Search This Blog

Friday, May 17, 2013

PAZIA LA LIGI KUU YA VODACOM LAFUNGWA KESHO - TIMU ZOTE 14 DIMBANI

Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kuwania ubingwa wa Tanzania Bara msimu huu (2012/2013) inafikia tamati kesho (Mei 18 mwaka huu) kwa timu zote 14 kupambana katika viwanja saba tofauti.

Mechi zote zitachezwa kuanzia saa 10 kamili jioni. Ni jukumu la kamishna wa mechi husika kuhakikisha mchezo unaanza katika muda uliopangwa, vinginevyo hatua za kinidhamu zitachukuliwa kwa mujibu wa Kanuni za Ligi Kuu ya Vodacom toleo la 2012.

Yanga ambayo tayari imeshatwaa ubingwa itakuwa mgeni wa Simba katika mechi namba 180 itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ambapo mwamuzi atakuwa Martin Saanya kutoka Morogoro na Kamishna ni Emmanuel Kavenga wa Mbeya.

Mgambo Shooting vs African Lyon (Uwanja wa Mkwakwani, Tanga. Mwamuzi ni Amon Paul wa Mara wakati Kamishna ni Ally Mkomwa kutoka Pwani), JKT Ruvu vs Mtibwa Sugar (Uwanja wa Azam Chamazi, Dar es Salaam. Mwamuzi ni Israel Mujuni wa Dar es Salaam wakati Kamishna ni Salum Kikwamba kutoka Kilimanjaro).

Tanzania Prisons vs Kagera Sugar (Uwanja wa Sokoine, Mbeya. Mwamuzi ni Ibrahim Kidiwa wa Tanga wakati Kamishna ni John Kiteve kutoka Iringa), Oljoro JKT vs Azam (Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha. Mwamuzi ni Athuman Lazi wa Morogoro wakati Kamishna ni Juma Mgunda kutoka Tanga).

Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro utatumika kwa mechi kati ya Polisi Morogoro na Coastal Union ya Tanga ambapo Mwamuzi atakuwa Said Ndege wa Dar es Salaam wakati Kamishna ni Hakim Byemba kutoka Dodoma. Toto Africans itacheza na Ruvu Shooting katika Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza ambapo mwamuzi ni Geoffrey Tumaini kutoka Dar es Salaam na Kamishna ni Josephat Magazi wa Singida.

MECHI ZA MARUDIANO RCL WIKIENDI HII
Mechi za marudiano za raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) zinachezwa wikiendi hii katika viwanja kumi tofauti wakati mechi ya Flamingo ya Arusha na Machava FC ya Kilimanjaro yenyewe itachezwa Jumatatu (Mei 20 mwaka huu).

Uamuzi wa mechi hiyo kuchezwa Jumatatu ni kutokana na Uwanja wa Sheikh Kaluta Amri Abeid kutumika kwa mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kesho wakati Jumapili utatumika kwa shughuli nyingine za kijamii kwa mujibu wa wamiliki wa uwanja huo (CCM Mkoa wa Arusha).

Mechi nyingine zitachezwa keshokutwa (Jumapili) ambapo Abajalo watakuwa wenyeji wa Red Coast kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam. Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara utatumika kwa mechi kati ya wenyeji Coast United na Kariakoo ya Lindi.

African Sports ya Tanga itaoneshana kazi na Techfort ya Ifakara mkoani Morogoro katika mchezo utakaochezwa Uwanja wa Mkwakwani. Nayo Simiyu United ya Simiyu itakuwa mgeni wa Magic Pressure ya Singida kwenye Uwanja wa Namfua, mjini Singida.

Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza ndiyo utakaotumika kuzikutanisha timu za Polisi Jamii Bunda kutoka Mara na wenyeji UDC wakati Biharamulo FC ya Kagera na Polisi SC ya Geita zitaumana kwenye Uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba.

Milambo FC ya Tabora itakuwa mwenyeji wa Saigon FC ya Kigoma kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi mjini Tabora huku Mbinga United ya Ruvuma ikiikaribisha Njombe Mji ya Njombe kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea.

Uwanja wa Kumbukumbu ya Samora mjini Iringa utatumika kwa mechi kati ya wenyeji 841 KJ dhidi ya Kimondo SC kutoka Mbeya. Nazo Rukwa United na Katavi Warriors zitapimana ubavu kwenye Uwanja wa Nelson Mandela mjini Sumbawanga.

Timu zitakazofuzu kucheza raundi ya pili zitacheza mechi zao za kwanza kati ya Mei 25 na 26 mwaka huu wakati mechi za marudiano ni kati ya Juni 1 na 2 mwaka huu.

No comments:

Post a Comment