Search This Blog

Thursday, September 12, 2013

TUHUMA ZA KUKAMATWA NA MADAWA KWA WANAMICHEZO, NI MSINGI MBAYA ULIOACHWA NA VIONGOZI WALIOPITA



Na Baraka Mbolembole

Pesa siyo kila kitu katika maisha, ila mwanadamu anatakiwa kuwa na kiasi Fulani cha  pesa ili kumuwezesha kuishi katika jamii yake anayoishi. Mtu anatakiwa kufanya kazi ili apate kipato chake halali, na kumuwezesha kupata mahitaji yake muhimu ( Chakula, Mavazi, na Malazi). Pesa ni sabuni ya roho, lakini Hasara ‘Roho’, pesa ni makaratasi tu. Kila binadamu atakula kutokana na urefu wa kamba yake, na Yule asiyefanya kazi na asile ‘asilani’, ndivyo maandiko ya mwenyezi Mungu.

Tamaa ya kupata kipato cha haraka, ni chukizo kwa mwenyezi Mungu, labda kama matendo yanayokuingizia kipato chako ni ya halali, na yanayompendeza mwenyezi Mungu na kukubalika katika jamii. ‘ Wingu’ zito limetanda katika ‘anga’ ya Tanzania, wiki moja iliyopita kuna meli kubwa iliyokuwa imebeba zaidi ya tani 30 za Bangi, ilikamatwa pembezoni ya nchi ya Italia, bendera waliyokuwa wanaitumia katika meli hiyo ni ya…… Ni aibu kuitaja lakini ndiyo ukweli huo. Na huko inatangazwa kuwa ni…….TANZANIA.

Vita dhidi ya madawa ya kulevya katika miaka michache iliyopita ilikuwa inawahusisha, Polisi na wavutaji, wale mawakala, na wauzaji pamoja na wananuzi wakubwa hawakuwa wakiguswa. Miaka imekwenda, na kuwakamata wavutaji pekee ya kuacha mizizi yake ikiendelea kuchipua imekuwa ni tatizo kubwa kwa nchi yetu. Sasa, serikali za nchi ambazo hazihitaji ‘SEMBE’ katika ardhi ya nchi zao imekuwa ikitusaidia kuwakamata, wasafirishaji na waingizaji ‘ ulevi huo haramu kwa wananchi wao’ kuwakamata na kuwahukumu, Watanzania wenzetu ambao wamekuwa wakitumia nafasi zao Fulani katika jamii kufanya biashara hiyo haramu.

Kumbuka kuhusu wale mabondia ambao walikamatwa huko Visiwa vya Komoro na kuhumiwa vifungo vya miaka 15. Wanamichezo wamekuwa wakitumia kila sifa zao nzuri wanazozipata kutokana na vipaji vyao kuwaadaa, maafisa wa polisi na kupitisha biashara hiyo haramu. Ni msingi mbaya ambao mimi tangu nikiwa na miaka saba, wakati timu ya Simba ikichezea fainali ya kombe la Caf dhidi ya Stella Abdjan, na kufungwa nimekuwa nikisikia habari za uwepo wa usafirishaji wa  madawa ya kulevya kutumia wanamichezo. Niliwahi kusikia mengi tu, lakini sasa kukamatwa kwa wasanii maarufu nchini, wachezaji maarufu, mabondia maarufu, na wanasoka maarufu wakiwa na ‘ mizigo’ ya mabilioni ya shilingi katika nchi mbalimbali barani Afrika, Asia, ni muendelezo wa ukweli ambao ulikuwa ukifichwa nchini kwetu.

Ni msingi mbaya uliwekwa na viongozi wetu waliopita katika sekta mbambali, na hata kwa wanamichezo hatua ambazo nchi yetu imefika ya kukosa walau medali ya shaba katika michuano ya Olimpiki, Madola, ama ile ya Afrika ni dalili kuwa viongozi wetu waliopita waliacha msingi mbaya. WAlikuwa ni wafanyabiasha wakubwa wa kimataifa ambao muda wote walipanga mipango ya namna ya kuingiza na kutoa biashara zao haramu. Sasa wanakamtwa, nje ya nchi, wanalitia aibu Taifa, wanatia aibu thamani ya bendera ya nchi yetu. Lakini walipata wapi, ujasiri huo? ‘Mtoto wa nyoka ni nyoka. Na ukiishi na mwizi na wewe utakuwa mwizi’’ na ndicho kinachoonekana sasa, kuwa wachezaji ambao walitumia vibaya vipaji vyao na wakati wao wa uchezaji, wameamua kuingia wao wenyewe katika biashara hii, sijui ni kwa ‘mgongo wa nani’ ila ni kutokana na kile ambacho walikuwa wakikiona au  kufanya wakiwa chini ya misingi ambayo viongozi wetu waliijenga.

