzia Mchikichini si tayari anajua? Amejiandaa kuwa wa kimataifa si siri.
Kuna vijana huku mtaani wakisikia Taifa stars au Kilimanjaro stars inacheza na wakajua yupo Samatta lazima wakalipie kwenye banda la mpira kumuona Samatta.  Wao wanasema wanatamani wawe kama yeye, unajua kwanini? Mi naamini si kipaji chake ila anavyojiweka nje na ndani ya uwanja.
Ndugu Malinzi naomba ulifanyie kazi ombi langu la “KIJINGA”, Raisi ajaye( sijui wa Tanganyika, ama Zanzibar, ama wa Muungano, maana hii rasimu ya katiba nasikia walioisoma wanasema tutakuwa na marais watatu, wewe chagua kati ya hao) atuletee mtu ambaye kazi yake itakuwa ni kuwafundisha wachezaji wetu wenye vipaji vilivyotukuka jinsi ya kuishi kama maprofessional. Hiyo ndo iwe kazi yake tu hapa Tanzania, na ikibidi kila klabu iajiri mtu wa aina hiyo aweze kuwafunda wachezaji wetu wapendwa jinsi ya kuishi angalau kama Tresor Mputu kama kuishi kama Christiano Ronaldo ni ngumu.
Ndugu Jamali Malinzi ombi langu la KIJINGA ndio hilo, Please! nakuomba katika mambo yako nalo hili uliweke. Enyi wachezaji wetu namaliza kwa kusema kuwa ombi langu la kijinga lilikuwa kwa ajili ya Raisi wa TFF sio ninyi, kwenu sio ombi ni lazima muishi kama wachezaji wa mpira sio wa bao kama mnataka kwenda huko ulaya mnakokutaja kila mara, na ngoja niliweke kwenye lugha hii ya kidhungu (maana kabila linaruhusu), Hey Tz Footballers, ethical responsibility and duty are an inherent part of your profession as a footballer.
ASANTENI SANA,
 ELPHACE RWESHABURA


                                                                  


  

.

3 comments:

  1. Ahsante sana mtoaji wa makala hii, nikweli kabisa wchezaji wetu hawajitambui imefika wakati wanatakiwa wawe ni wenye kujitambua, lkn mwandishi jarib kuwa na ufupishe wa maneno watu wakuelewe vzr umekusudia kuwafahamisha maadili lkn longolongo nyingi sana mpaka kufika ktk fundisho hilo la maadili,yani huyo mlengwa atasoma makala hii lkn mpaka akifika katikati ya kusoma kashasahau mwanzo jinsi longolongo zilivyokuwa nyingi,

    ReplyDelete
    Replies
    1. Watanzania tunapenda sana njia za makato...Barrack Obama licha ya majukumu yake anapata muda wa kusoma kitabu cha kurasa 500.Leo hii tunalalamika mwandishi kuandika kurasa tatu.
      Kumbe tusiwalaume wachezaji wanaolalamika mzaoezi ya kocha fulani wa kigeni kuwa ni magumu, ni zao la jamii yetu ambayo inapenda kila kiwe 'vodafasta'.

      Makala nzuri sana. Lovely efforts from the author.

      Delete
  2. Barak obama ni mtume mpaka umtolee ushahidi

    ReplyDelete