Search This Blog

Thursday, November 14, 2013

NANI MTANI JEMBE YAELEKEA KWA MASHABIKI WA TUNDUMA NA MOROGORO



Mashabiki wa Simba na Yanga kwenye miji ya Tunduma na Morogoro nao watapata fursa ya kuburudika katika michezo mbalimbali kupitia bonanza maalum la Nani Mtani Jembe lililoandaliwa na Bia ya Kilimanjaro Premium Lager litakalofanyika uwanja wa Mwaka mjini Tunduma na Kiwanja cha Ndege mjini Morogoro siku ya Jumapili wikendi hii.
Mratibu wa mabonanza hayo Lawrence Andrew, amesema kuwa michezo mbalimbali ikiwemo soka bonanza la wachezaji saba kila upande, kuvuta kamba, na pia mpira wa mezani maarufu kama fussball itapamba mabonanza hayo. Burudani mbalimbali pia zitapamba bonanza litakalofanyika Tunduma zikiwemo burudani ya muziki kutoka bendi ya High Class pamoja na wasanii mbalimbali wa muziki wa kizazi kipya wa mkoani Mbeya.

Kwa Mkoa wa Morogoro bendi maarufu mkoani humo ya Beacon Sound itatoa burudani kabambe kwa mashabiki watakaojumuika kushiriki bonanza hilo huku wasanii wa kundi maarufu la dansi GYT wakilishambulia jukwaa vilivyo.
Andrew pia amesema kuwa vilevile kuwa michezo mbalimbali ya kujifurahisha kama vile kufukuza kuku wa kienyeji, kukimbia na gunia na kupiga penati ukiwa umefungwa kitambaa usoni itapamba mabonanza hayo ambayo yatafanyika katika mikoa hiyo kwa mara ya kwanza kupitia Nani Mtani Jembe.

Kampeni hii ya aina yake inatoa fursa ya kipekee kwa mashabiki hao kujumuika pamoja na kuburudika na vile vile imeongeza chachu ya ushindani na utani wa jadi kati ya mashabiki hao huku ikiwapa fursa ya kipekee kuonyesha mapenzi kwa timu zao.
Mabonanza hayo yanalotarajiwa kuanza saa tatu asubuhi ni mwendelezo wa kampeni ya Nani Mtani Jembe ambayo ilizinduliwa Oktoba 2 na  inafanyika nchi nzima ikiwashirikisha mashabiki wa timu kongwe za Simba na Yanga. Kupitia kampeni hiyo, Kilimanjaro Premium Lager inayozidhamini timu za Simba ya Yanga imetenga kiasi cha shilingi milioni 100 na kisha kuzigawanya kwa timu hizo ambapo kila timu inazo shilingi milioni 50 ambazo zinashindaniwa na mashabiki wao.

Meneja wa Bia ya Kilimanjaro George Kavishe alisema kuwa mashabikiwa Simba na Yanga wanatakiwa kushindana kwa kushiriki kwenye kampeni hiyo ili kuhakikisha kuwa timu mojawapo inapata fedha nyingi zaidi ya timu nyingine.
Akielezea namna ya kushiriki, Kavishe alisema kuwa mpaka kila timu imetengewa shilingi milioni 50 na kuwa mshiriki wa shindano hilo la Nani Mtani Jembe ambaye ni shabiki wa Simba au Yanga anachotakiwa kufanya ni kununua bia ya Kilimanjaro Premium Lager ambayo kwenye kizibo chake kuna namba ya kushiriki.

Alisema baada ya shabiki kununua bia ya Kilimanjaro na kuona namba ya kwenye kizibo, anachotakiwa kufanya ni kuchukua simu yake ya kiganjani na kuandika ujumbe mfupi wa maneno akianza na jina la timu anayoshabikia kisha anaandika namba iliyo kwenye kizibo na kuituma kwenye namba 15440.

Alisema baada ya shabiki kutuma namba hiyo, atakuwa amepunguza shilingi 10,000 kutoka kwa timu pinzani yaani ikiwa shabiki aliyetuma ujumbe huo ni wa Simba atakuwa amefanikiwa kupunguza shilingi 10,000 kutoka kwenye fungu la Yanga na ikiwa shabiki ni wa Yanga pia atakuwa amepunguza shilingi 10,000 kutoka kwa Simba.

Kwa mujibu wa Kavishe matokeo ya uwiano wa fedha zinavyopungua kutoka Simba au Yanga yatangazwa kila siku hadi siku ya mwisho wa shindano hilo Desemba 14, mwaka huu.

Kwa mujibu wa matokeo kama ilivyotangazwa kwenye https://cms.rasello.com/kili  tovuti maalum ya Nani Mtani Jembe timu ya Yanga inaongoza kwa kuwa na kiasi cha shilingi 55,600,000 huku Simba ikiwa na shilingi 44,400,000 hii ikiwa ni baada ya Simba kuongoza kwa takribani wiki mbili sasa hatimaye Yanga wamewapita.

No comments:

Post a Comment