Search This Blog

Thursday, November 21, 2013

NI WAKATI MWAFAKA WA ADEN RAGE KUONDOKA SIMBA


Na Baraka Mbolembole

Kuelekea mwisho wa utawala wa Hassan Dalali kama mwenyekiti wa klabu ya soka ya Simba, timu hiyo ya ' Msimbazi' ilikuwa katika wakati mgumu kiutawala. Dalali, alikua aishi kuvurugana na aliyekuwa katibu wake mkuu, Mwina Kaduguda. 

Kwa mtazamo wa haraka, Dalali ndiye ' Mwanachama- kiongozi' anayekubalika zaidi na ' Wana- Simba', ila katika utendaji wake wa mambo muhimu katika makaratasi ilikuwa ni tatizo kubwa. Kumalizika kwa muda wa utawala wake, klabu ikaingia
katika uchaguzi huru na wa haki na hapo, Julai, 2010, Ismail Aden Rage akaingia madarakani.
Nchi yetu bwanaaa, kila mahali migomo tu, hadi wenye maduka wameingia katika hali hiyo ili kutetea usawa wao. Je, haki ni nini? Bila shaka haki ni kitu ambacho kinajiendesha chenyewe bila choyo, Mtu mwenye hekima na Busara hutembea na kitu hiki huku kikimuongoza katika harakati zake za maisha. Harakati ni nini? Harakati ni njia ya maisha tu. Ni lazima tuitende haki na kuisadiki. Yule mwenye kufanya dhuluma, atalipwa dhuluma, na malipo ya dhuluma hiyo huwa ni kubwa kuliko dhuluma yenyewe.

 'MTU MKUBWA NI MWANAFUZI'
Kwa, Rage bila shaka Simba, ilifikiriwa ingesogea hatua fulani mbele, ila matokeo yake ni watu kukosa imani zaidi kwa Mwenyekiti huyo wa zamani wa Moro United, na katibu mkuu wa zamani wa Chama cha Soka Nchini, FAT, ( Sasa, TFF).. Mimi kwa upande wangu nilikuwa mara zote nikiangukia katika upande wa hoja za Mh. Rage, si kutokana na ' Siasa' zake bali kutokana na aina ya mtazamo wake wakati akiwa anazungumzia mipango ya maendeleo.
Wakati akiingia klabuni Simba, kama Mwenyekiti wa klabu nilifikiri labda sasa Simba itakuwa katika hali fulani nafuu, kiuchumi, kiutawala, na kiuendeshaji. Matokeo yake imekuwa ni fedhea kubwa. Wakati huu, ' Wasomi' kama Rage wakitawala soka la Tanzania, ni wazi mawazo yao mapya yanaweza kupingwa na upande mwingine, hasa upande ule ambao wanaamini kuwa soka linaweza kuendeshwa na mwanasoka wa zamani. Hapana, kuondoka kwa Dalali, hakukuja kwa bahati mbaya, alikuwa kiongozi mzuri lakini elimu yake ikamuondoa huku kundi kubwa la wanachama likitaka aorodheshwe katika orodha ya mwisho ya wagombea kinyume na katiba.
Funzo la kuondoka madarakani kwa Dalali, huku wanachama wengi wakimpigania lilipita nje ya fikra za Rage ambaye alikuja kushinda kwa kishindo katika uchaguzi. Ahadi zake zilikuwa ni nzuri, zilimvutia kila mmoja na ndiyo maana alishinda. ' Mtu mkubwa ni Mwanafunzi, kwani hutamani vitu zaidi kuliko watu wengine', na kwa Rage jambo moja kubwa lililomuingiza madaraki ni kuhiimariasha klabu kutoka katika utegemezi wa pesa za watu binafsi. Alisema kuwa ndani ya utawala wake Simba itakuwa na uwanja wake binafsi. Muda umekwenda sasa, na suala la Mwenyekiti huyo aliyesimamishwa na kamati ya utendaji kutoitisha mkutano wa katiba mpya ya klabu limewakera wengi na kumuona ni mtu mbinafsi, hasiye shahurika na mwenye maamuzi mabaya kwa klabu.

