Search This Blog

Friday, January 3, 2014

KATA MTI PANDA MTI, TOM OLABA ASAINI MKATABA WA MIEZI 6 KUMRITHI MKWASA RUVU SHOOTING!!



Na Baraka Mpenja, Dar es salaam

MAAFANDE wa jeshi la kujenga Taifa wa mkoani Pwani, Ruvu Shooting, wamemsainisha mkataba wa miezi sita kocha, Tom  Alex Olaba ili kurithi mikoba ya kocha aliyetimkia Yanga, Charles Boniface Mkwasa `Masta`.

Afisa habari wa klabu hiyo, Masau Bwire amesema Olaba ameshafika Mabatini jioni ya leo na kila kitu kimemalizika baina ya pande mbili.

“Tunafurahi kutangaza kuwa tumempata mrithi wa Mkwasa. Olaba ni mwalimu mzuri na tuna uhakika atatuongoza vizuri mzunguko wa pili”. Alisema Masau.

Olaba ambaye amewahi kuifundisha Mtibwa Sugar ataanza kazi rasmi kesho kukinoa kikosi cha Ruvu Shooting kuelekea mzunguko wa pili wa ligi kuu soka Tanzania bara unaotarajia kuanza kutimu vumbi januari 25 mwaka huu.

Kwa upande wake Olaba alisema amefurahi kurudi ligi kuu Tanzania bara kwa mara nyingine, lakini hawezi kuzungumza lolote mpaka atakapoongea na wachezaji wake hapo kesho mazoezini.

“Nimechoka sana ndugu yangu, ujue nimetoka safarini. Hata hivyo kwasasa siwezi kuzungumza lolote mpakaa nikikutana na kuongea na wachezaji wangu. Kikubwa nimefurahi kurudi  katika changamoto ya ligi ya Tanzania”, Alisema Olaba.

No comments:

Post a Comment