Search This Blog

Tuesday, February 26, 2013

REVEALED:KIKULACHO KINGUONI MWAKO, KINACHOITAFUNA SIMBA HIKI HAPA-PART 2


KOCHA wa zamani wa Simba, Milovan Cirkovic amesema klabu hiyo ilimsitishia mkataba kishenzi baada ya kukataa kufanya kazi kwa ‘remote’ alipokuwa anaifundisha klabu hiyo.

Akizungumza katika mahojiano exclusive na mtandao huu, Milovan raia wa Serbia alisema muda mfupi baada ya kwenda likizo kwao Serbia baada ya mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Bara kuisha, alianzishiwa vituko kutoka kwa uongozi.

“Nilipokuwa likizo Serbia mambo hayakuwa mazuri kama ilivyokuwa awali, wakati zamani naenda likizo Simba walikuwa wakinipigia simu na kuzungumza mambo mbalimbali kuhusu maendeleo ya timu. Mara hii hawakufanya lolote kwangu nami nikakaa kimya,” anasema Milovan.


SIMBA WAMNYIMA TIKETI BILA SABABU


Kila mara Milovan anapokuwa kwao Serbia kwa likizo, uongozi wa Simba ulikuwa ukimtumia tiketi ya kurudi Tanzania. Hata tiketi ya kwenda huwa anakatiwa na Simba. Lakini yalibadilika ghafla.

“Muda ulipofika wa mimi kutumiwa tiketi kama ilivyo kawaida, kila nikiwapigia simu viongozi wananiambia subiri, muda ukawa unaenda nami kila nikiuliza jibu linakuwa lile lile kwamba subiri subiri.

“Wakati nafanya nao mazungumzo ya tiketi, hata siku moja sikuwahi kuongea nao vibaya. Sasa kuna kitu nikawa najiuliza hawa jamaa wana nia gani na mimi, Je, maendeleo ya kikosi yakoje? Sikupata jibu lakini kuna kitu nikaanza kuhisi,” anasema Milovan.


MKATABA WAKE WASITISHWA ‘KIAINA’


Wakati bado yupo Serbia, Milovan anasema wakati mazungumzo yake ya kudai tiketi yalipokuwa yakiendelea alikuwa akizungumza vizuri na viongozi wa Simba na hata siku moja hawakuwahi kumwambia wanamsitishia mkataba wake.

“Hatukuwa na mazungumzo mabaya hata siku moja, kila siku Simba walikuwa wakiniambia subiri tiketi, hata mara moja hawakuonyesha kama wamechukizwa nami au kuna jambo lingine wanalotaka kufanya,” anasema Milovan.

Milovan anasema taarifa za kibarua chake kuota nyasi alizijua baada ya kusoma katika vyombo vya habari kisha akaamua kuwasiliana na Simba na bado majibu yakawa yaleyale yanayomtaka kusubiri.


FRIENDS OF SIMBA, MESSI WAMPONZA


Milovan moja kwa moja anahisi kitendo chake cha kukataa kupangiwa timu ndicho kilichouuzi uongozi wa Simba na kuamua ‘kumchinjia baharini’ kwa kuwa alikuwa akienda kinyume na matakwa ya mabosi wake, hilo likawa tatizo kwa uongozi.

Kwa mfano, uongozi ulikuwa unataka kocha kumtumia kila mara mchezaji Ramadhani Singano ‘Messi’ katika kila mechi, Milovan hakutaka hali hiyo japokuwa alikuwa akikubali uwezo wa mchezaji huyo na kumpanga kila mara.

“Messi alikuwa mchezaji mzuri na mimi nlikuwa namtumia katika mechi zangu nyingi, tazama hata Kigali (Rwanda, katika mechi dhidi ya Kiyovu) nilimtumia na alifanya vizuri. Tatizo wao wakawa wanataka kila mara nimchezeshe, hilo llikuwa tatizo kwangu kwani mimi nina mipango yangu maalum na siyo nimfuate mtu anavyotaka,” anasema Milovan.

Milovan anatolea mfano Kundi la Friends of Simba lilivyokuwa likimwingilia katika upangaji wa timu na kila mara alikuwa akitofautiana nao huku ikionekana wazi kwamba wao ndiyo walioshikilia ajira yake kwa kiasi kikubwa.

“Kama ilivyokuwa kwa uongozi, Friends of Simba nao walikuwa na mambo yao, walikuwa wanataka kunipangia wachezaji wa kuwachezesha namna wanavyotaka na si vinginevyo, hapo sikukubaliana nao.

“Mimi nilikuwa natekeleza wajibu wangu katika kupanga kikosi, yeyote aliyekuwa akitaka kuniingilia katika upangaji timu sikusita kumwambia kwamba sihitaji hali hiyo. Yawezkana msimamo wangu huo haukupendwa na kundi hilo lenye nguvu ndani ya Simba,” anasema Milovan.

HAKUHUSISHWA KUSIMAMISHWA BOBAN, NYOSSO

Milovan anasema wakati wachezaji Haruna Moshi ‘Boban’ na Juma Said ‘Nyosso’ wanasimamishwa kuichezea Simba, hakuhusishwa kama kocha kitendo ambacho kilienda kinyume na maadili.

Simba ikiwa katika mechi zake za mwisho za mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Bara, ilimsimamisha Boban kutokana na utovu wa nidhamu na Nyosso alisimamishwa kupelekwa timu B kwa kile kilichoelezwa ameshuka kiwango.

Milovan anasema uongozi haukumshirikisha kuhusu wachezaji hao na ulichukua dhidi yao kabla ya kuwasiliana naye. Mbaya zaidi uongozi ulimuita katika kikao cha kuwajadili wachezaji hao wakiwa tayari wameshasimamishwa.

