Search This Blog

Thursday, August 29, 2013

MAKALA: YANGA DHIDI YA COASTAL ILIKUWA MECHI NZURI ILIYOHARIBIWA NA MWAMUZI

Na Baraka Mbolembole  
 
Kiki ya mkwaju wa penati kutoka kwa kiungo na nahodha wa timu ya Coastal Union, Mkenya, Jerry Santo katika dakika ya mwisho ya muda wa ziada, ilifanya timu hiyo kupata sare ya bao 1-1 dhidi ya Yanga. Didier Kavumbagu aliifungia Yanga bao la kuongoza katika dakika ya 69 akimalizia vizuri mpira uliokuwa umepigwa na mlinzi wa kushoto, David Luhende.


Katika pambano gumu na la kukamiana, mwamuzi, Martin Saanya alitoa kadi sita za njano kwa wachezaji, Juma Nyosso, na Haruna Moshi ' Boban' kwa mchezo mbaya wa rafu, na Suleiman Kassim ' Selembe' kwa kosa la kujiangusha kwa upande wa timu ya Coastal, huku, Salum Telela, na Saimon Msuva kwa upande wa Yanga, pia mwamuzi huyo alitoa kadi nyekundu za moja kwa moja kwa wachezaji, Msuva na Crispine Odula wa Coastal kwa kukosa uungwana mchezoni.


Mchezo ulianza taratibu, na kuzidi kuonekana mgumu kadri dakika zilivyokuwa zinasonga mbele, na katika dakika ya kwanza tu, Coastal walikuwa wamefika katika eneo la Yanga, lakini, kiungo mshambuliaji, Daniel Lyanga akawa katika eneo la kuotea.
 

ILIKUWA NI MECHI YA UFUNDI?.

 Kocha wa Coastal, Hemed Morocco aliwapanga, Santo, Boban, na Odula katika safu ya kiungo , wakati yule wa Yanga, aliamua kuwapanga, Telela, Frank Domayo, Msuva na Haruna Niyonzima, katika mfumo wa 4-4-

Achana na uchezeshaji ‘mbovu’ wa mwamuzi, Saanya na wasaidizi wake , Jesse Erasmo, na Charles Chambea, ambao walionekana kuzidiwa na presha ya mchezo na kujikuta wakifanya maamuzi yaliyowakera wengi. Katikati ya uwanja mpira ulipigwa, viungo wakacheze kwa kadri ya walivyoweza na kufanya asilimia kubwa ya mpira kuwa unazunguka katikati ya uwanja. Frank Domayo, alijaribu kadri alivyoweza kumsumbua Haruna Moshi ‘Boban’, Domayo alionekana kuwa juu ya Boban kimchezo na kupelekea kiungo huyo wa Coastal kumchezea rafu ambayo ilifanya apewe kadi ya manjano.
Salum Telela alikuwa na jukumu la kuhakikisha anaziba njia zote za Boban, kazi ambayo aliifanya vizuri kwa dakika chache na pale Boban alipokuwa akiendelea kupata ‘ moto’, Telela akajikuta akishindwa kutimiza majukumu yake ipasavyo. Hali ambayo iliwafanya viungo wawili wa ulinzi wa Coastal, Santo na Odula, nao kuwa na jukumu rahisi tu la kumzima, Niyonzima ( ambaye inasemekana alicheza huku akiwa na maumivu). Nilipenda namna Santo ilivyokuwa makini na mwenye maamuzi ya haraka, miguu yake mirefu ilimsaidia kucheza mipira ya ‘tackling’ kwa usahihi na alionekana akipandisha mashambulizi kwa tahadhari kubwa, akihofia uwepo wa Niyonzima. Alifanikiwa kwa kila alichofanya, alikuwa mlinzi wa walinzi wake, Marcus Ndehela na Nyosso.
 

