Search This Blog

Wednesday, January 11, 2012

MILOVAN: NIMERIDHISHWA NA UCHEZAJI WA TIMU YANGU


Head coach wa Simba, Milovan Cirkovic amesema ameridhishwa na kiwango kilichooneshwa na timu yake licha ya kufungwa mabao 2-0 na Azam FC, kwenye mchezo wa nusu fainali ya michuano ya Kombe la Mapinduzi juzi.

Wekundu hao wa Msimbazi walifungwa mabao hayo na washambuliaji, John Bocco na Gaudence Mwaikimba, lakini Mserbia huyo ameoneshwa kuridhishwa na kiwango cha timu
yake.

Bocco alifunga bao hilo kwa kumpiga chenga golikipa, Juma Kaseja ikiwa ni dakika ya tisa baada ya kuanza kwa mchezo huo.

Akitokea benchi, Mwaikimba aliongeza bao la pili kwa Azam ambalo ndilo liliwazima kabisa Simba.

Mshambuliaji huyo wa zamani wa Yanga, ambaye aliingia dimbani kuchukua nafasi ya kiungo wa kimataifa wa Ivory Coast, Kipre Balou, aliwatoka mabeki wa Simba kabla ya kumfunga Kaseja kwa shuti.

“Kufungwa mabao 2-0 dhidi ya Azam siyo matokeo mabaya kwa timu yangu na nina imani kubwa na vijana wa timu yangu. Kiukweli tulitawala mchezo, lakini tulishindwa kutumia nafasi tulizopata. Wapinzani wetu walitumia nafasi zote walizozipata,” alisema.

“Ilikuwa mechi nzuri kwa upande wangu, kwasababu ulikuwa mchezo mzuri dhidi ya timu bora kwa sasa hapa nchini. Nafikiri tulicheza vizuri zaidi usiku ule (Jumatatu), lakini
tulicheza na timu nzuri zaidi,” alisema.

Milovan alibainisha kwamba wachezaji wake wanazidi kuimarika jinsi siku zinavyosonga mbele, na kuahidi kwamba watafanya vizuri zaidi wakati wa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu inayoanza wiki mbili zijazo, pamoja na michuano ya Kombe la Shirikisho la CAF dhidi ya Kiyovu ya Rwanda mwezi ujao.

Naye kocha wa Azam FC, Stewart Hall raia wa Uingereza alisema kwamba timu yake ilifanya kazi kubwa na kuweza kupata ushindi huo.

Alisema licha ya wao kushinda, lakini Simba ilikuwa na safu nzuri zaidi ya ushambuliaji, ingawa ilishindwa kutumia nafasi nyingi ilizozipata.

Azam sasa itacheza na mshindi wa mchezo kati ya Mafunzo na Jamuhuri kwenye fainali ya Mapinduzi kesho kwenye Uwanja wa Amaan.

Mshindi wa mashindano hayo atajinyakulia zawadi ya Sh milioni 5 na mshindi wa pili Sh milioni 3.

No comments:

Post a Comment