Search This Blog

Friday, September 28, 2012

TFF,FA MIKOA NA NMB MNATUPELEKA WAPI ?

Habari zenu ndugu wasomaji. Leo nina maswali machache na hoja kadhaa ambazo nahitaji majibu toka kwa TFF, FA MIKOA na Benki ya NMB kama wadau wakubwa wa Soka hapa nchini.

Naamini kila mtu anakumbuka kozi za Walimu wa Soka zilizokuwa zinafanyika hapa nchini takiribani mikoa yote ya Tanzania na baadhi ya mikoa ilijirudia mara kadhaa, Na nyingi ziliendeshwa kwa Walimu wa Sekondari na Shule za msingi ili kuinua vipaji toka mashuleni, hii inatokana na TFF kuangahika kwa muda mrefu kutafuta Wadhamini na hatimaye Benki ya NMB kujitokeza na kudhamini kozi hizi kitu ambacho ni kizuri kinachohitajika katika kukuza Soka letu Tanzania.

Kilichonishtua ni mwaka 2009/2010 ilitakiwa kuendeshwa kozi hiyo kwa mikoa 26 ya Tanzania Bara na Benki ya NMB ilitoa fedha za kuendesha kozi hiyo pamoja na mipira 30 kila mkoa,koni 18 kila mkoa, jezi jozi moja kwa ajili ya mkufunzi na fedha walipewa TFF ili watume kwa kila FA mkoa kwa mikoa yote 26.

Lakini cha kushangaza hawa TFF walituma pesa hizi na vifaa hivyo kwa mikoa kama kumi tu ikiwamo Shinyanga, Mwanza, Singida, mikoa ya Kisoka Ilala,Temeke na Kinondoni na pia fedha Tshs 710,000 kwa ajili ya posho ya mkufunzi, chakula, malazi na mawasiliano sasa swali je fedha nyingine za mikoa 16 zimekwenda wapi mimi na wewe msomaji wangu hatujui.

FA za mikoa teule ambayo ilipewa fedha hizo pia nao walichakachua kwa mtindo wao na kutoa fedha hizo kwa ufinyo Mfano ni Mkoa wa Shinyanga ambao kozi iliendeshwa januari 26, 2010-Februari 7,210 na mkufunzi alikuwa Marehemu Suleiman Gwaje ambaye pia alilalamikia hili, pia ulitokea ugomvi na kurushiana maneno kati ya viongozi wa FA mkoa na Wajumbe Watendaji kutokana na fedha hizo mpaka baadhi ya wajumbe kutaka kupindua uongozi huliopo madarakani.

Utaratibu ulitakiwa kuwa hivi mkufunzi akabidhiwe fedha zake katika mchanganuo ufuatao: - Posho ya siku 16 @ Tshs30, 000 jumla 480, 000, Nauli Tshs 230,000 yaani kwenda na kurudi pamoja na mawasiliano akiwa katika kituo chake cha kazi. Matokeo yake haya hayakufanyika na mkufunzi alipelekwa katika migahawa ya ajabu yenye bei nafuu na huduma hisiolidhisha ili kupiga panga fedha hizo.

Wanafunzi waliotakiwa kushiliki kozi hizi walikuwa ni Walimu na idadi ni 45 kwa kila mkoa yaani katika ile mikoa 10 teule ya TFF. Kwa mjibu wa TFF wenyewe walisema gharama ya Cheti kimoja ni Tshs 10,000 na fedha hizi ulipwa na NMB na tayari zilishakabidhiwa kwa TFF lakini cha kushangaza hakuna hata mkoa moja kati ya mikoa hii 10 walioendesha kozi hii mwaka 2009/2010 wamepata Vyeti hivyo. Sasa piga hesebu mikoa 26, kila mkoa Walimu 45 na kila mmoja gharama ya cheti ndio hiyo je ni Shilingi ngapi zimechakachuliwa na hawa jamaa?