Unawezaje kumzima, Niyonzima kwa muda mwingi wa mchezo?. Kuwa na viungo kama Santo na Odula ambao wana uwezo mkubwa wa kuusoma mchezo na njia za hatari za wachezaji hatari za wapinzani wao ni sawa na kuwa na faida mara mbili zaidi, hawa wanakuwa viongozi wa ziada mchezoni, ni wachezaji ambao wanauwezo wa kuwatuliza wenzao hata wakiwa katika presha. Ndiyo maana hata pale, Niyonzima alipoamua kupandisha kiwango chake na kujaribu kukimbia uwanjani huku akiwachezesha washambuliaji wake, Jerry Tegete, ‘ Kavu’ na Msuva akakuta kote huko ‘ kumefungwa’ na walinzi wanne wa Coastal, Juma Ahmad ambaye aliweza kucheza kwa mtindo wa kupanda na kushuka katika beki ya kulia, Banda akawa na jukumu la kukimbia na Msuva kila mahali alipokuwa akipitishiwa mipira, huku Nyosso na Ndehela wakicheza ‘ ng’ando kwa ng’ando’ na Jerry na ‘ Kavu’.
Mechi ikazidi kuwa ngumu na ufundi wa walimu ukawa kando, Telela, akapote uwanjani kwa kuwa Uhuru Suleiman ( kabla hajaumia’ alikuwa akicheza kwa mtindo wa kubadilisha nafasi na Lyanga, na kumfanya Boban kushuka chini kidogo na kuanza kuisukuma timu mbele.


 Mshambuliaji, Yayo Lutimba bado anahitaji muda zaidi ili kuendana na ligi kuu, lakini akionekana kuwa ni mmoja ya washambuliaji ambao wanaweza kuja kufanya vizuri katika siku za usoni kwa sababu aliwafanya, walinzi Mbuyu Twite na Nadir Haroub ‘ Cannavaro’ kuwa bize kwa muda  fulani mchezo, aliwafanya wafanye makosa lakini uwezo wao mdogo katika umaliziaji uliwanyima mabao zaidi. Ilikuwa ni mechi nzuri iliyoharibiwa na waamuzi.

 SAANYA; Alichezesha mchezo wa Yanga na Coastal misimu miwili iliyopita wakati Yanga wakiwania nafasi ya pili na Coastal ikipigana kushuka daraja. Ilikuwa ni mechi iliyokuwa na presha kubwa, mashabiki wengi walitoka Dar hadi Tanga kushuhudia mchezo huo ‘ uliokuwa batili’ na Yanga kushinda kwa bao 1-0. Pia alichezesha mechi ya Simba na Yanga, Mei, mwaka huu, na alionesha udhaifu mkubwa wa kuendana na kasi ya mchezo kadri ilivyokuwa inaongezeka. Na jana ameishia kuonesha uchezeshaji wa kiwango cha chini zaidi katika mechi iliyokuwa na upinzani mkubwa. Hakuwa fair kwa maamuzi mengi, lakini atabaki ni mtu wa mwisho mwenye maamuzi makubwa zaidi katika mchezo huu wa soka hasa wakati mshindi anapotakiwa kuonekana.
Alitoa kadi za kutosha, alikuwa sahihi katika maamuzi yake na nilipenda alivyokuwa akisimamia maamuzi yake kwa kile alichokuwa anakiamua, lakini alifanya ujinga usio kuwa na maana na kuharibu mchezo wote pale alipomtoa nje Odula kwa kadi nyekundu ya moja kwa moja. Ni hadi lini tutakuwa na waamuzi kama, Saanya? Ilikuwa ni penati? Ulitaka mwamuzi afanye nini pale? Boban alikuwa katika ‘ moto’ na timu yote ya Coastal ilikuwa langoni mwa Yanga na mpira uliolazimishwa na Boban ukaishia katika mkono wa Niyonzima na Jerry Sato akatengeneza matokeo sahihi katika dakika ya mwisho ya mchezo.


 Soka linahitaji waamuzi kama Saanya ambao wakati mwingine wanapitiwa na kujikuta wakifanya makosa makubwa lakini yanayoongeza msisimko wa mchezo huu. Huyu ni mwamuzi wa mechi kubwa, tuendelee kumkosoa kwani bado anakua kiuchezeshaji. Samahani kama kauli hii itakukwanza. ‘ Mkuki, kwa Nguruwe kwa binadamu ni mchungu saaaaana’ Siyo lazima kila siku matokeo ya kushanaza yaletwe na Simba na Yanga, tunahitaji kuona nazo zikiadhibiwa katika muda mbaya.’ YANGA WALIFUNGA BAO LAO KATIKA MUDA MAALUMU, LAKINI WAKAFUNGWA KATIKA MUDA MAALUMU’

 0714 08 43 08

No comments:

Post a Comment