Search This Blog

Wednesday, May 18, 2011

KITUO CHA KUKUZA VIPAJI CHA TSA.



Kituo cha kukuza vipaji cha Tanzania Soccer Academy (TSA) kinachoendeshwa kwa
ubia kati ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na kampuni ya Kiliwood
kimesimamisha shughuli zake tangu mwaka jana.

Kamati ya Utendaji katika kikao chake cha kwanza mwaka huu ilishafanya uamuzi
juu ya uendeshaji wa kituo hicho na kutoa maelekezo kwa Sekretarieti ya TFF. Kwa
vile kituo hicho kilichokuwa kinachukua vijana wenye umri kuanzia miaka 17 hadi
20 ni cha ubia kati ya TFF na Kiliwood uamuzi wowote juu ya mustakabali wake ni
lazima uhusishe pande hizo mbili.

Kwa mantiki hiyo Sekretarieti kwa sasa inafanya mawasiliano na kampuni ya
Kiliwood ili pande hizo mbili zikutane na kuelezana juu ya uamuzi wa Kamati ya
Utendaji ya TFF juu ya mustakabali wa kituo hicho.


Wajibu wa TFF katika mkataba kati yake na Kiliwood juu ya uendeshaji wa kituo
hicho ni vitendea kazi (facilities) ambavyo ni hosteli na uwanja wa mazoezi.


KOZI YA WAKUFUNZI WA MAREFA
TFF kupitia Kurugenzi ya Ufundi imeandaa kozi ya wakufunzi wa marefa wa mikoa
itakayofanyika Dar es Salaam kuanzia Juni 1 hadi 4 mwaka huu.

Kozi hiyo inatarajia kushirikisha wakufunzi wa marefa zaidi ya 20 kutoka mikoa
yote ya Tanzania Bara. Mara ya mwisho kozi hiyo ilifanyika nchini mwaka 2008.


Wawezeshaji katika kozi hiyo ni Stanley Lugenge ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati
ya Waamuzi ya TFF, Leslie Liunda, Joseph Mapunda, Hafidh Ally na Juma Hamisi.


Boniface Wambura
Ofisa Habari TFF

No comments:

Post a Comment