Search This Blog

Friday, December 2, 2011

SIMBA: BASENA HANA CHAKE KWETU


Uongozi wa klabu ya Simba kupitia katibu mkuu wa klabu hiyo umesema hauna chochote unachodaiana na kocha Moses Basena baada ya kumalizanaye kisheria na hana sifa ya kudai fidia kimkataba.

Mbali na kauli hiyo pia uongozi huo umedai haukatishia mkataba na kocha huyo badala yake umesitisha kutokana na kutokuwa na vigezo kutokana na kukosa vyeti vya kufundisha kama kocha mwajiriwa.

Basena aliyechukua mikoba ya kuifundisha Simba toka mikononi mwa Mzambia Patric Phiri katika mzunguko wa pili wa ligi wa msimu uliopita jana alikaririwa na gazeti la mwananchi akidai kama Simba wamemkatishia mkataba wake ni vyema wamlipe kiasi cha Shs 99 Milioni kama mshahara wake baada ya kumatishia mkataba mbali na fidia ambayo ataafikia na uongozi huo.

Katibu mkuu wa Simba, Evodius Mtawala alisema ni vyema umma ukafahamu hawana nia mbaya na kocha huyo bali kisheria hana sifa ya kulipwa kimkataba kwani hakuwa na kibali rasmi cha kufundisha kama kocha.

"Napenda watu na mashabiki wa soka waelewe kitu kimoja, Basena hawezi kutudai tumlipe fidia kimkataba kwani hana sifa hiyo, hakuwa na kibali rasmi cha kufundisha na juzi ndio ametuma vyeti vyake ambavyo sisi kama uongozi tayari tumemsitishia baada ya kupata kocha mwingine na tunavyofahamu hatudai na sisi hatumdai,"alisema Mtawala.

Awali uongozi wa Simba ulidai Basena angewasili hapa nchini Disemba 6 kwa ajili ya kumalizana naye huku kocha huyo akisema hafahamu lolote kuhusu kukatishiwa mkataba huo na anakuja kwa ajili ya kuendelea na mzunguko wa pili wa ligi kuu.

Wakati hayo yakijiri tayari Simba amempa mkataba wa miezi6 kocha Mserbia Milovan Curcovic wa kuifundisha timu hiyo na anatarajia kuanza kazi rasmi Disemba10 mara baada ya kumalizika kwa michuano ya Chalenji.

No comments:

Post a Comment