Search This Blog

Wednesday, November 30, 2011

CHUJI KUANZA MAZOEZI YANGA LEO



Mchezaji Athumani Idd’Chuji’ aliyerudishwa kuichezea timu ya Yanga ni miongoni mwa wachezaji wanaotarajia kuanza mazoezi na timu hiyo Uwanja wa Kaunda, Dar es Salaam leo kujiandaa na mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

Chuji ambaye hajacheza mpira kwa muda mrefu sasa aliondoka Yanga muda mfupi baada ya kumalizika Ligi Kuu Tanzania Bara Aprili mwaka huu, kisha akajiunga na Simba aliyochezea Kombe la Kagame Julai mwaka huu, lakini alitemwa na timu hiyo kwenye usajili wa Ligi Kuu msimu huu.

Akizungumza Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa Yanga Selestine Mwesigwa alisema kuwa wamemrudisha kundini kiungo huyo na kwamba leo atakuwepo mazoezini.

Mwesigwa alisema wamemsajili kiungo huyo kwa kumpa mkataba wa miezi sita, ambao watamuongeza kulingana na uwezo atakaouonesha uwanjani.

“Tutakuwa naye mpaka msimu huu wa ligi utakapokwisha ,tutamuongeza kulingana na uwezo atakaouonesha,”alisema.

Pia alieleza kuwa wamewarudisha wachezaji wao chipukizi Salumu Telela na Omega Seme waliokuwa kwa mkopo Moro United.

Kuhusiana na wachezaji wengine timu hiyo iliowasajili Mwesigwa alisema bado usajili wao haujakamilika na kwamba wataweka wazi pindi utakapokamilika.

“Mimi napenda kuzungumza mambo yaliyokamilika kwani yana uhakika, tutaweka wazi majina ya wachezaji wengine pindi usajili wao utakapokamilika,” alisema.

No comments:

Post a Comment