Search This Blog

Friday, August 10, 2012

African Lyon yatambulisha kocha mpya kutoka Argentina

Kocha mpya wa timu ya African Lyon inayoshiriki  Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Pablo Ignacio Velez  kutoka Argentina wa kwanza kulia, akizungumzia nini atafanya akiwa  na timu hiyo kwa ajili ya msimu ujao uliopangwa kuanza Septemba Mosi mwaka huu. Kocha huyo amesaini mkataba wa miaka mitatu na timu hiyo. Wengine katika picha ni Charles Otieno ambaye ni mkurugenzi wa ufundi na Biashara wa timu hiyo na Meneja Mkuu na Mmiliki wa timu hiyo, Rahim Kangezi.

 
KOCHA mpya wa timu ya soka ya African Lyon, Pablo Ignacio Velez, amewasili nchini tayari kuanza kuinoa timu hiyo na kuomba apewe muda wa kukisuka upya kikosi hicho huku akiahidi mabadiliko zaidi ya soka kwenye timu hiyo.
Pablo raia wa Argentina aliyasema hayo jana baada ya kusaini mkataba wa mwaka mmoja kuitumikia timu hiyo na kusisitiza lengo lake kubwa ni kuhakikisha vijana wanapewa nafasi ya kuonyesha vipaji vyao na ndivyo itakavyokuwa Afrika Lyon.
"Sikuja Tanzania kutafuta pesa, ndoto yangu kubwa ilikuwa kufundisha soka barani Afrika hivyo wakati ni sasa," alisisitiza kocha anayezungumza lugha ya 'kiispanyola'.
Pablo alisema "kazi ya aina yoyote lazima ipewe muda na mchezaji lazima atengenezwe hivyo watanzania wawe na subira kwa ajili ya kupata matunda mazuri ya vijana hapo baadae kutoka African Lyon.
Kocha huyo aliyewai kuzichezea timu za taifa za vijana chini ya miaka 17 na 20 za Argentina hakusita kusisitiza suala la nidhamu kwa wachezaji wa timu hiyo ya ndani na nje ya uwanja.
"Nidhamu ni muhimu kwa wachezaji wangu cha msingi tushirikiane katika kufanikisha hili kwa vijana kwani mchezaji anatakiwa kati ya miaka 18 na 19 awe ametengeneza jina kupitia soka ,"  alisema Pablo.
Naye Mmiliki wa African Lyon, Rahmu Kangezi alisema lengo la kumleta kocha huyo ni kuhakikisha timu hiyo inajongea mbele zaidi.
Kangezi alisema licha ya kusaini mkataba wa mwaka mmoja lakini wanaweza kumtumia Pablo kwa kipindi kirefu kulingana na mfumo wa kuhakikisha wanaendeleza vijana katika timu yao.
"Pablo ni zaidi ya kocha, ana uwezo pia amecheza mpira pia ni kocha wa kwanza kutoka Argentina kuja Tanzania hivyo tunaimani timu yetu ya African Lyon itafika mbali zaidi kisoka," alisitiza Kangezi.
Pablo mwenye miaka 38 aliyechukua mikoba iliyoachwa na Jumanne Chale amewai kuifundisha  klabu ya Atletico Colo Colo De Chile (1998).
Klabu nyingine alizowai kufundisha ni Atletico Calchin (2000), Atletico Belgrano De Cordoba (1997), Atletico River Plate (1993-1995).
Klabu nyingine ni Banco De Cordoba (1991 na 1997), Deportivo Lasallano (1992) Atletico Argentino Penarol kwa miaka minne na klabu nyingine nyingi za Hispania na Argentina.

No comments:

Post a Comment