Kinachoendelea sasa kuna kampeni ya TFF ya chini kwa chini kuhamasisha makatibu wa TAFCA wa ile mikoa ambayo ilibahatika kufanya kozi hii kuwaomba Walimu walioshiriki kozi hii wachange elfu kumi (Tshs 10,000) ili watengenezewe Vyeti hivyo kwa kupitia kwa Katibu wa TAFCA Taifa ili kuficha hili lilofanyika ambalo pia limekwama kutokana na kutokuwa na imani tena na TFF, sasa mimi najiuliza Soka letu litakua kwa mtindo huu? TFF, FA MIKOA na Benki ya NMB wanatupeleka wapi?

Pia baadhi ya mikoa kozi hii ilifanyika mwezi Oktoba 2009 kama Singida, Mwanza na mingineyo lakini Shinyanga ilifanyika tarehe 26 Januari, 2010 pia badala ya kuwa na Walimu 45 wa sekondari na shule za msingi waliotakiwa kushiriki walishiriki 26 tu tena katika mazingira magumu kwani hapakuwa na hata maji ya kunywa na washiriki walio wengi walifanya kuwakamata tu barabarani na kuwataka washiriki kozi hii na hili lilifanywa makusudi kwani fedha ya kuendesha kozi hii kwa mkoa huu ilikuwa ishaliwa na viongozi wa FA mkoa.

Na maelezo kutoka TFF, washiriki walitakiwa kujigharamia chakula na malazi kitu ambacho walikifanya Walimu hawa tena bila kinyongo. Je ni kweli ndio mkataba unavyosema maana mkataba huu ni siri kati ya TFF na Benki ya NMB hakuna mdau wala TAFCA anayeufahamu mkataba huo sasa tujiulize watu wakikataa kujitokeza kushiriki kozi hizi tutamlaumu nani kwa ubabahishaji huu?
Na kwa nini fedha hizi zisikabidhiwe kwa chama cha makocha Taifa na kuwambia waendeshe kozi hizi badala ya FA za kila mkoa kwani wao ndo wanajua watu gani ambao wanapenda na wanataka kuwa walimu wa soka.

Mimi kama mimi siamini kama Benki ya NMB hailifahamu hili kwani kama hawafahamu inaamana hawafanyi ukaguzi wa fedha zao wanazotoa kwa TFF? Na kama wanafahamu wamechukua hatua gani? Na kama wamechukua mbona taarifa hatujaiona wala kuisikia? Kama hawajachukua hatua inamaana na wao pia wanahusika katika hili?

Mimi kama mdau wa Soka hili la Bongo inaniuma sana na kubakia na maswali TFF, FA MIKOA na Benki ya NMB wanatupeleka wapi? Na wapo kwa ajili ya kuendeleza Soka au maslahi yao binafsi? TFF Na Benki ya NMB naomba mchunguze au mtoe maelezo kuhusu hili maana linatia kinyaa na aibu katika Soka letu na kama hamna taarifa basi Habari ndiyo hiyo.


Na Magesa Japhari
E – Mail: japharimagesa@yahoo.com
Mobile phone: +255 784 269 812 or +255 764 318 844, +255 714 368 843.

NB:
Kwa haraka haraka tu, Fedha inayosadikika kutafunwa na TFF na FA MIKOA
Watu 45 @ mkoa × 10,000 gharama ya cheti × 26 mikoa iliyotakiwa kushiriki jumla 11,700,000.
FEDHA ya Wakufunzi mikoa 26,ilitolewa kwa mikoa 10, je mikoa 16@Tshs 710,000 × 16 mikoa ambayo haikutumiwa jumla 11,360,000
GRAND TOTAL Tshs 23,060,000
Hizi ndizo tulizojua kwa mjibu wa hesebu iliyopo je tusizozifahamu ni ngapi? AKILI KUMKICHWA!

No comments:

Post a Comment