Search This Blog

Wednesday, November 7, 2012

BAADA YA KIPIGO NA VURUGU ZA WANACHAMA: UONGOZI WA SIMBA WAMTETEA KASEJA - WAMTAKA MILOVAN NA BENCHI LA UFUNDI KUPELEKA RIPOTI YA CHANZO CHA MATOKEO MABOVU

UONGOZI wa Simba SC unapenda kuzungumza yafuatayo kuhusiana na matukio ya karibuni kuhusiana na klabu ya Simba.

  1. Uongozi umesononeshwa na matokeo ya siku za karibuni ya timu ya Simba hususani yale ya kufungwa mabao 2-0 na Mtibwa Sugar ya Morogoro. Kutokana na hali hiyo, Kamati ya Utendaji ya Simba imeliagiza benchi la ufundi la Simba kutoa ripoti kuhusiana na mwenendo wa timu katika mechi za karibuni.
Ikumbukwe kwamba Simba ilianza ligi kwa vishindo na hadi kufikia mechi ya 12, ilikuwa ikiongoza ligi na ilikuwa timu pekee ambayo haikuwa imepoteza mechi.

Mara baada ya ripoti ya benchi la ufundi kukamilika, Kamati ya Utendaji ya Simba itakutana na kutoa maamuzi kuhusiana na yaliyomo kwenye ripoti. Kutokana na hali hiyo, uongozi unaomba wapenzi na wanachama wake kuwa watulivu katika kipindi hiki ambapo uongozi na benchi la ufundi linatafuta suluhisho la kudumu kuwezesha timu kuendelea kushinda.

Hata hivyo, uongozi wa Simba unasisitiza kwamba hakuna kiongozi yeyote wa Simba –kuanzia wa juu zaidi hadi wa chini zaidi, ambaye amejiuzulu au kuachia ngazi ndani ya klabu.

Ifahamike kwamba uongozi huu ulipewa dhamana na wanachama miaka minne iliyopita ya kuiongoza klabu kisasa na kuipa maendeleo endelevu kwa kipindi hicho.

Chini ya uongozi huu, Simba ilikuwa mshindi wa pili misimu miwili iliyopita (ikiwa pointi sawa na mabingwa ila ikizidiwa kwa pointi, ilikuwa mabingwa msimu uliopita, iliingia hatua ya 16 bora michuano ya CAF, imesajili wachezaji msimu huu kwa fedha zake yenyewe (miradi mbalimbali) na inaendesha timu tatu za vijana.

Bado kuna kazi za kufanya na uongozi unatambua hilo. Ndiyo maana uongozi hauamini kwamba maneno mabaya yanayosambazwa dhidi ya viongozi yanatoka kwa wanachama wake. Kazi nzuri ya uongozi huu inaonekana na iko dhahiri.
Uongozi wa Simba unaomba wapenzi na wanachama wake kuwa wamoja katika kipindi hiki ili kuwezesha ushindi kupatikana dhidi ya Toto African ya Mwanza Jumamosi ijayo.


2. Kuhusu mchezaji Juma Kaseja

Uongozi umesikitishwa na vitendo ambavyo baadhi ya washabiki walivifanya dhidi ya nahodha wa Simba, Juma Kaseja. Washabiki hao walimtukana, kumkashifu, kumdhihaki na kumtishia maisha mchezaji huyo mara baada ya mechi dhidi ya Mtibwa.

Kaseja ni miongoni mwa wachezaji wanaoheshimika sana ndani na nje ya nchi. Vitendo vya kumkashifu si vya kiungwana na uanamichezo. Nahodha huyu ameitumikia Simba kwa moyo mmoja na ni mmoja wa wachezaji wenye kuheshimika sana miongoni mwa wachezaji.

Hatua ya kumtukana inaharibu heshima ya klabu. Ni mchezaji mgani mzuri atataka kujiunga na Simba iwapo ataona Kaseja anafanyiwa hivyo? Benchi la ufundi la Simba ni makini na iwapo kutakuwa na tatizo lolote la kiuchezaji, litafanya mabadiliko.

Kama Kaseja angekuwa anapendelewa Simba, asingechaguliwa kuwa kipa namba moja wa Taifa Stars na nahodha pia.

Tunachukua fursa hii kutangaza kwamba uongozi wa Simba, kuanzia sasa, hautavumilia matusi kwa wachezaji au viongozi wake. Wote watakaobainika kufanya matendo haya, sheria itachukua mkondo wake.

Imetolewa na

Ezekiel Kamwaga
Ofisa Habari
Simba SC

1 comment:

  1. Nasikitishwa sana na Radio iliyoaminika kama radio ya michezo na burudani inapogeuzwa chama cha siasa,hii habari imetoka jana lakini kwa sababu inamgusa ibrahim masoud ambaye ni kiongozi jana hajazungumzia kabisa habari za simba,vurugu hizi zingekuwa upande wa pili ungemsikia.Aibu kwenu Clouds kwa unazi

    ReplyDelete