' PESA NI MTEGO'.
 Palipo na pesa ndipo pajaapo watu, lakini mafanikio yoyote huletwa na mawazo na mikakati mizuri ambayo inatekelezeka kwa maslahi ya pande zote. Katika mambo haya, Falsafa na Saikolojia, ni vitu muhimu vya kuzingatiwa, ipi iwe mwanzo, Saikolojia na falsafa?. Tusisahau kuwa ndani ya mambo haya pia kuna wenye kupenda vya bure, kikawaida hao ndiyo ' wenye mradi halisi', na wapo wenye uzalendo na wanaojua na kupenda ukweli wa mambo utendeke, Kundi hili la mwisho namaanisha, ' Ni lazima uwape wazalendo watakalo, ili nao wakupe utakacho'. Sababu ya yote hayo ni pesa.

 Kwa Aden Rage, pesa imekuwa ikimvuruga kwa kila namna, ameshindwa kuifanya Simba kujiendesha bila kutegemea mifuko ya watu. Na wakati klabu ikiwa imeuza wachezaji kama Herry Joseph, Mbwana Samatta, Danny Mrwanda, Patric Ochan, Mwinyi Kazimoto, Emmanuel Okwi, ni zaidi ya billioni moja wachezaji hawa wameingiza. Kama si kweli, Je, hawakuuzwa au walikopeshwa, na Simba ilinufaika vipi na biashara hiyo?

Klabu ya soka ya Simba iliwahi kumaliza msimu wa 2009 / 10 pasipo kupoteza mchezo wowote na kufanikiwa kutwaa ubingwa wa ligi kuu. Baada ya mafanikio yale Simba imepitia vipindi vya kupanda na kushuka ndani ya uwanja, huku sehemu kubwa ya wachezaji wa kikosi kile ikiwa imepungua. Kuanzia katika benchi la ufundi mabadiliko yamekuwa ya mara kwa mara, Patrick Phiri ambaye alikuwa kocha wa kikosi kilichomaliza msimu bila kufungwa, aliondoka na tangu, majira ya kiangazi, mwaka 2010, makocha, Moses Basena, Milovan Curkovick na Patrick Liewig , Abdallah Kibadei  walishikiria nafasi hiyo .

 Sio tu mabadiliko katika benchi la ufundi bali hata waliokuwa wachezaji wa kikosi kile wamekuwa wakipungua kwa kiasi kikubwa msimu hadi msimu. Wapo wachezaji ambao wameuzwa, wapo ambao wameamua kuachana na timu hiyo kwa sababu za kimaslahi mara baada ya kumalizika kwa mikataba yao, wapo ambao wameondolewa kwa sababu za kinidhamu, na pia wapo wachezaji ambao wameondolewa kwa sababu za nje ya klabu ama za uwanjani mara baada ya kutofautiana na baadhi ya viongozi au wanachama matajri wenye pesa na ushawishi mkubwa kuliko Rage.

Mimi ni mtu ambaye napenda kupigania ukweli. Jukumu langu ni kutafuta na kuwaelekeza ' wazalendo' katika njia nzuri kama ipasavyo kuwa. Majira yanaendelea kugeuka, na umefika wakati wa watu kukataa kuchezwa ' shere' kwa ahadi za uongo. Huu ni wakati wa kutoa ahadi zilizoimarika na zitakazojidhihirisha baadaye. Ni wakati wa kuwaeleza watu kuwa ahadi hewa au zisizotekelezeka si garantii ya uongozi bora. " Kijana, hata serikali ilitumia miaka 50 kujenga uwanja" aliwahi kuniambia Rage wakati fulani nilipoandika makala kuhusu utendaji wake wa ' Kisiasa' ndani ya Simba. Ahadi ni deni na bila shaka wakati akiahidi kuwa atahakikisha klabu inakuwa na uwanja wake kabla ya kumalizika kwa utawala wake alimaanisha nini? Huu ni wakati mwafaka kwa Rage kuondoka Simba, alitakiwa ajiuzulu kwa hiari yake mwenyewe kwa kuwa ameshindwa kuwa mtendaji mzuri wa klabu, hukui ndani ya uwanja matokeo yakiwa ni mabaya kwa miezi 16 sasa.
   MASHABIKI, MWANACHAMA, KIONGOZI
Kwenye mchezo wa soka kuna mashabiki. Shabiki ni mtu anayependa sana mambo au kitu fulani, Pia kuna wanachama, ' Mwanachama' ni mtu aliyejiunga na wenzake na kushiriki nao katika shughuli za umoja huo. Achana na hao, pia kuna uongozi, Kiongozi ni mtangulizi wa jambo fulani, ' mtu mkubwa' anayesimamia shughuli maalumu kwa kueleza au kuelekeza. Haya ni makundi makubwa matatu yenye nguvu na uwiano tofauti lakini jukumu kubwa hapa ni kuhakikisha kila upande unakuwa sehemu ya malengo na mafanikio yanayotarajiwa. Simba pia ni timu ambayo imezungukwa na makundi haya matatu japo kuna kundi lingine ambalo ni la wachezaji. Hawa ni watendaji wa ndani ya uwanja, na pia kuna kundi la  mwisho la benchi la ufundi hapa kocha ndiye ' bosi mkubwa'.

