Search This Blog

Wednesday, December 14, 2011

ZANZIBAR KUSHIRIKI KOMBE LA DUNIA


TIMU ya Soka ya Zanzibar 'Zanzibar Heroes' kwa mara ya kwanza itashiriki fainali za Kombe la Dunia la Viva kwa nchi ambazo si wanachama wa Shirikisho la Soka la Dunia (Fifa).

Zanzibar Heroes imealikwa kushiriki mashindano hayo yaliyoandaliwa na Shirikisho la Bodi la Vyama Soka visivyokuwa mwanachama wa Fifa (NBF). Michuano itafanyika Juni nchini Iraq na kushirikisha nchi nane.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu msaidizi wa ZFA, Masoud Attai alisema tayari ZFA wamepokea mwaliko mashindano hayo ya kila baada ya miaka miwili.Attai alisema baada ya kupokea mwaliko huo viongozi wa ZFA watakutana mapema wiki ijayo ili kujadili ushiriki.

"Hii ni nafasi nzuri kwa timu yetu kuchuana katika mashindano makubwa kama haya, ni jambo la kheri na sisi kama viongozi tutakutana wiki ijayo ili kujadili ushiriki wetu ambao unahitaji maandalizi ya kina," alisema Attai.

Mara ya mwisho mashindano hayo yalifanyika Gozo katika visiwa vya Malta na timu ya Padania iliibuka mabingwa.

Nafasi ya pili ilichukuliwa na Iraq Kurdistan na ile ya tatu kwenda Occitania, mashindano yalifanyika katika Uwanja wa Gozo uliopo Xewkija na Sannat Ground uliopo Sannat.

Mwaliko huo wa NFB kwa ZFA umekuja ikiwa ni miezi michache imepita tangu Fifa walipoikataa ZFA kuwa mwanachama wake.

No comments:

Post a Comment