Search This Blog

Friday, October 28, 2011

TIMBE: YANGA WANILIPE MISHAHARA YANGU NA FEDHA ZA KUVUNJA MKATABA


Kocha Sam Timbe ambaye alifungashiwa virago na ‘Wanajangwani’ baada ya kurejeshwa kwa kocha aliyemtangulia, Mserbia Kostadin Papic, ameutaka uongozi wa klabu hiyo umlipe fedha zake ili aondoke zake nchini.

Akizungumza jana na kwenye hoteli ya Markham, Timbe alisema kuwa anasikitishwa na kile anachofanyiwa sasa na uongozi wa Yanga kwani aliamini kuwa watatanguliza uungwana na kumlipa stahili zake mara tu walipoamua kuvunja mkataba wake wa ajira.

"Ni wao ndio walioamua kuvunja mkataba… wanapaswa kunilipa haki yangu ili na mimi nifanye mambo mengine. Hadi sasa sijui ni lini watanilipa fedha zangu," alisema Timbe.

Alisema kuwa mbali na kuidai Yanga gharama ya kuvunja mkataba wake, pia anaidai klabu hiyo fedha za kuingia mkataba wa kuifundisha timu hiyo pamoja na mshahara wake wa mwezi uliopita hadi sasa.

"Niliposaini mkataba mwezi Mei mwaka huu walinilipa sehemu tu ya fedha tulizokubaliana na nyingine waliahidi kunilipa baadaye… lakini hadi walipovunja mkataba Oktoba 23, hawakuwa wamenilipa fedha zilizobakia na zote naamini kwamba watanilipa mara moja ili niondoke zangu,” alisema Timbe, ambaye aliongeza kuwa hajui ni kwanini ametimuliwa ghafla wakati timu aliyokuwa akiifundisha ilikuwa na mwelekeo mzuri na kukamata nafasi ya pili katika msimamo wa ligi kuu ya Bara.

"Baada ya mechi yetu dhidi ya Oljoro, nilipewa barua ya kunijulisha kikao na uongozi wa Yanga ili kujadili maboresho ya benchi la ufundi. Katika barua hiyo niliambiwa kwamba kikao kitakuwa cha watu wanne ambao ni mimi na viongozi watatu ambao wangefika hapa hotelini ninakoishi," alisema.

Hata hivyo, Timbe anasema kuwa alishangaa kuona kuwa kesho yake anafuatwa na kiongozi mmoja na kupewa barua ya kuvunja mkataba, bila kupewa maelezo zaidi.

"Mimi sikuwa na jinsi isipokuwa ni kudai haki yangu. Ila iliniuma moyoni nilipokuja kufahamu kuwa tayari walishamleta kocha mwingine wa kutwaa nafasi yangu. Jambo hili limenisikitisha sana," alisema Timbe.

1 comment:

  1. POle Timbe,Yanga watakukumbuka sanaaa,you are the good coach.
    Ngoja kesho wapigwe mkono na SIMBA utaona wanapigana bakora na wengine kukukumbuka.

    ReplyDelete