Search This Blog

Thursday, December 20, 2012

TAIFA STARS VS ZAMBIA - KIM POULSEN NA RENARD KUZUNGUMZA NA WAANDISHI KESHO - NUSU FAINALI YA UHAI CUP KARUME

Makocha wa Tanzania (Taifa Stars), Kim Poulsen na Zambia (Chipolopolo) watakuwa na mkutano na waandishi wa habari utakaofanyika kesho (Desemba 21 mwaka huu) kuzungumzia pambano lao litakalochezwa Jumamosi (Desemba 22 mwaka huu) Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mkutano huo utafanyika saa 5 asubuhi kwenye ukumbi wa mikutano wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF). Makocha hao watazungumzia maandalizi yao ya mwisho kabla ya pambano hilo litakalochezeshwa na mwamuzi Sylvester Kirwa kuanzia saa 10 kamili jioni.

Pia makocha hao watajibu maswali kutoka kwa waandishi wa habari kuhusu pambano hilo litakalokutanisha timu hizo ambazo zimefanya vizuri kwenye orodha ya viwango vya ubora vya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) vilivyotolewa jana (Desemba 19 mwaka huu).

Wakati Zambia ambao ni mabingwa wa Afrika wamepanda juu kwa viwango vya ubora kwa nafasi nne, Taifa Stars ambayo katika mchezo uliopita iliifunga Kenya (Harambee Stars) bao 1-0 imepanda kwa nafasi nne.

Taifa Stars ambayo inadhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager iko kambini tangu Desemba 12 mwaka huu kujiandaa kwa mechi hiyo kubwa ya kirafiki inayotarajiwa kuwa ya kuvutia.

TENGA ATOA NOTISI YA MKUTANO MKUU TFF
Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga ambaye ndiye Mwenyekiti wa Mkutano Mkuu wa Shirikisho hilo tayari ametoa notisi ya mkutano huo utakaofanyika Februari 23 na 24 mwakani jijini Dar es Salaam.

Mkutano huo utafanyika Februari 23 mwakani na kufuatiwa na ajenda ya uchaguzi siku inayofuata. Ajenda ya uchaguzi iko chini ya Kamati ya Uchaguzi ya TFF.

Notisi hiyo imetumwa kwa wajumbe wa Mkutano Mkuu ambao ni kutoka vyama vya mpira wa miguu vya mikoa, vyama shiriki, klabu za Ligi Kuu ya Vodacom na wajumbe wa Kamati ya Utendaji ya TFF.

Ajenda za Mkutano Mkuu zitatumwa kwa wajumbe siku 15 kabla ya mkutano huo wenye wajumbe zaidi ya 100.

NUSU FAINALI UHAI CUP KUPIGWA KARUME
Mechi za nusu fainali ya michuano ya Kombe la Uhai 2012 inayoshirikisha timu za vijana wenye umri chini ya miaka 20 za klabu za Ligi Kuu ya Vodacom zitachezwa kesho (Desemba 21 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam.

Nusu fainali ya kwanza ya michuano hiyo inayodhaminiwa na kampuni ya Said Salim Bakhresa kupitia maji Uhai itazikutanisha timu za Mtibwa Sugar ya Morogoro na Azam na itafanyika kuanzia saa 2 kamili asubuhi.

Simba na Coastal Union zitacheza nusu fainali ya pili kuanzia saa 10 kamili jioni kwenye uwanja huo huo. Mtibwa Sugar imepata tiketi ya nusu fainali baada ya kuichapa African Lyon mabao 3-1 wakati Simba iliilaza Oljoro JKT mabao 2-0.

Nayo Azam iliindoa JKT Ruvu kwenye robo fainali kwa bao 1-0 huku Coastal Union ikipata ushindi wa penalti 4-3 dhidi ya Ruvu Shooting kwenye mechi ya mwisho ya robo fainali.

Mechi ya fainali na ile ya kutafuta mshindi wa tatu zitachezwa Jumapili (Desemba 23 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam. Mechi ya mshindi wa tatu itaanza saa 2 kamili asubuhi wakati ya fainali itakuwa saa 10 kamili jioni.

No comments:

Post a Comment