Search This Blog

Tuesday, October 23, 2012

AZAM KUIPIKU SIMBA KILELNI KESHO - YANGA DHIDI YA VIBONDE POLISI MOROGORO

Michuano ya Ligi Kuu ya Vodacom kuwania ubingwa wa Tanzania Bara inaendelea kesho (Oktoba 24 mwaka huu) kwa mechi nne za raundi ya tisa huku Azam ikiusaka usukani wa ligi hiyo ikiwa mwenyeji wa Ruvu Shooting.
 
Mechi hiyo namba 60 ambayo kama Azam itashinda itafikisha pointi 20, hivyo kuwa kileleni mwa Ligi Kuu ya Vodacom itachezwa Uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam. Viingilio katika mechi hiyo ni sh. 3,000 kwa sh. 10,000.
 
Yanga itawakaribisha Polisi Morogoro ambao ndiyo wa mwisho kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya Vodacom hivi sasa katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kwa kiingilio cha sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000.
 
Alex Mahagi kutoka Mwanza ndiye atakayepuliza filimbi kwenye mechi hiyo namba 62. Waamuzi wasaidizi ni Frank Komba na Michael Mkongwa, wote kutoka Iringa wakati mwamuzi msaidizi ni Oden Mbaga anayetambuliwa na Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) wa Dar es Salaam.
 
Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya African Lyon ya Dar es Salaam ambao ni wageni wa Coastal Union inayonolewa na Hemed Moroco. Nayo Mtibwa Sugar itaikaribisha Kagera Sugar kwenye Uwanja wa Manungu ulioko kwenye mashamba ya miwa Turiani mkoani Morogoro.
 
MTIBWA SUGAR, JKT RUVU SASA KUCHEZA NOV 7
Mechi namba 79 ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Mtibwa Sugar na JKT Ruvu iliyopangwa kuchezwa Novemba 3 mwaka huu Uwanja wa Manungu mkoani Morogoro, sasa itafanyika Novemba 7 mwaka huu.
 
Mabadiliko hayo yamefanyika kwa vile Novemba 4 mwaka huu, Mtibwa Sugar itacheza mechi namba 30 dhidi ya Simba kwenye Uwanja wa Jamhuri, mjini Morogoro. Mechi hiyo awali ilikuwa ichezwe Oktoba 3 mwaka huu lakini ikabadilishwa ili kutoa fursa kwa mechi za Super Week zilizooneshwa moja kwa moja na kituo cha televisheni cha Super Sport cha Afrika Kusini.
 
VITAMBULISHO FAINALI ZA AFCON 2013 MWISHO NOV 7
Waandishi wa Habari wanaotaka kuripoti fainali za mataifa ya Afrika (AFCON) zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini wanatakiwa kutuma maombi ya kupatiwa vitambulisho (Accreditation) kabla ya Novemba 7 mwaka huu.
 
Maombi hayo yatumwe Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kupitia CAF Medial Channel inayopatikana katika mtandao wa Shirikisho hilo wa www.cafonline.com
 
FDL KUANZA KUTIMUA VUMBI OKT 24
Michuano ya Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inaanza kutimua vumbi kesho (Oktoba 24 mwaka huu) kwenye viwanja mbalimbali nchini.
 
Kundi A kutakuwa na mechi tatu ambapo Burkina Faso itacheza na Mbeya City kwenye Uwanja wa Jamhuri mjini Morogoro wakati JKT Mlale itakuwa mwenyeji wa Small Kids kwenye Uwanja wa Majimaji, Songea.
 
Nayo Kurugenzi itaumana na Majimaji katika Uwanja wa Wambi ulioko Mufindi mkoani Iringa. Kundi hilo litamaliza raundi ya kwanza keshokutwa (Oktoba 25 mwaka huu) kwa mchezo kati ya Mkamba Rangers na Polisi Iringa utakaofanyika Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.
 
Mechi za kundi B kwa kesho ni Ndanda dhidi ya Transit Camp katika Uwanja wa Nangwanda Sijaona mjini Mtwara na Villa Squad itakipiga na Moro United kwenye Uwanja wa Mabatini mjini Mlandizi. Oktoba 25 mwaka huu ni Green Warriors v Tessema (Mabatini, Mlandizi) na Polisi Dar v Ashanti United (Uwanja wa Chamazi).
 
Kundi C kesho (Oktoba 24 mwaka huu) ni Kanembwa FC v Polisi Dodoma (Uwanja wa Lake Tanganyika, Kigoma), Mwadui v Morani (Kambarage, Shinyanga), Pamba vs Polisi Mara (Kirumba, Mwanza) na Rhino Rangers vs Polisi Tabora (Ali Hassan Mwinyi, Tabora).

No comments:

Post a Comment