“Viongozi waliwasimamisha Nyosso na Boban bila kunitaarifu halafu baadaye wakaniita kuwajadili wachezaji hao, hii si taaluma. Anayejua kuhusu kushuka kiwango cha mchezaji ni kocha, sasa iweje viongozi waseme mchezaji kashuka kiwango? Hii haikuwa haki na niliueleza uongozi,” anasema Milovan.

SIMBA YAMLIPA MAMILIONI

Milovan anasema amekuja nchini kufuatilia malipo ya kusitishwa kwa mkataba wake ambao ulipaswa kuisha Julai mwaka huu. Japokuwa Milovan hakuwa tayari kuweka wazi mshahara wake, mtandao huu unaamini kocha huyo anaweza kulipwa zaidi ya Sh. 52 milioni ambazo ni sawa na dola 35,000 za kimarekani.

“Wanatakiwa wanilipe stahili zangu zote, mimi mkataba wangu unaisha Julai mwaka huu wao wameuvunja tena kienyeji, unategemea nini? Lazima wanilipe ili kila mtu aweze kuwa salama,” anasema Milovan.

Aliyelipa fedha kwa Milovan si uongozi wa Simba ambao ulimterekeza, bali ni mmoja wa wanakamati wake wa kamati ya fedha, Rahma Al Kharuus ambaye pia ni mkurugenzi mtendaji wa kampuni ya RBP Oil.

ENDELEA KUSOMA MTANDAO HUU KWA SEHEMU YA 3 YA ALICHOSEMA MILOVAN KWA SIMBA

6 comments:

  1. MATHIAS DANIEL 27/2/2013

    In order forSIMBA SPORTS CLUB to succed,every person within a club must observe his/her specific duties,such an interference that Milovan speaks about meant that there's no need for club to look for qualified coaches since it seems that they know everything and that's the maim factor why we have lost the previous games, I THING MILOVAN STILL HAVE A CHANCE TO DO WITH SIMBA,IF THERE;S NO ANY INTERFERENCE!!!!!!!!!!!!

    ReplyDelete
  2. Milovan anatakiwa aeleze ni nani ktk friends of simba alikuwa akimpangia timu maana sidhani kama kundi zima lilifanya hivyo. Pia anatakiwa aeleze wachezaji wengi waliosajiliwa wakati wake na kulipwa fedha nyingi baada ya yeye kuwakubali lakini wakaondolewa muda mfupi baada ya kugundulika hawafai. Tatizo la usajili chini ya Milovan nadhani ndilo linaiumiza Simba hadi leo pamoja na kutia hasara kubwa club.

    ReplyDelete
  3. kuna kauli mbili za milovani ndio zinaiua simba, ingawa zote zinamaanisha kitu moja, ya kwanza ni friend of simba ndio wanaoshikilia ajira yake, na hela kulipwa na malkia wa nyuki mamaa rahma. klabu kubwa kama simba kukosa maana na kutegemea watu na tumikataba twao hatuwezi kufika, angalia wamemuuza okwi hela haziongelewi tena sababu alikuwa na mkataba na watu sio simba, hebu tuanze kujifunza kwa manji hata kama ni mpinzani, watu walitegemea atakuja yanga kutoa mahela hovyo, sasa anaitengeneza klabu iweze kujiendesha kwa hela zake najua watamchukia muda si mrefu waliotegemea miujiza, ila akiachwa na akili yake ya biashara, yanga itaenda level ingine kabisa kwa hela zake yenyewe, hizi klabu tajiri sana jamani, jaribu kutathmini mitaani sasa jezi za ulaya adimu siku hizi, watu wanapenda sana timu hizi. watu wanajiuzia jezi kwa logo za klabu mbila mpangilio inauma sana. change ni mimi na wewe.

    ReplyDelete
  4. inasikitisha klabu kubwa kama simba inapaswa kuendeshwa kimisingi ya utawala ya kisoka kila mtu akunbuke kupanga timu si hoja hoja nikukumbuka kuwa kesho timu itakuwaje je nyoso,kaseja bobani mafisango na okwi atakuja nani kuziba nafasi zao?!!!

    ReplyDelete
  5. ndiyo karaha ya kuwa na viongozi wababishaji ......wanachama wa simba wanatakiwa kuangalia aina ya viongozi ambao wana nia ya dhati na c hawa kina rage kwani wanaonekana kabisa ni wababaishaji na wapo kwa maslai yao binafsi, jaribu kuangalia swala la mafisango, kelvin yondan, mbuyi twite kuuzwa kwa okwi au kumnunua kipa na kulimlipa mshahara mwingi wakati anakaa bench... Ni busara wakatuachia simba yetu tu na waendelee na maswala yao.

    ReplyDelete
  6. Simba acheni siasa mpirani chukueni maamuzi magumu! Chanzo cha matatizo yote haya ni uongozi mbovu usio na maono na Klabu. na nadhani system za uongozi wa vilabu vyetu una kasoro. tuige wenzetu tufike tunapopataka haiezekani uongozi wenye sura za vyama vya siasa kuendeleza soka. Tubadilikeni. Muwe mnaangalia na kumbukumbu za nyuma watu hawa walifanya nini huko nyuma kwenye FAT? Maendeleo hakuna, jengo lilelile miaka nenda miaka rudi, uwanja wa klabu ndo kabisa ndoto za alnacha. Mauzo ya wachezaji ndo hayajulikani ht yanachofanya! Tutafika? wakati umefika tuamue kiume na tubdili mfumo wa uendeshaji wa vilabu vyetu. Naomba kuwasilisha. NURU SPORTS MSM

    ReplyDelete