 Makundi yote haya ndiyo ambao ujenga timu, na umoja unaokuwepo ndiyo hutoa timu bora inayotoa zawadi ya ushindi kwa mashabiki, wanachama, viongozi, wachezaji na atimaye furaha hiyo huwa kubwa zaidi kwa benchi la ufundi. FALSAFA na SAIKOLOJIA, Falsafa ni mwendo wa maisha ya binadamu, Saikolojia ni ufahamu na utendaji kazi wa nafsi au akili ya mwanadamu. Hivyo basi
 Simba kama timu inayoendeshwa na kuzungukwa na makundi ya watu inaweza kuwa timu kama tu makundi hayo yatakuwa na umoja wenye nia moja.

 MAMBO HAYA NI MUHIMU PIA KUTAZAMWA
MASHABIKI' Hili ni kundi ambalo lipo mbali sana na klabu, ni kundi kubwa la watu ambalo mara zote hupata hisia za ukweli za uchungu kipindi timu inapokuwa inatoa matokeo mabaya uwanjani. Kundi hili huwa halipati taarifa muhimu za klabu, kuingia katika mikutano muhimu ya klabu, kwa sababu katiba ya Simba inaonesha, ' Simba ni timu ya Wanachama hai'. Mashabiki wana nguvu sana kuliko makundi yote yaliyomo ndani ya klabu na mara nyingi huwa tatizo kubwa, hasa pale wanapokuja juu na kushinikiza jambo fulani. Na, kwa Aden Rage naye amekutana na hasira za mashibi wa klabu hiyo ambao wamekuchikizwa na hali ya mambo inavyoendeshwa.
 Ila, nao wanatakiwa kufahamu kuwa katika soka kuna matokeo ya aina tatu za matokeo: Sare, Kushinda, ama Kufungwa. '

