Search This Blog

Friday, August 16, 2013

BAADA YA TAREHE ZA UCHAGUZI WA TFF NA MECHI YA SIMBA NA YANGA KUINGILIANA: KAMATI YA UCHAGUZI YAITISHA KIKAO

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limemwandikia Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ili kufanya uamuzi wenye manufaa kwa washabiki wa mpira wa miguu baada ya tarehe ya uchaguzi aliyotangaza kuingilia na mechi ya watani wa jadi (Simba na Yanga) ya Ligi Kuu ya Vodacom.

Sekretarieti ya TFF imepokea maoni kutoka kwa wapenzi mbalimbali wa mpira wa miguu wakiomba matukio hayo mawili (Uchaguzi wa TFF na mechi ya Simba na Yanga) yafanyike katika siku tofauti.

Wakati Kamati ya Uchaguzi inatangaza uchaguzi kufanyika Oktoba 20 mwaka huu tayari ratiba ya Ligi Kuu ya Vodacom ilikuwa imeshatoka, na ikionesha kuwa timu ambazo zina historia ya kipekee katika mpira wa miguu zitacheza siku hiyo.

Sekretarieti imelazimika kumwandikia Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi kwa vile yeye na kamati yake ndiye wenye mamlaka ya kuitisha Mkutano wa Uchaguzi. Huko nyuma TFF imeshafanya mikutano huku kukiwa na mechi za timu ya Taifa (Taifa Stars), jambo ambalo liliwezekana kutokana na mikutano hiyo kuwa na ajenda moja tu.

Tayari Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Hamidu Mbwezeleni ameitisha kikao cha kamati yake kujadili barua hiyo ya sekretarieti.

COCA COLA YATOA MIPIRA 100, FULANA 800
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linatoa shukrani kwa kampuni ya Coca Cola kwa kukabidhi fulana 800 na mipira 100 kwa ajili ya ngazi ya mashindano ya vijana wenye umri chini ya miaka 15 ngazi ya mikoa yanayoanza Septemba Mosi mwaka huu.

Coca Cola ndiyo inayodhamini mashindano hayo yaliyoanzia ngazi ya wilaya ambapo mwaka huu yatachezwa kwa kanda na baadaye fainali itakayochezwa kuanzia Septemba 7-14 mwaka huu jijini Dar es Salaam ikishirikisha mikoa 16 itakayokuwa imefanya vizuri katika ngazi ya kanda.
Kila mkoa utapata fulana 25 na mipira mitatu ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya timu zao kwa ajili ya michuano hiyo ngazi ya kanda itakayomazika Septemba 6 mwaka huu.

Kanda hizo ni Mwanza itakayokuwa na timu za mikoa ya Geita, Kagera, Kigoma, Mara, Mwanza, Shinyanga, Simiyu na Tabora. Mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Manyara na Singida inaunda Kanda ya Arusha.

Zanzibar itakuwa na Kaskazini Pemba, Kusini Pemba na mikoa miwili ya Unguja wakati Kanda ya Dar es Salaam ina Ilala, Kinondoni, Lindi, Mtwara, Temeke na mkoa mmoja wa Unguja.

Kanda ya Mbeya inaundwa na Iringa, Katavi, Mbeya, Njombe, Rukwa na Ruvuma wakati Dodoma, Morogoro, Pwani na Tanga zinaunda Kanda ya Morogoro.

Mwanza itatoa timu nne kucheza hatua ya fainali wakati kanda nyingine za Arusha timu mbili, Zanzibar (2), Mbeya (3) na Kanda ya Morogoro itaingiza timu mbili.

Wakati huo huo, semina ya makocha 32 wa timu za mikoa zitakazoshiriki michuano ya U15 FIFA Copa Coca-Cola iliyokuwa ikiendeshwa na mkufunzi Govinder Thondoo kutoka Mauritius inafungwa leo (Agosti 16 mwaka huu) saa 9 alasiri kwenye ukumbi wa Msimbazi Center, Dar es Salaam.

RAMBIRAMBI MSIBA WA MWANDISHI GRACEMO BAMBAZA
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha aliyekuwa mwandishi wa habari za michezo wa Radio ABM ya Dodoma, Gracemo Bambaza kilichotokea Agosti 14 mwaka huu katika Hospitali ya Ocean Road, Dar es Salaam.

Msiba huo ni mkubwa katika sekta ya habari na mpira wa miguu kwani Bambaza kwa kipindi chote akiwa mwandishi alikuwa akifanya kazi nasi, hivyo mchango wake katika mpira wa miguu tutaukumbuka daima.

Bambaza aliyezaliwa mwaka 1973 na ambaye pia aliwahi kufanya kazi katika vituo vya redio vya Wapo cha Dar es Salaam na Pride cha Mtwara amesafirishwa jana (Agosti 15 mwaka huu) kwenda Karagwe mkoani Kagera kwa ajili ya mazishi.

TFF tunatoa pole kwa familia ya marehemu Bambaza, ABM Radio na Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.

Mungu aiweke roho ya marehemu Bambaza mahali pema peponi. Amina

TIKETI MECHI YA YANGA, AZAM KUUZWA ASUBUHI
Tiketi kwa ajili ya mechi ya Ngao ya Jamii kati ya Yanga na Azam itakayochezwa kesho (Agosti 17 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam zitaanza kuuzwa saa 3 asubuhi.

Vituo vitakavyouza tiketi hizo Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Sokoni Kariakoo, mgahawa wa Steers ulioko mtaa wa Ohio/Samora, Oilcom Ubungo, Kituo cha Mafuta Buguruni, Dar Live Mbagala na BMM Barber Shop iliyoko Sinza Madukani.

Katika vituo hivyo tiketi zitauzwa katika magari maalumu. Magari yote yanayouza tiketi yatahamia uwanjani saa 7 kamili mchana.

Viingilio katika mechi hiyo ni sh. 7,000 kwa viti vya rangi ya kijani na bluu wakati viti vya rangi ya chungwa ni sh. 10,000. Watakaiongia viti vya VIP C watalipa sh. 15,000, viti vya VIP B ni sh. 20,000 wakati VIP A watalipa sh. 30,000.

No comments:

Post a Comment