Search This Blog

Saturday, August 20, 2011

AFRICAN LYON KULIPA WACHEZAJI KWA MAKATO

Timu ya African Lyon imeomba kuwalipa kwa makato ya mlangoni wachezaji wake wawili wanaoidai; Godfrey Komba na Abdul Masenga ambao ilikatiza mikataba yao msimu uliopita. Awali Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji iliiagiza Lyon kuwalipa wachezaji hao kufikia Agosti 17 mwaka huu vinginevyo isingeruhusiwa kushiriki Ligi Kuu ya Vodacom inayoanza leo (Agosti 20 mwaka huu).

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) liliitaka Lyon ithibitishe kwa maandishi kuwa itakatwa kwenye mapato yake ya mlangoni katika mechi hadi deni la wachezaji hao litakapomalizika. Lyon imetekeleza maagizo hayo, hivyo imeruhusiwa kucheza mechi yake ya leo (Agosti 20 mwaka huu) dhidi ya Polisi Dodoma kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Dodoma.

Hivyo Lyon itakatwa katika mechi yake ya leo ili kulipa deni hilo. Kama fedha ilizopata katika mgawo hazitatosha kulipa deni hilo itakatwa sehemu iliyobaki katika mechi inayofuata.

Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji katika kikao chake cha Januari 7 mwaka huu chini ya Mwenyekiti wake Alex Mgongolwa kiliiagiza Lyon iwalipe wachezaji hao baada ya kusitisha mikataba yao nje ya taratibu za kimikataba. Masenga na Komba kila mmoja anadai sh. milioni 4.3.

Wachezaji hao wataarifiwa juu ya utaratibu wa malipo yao ambapo TFF ndiyo itakayofanya makato kwa niaba yao.

No comments:

Post a Comment