Search This Blog

Thursday, March 14, 2013

MAKALA: AZAM FC NDIO TIMU MKOMBOZI WA SOKA LA TANZANIA


Sikumbuki mwaka, mwezi wala tarehe, ninachokumbuka ilikua siku ya jumapili. Wakati natoka kanisani kuna ishara nyingi sana nilikutana nazo barabarani, ama kwa hakika ilikuwa siku special sana. Sikuweza kuendelea kufanya utafiti zaidi kutokana na hali yangu ya kiafya, kwa muda huo kichwa kilikua kinagonga huku nikiwa nahisi homa kali sana. Sikuwa na muda wa kupoteza tena njiani. Moja kwa moja nikaendelea na safari ya kuelekea nyumbani, kituo cha kwanza sebuleni huku machozi yakinilenga machoni, usishangae sana kipindi hiko nilikuwa na umri kati ya miaka 8 au 9. Mama yangu hakuwahi kupata mafunzo ya udaktari lakini hakukuwa na dokta mwaminifu kwangu kama mama. Akaacha kazi zake za jikoni na kuniletea dawa mezani sebuleni, sikuwa na haja wala sikumuuliza mama ni dawa gani, nikachukua maji yetu ya bombani na kusukuma dawa mdomoni, taraatibu nikaenda kupumzika kitandani.

Kikosi cha zamani cha simba

Huku nikiwa nasikilizia homa na kichwa kitandani, nikaanza kuvuta taswira ya niliyokutana nayo barabarani, ooops usingizi ulinichukua wakati naanza kutafakari. Sikumbuki baada ya muda gani tangu kuchukuliwa na usingizi. Nikashtushwa kwa kelele kali, nikaamka na kuanza kukimbia huku nikijiuliza ni mwizi au Nyumba Inaungua? Baada ya kufika nje ya kibaraza chetu nikakuta watu wengi sana, wengine wanashangilia wengine wamenuna, nikamuona mama amevalia tisheti nyeupe na kanga nyeupe iliyokuwa na vidoti vya rangi nyekundu Akifurahi na kushangilia sana. Nikatupia jicho upande wa pili nikamuona mzee amevalia tisheti ya njano yenye picha ya mtu fulani hivi Iliyoandikwa Chagua Mkapa, Chagua CCM. Mzee alikuwa amekaa karibu na radio kubwa, ungemuangalia kwa karibu ungelifikiri ni Dj, maskini baba alikuwa na sura ya huzuni sana.


Nikashindwa kuelewa hapa kuna msiba au sherehe? Baba amenuna mama anacheka. Mara watu wote waliokuwa wakishangilia wakanyamaza na kutegesha masikio yao kwenye uelekeo wa radio. Moja kwa moja na mimi nikafanya vivyo hivyo, ikasikika sauti ya mtangazaji mmoja wa RTD sikumbuki kama alikuwa Swedi Mwinyi au Juma Nkamia ikisema “Ni Yule Yule, kwa mara nyingine, Joseph Kaniki anaiandikia Simba bao la kuongoza, Simba moja Yanga sifuri” Waliovaa nyeupe na nyekundu wakapiga mayowe kwa kitambo, huku waliovaa njano na kijani wakiinamisha vichwa vyao chini. Hapo ndipo nilipojiwa na kumbukumbu ya kuwa kulikuwa na mechi kati ya Simba na Yanga. Nikakumbuka bendera za njano na nyekundu zilizokua zinapepea kila kona ya mtaa kipindi natoka kanisani. Nikakumbuka watu jinsi walivyokua wanabishana kila nilipokatiza. Hakika si Mama na Baba yangu peke yao waliyosimamisha kazi zao, bali nchi yote ilisimama.


wachezaji wa zamani


Miaka ya karibuni, mechi ya Simba na Yanga imepoteza mvuto. Ule umati uliokusanyika mbele ya kibaraza chetu utaukuta kwenye msiba au sherehe na si mechi ya Simba na Yanga.


Utawala wa Simba na Yanga umefanya ligi yetu isiwe na mvuto na kupelekea watu kupoteza hamu ya kupenda ligi yetu na mechi ya watani kwa ujumla. Leo hii mama yangu hana muda hata wa kuangalia wala kusikiliza mpira. Mzee ndio kabisa ameshasahau kama kuna kitu kinaitwa Simba na Yanga hapa Tanzania. 

