Search This Blog

Friday, June 14, 2013

WATOTO WA PELE WAKUBALI KUREJEA KUITUMIKIA TIMU YA TAIFA YA GHANA

Andre na Jordan Ayew kwa pamoja wamekubali kurejea nyumbani baada ya kufanya mashauriano na rais wa Ghana John Mahama mjini Accra.
Ndugu hao wawili walitangaza kuwa hawataichezea tena timu ya taifa ya Ghana mwezi Februari, baada ya kutofautiana na wasimamizi wa timu hiyo ya taifa ya Black Stars.
Ripoti zinasema wachezaji hao wawili wa klabu ya Marseille ya Ufaransa walifanya mazungumzo na rais Mahama wakati alipokuwa ziarani nchini Ufaransa.
Na katika mkutano wao wa pili, hii leo wachezaji hao waliafikiana kurejea tena nyumbani ili kuichezea Black Stars.
''Sasa tumerejea tena na tutafanya kila juhudi ili kuhakikisha kuwa Ghana imefuzu kwa kombe la dunia'' walisema wanandugu hao wawili.
Andre Ayew, aliacha kuichezea Black Stars, akidai kuwa hana uhusiano mzuri na viongozi wa shirikisho la mchezo wa soka nchini humo naye Jordan hakufurahishwa na uamuzi wa viongozi hao wa kumuacha nje ya kikosi kilichocheza nchini Afrika Kusini.
Ayew amesema wameamua kurejea tena katika timu hiyo ya taifa bila masharti yoyote.
Waziri wa michezo Elvis Afriyie Ankrah amesema rais wa nchi hiyo aliingilia kati mzozo huo kwa sababu anaamini kuwa timui ya taifa ya Ghana ni sharti iwe na wachezaji wake wote wenye vipaji na walio katika hali nzuri ili kuandikisha matokeo mema.
Wachezaji hao wawili sasa watajumuishwa kwenye kikosi cha Ghana kitakachocheza mechi za kufuzu kwa kombe la dunia dhidi ya Zambia Septemba mwaka huu.
Hata hivyo wengi wanasubiri kuona ikiwa kocha wa Ghana Kwesi Appiah atawashirikisha wachezaji hao wawili katika kikosi chake.

No comments:

Post a Comment