Na ilikuwaje kuhusu safari yako ya Ujerumani, tuliambiwa ulikwenda kufanya majaribio ? Kuna mchezaji niliwahi kumuuliza swali hili, naye akanijibu

Bwana Kule kiukweli kuna Siri nzito maana hata aliyenipeleka kanisihi sana nisiseme , lakini nilifanya majaribio kwa mwezi mzima,  ila ikatokea ishu ambayo ile timu hawakupendezwa nayo ikabidi nirudi nyumbani”

Nikamuuliza tena,

Ilikuhusu wewe au, na nani aliyekuwa wakala aliyekusimamia katika safari ile?

“  Haikunihusu mimi, ilimuhusu wakala wangu”

 Nikaendelea kudadisi….

Labda kwa ufupi kitu gani kilitokea kwani ulipata muda mrefu wa kujaribiwa?

“ Kweli nilipata muda mrefu kule, ila Daah! Ila kweli suala lililotokea siwezi  kusema kaka”

 Huyu ni mchezaji wa timu ya taifa na klabu kubwa nchini. Umewahi kuchunguza muda ambao wachezaji wetu huchukuliwa na mawakala na kupekwa nje ya nchi kufanya majaribio? Huwa ni kipindi ambacho dirisha la usajili limekuwa limefungwa, ndiyo hatukatai kuwa mchezaji anaweza kufanya vizuri na baadae akapewa nafasi ya kusajiliwa wakati wa usajili ukufika. Lakini ni wangapi ambao tumekuwa tukiambiwa kuwa wamefuzu, na watarudi tena wakati wa usajili na tunaendelea kuwaona katika viwanja vya Tanzania. Soka la kisasa linaenda kisasa, muda ni muhimu kuzingatiwa, rekodi ni muhimu na video ni muhimu pia.

Tazama tangu safari za Mrisho Ngassa, West Ham, na Seatlle Sounders, Abdulhalim Humud, Afrika ya Kusini, Mussa Hassan Mgosi, India, Shadrack Nsajigwa, Ufaransa, Zahoro Pazi, Ujerumani, na Afrika ya Kusini, wote hawa tuliambiwa wamefuzu majaribio walipokwenda kufanya na wangerudi tena. Kweli, Ngassa karudi Tena Yanga, Humud karudi tena, Simba, Zahoro kahama Azam katua Simba, Mgosi amerudi Mtibwa Sugar tena, kweli majira yanakwenda haraka sana. Biashara kwanza michezo baadae, kwa mwanasoka, kucheza soka la kulipwa hakutakuja kwa maribio bali ni kuonesha kiwango kama Mbwana Samatta na kutoka nje. Labda kama tutawaondoa wafanyabiashara wakubwa katika mpira.

 AFANDE SELE, mwanamuzi mshindi wa tuzo ya mfalme wa mashairi nchini aliwajhi kuimba Pesa, na kusema…..

" Achinjwe binadamu, na pesa ipakazwe damu...., Watu wataifuta, kisha wataitumia...., Watanunulia, misahafu na bibilia, na waumini wataipokeaaa...

 WATU, NAZO PESA... wewe zinakutesaaa,
MIMI ZINANITESAAA, pesaaa....
“Kweli, pesa ni tamu saaana, Ni tamu kwa kila namnaaa..., Kijana akikamata, madingi watamwita bwana... Dingi akikamata anaonekana ni kijanaaa..."

  0714 08 43 08

1 comment:

  1. Hali inatisha kaka,leo umeandika kitu cha maana sana,hongera kwa hilo.
    lkn mimi nikupinge kidogo kwa kuwalaumu viongozi,ifike wakati tuwe wakweli,tamaa ndio inayo wasukuma vijana kufanya mambo hayo kwani hakuna anaye shikwa mkono ila wao wenyewe pia wanazitaka hizo safari kwani wanajua wanacho pata.

    ReplyDelete