Unajua kwanini League ya Uingereza inapendwa? Kabla ya Barclays premier league mwaka 1992/93 mwaka mmoja nyuma Arsenal na Liverpool walichuana vikali kugombea ndoo ya ligi. Lakini kwenye msimu wa kwanza wa Barclays ni Aston villa waliokua wanatishia ndoto za Fergson na vitoto vyake kuchukua kombe hilo kwa mara ya kwanza. 

Kumbuka Man United walivyokuwa wanasubiria kombe hilo kwa miaka 26, na Fergi kwa miaka 6. Waliwaacha Aston Villa kwa point 10 na kukata kiu yao huku Norwich City ikikamata nafasi ya tatu, msimu uliofuata mambo yakawa tofauti kwa Villa na Norwich baada ya Blackburn na The magpies Newcastle kuwaondoa kwenye namba 2 na 3, 1994/95 mambo yakawa tofauti si Man u, Leeds, Liverpool wala Nottingham Forest aliyethubutu kuchukua kombe hilo mbele ya paka weusi(Blackburn Rovers), huku Alan Shearer akifikia rekodi ya Andy cole ya kufunga magoli mengi kwenye league kwa msimu mmoja magoli 34, na rekodi hiyo haijavunjwa mpaka hii leo.

Arsenal ilipoteana kabisa, ikaja kuibuka msimu wa mwaka 1995/96 kwa kushika nafasi ya nne na msimu unaofuata kukamata namba tatu, kabla ya kuchukua ubingwa msimu wa mwaka 1997/98, Hapo utaona kupanda na kushuka kwa timu nyingi sana. Ndani ya ligi kuna mechi ngumu na nzuri ukiacha mechi za watani. Pia kwenye ligi hiyo kuna timu nyingi zenye uwezo wa kuchukua ubingwa. 

Kwanini usipende ligi yao? Unayo kila sababu ya kuipenda, hata mimi naipenda sana. Wakati huo watu wana hamasa kubwa ya mechi ya Simba na Yanga kulikua na Timu ya Mtibwa sugar iliyotoka kuwa bingwa mara mbili mfululizo miaka ya mwisho ya karne ya 20. Angalau kulikua na mechi ya Mtibwa vs Simba au Yanga kabla ya mechi ya watani. Wakaja Moro wakapotea. Na Sasa ni Zamu ya Azam FC kuturudisha tena kwenye Ligi ya bongo.



Timu hii ya Azam ilianzishwa mwaka 2007 na wafanyakazi wa kiwanda cha Bakhresa kama timu ya mazoezi. Shukrani zimuendee Yusuph Bakhresa aliyekuwa na maono ya kuwa na timu ya mashindano. Kwa hekima maarifa na nguvu ya pesa msimu wa mwaka 2008/09 kwa mara ya kwanza Azam wakashiriki ligi kuu na kumaliza kwenye nafasi ya 8. Msimu uliofuata wakakamata nafasi ya tatu. Msimu uliyopita wakamaliza nafasi ya pili na kujikatia tiketi ya kushiriki kwenye mashindano ya kimataifa na mpaka sasa ni timu pekee ya Bongo iliyobaki kwenye mashindano hayo baada ya timu nyingine kuondolewa kwa vipigo vya mbwa mwizi. Achana na Simba na Yanga, Azam ina uwanja wa kisasa na Academy bora kabisa ya soka nchini bila kusahau gym na hostel za bei mbaya.


Azam si timu ya siasa, Mzee Bakhresa ana dhamira na nia ya dhati ya kufanya yaliofanywa na Motsepe na Katumbi. Nashukuru juzi niliungana tena na mama yangu kuangalia mechi ya Azam na Al Nasri, ni takribani miaka kumi imepita tangu mama kuangalia mechi. Ama kwa hakika amesikia sifa za Azam, na bila shaka anaipenda na kuishabikia Azam. Ahsante Azam kwa kumrudisha Mama kwenye Ulimwengu wa soka, najua si mama pekee aliyerudishiwa hamu ya kupenda mpira wa bongo. Soka letu sasa linapata afya kutoka kwa Azam. Watanzania Tunajivunia kuwa na Azam. Na mimi najivunia kua mshabiki wa Azam.



Timu moja, hatima moja Azam fc kwa ajili yangu na kwa ajili yako


By kaijage jr……

Middle ya juu


1 comment:

  1. hawana jipya sababu na wenyewe wanasumbuliwa na kirusi cha usimba na uyanga, kwahiyo tuwape muda kidogo kabla hawajapotea.

    ReplyDelete