Search This Blog

Friday, October 21, 2011

TANZANIA YASHIKA NAFASI YA 131 KWA UBORA WA SOKA DUNIANI


TANZANIA imezidi kuporomoka katika viwango vya kila mwezi vinavyotolewa na Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa).

Katika orodha ya Oktoba iliyotolewa jana na shirikisho hilo, Tanzania imeshuka kwa nafasi nne kutoka ya 127 hadi 131 duniani. Kwa upande wa Afrika imeshuka kutoka nafasi ya 32 hadi 34.

Kuporomoka huko kunatokana na timu ya taifa ‘Taifa Stars’ kuchapwa mabao 3-1 na Morocco katika mchezo wa kufuzu fainali za Mataifa Afrika mwezi uliopita ambapo kwa mara nyingine Tanzania imeshindwa kufuzu.

Hali hiyo inazidi kukatisha tamaa pamoja na nguvu nyingi ambazo serikali na wafadhili wameelekeza kwenye soka kwa sasa.

Katika nchi za Afrika Mashariki Uganda wanashika nafasi ya 88 duniani na 22 Afrika, wakati Kenya wapo nafasi ya 135 duniani na 36 Afrika.

Kwa upande wa Afrika, Ivory Coast bado wameendelea kutamba kileleni pamoja na kushuka kwa nafasi tatu katika viwango vipya vya Fifa.

Rwanda wamekuwa nchi ya Afrika ambayo imepanda kwa nafasi nyingi Oktoba. Nchi hiyo imepanda kwa nafasi 31 na kushika nafasi ya 29 Afrika na 112 duniani.

Nafasi tatu za juu Afrika hakuna mabadiliko baada ya Misri na Ghana kuendelea kubaki kwenye nafasi ya pili na tatu.

Vijana wa Pharao wameendelea kubaki nafasi ya pili kutokana na ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Niger kwenye mechi za kufuzu Mataifa ya Afrika mwezi uliopita.

Benin wamekuwa timu iliyoshuka kwa nafasi nyingi 27 na kushika nafasi ya 199 baada ya kipigo cha bao 1-0 nyumbani kutoka kwa Rwanda mwezi uliopita.

Nchi zinazoshika nafasi 10 bora Afrika na nafasi zao duniani kwenye mabano ni Ivory Coast (19), Misri (29), Ghana (33), Algeria (35), Senegal (42), Nigeria (44), Cameroon (47), Afrika Kusini (49), Burkina Faso (54) na Morocco (56).

Mabingwa wa Dunia Hispania wameendelea kupanda kwa kuongoza katika orodha ya viwango duniani.

Mbali na Hispania nchi zilizo kwenye 10 bora duniani nyingine ni Uholanzi (2), Ujerumani (3), Uruguay (4), Brazil (5), Italia (6), England (7), Ugiriki na Ureno (8), Argentina na Denmark (10).


1 comment:

  1. tushazoea ila tatizo linajulikana lakini wahusika hawataki kubadilika kwanini wasichukue vijana wamitaani na kuwa train atleast 4yrs na kusitisha timu ya taifa isishiriki michuano yoyote ya kimataifa isipo kuwa challenge cup.Najua hili kwa Tanzania yetu TFF ilivyo kuwa walafi wa fedha za wazamini hawatawezakukubali timu ikae kwa kipindi cha miaka minne huku wakiandaa timu lakini yote kwa yote wajaribu kuboresha ligi yetu kwa kuakikisha nakufatilia kila klabu iwe na academy yake

    ReplyDelete