Search This Blog

Thursday, February 27, 2014

OFFICIAL: KIM POULSEN ATEMESHWA KIBARUA TAIFA STARS - SALUM MADADI NA HAFIDH BADRU KUONGOZA JAHAZI

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Kocha wa Taifa Stars, Kim Poulsen wamekubaliana kuvunja mkataba katika makubaliano ambayo ni siri kwa pande zote mbili.

Uamuzi huo umetangazwa leo (Februari 27 mwaka huu) jijini Dar es Salaam kwa pamoja na Rais wa TFF, Jamal Malinzi na Kocha Poulsen mbele ya waandishi wa habari.

Rais Malinzi kwa niaba ya TFF ametoa shukrani za dhati kwa Kocha Poulsen kwa ushirikiano na mchango ambao ameutoa kwa Tanzania kuanzia kwenye mpira wa miguu wa vijana.

Naye Kim amewashukuru Watanzania kwa ushirikiano waliompatia kwa kipindi cha miaka mitatu alichokaa nchini kuanzia Mei 2011 alipoteuliwa kuwa kocha wa timu za Taifa za vijana, na baadaye Taifa Stars.

Akizungumzia benchi jipya la ufundi la Taifa Stars, Rais Malinzi amesema linatarajiwa kutangazwa hivi karibuni likiongozwa na kocha kutoka nje ya Tanzania.

Amesema kwa upande wa mechi dhidi ya Namibia itakayochezwa Machi 5 mwaka huu jijini Windhoek, Stars itaongozwa na Kaimu Mkurugenzi wa Ufundi, Salum Madadi akisaidiwa na kocha Hafidh Badru kutoka Zanzibar.

Katika hatua nyingine, Kocha Madadi amewaondoa wachezaji watano wa Yanga katika kikosi kilichotajwa awali ili wapate fursa ya kuitumikia timu yao kwenye mechi mbili za Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Al-Ahly ya Misri.

Wachezaji hao ni Athuman Idd, David Luhende, Deogratius Munishi, Frank Domayo, Kelvin Yondani na Mrisho Ngasa. Pia kipa Ivo Mapunda ameondolewa katika kikosi hicho baada ya kupata msiba.
Nafasi zao zimezibwa na wachezaji Abdi Banda (Coastal Union), Himid Mao (Azam), Juma Luizio (Mtibwa Sugar), Said Moradi (Azam) na Shabani Kado (Coastal Union).

Taifa Stars itaingia kambini keshokutwa (Machi 1 mwaka huu) jioni kwenye hoteli ya Accomondia jijini Dar es Salaam, na itaondoka Machi 3 mwaka huu alfajiri kwa ndege ya South African Airways na kurejea nchini Machi 7 mwaka huu saa 8.15 mchana.


2 comments:

  1. Soka la Tanzania sasa liko ICU,huyo Madadi kwa mara ya mwisho alifundisha soka 1999 leo hii baada ya miaka 15 anapewa timu ya Taifa.Kweli ukstaajabu ya Musa utaona ya Firauni.Tumekabidhi TFF kwa watu wasio na uzoefu na uongozi wa soka na matokeo yake ndiyo haya.Naamini Mtinginjola alikuwa sahihi kumuengua Malinzi kwenye uchaguzi ule kwa kigezo cha kukosa uzoefu na sasa tunashuhudia udhaifu huo,Huyu alikuwa promota wa ngumi za kulipwa na kama kweli angekuwa na uwezo wa kuongoza soka tungeona mabadiliko katika mkoa wa Kagera ambako Malinzi ni mwenyekiti wa FA ya mkoa lakini hadi leo una timu moja tu ya ligi kuu ambayo hata yeye ameikuta na hakuna timu ya ligi daraja la kwanza..Hakuna maendeleo yoyote yatakayoletwa zaidi ya kuturudisha enzi za FAT na watakaofaidika ni yeye binafsi na wapambe wake Rutahyuga,Kidao na Nyenza

    ReplyDelete
  2. Soka letu bado lina safari ndefu sana, bado tunaangalia tulipoangukia na hatuangalii tulipo jikwaa.

    ReplyDelete