  WANACHAMA'.
 Simba ni klabu ya wanachama hai. Na ndani ya kundi hili ndipo hupatikana viongozi wa juu wa klabu. Wanapatikanaje?. Yule mwenye sera na mtazamo mzuri kwa klabu ndiye anaweza kupata kura ambazo zitamuwezesha kuongoza klabu katika mwendo unaotakiwa. Lakini chaguzi nyingi za klabu huwaingiza madarakani watu wenye mtazamo tofauti na mitazamo inayokusudiwa na klabu. Kama kila mwanachama atazingatia na kufikiria sana anapopata nafasi ya kupiga kura. Itamlazimu achague viongozi ambao watawakilisha katika njia ya manufaa. Lakini sivyo inavyokuwa. Si wapembuzi wa fikra, hawafikirii kuhusu baade, zaidi ya wakati uliopo. Ni wao ndiyo waliomuingiza madarakani Rage
   HIVI NDIVYO NILIVYOVUNJA IMANI YANGU KWA RAGE
Ilikuwa ni wakati ambao kiongozi huyo aliponipigia simu na kuniambia kuwa 'Usiandike tena kuhusu mimi', alifikia hatua ya kusema hivyo baada tu ya kumfananisha na ' mwanasiasa mahiri'. Aliniuliza kuhusu makala yangu na kila swali lake nilimpatia majibu, ila nilipokuwa nikitaka kumuuliza mimi alikuwa akinijibu majibu yaliyonikera.
Ilikuwa ni baada ya kuwaadaa wanachama katika mkutano wa mwaka wa klabu, agosti, 2012. Katika mkutano ule ambao hofu ya kupinduliwa kwake ilikuwa kubwa, wanachama walikwenda na hoja moja muhimu kuhusu ahadi yake ya uwanja na namna mradi huo unavyoendelea hadi sasa.  Rage, akawajibu kuwa kila kitu kinashindikana kutokana na klabu kukosa millioni 30 ili waongezee katika millioni 50 walizokuwa nazo ili kulipia hati ya kiwanja serikalini. Wakachangishana, bwanaaa. Ikapatikana millioni 32 hivi, wanachama wakafurahi sana na kushangilia.
Vyombo vingi vya habari vikaripoti, ' Wanachama Simba wachanga zaidi ya millioni 30', lakini hao wanachama wenyewe waliochanga, Zacharia Hans Pope alitoa kiasi cha millioni 10 , Rage akatoa millioni tano sawa na aliyekuwa makamu wake mwenyekiti, Geofrey Nyange Kaburu ambaye pia alitoa millioni tano. Nikafikiria nikaandika '; Simba, katikati ya wanasiasa, ila itavuka'.
 Katika makala hiyo niliwalaumu sana wanachama wa klabu kwa kudanganywa kila siku. Eti, klabu ilikuwa imekosa millioni 30 ili wapate hati ya uwanja, wakati ndani ya siku mbili walitumia zaidi ya millioni 50 kuwasajili Mrisho Ngassa na Ramadhan Chombo. Nikagusia pia kuhusu hilo na kusema kuwa waliwatafuta wachezaji wa kuvunja nguvu ya mapinduzi baada ya timu kuwa dhaifu katika michuano ya Kagame Cup.
Niligusia vitu vingi kiukweli na pengine niliviweka wazi tu. Vilimkera sana  Rage. Aliniambia ' Kuna watu wamekuwa wakiniuliza huyo kijana una matatizo naye' hawa ni watu wake ambao walikuwa wakimpigia simu na kumuuliza kama amesoma makala hiyo. Aliongea mengi sana, Ila nikamuomba anisomee mahali ambapo anafikiri kuna makosa, ' Hakuna makosa, ila nilishakwambia usiandike kuhusu mimi'. Kweli, sijawahi kumuandika tena Aden Rage, na wala sitaandika makala kuhusu yeye, ila kwa jambo kama hili naweza kusema. ' Mtu mkubwa ni mwanafunzi', Ila hata awe na akili nyingi kiasi gani, hawezi kubadili mwendo wa historia, anachoweza kufanya ni kubadilisha baadhi ya mambo na kuyafanya yawe safi. Labda, Rage atakumbukwa kutokana na Siasa zake ndani ya Simba, ila angeacha heshima kubwa kama angeweza kuisadia klabu kuwa na uwanja wake wa mazoezi.
Ni wakati sahihi wa Rage kuondoka? Acha tu aondoke, angefanya kwa hiari yake mwenyewe kung'atuka.  ' MAADILI' Ni tawi la falsafa ambalo hutafakari masuala ya mwendo wa jamii ili kubaini tabia nzuri na mbaya, tabia zisizo sahihi na potofu. Ethiki
, hutathimini mwendo wa jamii ili kuhakikisha kuwa maisha yanakuwa ya haki, amani na usawa. Masuala ya maadili  hayalingani katika jamii zote, ila kwa Aden Rage, Simba ilikuwa katika mwendo mbaya
0714 08 43 08

3 comments:

  1. Andika habari za Yanga wewe! Za simba huziwezi japo unajitahidi kuzilazimishia!!Wewe asili yako ya ndala FC huwezi kuificha!Hiki ndicho kitu kinachokuangusha mpaka makala zako zinaonekana za unazi! - Ni kama ile vita ya Amini na Tz,Eti Ghadafi anataka kuwa msuluhishi wakati huohuo yeye ni rafiki wa Amini!!Enzi zile Nyerere alistukia chezo.We Mbole mbole toka lini uka comment mazuri ya Simba na Rage!!

    ReplyDelete
  2. Rage ni muongo,mwizi,mbinafsi na mtu asie shaurika wewe unayemtetea una akili za mtindi usiyejua lolote zumbukuku hata hujui kama kwao Tabora pia wanajuta.Mwisho wa yote atakuja fungwa tena jela aondoke hatumtaki

    ReplyDelete
  3. Hiyo hadithi yako ya kizushi na kinafiki inatufundisha nini!!!? Ni miezi mingapi imebaki uchaguzi ufanyike ndani ya club ya simba, kwanini unataka Rage ang'orewe leo!!!? ili ufaidike kitu gani!!? Au timu iharibu zaidi ndo mpate kushangilia!!? Acheni ujinga acha simba wamalize mambo yao wenyewe na si nyie wanazi uchwara. Hans Pope alitoa milion 10 na Kaburu alitoa milion 5 unafikiri wao ni wajinga waone pesa yao inaliwa na Rage bila kusema neno!!? acheni uzushi wao wanajua pesa yao ilifanya nini si wajinga wakae kimya tu huku wanajua pesa yao ilibwengwa. Huna cha kutuandikia acha hizi si habari unatuandikia then unatupa mpaka majibu yake unayotaka wewe

    ReplyDelete