Search This Blog

Thursday, November 1, 2012

STEWART HALL ARUDI AZAM KWA MAPOKEZI MAKUBWA - KUTAMBULISHWA LEO DHIDI WAGOSI

Kocha Muingereza Stewart Hall akivishwa mataji baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam usiku wa leo

Kocha Muingereza Stewart Hall akipozi kwa picha baada ya kuwasili kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam usiku wa leo

Mashabiki wa Azam wakipiga ngoma na kupuliza vuvuzela wakati wa mapokezi ya kocha Muingereza Stewart Hall kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam usiku wa leo


KOCHA Muingereza Stewart Hall ametua jijini Dar es Salaam usiku huu huku akiitaka Azam kushinda kila mechi baada ya kurejea kuifundisha timu hiyo ya Ligi Kuu ya Tanzania Bara kwa mara ya pili.

Hall amerejea katika klabu yake ya zamani ya Azam baada klabu aliyokuwa akiifundisha Sofapaka ya Kenya inayomilikiwa na tajiri kukiri kwamba haiwezi kupambana na kampuni kubwa ya Azam ambayo imeahidi kumpa mshahara mara mbili ya waliokuwa wakimlipa Wakenya hao.

Mashabiki waliokuwa uwanjani hapo wakipuliza mavuvuzela na kupiga ngoma, waliimba nyimbo mbalimbali ukiwamo uliosema "Hall amerejea, homa na presha za Simba na Yanga ziko juu."

Baada ya kutua kocha huyo, alivishwa mataji ya maua na viongozi wa Azam waliokuwapo kwenye Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere
kwa ajili ya kumpokea.

"Nimejisikia vizuri kwa mapokezi haya mazuri. Naahidi kufanya mazuri. Nataka Azam ishinde kila mechi. Mambo yataanza kesho," alisema Hall ambaye aliondoka katika klabu hiyo baada kutofautiana na uongozi kufuatia kumchezesha winga Mrisho Ngassa katika mechi ya fainali ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame) dhidi ya Yanga, siku chache baada ya winga huyo kupigwa picha akiibusu logo ya jezi ya klabu yake ya zamani ya Yanga.

Uongozi wa Azam ulisema kwamba utafanya mkutano na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam kesho kwa ajili ya kumtambulisha kocha huyo aliyeifundisha kimafanikio timu hiyo kwa kuiwezesha kumaliza ikiwa ya pili katika ligi kuu ya Tanzania Bara msimu uliopita na pia kuifikisha katika fainali ya Kombe la Kagame katika msimu wake wa kwanza kushiriki. Ilifungwa 2-0 na Yanga katika fainali ya Kagame.

Azam iliyomtimua kocha wake aliyemrithi Hall, Mserbia Boris Bunjak, baada ya timu kuangukia katika nafasi ya nne ya msimamo wa ligi kuu, kesho itacheza dhidi ya Coastal Union ya Tanga inayoshika nafasi ya tatu kwenye Uwanja wa Azam Complex Chamazi.


Source: http://straikamkali.blogspot.com/ 

No comments:

Post a Comment